Somo la 8
Maisha ya Familia Yanayompendeza Mungu
Mume ana cheo gani katika familia? (1)
Mume apaswa amtendeeje mke wake? (2)
Baba ana madaraka gani? (3)
Mke ana fungu gani katika familia? (4)
Mungu hutaka wazazi na watoto wafanye nini? (5)
Maoni ya Biblia ni nini kuhusu kutengana na talaka? (6, 7)
1. Biblia husema kwamba mume ndiye kichwa cha familia yake. (1 Wakorintho 11:3) Ni lazima mume awe na mke mmoja tu. Wao wapaswa kuwa wameoana ifaavyo kisheria.—1 Timotheo 3:2; Tito 3:1.
2. Mume apaswa ampende mke wake kama vile ajipendavyo mwenyewe. Apaswa amtendee kwa njia ambayo Yesu huwatendea wafuasi wake. (Waefeso 5:25, 28, 29) Hapaswi kamwe kumpiga mke wake wala kumtenda vibaya kwa njia yoyote ile. Badala ya hivyo, apaswa amwonyeshe heshima na staha.—Wakolosai 3:19; 1 Petro 3:7.
3. Baba apaswa afanye kazi kwa bidii ili kutunza familia yake. Ni lazima baba awaandalie mke na watoto wake chakula, mavazi, na nyumba. Ni lazima baba aandalie pia mahitaji ya kiroho ya familia yake. (1 Timotheo 5:8) Yeye huongoza katika kusaidia familia yake ijifunze kumhusu Mungu na makusudi Yake.—Kumbukumbu la Torati 6:4-9; Waefeso 6:4.
4. Mke apaswa awe msaidizi mwema kwa mume wake. (Mwanzo 2:18) Yeye apaswa kumsaidia mume wake katika kufundisha na kuzoeza watoto wao. (Mithali 1:8) Yehova humtaka mke ashughulikie familia yake kwa upendo. (Mithali 31:10, 15, 26, 27; Tito 2:4, 5) Yeye apaswa awe na staha yenye kina kwa mume wake.—Waefeso 5:22, 23, 33.
5. Mungu hutaka watoto wawatii wazazi wao. (Waefeso 6:1-3) Yeye huwatazamia wazazi wawafundishe na kuwasahihisha watoto wao. Wazazi huhitaji kutumia wakati pamoja na watoto wao na kujifunza Biblia pamoja nao, wakishughulikia mahitaji yao ya kiroho na ya kihisia-moyo. (Kumbukumbu la Torati 11:18, 19; Mithali 22:6, 15) Wazazi hawapaswi kamwe kuwatia nidhamu watoto wao kwa njia yenye ukali bila huruma au iliyo katili.—Wakolosai 3:21.
6. Wenzi wa ndoa wanapokuwa na matatizo ya kupatana, wanapaswa kujaribu kutumia shauri la Biblia. Biblia hutuhimiza tuonyeshe upendo na kuwa wenye kusamehe. (Wakolosai 3:12-14) Neno la Mungu halipendekezi kutengana kuwa njia ya kusuluhisha matatizo madogo. Lakini huenda mke akachagua kumwacha mume wake ikiwa (1) mume akataa kishupavu kutegemeza familia yake, (2) yeye ni mjeuri sana hivi kwamba afya na uhai wa mke umo hatarini, au (3) upinzani wake wa kupita kiasi hufanya isiwezekane kwa mke kumwabudu Yehova.—1 Wakorintho 7:12, 13.
7. Ni lazima wenzi wa ndoa wawe waaminifu kwa mmoja na mwenzake. Uzinzi ni dhambi dhidi ya Mungu na dhidi ya mwenzi wa mtu. (Waebrania 13:4) Mahusiano ya kingono nje ya ndoa ndio msingi pekee wa Kimaandiko kwa talaka inayoruhusu mtu aoe au aolewe tena. (Mathayo 19:6-9; Warumi 7:2, 3) Yehova huchukizwa wakati watu wanapotalikana bila misingi ya Kimaandiko na kuoa au kuolewa na mtu mwingine.—Malaki 2:14-16.
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Mungu huwatazamia wazazi wawafundishe watoto wao na kuwasahihisha
[Picha katika ukurasa wa 17]
Baba mwenye upendo huiandalia familia yake kimwili na kiroho