SURA YA KUMI NA MOJA
Dumisha Amani Nyumbani Mwako
1. Ni baadhi ya mambo gani ambayo huenda yakasababisha migawanyiko katika familia?
WENYE furaha ni wale walio sehemu ya familia ambamo kuna upendo, uelewevu, na amani. Yatumainiwa, familia yako ni ya jinsi hiyo. Yahuzunisha kwamba, familia nyingi sana hushindwa kufaana na ufafanuzi huo na zinagawanywa kwa sababu moja au nyingine. Ni nini kinachogawanya nyumba mbalimbali? Katika sura hii tutazungumzia mambo matatu. Katika familia fulani, washiriki wote hawashiriki dini ileile. Katika nyingine, huenda watoto wasiwe na wazazi walewale halisi. Katika nyingine bado, shindano la kupata riziki au tamaa ya kuwa na vitu zaidi vya kimwili huonekana kuwalazimisha washiriki wa familia wagawanyike. Hata hivyo, hali zinazogawanya nyumba moja huenda zisiathiri nyingine. Tofauti ni nini?
2. Watu fulani hutafuta wapi mwongozo katika maisha ya familia, lakini ni nini kilicho chanzo bora zaidi cha mwongozo huo?
2 Jambo moja ni maoni. Ukijaribu kwa moyo mweupe kuelewa maoni ya yule mtu mwingine, unaelekea zaidi kutambua jinsi ya kuhifadhi nyumba iliyounganika. Jambo la pili ni chanzo chako cha mwongozo. Watu wengi hufuata shauri la wafanyakazi wenzao, majirani, waandikaji wa safu za magazeti ya habari, au viongozi wengine wa kibinadamu. Lakini, watu fulani wamepata kujua yale ambayo Neno la Mungu husema kuhusu hali yao, kisha wakatumia yale waliyokuwa wamejifunza. Kufanya hivyo kwaweza kusaidiaje familia idumishe amani nyumbani?—2 Timotheo 3:16, 17.
IKIWA MUME WAKO ANA IMANI TOFAUTI
Jaribu kuelewa maoni ya yule mtu mwingine
3. (a) Shauri la Biblia ni nini kuhusu kufunga ndoa na mtu aliye wa imani tofauti? (b) Ni baadhi ya kanuni zipi za msingi zinazotumika ikiwa mwenzi mmoja wa ndoa ni mwamini na yule mwingine si mwamini?
3 Biblia hutushauri kwa uthabiti dhidi ya kufunga ndoa na mtu aliye na imani tofauti ya kidini. (Kumbukumbu la Torati 7:3, 4; 1 Wakorintho 7:39) Hata hivyo, huenda ikawa kwamba ulijifunza kweli kutoka Biblia baada ya ndoa yako lakini mume wako hakujifunza. Iweje basi? Bila shaka, nadhiri za ndoa zingali halali. (1 Wakorintho 7:10) Biblia hukazia udumu wa kifungo cha ndoa na hutia moyo watu waliooana wasuluhishe tofauti zao badala ya kuzitoroka. (Waefeso 5:28-31; Tito 2:4, 5) Lakini, namna gani ikiwa mume wako hupinga kwa nguvu kufuata kwako dini ya Biblia? Huenda akajaribu kukuzuia usiende kwenye mikutano ya kutaniko, au huenda akasema kwamba hamtaki mke wake aende nyumba hadi nyumba, akiongea kuhusu dini. Utafanya nini?
4. Mke aweza kuonyesha hisia-mwenzi katika njia gani ikiwa mume wake hashiriki imani yake?
4 Jiulize hivi, ‘Kwa nini mume wangu huhisi hivyo?’ (Mithali 16:20, 23) Ikiwa kwa kweli haelewi lile unalofanya, huenda akakuhangaikia. Au huenda akawa anasongwa na watu wa ukoo kwa sababu wewe hushiriki tena katika desturi fulani zilizo za maana kwao. “Nikiwa peke yangu nyumbani, nilihisi nimeachwa,” akasema mume mmoja. Mtu huyu alihisi kwamba alikuwa akimpoteza mke wake kwa sababu ya dini fulani. Hata hivyo kiburi kilimzuia asikiri kwamba alikuwa mpweke. Huenda mume wako akahitaji uhakikishio kwamba kumpenda kwako Yehova hakumaanishi kwamba sasa wampenda mume wako kidogo zaidi kuliko wakati uliopita. Hakikisha unatumia wakati ukiwa pamoja naye.
5. Ni usawaziko gani ambao lazima uwekwe na mke ambaye mume wake ni wa imani tofauti?
5 Hata hivyo, jambo lililo la maana hata zaidi lazima lifikiriwe ikiwa utashughulikia hiyo hali kwa hekima. Neno la Mungu huhimiza wake hivi: “Iweni katika ujitiisho kwa waume zenu, kama inavyofaa katika Bwana.” (Wakolosai 3:18) Hivyo, laonya dhidi ya roho ya kutaka kujitegemea. Kwa kuongezea, kwa kusema “kama inavyofaa katika Bwana,” andiko hili laonyesha kwamba ujitiisho kwa mume wa mtu wapaswa pia utie ndani ujitiisho kwa Bwana. Lazima kuwe na usawaziko.
6. Ni kanuni gani zizingatiwe akilini mwa mke Mkristo?
6 Kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kutolea wengine ushahidi kuhusu imani ya mtu yenye msingi wa Biblia, ni sehemu za maana za ibada ya kweli ambazo Mkristo hapaswi kuzipuuza. (Waroma 10:9, 10, 14; Waebrania 10:24, 25) Ungefanyaje basi, ikiwa binadamu fulani angekuamuru moja kwa moja usitii takwa hususa la Mungu? Mitume wa Yesu Kristo walitangaza hivi: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kielelezo chao chaandaa mfano ambao waweza kutumika katika hali nyingi maishani. Je, kumpenda Yehova kutakusukuma umtolee ujitoaji ulio haki yake? Wakati uleule, je, kumpenda na kumstahi mume wako kutakufanya ujaribu kufanya hivyo kwa njia inayokubalika kwa mume wako?—Mathayo 4:10; 1 Yohana 5:3.
7. Mke Mkristo lazima awe na azimio gani?
7 Yesu alionyesha kwamba hilo lisingewezekana sikuzote. Alionya kwamba kwa sababu ya upinzani kwa ibada ya kweli, washiriki waamini wa baadhi ya familia wangehisi wamekatiliwa mbali, kana kwamba upanga ulikuwa umekuja kati yao na wengine wa familia. (Mathayo 10:34-36) Mwanamke mmoja Japani alipatwa na hilo. Yeye alipingwa na mume wake kwa miaka 11. Mume huyo alimtenda vibaya kwa kudhulumu na mara nyingi alimfungia nje ya nyumba kwa kufuli. Lakini mke alivumilia. Marafiki katika kutaniko la Kikristo walimsaidia. Yeye alisali bila kukoma akapata kitia-moyo kingi kutokana na 1 Petro 2:20. Mwanamke huyu Mkristo alisadikishwa kwamba ikiwa angeendelea kuwa imara, siku moja mume wake angejiunga naye katika kumtumikia Yehova. Na mume akafanya hivyo.
8, 9. Mke atendeje ili aepuke kumwekea mume wake vipingamizi visivyo vya lazima?
8 Kuna mambo mengi yenye kutumika ambayo wewe waweza kufanya ili kuathiri mtazamo wa mwenzi wako. Kwa kielelezo, ikiwa mume wako apinga dini yako, usimpe sababu halali za kulalamikia mambo mengine. Dumisha nyumba ikiwa safi. Tunza sura yako ya kibinafsi ikiwa safi. Uwe mkarimu na maneno ya kuonyesha upendo na uthamini. Badala ya kuchambua, uwe mwenye kuunga mkono. Onyesha kwamba wamtegemea yeye akiwa kichwa. Usilipize kisasi ukihisi umekosewa. (1 Petro 2:21, 23) Kumbuka hali ya kutokamilika kwa kibinadamu, na bishano likitokea, uwe wa kwanza kuomba radhi kwa unyenyekevu.—Waefeso 4:26.
9 Usiruhusu kuhudhuria kwako mikutano kuwe sababu ya kuchelewa kwa milo yake. Huenda pia ukachagua kushiriki katika huduma ya Kikristo wakati ambapo mume wako hayuko nyumbani. Ni jambo la hekima kwa mke Mkristo kuepuka kumhubiri mume wake wakati mume hataki hivyo. Badala ya hivyo, mke hufuata shauri hili la mtume Petro: “Nyinyi wake, iweni katika ujitiisho kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa neno, wapate kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kuwa mashahidi wa kujionea mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:1, 2) Wake Wakristo hushughulikia kudhihirisha kikamili zaidi matunda ya roho ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23.
MKE ASIPOKUWA MWENYE KUFUATA UKRISTO
10. Mume mwamini atendeje kuelekea mke wake ikiwa mke ni wa itikadi tofauti?
10 Namna gani ikiwa mume ndiye mwenye kufuata Ukristo na mke hafuati? Biblia hutoa mwongozo kwa hali za jinsi hiyo. Hiyo husema: “Ikiwa ndugu yeyote ana mke asiyeamini, na bado ni mwenye kukubali kukaa pamoja naye, na asimwache.” (1 Wakorintho 7:12) Hiyo huonya pia kwa upole hivi: “Fulizeni kuwapenda wake zenu.”—Wakolosai 3:19.
11. Mume aweza kuonyeshaje ufahamu na kutumia ukichwa kwa busara juu ya mke wake ikiwa mke si mwenye kufuata Ukristo?
11 Ukiwa mume wa mke aliye na imani iliyo tofauti na yako, uwe mwangalifu hasa kumwonyesha mke wako staha na ufikirio kwa hisia zake. Akiwa mtu mzima, yeye astahili kadiri fulani ya uhuru ili afuate itikadi zake za kidini, hata ikiwa hukubaliani nazo. Mara ya kwanza unapoongea naye kuhusu imani yako, usimtazamie aachie mbali itikadi ambazo ameshika kwa muda mrefu ili kuweza kufuata jambo fulani jipya. Badala ya kusema bila busara kwamba mazoea ambayo yeye na familia yake wamependa sana kwa muda mrefu si ya kweli, jitahidi kwa subira kusababu naye kutoka Maandiko. Huenda mke wako akawa ahisi amepuuzwa ukitumia wakati mwingi mno ukishughulikia utendaji mbalimbali wa kutaniko. Huenda akapinga jitihada zako za kumtumikia Yehova, lakini huenda ujumbe wa msingi ukawa tu: “Nahitaji wakati wako mwingi zaidi!” Uwe mwenye subira. Hatimaye, kwa ufikirio wako wenye upendo, huenda akasaidiwa akubali ibada ya kweli.—Wakolosai 3:12-14; 1 Petro 3:8, 9.
KUWAZOEZA WATOTO
12. Hata ikiwa mume na mke wake ni wa imani tofauti, kanuni za Kimaandiko zitumiweje katika kuzoezwa kwa watoto wao?
12 Katika nyumba isiyounganika katika ibada, nyakati nyingine mafunzo ya kidini kwa watoto huwa suala. Kanuni za Kimaandiko zitumiweje? Biblia humgawia baba daraka kuu la kuwafunza watoto, lakini mama ana fungu la maana pia. (Mithali 1:8; linganisha Mwanzo 18:19; Kumbukumbu la Torati 11:18, 19.) Hata asipokubali ukichwa wa Kristo, baba angali ndiye kichwa cha familia.
13, 14. Mume akimkataza mke wake asiwapeleke watoto kwenye mikutano ya Kikristo au kujifunza nao, yeye aweza kufanya nini?
13 Akina baba fulani ambao si waamini hawakatai ikiwa mama awafunza watoto mambo ya kidini. Wengine hukataa. Namna gani ikiwa mume wako akataa kukuruhusu uwapeleke watoto kwenye mikutano ya kutaniko au hata akukataza ujifunze Biblia nao nyumbani? Sasa ni lazima usawazishe wajibu mbalimbali—wajibu wako kwa Yehova Mungu, kwa ukichwa wa mume wako, na kwa watoto wako wapendwa. Unaweza kupatanishaje hayo?
14 Kwa hakika utasali kuhusu hilo jambo. (Wafilipi 4:6, 7; 1 Yohana 5:14) Lakini hatimaye, wewe ndiwe upaswaye kuamua mwendo wa kuchukua. Ukifanya mambo kwa busara, ukielewesha wazi kwa mume wako kwamba hupingi ukichwa wake, huenda upinzani wake ukapungua hatimaye. Hata ikiwa mume wako akukataza usiwapeleke watoto wako kwenye mikutano au uwe na funzo rasmi la Biblia pamoja nao, waweza bado kuwafundisha. Kwa mazungumzo yako ya kila siku na kielelezo chako chema, jaribu kukaza kikiki ndani yao kadiri fulani ya kumpenda Yehova, kuwa na imani katika Neno lake, kustahi wazazi—kutia na baba yao—upendo wenye ufikirio kwa watu wengine, na kuthamini mazoea ya kazi ya kudhamiria. Hatimaye, huenda baba akaona matokeo mazuri na huenda akaona thamani ya jitihada zako.—Mithali 23:24.
15. Baba mwamini ana daraka gani katika elimu ya watoto?
15 Ukiwa mume aliye mwamini na mke wako si mwamini, basi ni lazima uchukue daraka la kuwalea watoto wako “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Ufanyapo hivyo, bila shaka wapaswa uwe mwenye fadhili, mwenye upendo, na mwenye kiasi katika kushughulika na mke wako.
IKIWA DINI YAKO SI ILE YA WAZAZI WAKO
16, 17. Ni kanuni gani za Biblia ambazo ni lazima watoto wakumbuke ikiwa wanakubali imani iliyo tofauti na ile ya wazazi wao?
16 Si jambo lisilo la kawaida tena kwa hata watoto wadogo kukubali maoni ya kidini yaliyo tofauti na yale ya wazazi wao. Je, umefanya hivyo? Ikiwa ndivyo, Biblia ina shauri kwako.
17 Neno la Mungu husema: “Iweni watiifu kwa wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni lenye uadilifu: ‘Heshimu baba yako na mama yako.’” (Waefeso 6:1, 2) Hilo latia ndani staha ifaayo kwa wazazi. Hata hivyo, ingawa utii kwa wazazi ni wa maana, haupasi kuonyeshwa bila kumjali Mungu wa kweli. Mtoto anapofikia umri wa kutosha kuanza kufanya maamuzi, yeye huwa na kiasi kilichoongezeka cha daraka kwa matendo yake. Hilo ni kweli si kwa habari ya sheria ya kimwili tu bali hasa kuhusiana na sheria ya kimungu. “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe,” Biblia hutaarifu.—Waroma 14:12.
18, 19. Ikiwa watoto wana dini iliyo tofauti na ile ya wazazi wao, wao waweza kusaidiaje wazazi wao waelewe imani yao vizuri zaidi?
18 Itikadi zako zikikusababisha ufanye mabadiliko maishani mwako, jaribu kuelewa maoni ya wazazi wako. Ni yamkini wao watapendezwa ikiwa, likiwa tokeo la kujifunza kwako na kutumia mafundisho ya Biblia, unakuwa mwenye staha zaidi, mwenye utii zaidi, mwenye bidii zaidi ya kuendelea katika yale wanayokuomba ufanye. Hata hivyo, imani yako mpya ikikufanya pia ukatae katakata itikadi na desturi wanazopenda sana kibinafsi, huenda wakahisi kwamba unapuuza urithi waliotafuta kukupa. Huenda pia wakahofia hali yako njema ikiwa yale unayofanya hayapendwi na watu wote katika jumuiya au ikiwa yanaelekeza uangalifu wako mbali na vifuatio ambavyo wao huona vingeweza kukusaidia ufanikiwe kimwili. Kiburi kingeweza kuwa kizuizi pia. Huenda wakahisi kwamba, ni kama unasema kwamba wewe unafanya lililo sawa na wao wanafanya makosa.
19 Kwa hiyo, upesi iwezekanavyo, jaribu kupanga ili wazazi wako wakutane na baadhi ya wazee au Mashahidi wengine walio wakomavu kutoka katika kutaniko la kwenu. Watie moyo wazazi wako watembelee Jumba la Ufalme ili wasikie wenyewe yale yanayozungumzwa na wajionee wenyewe Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani. Hatimaye, huenda mtazamo wa wazazi wako ukalainika. Hata wazazi wanapokuwa wenye kupinga sana, wanapoharibu fasihi za Biblia, na kuwakataza watoto wasihudhurie mikutano ya Kikristo, kwa kawaida kuna fursa za kusoma kwingineko, kuongea na Wakristo wenzetu, na kuwatolea wengine ushahidi na kuwasaidia kwa njia isiyo rasmi. Waweza pia kusali kwa Yehova. Vijana fulani wanalazimika kungojea hadi wanapokuwa wenye umri wa kutosha kuishi nje ya nyumba ya familia kabla ya wao kuweza kufanya mengi zaidi. Hata hivyo, hali iwe ni nini nyumbani, usisahau ‘kuheshimu baba yako na mama yako.’ Fanya sehemu yako ili kuchangia amani nyumbani. (Waroma 12:17, 18) Zaidi ya yote, fuatia amani pamoja na Mungu.
UGUMU WA KUWA MZAZI WA KAMBO
20. Huenda watoto wakawa na hisia gani ikiwa baba au mama yao ni mzazi wa kambo?
20 Katika nyumba nyingi hali inayotokeza ugumu mkubwa zaidi si ya kidini bali ni ya kiuzazi. Nyumba nyingi leo hutia ndani watoto kutoka ndoa za awali za mzazi mmoja au wote wawili. Katika familia ya jinsi hiyo, huenda watoto wakawa na hali ya wivu na uchungu au labda kupingana kwa uaminifu-mshikamanifu. Likiwa tokeo, huenda wakapinga jitihada zenye moyo mweupe za mzazi huyo wa kambo za kuwa baba au mama mwema. Ni nini kiwezacho kusaidia kufanya familia ya kambo iwe yenye mafanikio?
Uwe ni mzazi asili au mzazi wa kambo, tegemea Biblia ili kupata mwongozo
21. Zijapokuwa hali zao za pekee, kwa nini wazazi wa kambo waendee kanuni zinazopatikana katika Biblia ili kupata msaada?
21 Ng’amua kwamba zijapokuwa hali za pekee, kanuni za Biblia ziletazo mafanikio katika nyumba nyinginezo hutumika hapa pia. Kupuuza kanuni hizo huenda kukaonekana kutuliza tatizo fulani kwa muda, lakini ni yamkini kutaongoza kwenye maumivu ya moyoni baadaye. (Zaburi 127:1; Mithali 29:15) Sitawisha hekima na ufahamu—hekima ya kutumia kanuni za kimungu ukifikiria manufaa zenye kudumu muda mrefu, na ufahamu wa kutambua ni kwa nini washiriki wa familia husema na kufanya mambo fulani. Kuna uhitaji pia wa hisia-mwenzi.—Mithali 16:21; 24:3; 1 Petro 3:8.
22. Kwa nini huenda watoto wakaliona kuwa jambo gumu kumkubali mzazi wa kambo?
22 Ikiwa wewe ni mzazi wa kambo, huenda ukakumbuka kwamba ukiwa rafiki ya hiyo familia, labda ulikaribishwa na watoto. Lakini ulipogeuka kuwa mzazi wao wa kambo, huenda ikawa mtazamo wao ulibadilika. Wakimkumbuka mzazi wao halisi ambaye haishi nao tena, huenda watoto wakawa wanang’ang’ana na kupingana kwa uaminifu-mshikamanifu, labda wakihisi kwamba wewe wataka kuondolea mbali shauku waliyo nayo kuelekea mzazi ambaye hayupo. Nyakati nyingine, huenda wakakukumbusha kwa njia isiyo ya adabu kwamba wewe si baba yao au si mama yao. Maneno hayo yanaumiza. Hata hivyo, “usifanye haraka kukasirika [“kuwa mwenye kuudhika,” NW] rohoni mwako.” (Mhubiri 7:9) Ufahamu na hisia-mwenzi zahitajiwa ili kushughulikia hisia-moyo za watoto.
23. Huenda nidhamu ikashughulikiwaje katika familia yenye watoto wa kambo?
23 Sifa hizo ni muhimu wakati mtu anapotia nidhamu. Nidhamu isiyo na ugeugeu ni muhimu. (Mithali 6:20; 13:1) Na kwa kuwa watoto wote si sawasawa, huenda nidhamu ikawa tofauti katika hali moja na nyingine. Wazazi fulani wa kambo huona kwamba, angalau mwanzoni, huenda ikafaa zaidi kwa aliye mzazi halisi kushughulikia sehemu hii ya kuwa mzazi. Lakini, ni muhimu kwamba wazazi wote wawili wakubaliane juu ya nidhamu na waiunge mkono, bila kupendelea mzao asili zaidi ya mtoto wa kambo. (Mithali 24:23) Utii ni wa maana, lakini hali ya kutokamilika yahitaji kufikiriwa. Usiitikie kupita kiasi. Tia nidhamu kwa upendo.—Wakolosai 3:21.
24. Ni nini kiwezacho kusaidia kuzuia matatizo ya kiadili kati ya washiriki wa jinsia tofauti katika familia ya kambo?
24 Mazungumzo ya familia yaweza kuchangia sana kuzuia taabu. Haya yaweza kusaidia familia iendelee kukazia fikira mambo yaliyo ya maana zaidi maishani. (Linganisha Wafilipi 1:9-11.) Yaweza pia kusaidia kila mmoja aone jinsi awezavyo kuchangia kufikia miradi ya familia. Kwa kuongezea, mazungumzo ya familia yaliyo wazi yaweza kuzuia matatizo ya kiadili. Wasichana wahitaji kuelewa jinsi ya kuvaa na kujiendesha kiadabu wakiwa karibu na baba yao wa kambo na ndugu wowote wa kambo, na wavulana wahitaji shauri juu ya mwenendo ufaao kuelekea mama yao wa kambo na dada wowote wa kambo.—1 Wathesalonike 4:3-8.
25. Ni sifa gani ziwezazo kusaidia kudumisha amani katika familia ya kambo?
25 Katika kukabiliana na ugumu wa pekee wa kuwa mzazi wa kambo, uwe mwenye subira. Inachukua wakati kusitawisha mahusiano mapya. Kujipatia upendo na staha ya watoto ambao si wako kihalisi ni kazi ngumu sana. Lakini inawezekana. Moyo wenye hekima na wenye ufahamu, pamoja na tamaa yenye nguvu ya kumpendeza Yehova, ndio ufunguo wa kupata amani katika familia ya kambo. (Mithali 16:20) Sifa hizo zaweza pia kukusaidia ukabiliane na hali nyinginezo.
JE, VIFUATIO VYA KIMWILI HUGAWANYA NYUMBA YAKO?
26. Matatizo na mitazamo kuhusiana na mambo ya kimwili yaweza kugawanya familia katika njia zipi?
26 Matatizo na mitazamo kuhusiana na vitu vya kimwili yaweza kuigawanya familia katika njia nyingi. Kwa huzuni, baadhi ya familia zinavurugwa na majibizano juu ya fedha na tamaa ya kuwa tajiri—au angalau kuwa tajiri zaidi kidogo. Migawanyiko huenda ikatokea wakati wenzi wote wawili hufanya kazi za kimwili na kusitawisha mtazamo wa “fedha zangu, fedha zako.” Hata ikiwa majibizano yanaepukwa, wenzi wote wawili wafanyapo kazi huenda wakajipata wenyewe wakiwa na ratiba inayoruhusu wakati mchache kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Mwelekeo unaozidi kukua ulimwenguni ni kwa akina baba kuishi mbali na familia zao kwa vipindi vilivyo virefu—miezi au hata miaka—ili kuchuma fedha zaidi kuliko vile wangeweza kuchuma wakati wowote nyumbani. Hili laweza kuongoza kwenye matatizo mazito sana.
27. Ni nini baadhi ya kanuni ziwezazo kusaidia familia iliyo chini ya msongo wa kifedha?
27 Hakuna sheria ziwezazo kuwekwa kwa kushughulikia hali hizi, kwa kuwa familia tofauti zalazimika kushughulikia misongo na mahitaji yaliyo tofauti. Hata hivyo, shauri la Biblia laweza kusaidia. Kwa kielelezo, Mithali 13:10 huonyesha kwamba kushindana bure kwaweza kuepukwa nyakati nyingi kwa ‘kushauriana.’ Hilo latia ndani si kule kusimulia tu kwa mtu maoni yake mwenyewe lakini kutafuta shauri na kupata kujua jinsi yule mtu mwingine huona jambo hilo. Isitoshe, kupanga bajeti ya kihalisi kwaweza kusaidia kuunganisha jitihada za familia. Nyakati nyingine kwahitajika—labda kwa muda—kwa wenzi wote wawili kufanya kazi nje ya nyumbani ili kulipia gharama zilizoongezeka, hasa kukiwa na watoto au wengine wenye kuwategemea. Hali inapokuwa hivyo, mume aweza kumhakikishia mke wake kwamba angali ana wakati kwa ajili yake. Yeye pamoja na watoto waweza kusaidia kwa upendo na baadhi ya kazi ambayo huenda akashughulikia peke yake kama kawaida.—Wafilipi 2:1-4.
28. Ni vikumbusha gani, vikifuatwa, vitakavyosaidia familia ijitahidi kuelekea muungano?
28 Hata hivyo, kumbuka kwamba ingawa fedha ni jambo la lazima katika mfumo huu wa mambo, hizo hazileti furaha. Kwa hakika hazitoi uhai. (Mhubiri 7:12) Kwa kweli, kukazia kupita kiasi mambo ya kimwili kwaweza kusababisha uharibifu wa kiroho na wa kiadili. (1 Timotheo 6:9-12) Ni bora zaidi kama nini kutafuta Ufalme wa Mungu kwanza na uadilifu wake, kukiwa na uhakikishio wa kuwa na baraka zake juu ya jitihada zetu za kupata mahitaji ya lazima ya maisha! (Mathayo 6:25-33; Waebrania 13:5) Kwa kuweka masilahi ya kiroho kwanza na kwa kufuatia amani na Mungu kwanza, huenda ukapata kwamba nyumba yako, ingawa imegawanywa na hali fulani, itakuwa moja iliyounganika kikweli katika njia za maana zaidi.