Yesu Kristo—Yeye Ni Nani?
“HATA watu wengi wasio Wakristo huamini kwamba Yeye alikuwa mwalimu mkuu na mwenye hekima. Hakika yeye alikuwa mmojawapo wa watu wenye uvutano zaidi aliyepata kuishi.” (The World Book Encyclopedia) “Yeye” ni nani? Yesu Kristo, mwanzilishi wa Ukristo. Je, wajua yeye ni nani? Je, anaathiri maisha yako kwa njia yoyote?
Matukio ya huduma ya Yesu yamerekodiwa ndani ya Biblia katika vitabu vinne vya kihistoria viitwavyo Gospeli. Masimulizi hayo ni ya kweli kadiri gani? Baada ya kuyachunguza, mwanahistoria mwenye kujulikana sana Will Durant aliandika hivi: “Kwamba wanaume wachache wa kikawaida wangeweza katika kizazi kimoja kubuni mtu mwenye nguvu na mwenye uvutano mwingi kadiri hiyo, elimu ya maadili ya hali ya juu kadiri hiyo na njozi yenye kuchochea kadiri hiyo ya udugu wa kibinadamu, ungekuwa muujiza wenye kustaajabisha mno zaidi ya wowote ulioandikwa katika Gospeli.”
Ingawa hivyo, kwa mamilioni ya watu katika Mashariki na kwingineko, Yesu Kristo ni mtu asiyejulikana. Huenda wakaamini kwamba alikuwepo, lakini hawafikiri kwamba ana uvutano wowote katika maisha yao. Wengine humwona Yesu kuwa asiyestahili uangalifu wao kwa sababu ya mambo ambayo yamefanywa na wale wanaodai kuwa wafuasi wake. ‘Waliangusha bomu la atomu Nagasaki,’ watu fulani huko Japani wangesema hivyo, ‘jiji lililo na Wakristo wengi zaidi kuliko majiji mengi huko Japani.’
Lakini, je, ungemlaumu daktari kama mgonjwa angeshindwa kutii maagizo ya daktari? Bila shaka la. Watu wa Jumuiya ya Wakristo wamepuuza maagizo ya Yesu ya kutatua matatizo yao ya kila siku kwa muda mrefu sana. Kwa hiyo, badala ya kumkataa Yesu kwa sababu wale waitwao eti Wakristo hawafuati maagizo yake, kwa nini wewe mwenyewe usijifunze jambo fulani kumhusu? Ichunguze Biblia, uone Yesu kwa kweli ni nani na jinsi anavyoweza hata kubadilisha maisha yako.
Upendo—Ndio Agizo Lake
Yesu Kristo alikuwa mwalimu mkuu aliyeishi Palestina karibu miaka 2,000 iliyopita. Si mengi yanayojulikana kuhusu utoto wake. (Mathayo, sura ya 1 na ya 2; Luka, sura ya 1 na ya 2) Alipokuwa na umri wa miaka 30, Yesu alianza huduma yake ya ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ (Yohana 18:37; Luka 3:21-23) Watu wanne walioripoti mambo ya kihistoria ya maisha ya Yesu walikazia huduma yake ya hadharani, miaka mitatu na nusu ya mwisho ya maisha yake ya muda mfupi duniani.
Wakati wa huduma yake, Yesu aliwapa wanafunzi wake ufunguo wa kushughulika na matatizo tofauti-tofauti katika maisha yao. Ufunguo huo ulikuwa nini? Ulikuwa upendo. Katika mojawapo ya mahubiri yenye kujulikana zaidi katika historia, yaitwayo Mahubiri ya Mlimani, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kuonyesha wanadamu wenzao upendo. Yeye alisema hivi: “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Kanuni hii yaitwa Kanuni Bora. Wale “watu” ambao Yesu aliwarejezea hapa hutia ndani hata maadui wa mtu. Katika mahubiri hayohayo, yeye alisema hivi: “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi.” (Mathayo 5:44) Je, upendo kama huo haungetatua matatizo mengi tunayokabili leo? Kiongozi Mhindi Mohandas Gandhi alifikiri hivyo. Ananukuliwa akisema hivi: “Wakati [tutakapoungana] juu ya mafundisho aliyofundisha Kristo katika haya Mahubiri ya Mlimani, sisi tutakuwa tumetatua matatizo . . . ya ulimwengu mzima.” Mafundisho ya Yesu juu ya upendo, yakitumiwa, yanaweza kutatua matatizo ya wanadamu.
Adhihirisha Upendo Wake
Yesu alitenda kupatana na yale aliyofundisha. Alitanguliza mapendezi ya wengine kuliko yake naye akaonyesha upendo kwa kutenda. Siku moja, Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakiwatumikia watu wengi, bila kuwa na wakati wa kula mlo. Yesu aliona uhitaji wa wanafunzi wake ‘kupumzika kidogo,’ kwa hiyo wakaenda mahali palipojitenga. Lakini umati uliwatangulia na ulikuwa ukiwangojea wafike. Je, wewe ungeitikiaje ikiwa ungekuwa katika hali kama ya Yesu? Yesu “akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao” naye “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:30-34) Sikitiko hilohilo kubwa lilimsukuma awasaidie wengine.
Yale ambayo Yesu alifanya kwa faida ya wengine hayakuwa mafundisho ya kiroho tu. Pia alitoa msaada wenye kutumika. Kwa kielelezo, alilisha wanaume 5,000 (kwa kuongezea wanawake na watoto) ambao walikuwa wakimsikiliza hadi jioni siku moja. Katika kisa kingine, alilisha wengine 4,000. Katika kisa cha kwanza, alitumia mikate mitano na samaki wawili, na kile cha baadaye, mikate saba na samaki wachache. (Mathayo 14:14-21; 15:32-38; Marko 6:35-44; 8:1-9) Miujiza, siyo? Ndiyo, alikuwa mfanya-miujiza.
Pia Yesu aliponya watu wengi waliokuwa wagonjwa. Aliponya vipofu, viwete, wenye ukoma, na viziwi. Kwani, hata alifufua wafu! (Luka 7:22; Yohana 11:30-45) Wakati mmoja, mwenye ukoma alimsihi hivi: “Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.” Yesu aliitikiaje? “[Alinyoosha] mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’” (Marko 1:40, 41) Yesu alichochewa na tamaa yenye nguvu ya kuwasaidia. Kupitia miujiza hiyo, alionyesha upendo wake kwa waliotaabika.
Je, ni vigumu kuamini? Yesu alifanya miujiza yake mingi hadharani. Hata wapinzani, waliojaribu kutafuta kasoro kwake kila pindi, hawangeweza kukana uhakika wa kwamba alifanya miujiza. (Yohana 9:1-34) Mbali na hilo, miujiza yake ilikuwa na kusudi. Ilisaidia watu kumtambulisha Yesu kuwa yule aliyetumwa na Mungu.—Yohana 6:14.
Kuchunguza kifupi tu mafundisho ya Yesu na maisha yake hutuvuta kwake na hutuchochea kutaka kuuiga upendo wake. Hata hivyo, hiyo si njia pekee ambayo Yesu aweza kuathiri maisha yako. Yeye hakuwa tu mwalimu mkuu aliyefunza juu ya upendo. Alionyesha kwamba alikuwapo kabla hajawa binadamu akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. (Yohana 1:14; 3:16; 8:58; 17:5; 1 Yohana 4:9) Pia anaishi baada ya kuwa binadamu, hiyo ikimfanya awe mtu wa maana hata zaidi kwako. Biblia huonyesha kwamba Yesu alifufuliwa na sasa yeye ni Mfalme aliyetawazwa wa Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 11:15) Yesu alisema: “Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3; 20:31) Kwa kweli, kutwaa ujuzi juu ya Yesu Kristo kwaweza kumaanisha uhai usio na mwisho katika Paradiso! Hilo lawezekanaje? Kwa nini usijifunze mengi juu ya Yesu na kuona jinsi ambavyo “upendo alio nao Kristo hutushurutisha” tumwige yeye? (2 Wakorintho 5:14) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.—Yohana 13:34, 35.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kiebrania ni kutoka katika Union Version ya Kiswahili chapa ya 1994, na manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ni kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mahali ambapo herufi NW zinafuata nukuu, zaonyesha kwamba tafsiri inatoka katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References ya Kiingereza.