Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 7/1 kur. 4-7
  • Yesu Anaweza Kubadilishaje Maisha Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu Anaweza Kubadilishaje Maisha Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mafundisho Yake
  • Vitendo Vyake
  • Dhabihu Yake
  • Yesu Kristo—Yeye Ni Nani?
    Yesu Kristo—Yeye Ni Nani?
  • Yesu Kristo—Alitumwa na Mungu?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Yesu Kristo, Yeye Ambaye Kupitia Kwake Mungu Hubariki Wanadamu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mungu Anataka Tufanye Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 7/1 kur. 4-7

Yesu Anaweza Kubadilishaje Maisha Yako?

YESU KRISTO alikuwa Mwalimu Mkuu aliyeishi Palestina karibu miaka 2,000 iliyopita. Ni mambo machache sana yanayojulikana kuhusu maisha yake ya utotoni. Hata hivyo, imethibitishwa vema kwamba alipokuwa na umri upatao miaka 30, alianza huduma yake ya “[kutoa] ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37; Luka 3:21-23) Wanafunzi wanne walioandika masimulizi ya maisha yake hukazia ile miaka mitatu na nusu iliyofuata.

Wakati wa huduma yake, Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake amri inayoweza kutatua matatizo mengi ya ulimwengu. Hiyo ilikuwa amri gani? Yesu alisema hivi: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane.” (Yohana 13:34) Naam, utatuzi wa matatizo mengi ya wanadamu ni upendo. Pindi nyingine, Yesu alipoulizwa ni amri ipi iliyo kubwa zaidi, alijibu hivi: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri kubwa zaidi sana na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—Mathayo 22:37-40.

Yesu alituonyesha kwa maneno na kwa vitendo jinsi ya kumpenda Mungu na wanadamu wenzetu. Acheni tuchunguze vielelezo vichache na tuone tunachoweza kujifunza kutoka kwake.

Mafundisho Yake

Katika moja ya mahubiri yanayojulikana sana katika historia, Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Hakuna awezaye kutumikia kama mtumwa mabwana-wakubwa wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia kama watumwa Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Je, fundisho la Yesu juu ya kuweka Mungu kwanza maishani mwetu lingali latumika leo, wakati watu wengi sana huamini kwamba pesa hutatua matatizo yote? Ni kweli, twahitaji pesa ili kujiruzuku. (Mhubiri 7:12) Ingawa hivyo, tukiruhusu “Utajiri” uwe bwana-mkubwa wetu, hali ya “kupenda fedha” itatudhibiti, ikitawala maisha yetu yote. (1 Timotheo 6:9, 10) Wengi ambao wamenaswa katika mtego huo hatimaye wamepoteza familia yao, afya yao, na hata uhai wao.

Kwa upande mwingine, kumtegemea Mungu akiwa Bwana-Mkubwa wetu huyapa maisha yetu maana. Akiwa Muumba, yeye ndiye Chanzo cha uhai, na hivyo ni yeye pekee anayestahili ibada yetu. (Zaburi 36:9; Ufunuo 4:11) Wale wanaojifunza kuhusu sifa zake na kuanza kumpenda wanachochewa kushika amri zake. (Mhubiri 12:13; 1 Yohana 5:3) Twajinufaisha wenyewe tukifanya hivyo.—Isaya 48:17.

Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu pia aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kuwaonyesha wanadamu wenzao upendo. Alisema hivi: “Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Neno “watu” ambalo Yesu alitumia hapa hutia ndani hata maadui wa mtu. Katika mahubiri hayohayo, alisema hivi: “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi.” (Mathayo 5:43, 44) Je, upendo kama huo si ungetatua matatizo mengi tunayokabili leo? Kiongozi Mhindu Mohandas Gandhi aliona hivyo. Yeye anukuliwa akisema hivi: “Wakati [tutakapokubaliana] juu ya mafundisho yaliyotolewa na Kristo katika haya Mahubiri ya Mlimani, tutakuwa tumeyatatua matatizo . . . ya ulimwengu mzima.” Mafundisho ya Yesu juu ya upendo, yakitumiwa, yaweza kutatua matatizo mengi ya wanadamu.

Vitendo Vyake

Yesu alifundisha kweli zenye kina kuhusu jinsi ya kuonyesha upendo, na zaidi ya hayo, yeye alifanya yale aliyofundisha. Kwa mfano, alitanguliza masilahi ya wengine kuliko yake mwenyewe. Siku moja, Yesu na wanafunzi wake walikuwa na shughuli nyingi sana za kuwasaidia watu hivi kwamba hata hawakuwa na wakati wa kula mlo. Yesu alitambua kuwa wanafunzi wake wanahitaji kupumzika kidogo, naye akawapeleka mahali pa upweke. Lakini walipofika hapo, walikuta umati ukiwasubiri. Wewe ungeitikiaje uonapo umati ukikutazamia ufanye kazi ilhali unahisi kwamba wahitaji kupumzika kidogo? Yesu “a[li]sukumwa na sikitiko kwa ajili yao” naye “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Sikuzote hangaiko hilo kwa ajili ya wengine lilimfanya Yesu awasaidie.

Yesu aliwafanyia watu mambo mengi zaidi ya kuwafundisha tu. Yeye alitoa pia msaada wenye kutumika. Kwa mfano, pindi moja aliwalisha watu wanaozidi 5,000 waliokuwa wamemsikiliza hadi jioni. Mara baada ya hapo, aliwalisha watu wengine wengi—pindi hii wakiwa zaidi ya 4,000—ambao walikuwa wamemsikiliza kwa siku tatu na hawakuwa na chakula chochote kilichobaki. Katika pindi ya kwanza, alitumia mikate mitano na samaki wawili, na pindi iliyofuata, akatumia mikate saba na samaki wadogo wachache. (Mathayo 14:14-22; 15:32-38) Miujiza? Ndiyo, yeye alikuwa mfanya-miujiza.

Yesu pia aliwaponya watu wengi waliokuwa wakiugua. Aliponya vipofu, vilema, wakoma, na viziwi. Hata alifufua wafu! (Luka 7:22; Yohana 11:30-45) Siku moja, mkoma fulani alimsihi hivi: “Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.” Yesu aliitikiaje? “Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’” (Marko 1:40, 41) Kupitia miujiza kama hiyo, Yesu alionyesha upendo wake kwa wanaotaabika.

Je, wewe huona ni vigumu kuamini miujiza ya Yesu? Wengine huona hivyo. Hata hivyo, kukumbuka kwamba Yesu alifanya miujiza yake hadharani. Hata wapinzani wake, waliojaribu kumkosoa-kosoa kila wakati, hawangeweza kukana kwamba yeye alikuwa mfanya-miujiza. (Yohana 9:1-34) Mbali na hayo, miujiza yake ilikuwa na kusudi. Iliwasaidia watu watambue kuwa yeye ndiye Yule aliyetumwa na Mungu.—Yohana 6:14.

Yesu hakuwa akitafuta kujionyesha alipofanya miujiza. Badala yake, alimtukuza Mungu, aliye Chanzo cha nguvu zake. Siku moja alikuwa katika nyumba iliyojaa watu huko Kapernaumu. Mtu aliyepooza alitaka kuponywa lakini hakuweza kuingia ndani. Kwa hiyo rafiki zake wakamteremsha kupitia paa, akiwa kitandani. Yesu alipoona imani yao, akamponya huyo mwenye kupooza. Tokeo ni kwamba watu “wa[li]mtukuza Mungu” na kusema: “Hatujaona kamwe lenye kufanana na hilo.” (Marko 2:1-4, 11, 12) Miujiza ya Yesu ilimletea sifa Yehova, Mungu wake, na kuwasaidia wale waliokuwa na uhitaji.

Hata hivyo, kuponya wagonjwa kimwujiza halikuwa ndilo jambo kuu la huduma ya Yesu. Mmoja aliyeandika simulizi la maisha ya Yesu alieleza hivi: “Haya yameandikwa ili mpate kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu, na kwamba, kwa sababu ya kuamini, nyinyi mpate kuwa na uhai kwa njia ya jina lake.” (Yohana 20:31) Naam, Yesu alikuja duniani ili wanadamu wanaoamini wapate uhai.

Dhabihu Yake

‘Yesu alikuja duniani?’ huenda ukauliza. ‘Yeye alitoka wapi?’ Yesu mwenyewe alisema hivi: “Nimeteremka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” (Yohana 6:38) Yeye alikuwako akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu kabla ya kuwa mwanadamu. Basi, mapenzi ya Yule aliyemtuma duniani yalikuwa nini? “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake,” asema Yohana, mmoja wa waandikaji wa Gospeli, “ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Hilo liliwezekanaje?

Biblia hufunua jinsi kifo kilivyokuja kuwa jambo ambalo wanadamu hawawezi kuepuka. Wenzi wa kwanza wa kibinadamu walipokea kutoka kwa Mungu uhai na tazamio la kuishi milele. Ingawa hivyo, waliamua kuasi dhidi ya Mfanyi wao. (Mwanzo 3:1-19) Likiwa tokeo la tendo hilo, dhambi ya kwanza ya mwanadamu, uzao wa Adamu na Hawa ukapata urithi usiofaa, kifo. (Waroma 5:12) Ili wanadamu wapewe uhai ulio halisi, ni lazima dhambi na kifo viondolewe mbali.

Hakuna mwanasayansi yeyote awezaye kuondolea mbali kifo kupitia mbinu fulani ya kubadili jeni. Ingawa hivyo, Muumba wa wanadamu ana uwezo wa kuwaleta wanadamu watiifu kwenye ukamilifu ili waweze kuishi milele. Katika Biblia, uandalizi huu huitwa fidia. Wenzi wa kwanza wa kibinadamu walijiuza wenyewe na pia uzao wao katika dhambi na kifo. Waliubadili uhai mkamilifu wa kibinadamu kwa uhai wa kujitegemea wenyewe bila Mungu, wakifanya maamuzi yao wenyewe kuhusiana na lililo sawa na lililo baya. Ili kununua tena uhai mkamilifu wa kibinadamu, ilibidi bei inayolingana na uhai mkamilifu ambao wazazi wetu wa kwanza walipoteza ilipwe. Kwa kuwa wanadamu walikuwa wamerithi kutokamilika, hawakustahili kuandaa bei hiyo.—Zaburi 49:7.

Kwa hiyo, Yehova Mungu akaingilia kati ili kusaidia. Aliuhamishia uhai mkamilifu wa Mwana mzaliwa-pekee wake kwa tumbo la uzazi la bikira, aliyemzaa Yesu. Miaka kadhaa iliyopita, huenda ungekataa wazo la bikira kuzaa. Hata hivyo, leo wanasayansi wamezalisha wanyama bila kuunganisha mbegu ya kike na ya kiume na pia wakahamisha jeni kutoka kwa mnyama mmoja hadi mnyama mwingine. Basi, ni nani awezaye kwa kufaa kutilia shaka uwezo wa Muumba wa kutokeza uzao pasipo kutumia njia ya kawaida ya uzazi?

Kwa kuwa uhai mkamilifu wa kibinadamu ulikuwepo, bei ya kukomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo ikapatikana. Ingawa hivyo, ilimbidi Yesu, aliyezaliwa duniani akiwa mtoto mchanga, akue ili awe “tabibu” awezaye kuandaa “dawa” ya kuponya matatizo ya wanadamu. Alifanya hivyo kwa kuishi maisha makamilifu, yasiyo na dhambi. Yesu aliona maumivu makali ya wanadamu walio chini ya dhambi na pia akapatwa na upungufu wa kimwili unaowapata wanadamu. Hilo lilimfanya kuwa tabibu mwenye huruma hata zaidi. (Waebrania 4:15) Maponyo ya kimwujiza aliyofanya wakati wa maisha yake duniani yalithibitisha kuwa ana nia na uwezo wa kuponya wagonjwa.—Mathayo 4:23.

Baada ya huduma ya miaka mitatu na nusu hapa duniani, Yesu aliuawa na wapinzani wake. Alionyesha kwamba mwanadamu mkamilifu aweza kuwa mtiifu kwa Muumba hata kukiwa na majaribu makubwa zaidi. (1 Petro 2:22) Uhai wake wa kibinadamu mkamilifu aliotoa ukiwa dhabihu ukawa bei ya fidia, inayoweza kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Yesu Kristo alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:13) Yesu alifufuliwa kwenye uhai wa kiroho siku ya tatu baada ya kifo chake, na majuma kadhaa baadaye, akapaa mbinguni ili kumkabidhi Yehova Mungu bei ya fidia. (1 Wakorintho 15:3, 4; Waebrania 9:11-14) Kwa kufanya hivyo, Yesu angeweza kutumia ustahili wa dhabihu ya fidia yake kwa wale wanaomfuata.

Je, ungependa kunufaika na njia hii ya kuponya magonjwa ya kiroho, ya kihisia-moyo, na ya kimwili? Kufanya hivyo kwahitaji imani katika Yesu Kristo. Kwa nini wewe mwenyewe usije kwa Tabibu huyo? Waweza kufanya hivyo kwa kujifunza juu ya Yesu Kristo na fungu lake katika kuokoa wanadamu waaminifu. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yesu ana nia na pia uwezo wa kuponya wagonjwa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kifo cha Yesu hukuathirije?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki