Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kl sura 11 kur. 98-107
  • Hizi Ndizo Siku za Mwisho!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hizi Ndizo Siku za Mwisho!
  • Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SEHEMU ZA SIKU ZA MWISHO
  • UITIKIE UTHIBITISHO
  • Je, Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Je, Kweli Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu!
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! Wewe Utatii Onyo la Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
kl sura 11 kur. 98-107

Sura 11

Hizi Ndizo Siku za Mwisho!

1. Sababu gani wengi huhisi hawajui la kufanya wanapofikiria hali ya ulimwengu, lakini ufafanuzi wenye kutegemeka wa matukio ya ulimwengu waweza kupatikana wapi?

ULIMWENGU wetu wenye msukosuko ulifikiaje hatua hii? Sisi tunaelekea wapi? Je, umepata kujiuliza maswali hayo? Wengi huhisi hawajui la kufanya wanapotazama hali ya ulimwengu. Mambo halisi kama vita, maradhi, na uhalifu huacha watu wakijiuliza wakati ujao utakuwa na nini? Viongozi wa serikali hawatoi tumaini kubwa. Hata hivyo, ufafanuzi wenye kutegemeka wa siku hizi zenye taabu hupatikana kutoka kwa Mungu katika Neno lake. Kwa kutegemeka, Biblia hutusaidia tuone mahali tulipo katika mkondo wa wakati. Hiyo hutuonyesha kwamba tumo katika “siku za mwisho” za mfumo wa mambo uliopo.—2 Timotheo 3:1.

2. Yesu aliulizwa swali gani na wanafunzi wake, naye alijibuje?

2 Kwa kielelezo, fikiria jibu ambalo Yesu alitoa kwa baadhi ya maswali yaliyotokezwa na wanafunzi wake. Siku tatu kabla ya Yesu kufa, wao walimuuliza hivi: “Ni nini itakuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”a (Mathayo 24:3, NW) Kwa kujibu, Yesu alisema juu ya matukio na hali hususa za ulimwengu ambazo zingeonyesha kwa wazi kwamba mfumo huu usiomwogopa Mungu ungekuwa umeingia siku zao za mwisho.

3. Sababu gani hali duniani zilikuwa mbaya zaidi wakati Yesu alipoanza kutawala?

3 Kama vile ilivyoonyeshwa katika sura iliyotangulia, kronolojia ya Biblia huelekeza kwenye mkataa wa kwamba Ufalme wa Mungu umeanza kutawala tayari. Lakini hilo lawezaje kuwa hivyo? Mambo yamezidi kuwa mabaya, si mazuri. Kwa kweli, hii ni ishara thabiti kwamba Ufalme wa Mungu umeanza kutawala. Sababu gani hivyo? Zaburi 110:2 hutujulisha kwamba kwa muda fulani Yesu angetawala ‘kati ya adui zake.’ Kwa kweli, tendo lake la kwanza akiwa Mfalme wa kimbingu lilikuwa kutupa chini Shetani na malaika zake walio roho waovu, kwenye ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:9) Tokeo lilikuwa nini? Lilikuwa tu kama vile Ufunuo 12:12 lilivyotabiri: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Sisi tunaishi sasa katika “wakati [huo] mchache tu.”

4. Ni nini baadhi ya sehemu za siku za mwisho, nazo zinaonyesha nini? (Ona sanduku.)

4 Basi, si ajabu kwamba Yesu alipoulizwa ni nini ingekuwa ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo, jibu lake lilikuwa lenye kutia uzito. Sehemu mbalimbali za ishara hiyo zinapatikana katika sanduku kwenye ukurasa 102. Kama vile unavyoweza kuona, wale mitume Wakristo Paulo, Petro, na Yohana wanatupa sisi habari zaidi kuhusu siku za mwisho. Ni kweli, sehemu zilizo nyingi za ishara na za siku za mwisho zinahusisha hali zenye kusononesha. Hata hivyo, utimizo wa unabii huo mbalimbali watosha kutusadikisha kwamba mfumo huu mwovu uko karibu na mwisho wao. Acheni tuchunguze kwa ukaribu baadhi ya sehemu kuu za siku za mwisho.

SEHEMU ZA SIKU ZA MWISHO

5, 6. Unabii mbalimbali unaohusu vita na njaa kuu unatimizwaje?

5 “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme.” (Mathayo 24:7, NW; Ufunuo 6:4, NW) Mwandikaji Ernest Hemingway aliita Vita ya Ulimwengu 1 “uchinjaji mkubwa zaidi mno, wenye uuaji kimakusudi na wa ovyoovyo zaidi, ambao umepata kutukia duniani wakati wowote ule.” Kulingana na kitabu The World in the Crucible—1914-1919, huo ulikuwa “upeo mpya wa vita, vita ya kwanza ya ujumla iliyopata kuonwa na wanadamu. Muda wayo, ukali wayo, na kadiri yayo ilipita chochote kile kilichojulikana kimbele au kutarajiwa na watu kwa ujumla.” Kisha Vita ya Ulimwengu 2 ikaja, iliyothibitika kuwa yenye uharibifu mkubwa zaidi kuliko Vita ya Ulimwengu 1. “Karne ya ishirini,” asema Hugh Thomas, profesa wa historia, “imeongozwa na bunduki mimina-risasi, vifaru, ndege zinazoangusha makombora aina ya B-52, makombora ya nyukilia na, mwishowe, makombora ya kurushwa mbali. Imekuwa yenye vita ambavyo ni vya umwagaji-damu zaidi na vyenye uharibifu zaidi kuliko vile vya enzi nyingine yoyote.” Ni kweli, mengi yalisemwa juu ya kupunguza silaha baada ya ile Vita Baridi kuisha. Bado, ripoti moja yakadiri kwamba baada ya mapunguzo yaliyoazimiwa, silaha za nyukilia zipatazo 10,000 hadi 20,000 zitabaki—nguvu ya kivita iliyo kubwa mara 900 zaidi ya ile iliyotumiwa wakati wa Vita ya Ulimwengu 2.

6 “Kutakuwako upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7, NW; Ufunuo 6:5, 6, 8, NW) Tangu 1914 kumekuwa angalau visa 20 vya njaa kuu. Sehemu zilizokumbwa zinatia ndani Bangladesh, Burundi, China, Ethiopia, India, Kambodia, Nigeria, Rwanda, Somalia, Sudan, Ugiriki, na Urusi. Lakini njaa kuu haisababishwi sikuzote na ukosefu wa chakula. “Akiba ya chakula ya ulimwengu katika miongo ya miaka ya juzijuzi imeongezeka upesi zaidi kuliko idadi ya watu [ulimwenguni],” ndio mkataa uliofikiwa na kikundi fulani cha wanasayansi na wanauchumi wa kilimo. “Lakini kwa sababu watu angalau milioni 800 wangali katika hali ya umaskini sana, . . . wao hawawezi kununua sehemu ya kutosha ya wingi wa chakula kinachotolewa ulimwenguni ili kujiondoa katika utapiamlo wa kudumu.” Katika visa vingine kujiingiza kisiasa kwahusika. Dakt. Abdelgalil Elmekki wa Chuo Kikuu cha Toronto ataja vielelezo viwili ambavyo katika hivyo maelfu walikufa njaa kali hali nchi zao zilikuwa ziki­safirisha nje kiasi kikubwa sana cha chakula. Serikali hizo zilionekana zikihangaikia zaidi kukusanywa kwa fedha za kigeni ili kugharimia vita vyao kuliko kulisha raia wazo. Mkataa wa Dakt. Elmekki ulikuwa nini? Mara nyingi njaa kuu ni “jambo linalotegemea ugawanyaji na sera ya serikali.”

7. Ni nini yaliyo mambo ya hakika juu ya magonjwa ya kuambukiza leo?

7 “Magonjwa ya kuambukiza.” (Luka 21:11, NW; Ufunuo 6:8, HNWW) Homa ya Kihispania ya 1918-1919 iliua watu angalau milioni 21. “Ulimwengu haukuwa umepata kamwe katika historia kukumbwa na muuaji aliyeua wanadamu wengi sana upesi hivyo,” aandika A. A. Hoehling katika The Great Epidemic. Leo, magonjwa ya kuambukiza yaendelea kuenea bila kuzuilika. Kila mwaka, kansa huua watu milioni tano, maradhi yenye kuharisha huua vitoto vichanga na watoto zaidi ya milioni tatu, na kifua kikuu huua watu milioni tatu. Maambukizo ya viungo vya kupumua, hasa ugonjwa wa pafu, huua kila mwaka wachanga milioni 3.5 walio chini ya umri wa miaka mitano. Na idadi ya kushtua ya watu milioni elfu 2.5—nusu ya idadi ya watu ulimwenguni—hupatwa na magonjwa yanayotokana na kutokuwa na maji ya kutosha au kuwa na maji machafu na hali zisizo safi kwa afya. UKIMWI hutoa kikumbusha cha ziada cha kwamba mwanadamu, yajapokuwa matimizo yake makubwa ya kitiba, hawezi kuangamiza magonjwa ya kuambukiza.

8. Watu wanathibitikaje kuwa “wenye kupenda fedha”?

8 “Watu watakuwa . . . wenye kupenda fedha.” (2 Timotheo 3:2) Katika nchi zilizo kotekote ulimwenguni, watu huonekana wakiwa na tamaa isiyoridhika ya kupata mali nyingi zaidi. Mara nyingi “ufanisi” hupimwa kulingana na kiasi cha mshahara wa mtu, “matimizo” hupimwa kulingana na mali za mtu. “Ufuatiaji wa vitu vya kimwili utaendelea kuwa mojapo kani zenye kuchochea katika jamii ya Marekani . . . na [ufuatiaji huo utakuwa] kani inayozidi kuwa yenye maana katika mashirika mengine makuu pia,” akatangaza makamu wa rais wa shirika fulani la utangazaji. Je, hili linatukia mahali unapoishi?

9. Ni nini kinachoweza kusemwa juu ya kutokutii wazazi kulikotabiriwa?

9 “Wasiotii wazazi.” (2 Timotheo 3:2) Wazazi, walimu, na wengine wa siku hii wana uthibitisho ambao wamejionea wa kwamba watoto wengi wanakosa staha na ni wenye kutokutii. Baadhi ya vijana hawa ama wanaitikia ama wanaiga mwenendo mbaya wa wazazi wao. Idadi zenye kuongezeka za watoto wanapoteza imani katika—na kuasi dhidi ya—shule, sheria, dini, na wazazi wao. “Likiwa ndilo elekeo,” asema mwalimu mmoja wa siku nyingi, “wao huonekana wakiwa na heshima kidogo sana kwa kitu chochote.” Hata hivyo, ni kwa furaha kwamba watoto wengi wanaomhofu Mungu ni wenye kielelezo chema katika mwenendo wao.

10, 11. Kuna uthibitisho gani kwamba watu ni wakali na hawana shauku ya kiasili?

10 “Wakali.” (2 Timotheo 3:3) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “wakali” lamaanisha ‘wasiofugika, wa mwituni, wasio na huruma na hisia ya kibinadamu.’ Hilo lawafaa vizuri kama nini wale wengi watendao ujeuri wa leo! “Maisha ni yenye kuhuzunisha sana, yakiwa yamejaa sana machukio ya umwagaji-damu hivi kwamba ni lazima mtu ajikaze kihisia ili asome habari za kila siku,” ikasema safu moja ya uhariri. Askari wa jengo moja alisema kwamba vijana wengi waonekana wakijipofusha wasione matokeo ya matendo yao. Alisema: “Kuna maoni ya kwamba, ‘Mimi sijui ya kesho. Nitapata ninayotaka leo.’”

11 “Wasio na shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:3, NW) Fungu hilo la maneno limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “bila huruma, -enye ukatili” na kuonyesha “ukosefu wa shauku ya familia, iliyo ya kiasili.” (The New International Dictionary of New Testament Theology) Ndiyo, mara nyingi shauku haimo katika mazingira yenyewe ambamo inapaswa kusitawi—nyumbani. Ripoti za kutenda vibaya wenzi wa ndoa, watoto, na hata wazazi wazee-wazee zimekuwa za kawaida kwa njia ya kufadhaisha. Kikundi kimoja cha utafiti kilieleza hivi: “Ujeuri wa kibinadamu—uwe ni kupiga kofi au kusukuma, kuchoma kwa kisu au kufyatuliana risasi—hutokea mara nyingi zaidi katika familia kuliko kwingineko katika jamii yetu.”

12. Sababu gani inaweza kusemwa kwamba watu wana namna tu ya ujitoaji kimungu?

12 “Wakiwa na namna ya ujitoaji kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya huo.” (2 Timotheo 3:5, NW) Biblia ina nguvu ya kubadili maisha ili ziwe bora zaidi. (Waefeso 4:22-24) Hata hivyo, wengi leo hutumia dini yao kama kisetiri cha kuficha utendaji wao mbalimbali usio wa uadilifu ambao haumpendezi Mungu. Mara nyingi kusema uwongo, kuiba, na kuwa na mwenendo mbaya katika ngono huachiliwa na viongozi wa kidini. Dini nyingi huhubiri juu ya kuwa na upendo lakini huunga mkono vita. “Kwa jina la Muumba Mkuu,” yaonelea safu ya uhariri katika gazeti India Today, “wanadamu wametenda matendo ya kikatili yenye kuchukiza kuliko yote dhidi ya viumbe wenzao.” Kwa kweli, yale mapigano mawili ya nyakati za juzijuzi yenye umwagaji-damu mwingi zaidi—Vita vya Ulimwengu 1 na 2—yalianza katika kitovu cha Jumuiya ya Wakristo.

13. Kuna uthibitisho gani kwamba dunia inaharibiwa?

13 ‘Kuiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Wanasayansi zaidi ya 1,600, kutia ndani washindi 104 wa tuzo ya Nobeli, kutoka kotekote ulimwenguni walikubaliana na onyo, lililotolewa na shirika la Muungamano wa Wanasayansi Wanaohangaika (UCS), uliosema hivi: “Wanadamu na ulimwengu wa asili wamo karibu kugongana. . . . Ni miongo michache tu ya miaka inayobaki kabla nafasi ya kuondoa matisho [yanayotukabili] haijapotea.” Ripoti hiyo ilisema kwamba mazoea ya mwanadamu yenye kutisha uhai “yaweza kuubadili sana ulimwengu hivi kwamba hautaweza kutegemeza uhai kwa njia tunayojua.” Upungufu wa ozoni, uchafuzi wa maji, uharibifu wa misitu, kupungukiwa kwa uwezo wa ardhi kuzaa mimea, na kutoweka kwa jamii nyingi za wanyama na mimea yalitajwa kuwa matatizo yenye uharaka ambayo ni lazima yashughulikiwe. “Kuvuruga kwetu muundo wa uhai,” likasema lile shirika la UCS, “kungeweza kuchochea matokeo yenye kuenea sana, kutia ndani kuharibika kwa mifumo ya kibiolojia ambayo hatuelewi kikamilifu utendaji wayo mbalimbali.”

14. Ungeweza kuthibitishaje kwamba Mathayo 24:14 linatimizwa katika siku yetu?

14 “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote.” (Mathayo 24:14) Yesu alitabiri kwamba habari njema ya Ufalme ingehubiriwa duniani pote, kuwa ushahidi kwa mataifa yote. Kwa msaada na baraka ya kimungu, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova hutoa maelfu ya mamilioni ya saa kwa kazi hii ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Ndiyo, Mashahidi hutambua kwamba wangekuwa na hatia ya damu ikiwa wasingetangaza habari njema. (Ezekieli 3:18, 19) Lakini wanafurahi kwamba kila mwaka maelfu huitikia ujumbe wa Ufalme kwa shukrani na kuchukua msimamo wao wakiwa Wakristo wa kweli, yaani, kuwa Mashahidi wa Yehova. Ni pendeleo lenye thamani kumtumikia Yehova na hivyo kueneza ujuzi juu ya Mungu. Na baada ya habari hii njema kuhubiriwa katika dunia yote inayokaliwa, mwisho wa mfumo huu mwovu utakuja.

UITIKIE UTHIBITISHO

15. Mfumo mwovu uliopo utaishaje?

15 Mfumo huu utaishaje? Biblia inatabiri juu ya “dhiki kubwa” itakayoanza wakati “Babiloni Mkubwa,” ile milki ya ulimwengu ya dini bandia, inaposhambuliwa na sehemu ya kisiasa ya ulimwengu huu. (Mathayo 24:21, NW; Ufunuo 17:5, 16, NW) Yesu alisema kwamba katika kipindi hicho ‘jua lingetiwa giza, na mwezi haungetoa mwanga wake, na nyota zingeanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zingetikisika.’ (Mathayo 24:29) Huenda hilo likaonyesha matukio halisi ya kimbingu. Kwa vyovyote vile, wale wanaong’aa kama nuru katika ulimwengu wa kidini watafunuliwa na kuondolewa mbali. Ndipo Shetani, aitwaye “Gogu, wa nchi ya Magogu,” atatumia wanadamu waliofisidiwa kufanya shambulio la kufa na kupona juu ya watu wa Yehova. Lakini Shetani hatafanikiwa, kwani Mungu atawaokoa. (Ezekieli 38:1, 2, 14-23) Hiyo “dhiki kubwa” (NW) itafikia upeo wayo katika Har–Magedoni, “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Itaondolea mbali kila baki la mwisho la tengenezo la Shetani la kidunia, ikiwezesha baraka za milele ziwatiririkie wanadamu wanaookoka.—Ufunuo 7:9, 14; 11:15; 16:14, 16; 21:3, 4.

16. Twajuaje kwamba sehemu za siku za mwisho ambazo unabii ulitolewa juu yazo zinahusu wakati wetu?

16 Baadhi ya zile sehemu moja-moja za unabii mbalimbali unaofafanua siku za mwisho huenda zenyewe, zikahusu vipindi vinginevyo vya historia. Lakini yanapounganishwa pamoja, mathibitisho hayo ambayo unabii ulitolewa juu yayo huelekeza kwenye siku yetu. Kutoa kielezi: Mistari inayofanyiza alama ya vidole vya mtu huwa na namna isiyoweza kuwa ya mtu mwingine yeyote. Vivyo hivyo, siku za mwisho zina namna yazo zenyewe za alama, au matukio. Hizo hufanyiza “alama ya vidole” isiyoweza kuwa ya kipindi kingine chochote cha wakati. Uthibitisho unapochunguzwa pamoja na ishara za Biblia zinazoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu wa kimbingu unatawala sasa, huo huandaa msingi thabiti wa kukata maneno kwamba hizi kwa kweli ndizo siku za mwisho. Zaidi ya hayo, kuna ithibati ya Kimaandiko iliyo wazi kwamba mfumo mwovu uliopo utaharibiwa karibuni.

17. Ujuzi wa kwamba hizi ndizo siku za mwisho unapaswa utusukume tufanye nini?

17 Wewe utaitikiaje uthibitisho wa kwamba hizi ndizo siku za mwisho? Fikiria hili: Ikiwa dhoruba yenye nguvu sana inakaribia, sisi huchukua hatua za kujihadhari bila kukawia. Basi, yale ambayo Biblia hutabiri kuangukia mfumo huu uliopo yanapaswa yatusukume tutende. (Mathayo 16:1-3) Tunaweza kuona kwa wazi kwamba tunaishi katika siku za mwisho wa mfumo wa ulimwengu huu. Hilo lapaswa lituchochee tufanye marekebisho yanayohitajiwa ili kupata upendeleo wa Mungu. (2 Petro 3:3, 10-12) Akijirejezea kuwa wakili wa wokovu, Yesu atoa mwito huu wenye uharaka: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:34-36.

[Maelezo ya Chini]

a Biblia fulani-fulani hutumia neno “ulimwengu” badala ya “mfumo wa mambo.” Kamusi iitwayo Expository Dictionary of New Testament Words ya W. E. Vine, husema kwamba neno la Kigiriki ai·onʹ “humaanisha kipindi cha muda usio dhahiri, au wakati unaoonwa kwa kuhusiana na yale yanayotukia katika hicho kipindi.” Nayo kamusi iitwayo Greek and English Lexicon to the New Testament ya Parkhurst (ukurasa 17) hutia ndani usemi “mfumo huu wa mambo” katika kuzungumzia matumizi ya ai·oʹnes (kwa wingi) kwenye Waebrania 1:2. Kwa hiyo fasiri hii “mfumo wa mambo” inapatana na maandishi-awali ya awali ya Kigiriki.

TAHINI UJUZI WAKO

Biblia ilitabiri nini juu ya matukio ya ulimwengu mwanzoni mwa utawala wa Kristo?

Ni nini baadhi ya sehemu za siku za mwisho?

Ni nini kinachokusadikisha kwamba hizi ndizo siku za mwisho?

[Sanduku katika ukurasa wa 102]

BAADHI YA SEHEMU ZA SIKU ZA MWISHO

• Vita visivyo na kifani.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:4.

• Njaa kuu.—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:5, 6, 8.

• Magonjwa ya kuambukiza.—Luka 21:11; Ufunuo 6:8.

• Kuongezeka kwa uasi-sheria.—Mathayo 24:12.

• Kuharibiwa kwa dunia.—Ufunuo 11:18.

• Matetemeko ya dunia.—Mathayo 24:7.

• Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.—2 Timotheo 3:1.

• Upendo wa fedha wenye kupita kiasi.—2 Timotheo 3:2.

• Kutokutii wazazi.—2 Timotheo 3:2.

• Ukosefu wa shauku ya kiasili.—2 Timotheo 3:3.

• Kupenda anasa kuliko kumpenda Mungu.—2 Timotheo 3:4.

• Ukosefu wa kujidhibiti.—2 Timotheo 3:3.

• Kutopenda wema.—2 Timotheo 3:3.

• Kutokujali hatari inayokaribia sana.—Mathayo 24:39.

• Wenye kudhihaki wakataa katakata ithibati ya siku za mwisho.—2 Petro 3:3, 4.

• Kuhubiriwa kwa Ufalme wa Mungu duniani pote.—Mathayo 24:14.

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 101]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki