Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ip-1 sura 6 kur. 61-72
  • Yehova Mungu Awarehemu Mabaki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Mungu Awarehemu Mabaki
  • Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Chipukizi la Yehova’
  • Mabaki Wawa Watakatifu kwa Yehova
  • Ahadi ya Utunzaji Wenye Upendo
  • Endelea Kumngojea Yehova
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Wokovu na Kushangilia Chini ya Utawala wa Mesiya
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—I
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • ‘Mkashangilie Daima kwa Ajili ya Hivi Niviumbavyo’
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
Pata Habari Zaidi
Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
ip-1 sura 6 kur. 61-72

Sura ya 6

Yehova Mungu Awarehemu Mabaki

Isaya 4:2-6

1, 2. Nabii Isaya atabiri nini juu ya Yuda na Yerusalemu?

DHORUBA kali yapiga eneo lenye wakazi wengi. Pepo kali, mvua kubwa, na mafuriko makubwa zafagilia mbali sehemu ya nchi, zikiharibu makao, mimea, na kuua watu. Lakini dhoruba hiyo yapita mara, na kipindi chenye utulivu chafuatia. Kwa wale waliookoka, sasa ni wakati wa kurudisha hali ya awali na kujenga upya.

2 Nabii Isaya atabiri jambo kama hilo juu ya Yuda na Yerusalemu. Mawingu ya dhoruba ya hukumu ya Mungu yanakaribia sana kwa kitisho—kukiwa na sababu nzuri! Hatia ya taifa hilo ni kubwa. Watawala pamoja na watu wamejaza ukosefu wa haki na umwagaji wa damu katika nchi. Kupitia Isaya, Yehova afunua hatia ya Yuda na kuonya kwamba Yeye atatekeleza hukumu juu ya taifa hilo halifu. (Isaya 3:25) Nchi ya Yuda itabaki ukiwa kabisa baada ya dhoruba hiyo. Hapana shaka tazamio hilo lamhuzunisha Isaya.

3. Ujumbe uliopuliziwa katika Isaya 4:2-6 una habari gani njema?

3 Ijapokuwa hivyo, kuna habari njema! Dhoruba ya hukumu ya Yehova yenye uadilifu itakwisha, na mabaki wataokoka. Naam, hukumu ya Yehova juu ya Yuda itakuwa yenye rehema! Ujumbe wa Isaya uliopuliziwa ambao umerekodiwa katika Isaya 4:2-6 waelekeza kwenye wakati huo wenye baraka. Ni kana kwamba jua lachomoza mawinguni; maonyesho na sauti za hukumu—zinazotajwa katika Isaya 2:6–4:1—zageuka kuwa nchi nzuri na watu waliotiwa nguvu.

4. Kwa nini twapaswa kuuchunguza unabii wa Isaya unaohusu kurudishwa kwa mabaki?

4 Unabii wa Isaya unaohusu kurudishwa kwa mabaki na usalama wanaopata unatimizwa wakati wetu pia—“siku za mwisho.” (Isaya 2:2-4) Hebu tuuchunguze ujumbe huo wa wakati unaofaa, kwa sababu licha ya kuwa na umuhimu wa unabii, huo pia hutufundisha juu ya rehema ya Yehova na jinsi sisi binafsi tuwezavyo kuipata.

‘Chipukizi la Yehova’

5, 6. (a) Isaya aufafanuaje wakati wenye amani baada ya tufani inayokuja? (b) Ni nini maana ya neno “chipukizi,” nalo laonyesha nini juu ya nchi ya Yuda?

5 Sauti ya Isaya yachangamka atazamapo mbele kwenye kipindi cha amani baada ya tufani inayokuja. Aandika: “Siku hiyo chipukizi la BWANA [“Yehova,” “NW”] litakuwa zuri, lenye utukufu, na matunda ya nchi yatakuwa mema sana, na kupendeza, kwa ajili ya Waisraeli wale waliookoka.”—Isaya 4:2.

6 Hapo Isaya azungumza juu ya urudisho. Neno la Kiebrania linalofasiriwa “chipukizi” larejezea ‘kile kinachoanza kuchipuka, mche, tawi.’ Hilo huhusianishwa na ufanisi, ongezeko, na baraka kutoka kwa Yehova. Kwa hiyo Isaya atoa wazo la tumaini—ukiwa unaokuja hautadumu milele. Kwa baraka ya Yehova, nchi ya Yuda iliyokuwa imesitawi hapo awali itazaa tena matunda mengi.a—Mambo ya Walawi 26:3-5.

7. Chipukizi la Yehova litakuwaje “zuri, lenye utukufu”?

7 Isaya atumia maneno dhahiri kufafanua utukufu wa mabadiliko yaliyo mbele. Chipukizi la Yehova “litakuwa zuri, lenye utukufu.” Neno “zuri” latukumbusha juu ya uzuri wa Bara Lililoahidiwa wakati ambapo Yehova aliwapa Israeli bara hilo karne kadhaa mapema. Lilikuwa zuri sana hivi kwamba lilionwa kuwa “utukufu [“kito,” New American Bible] wa nchi zote.” (Ezekieli 20:6) Hivyo, maneno ya Isaya yawahakikishia watu hao kuwa nchi ya Yuda itarudishwa kwenye utukufu na uzuri wake wa hapo awali. Kwa kweli, itakuwa kama kito kitukufu duniani.

8. Ni nani watakaokuwapo ili kufurahia uzuri uliorudishwa wa nchi, na Isaya aelezaje hisia zao?

8 Japo hivyo, ni nani watakaokuwapo ili kufurahia uzuri uliorudishwa wa nchi hiyo? “Waisraeli wale waliookoka,” aandika Isaya. Naam, baadhi ya watu wataokoka uharibifu wenye kufedhehesha uliotabiriwa hapo awali. (Isaya 3:25, 26) Mabaki ya wenye kuokoka watarudi Yuda nao watashiriki kuirudisha. Kwa hao waliorudishwa—“walioponyoka”—mazao mengi ya nchi yao iliyorudishwa “yatakuwa mema sana, na kupendeza.” (Isaya 4:2; NW, kielezi-chini) Fedheha iliyoletwa na ukiwa itabadilika na kuwa hali mpya ya kujionea fahari.

9. (a) Maneno ya Isaya yalitimizwaje mwaka wa 537 K.W.K.? (b) Kwa nini yaweza kusemwa kuwa “walioponyoka” hutia ndani baadhi ya wale waliozaliwa uhamishoni? (Ona kielezi-chini.)

9 Kupatana na maneno ya Isaya, dhoruba ya hukumu ilifika mwaka wa 607 K.W.K. Wababiloni walipoharibu Yerusalemu na Waisraeli wengi wakaangamia. Baadhi yao waliokoka na kupelekwa uhamishoni huko Babiloni, lakini isingekuwa kwa sababu ya rehema ya Mungu, hakuna yeyote ambaye angeokoka. (Nehemia 9:31) Hatimaye, Yuda iliachwa ukiwa kabisa. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21) Ndipo, mwaka wa 537 K.W.K., Mungu wa rehema akawaruhusu “walioponyoka” warejee Yuda ili kuirudisha ibada ya kweli.b (Ezra 1:1-4; 2:1) Toba ya dhati ya wahamishwa hao waliokuwa wakirudi yasimuliwa vema katika Zaburi 137, ambayo labda iliandikiwa utekwani au muda mfupi baadaye. Waliporudi Yuda, walilima na kupanda mbegu nchini humo. Hebu wazia jinsi ambavyo hapana budi walihisi walipoona kwamba Mungu anabariki juhudi zao, akiifanya nchi kuchipuka kama “bustani ya Edeni” yenye kuzaa sana!— Ezekieli 36:34-36, BHN.

10, 11. (a) Wanafunzi wa Biblia walikuwaje katika utekwa kwa “Babiloni Mkubwa” mapema katika karne ya 20? (b) Yehova alibarikije mabaki ya Waisraeli wa kiroho?

10 Kurudishwa kama huko kumetukia katika siku yetu. Mapema katika karne ya 20, Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo, waliingia katika utekwa wa kiroho kwa “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 17:5) Ingawa walikuwa wameyakataa mafundisho mengi ya kidini yasiyo ya kweli, Wanafunzi wa Biblia walikuwa bado wana doa la mawazo na mazoea fulani ya Kibabiloni. Upinzani uliochochewa na makasisi ulifanya baadhi yao watiwe gerezani kihalisi. Nchi yao ya kiroho—eneo lao la kidini, au la kiroho—iliachwa ukiwa.

11 Lakini katika masika ya mwaka wa 1919, Yehova aliwarehemu mabaki hao wa Waisraeli wa kiroho. (Wagalatia 6:16) Aliona toba yao na tamaa yao ya kumwabudu katika roho na kweli, kwa hiyo akaelekeza kuachiliwa kwao kutoka katika kifungo halisi gerezani na, la muhimu zaidi, kutoka katika utekwa wa kiroho. “Walioponyoka” hao walirudishwa kwenye eneo lao la kiroho, alilowapa Mungu na kulifanya lichipuke kwa wingi. Eneo hilo la kiroho limedhihirisha sura nzuri na yenye kuvutia ambayo imewachochea mamilioni ya watu wengine wenye kumhofu Mungu wajiunge na mabaki katika ibada ya kweli.

12. Maneno ya Isaya yatukuzaje rehema ya Yehova kwa watu wake?

12 Hapo maneno ya Isaya yatukuza rehema ya Mungu juu ya watu wake. Ingawa Waisraeli wakiwa taifa walimwasi Yehova, yeye aliwarehemu mabaki wenye toba. Twaweza kufarijika kwa kufahamu kuwa hata wale wanaotenda makosa mazito wanaweza kumrudia Yehova wakiwa na tumaini. Wenye kutubu hawapaswi kuhisi kuwa hawawezi kupata rehema ya Yehova, kwa sababu yeye haukatai moyo wenye huzuni. (Zaburi 51:17) Biblia yatuhakikishia: “BWANA amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA [“Yehova,” NW] anavyowahurumia wamchao.” (Zaburi 103:8, 13) Kwa hakika, Mungu huyo mwenye rehema astahili sifa zetu zote!

Mabaki Wawa Watakatifu kwa Yehova

13. Isaya afafanuaje mabaki ambao Yehova angewarehemu, kama ilivyorekodiwa katika Isaya 4:3?

13 Tayari tumefahamishwa juu ya mabaki ambao Yehova angerehemu, lakini sasa Isaya awafafanua kinaganaga. Aandika: “Itakuwa ya kwamba yeye aliyebaki katika Sayuni, na yeye aliyeachwa ndani ya Yerusalemu, ataitwa mtakatifu; yaani, kila mmoja aliyeandikwa miongoni mwa hao walio hai ndani ya Yerusalemu.”—Isaya 4:3.

14. “Aliyebaki” na “aliyeachwa” ni nani, na kwa nini Yehova atawarehemu?

14 “Aliyebaki” na “aliyeachwa” ni nani? Hao ndio wale walioponyoka watajwao katika mstari unaotangulia—wahamishwa Wayahudi watakaoruhusiwa kurejea Yuda. Sasa Isaya aonyesha ni kwa nini Yehova atawarehemu—watakuwa ‘watakatifu’ kwake. Utakatifu wamaanisha “usafi au utakato wa kidini; utakatifu.” Kuwa mtakatifu kwahusisha kuwa safi, kutakata, katika neno na tendo, kushikamana na kiwango cha Yehova juu ya lililo sawa na lenye kustahili. Naam, Yehova atawarehemu walio ‘watakatifu’ kwake, naye atawaruhusu warudi katika “mji mtakatifu,” Yerusalemu.—Nehemia 11:1.

15. (a) Usemi ‘walioandikwa kwa ajili ya uhai ndani ya Yerusalemu’ watukumbusha desturi gani ya Wayahudi? (b) Maneno ya Isaya yadokeza onyo gani linalofaa kuzingatiwa?

15 Je, mabaki waaminifu hao watadumu humo? “[Wata]andikwa miongoni mwa hao walio hai [“wataandikwa kwa ajili ya uhai,” NW] ndani ya Yerusalemu,” Isaya aahidi. Hilo latukumbusha desturi ya Wayahudi ya kuweka rejesta za familia na makabila ya Israeli kwa makini. (Nehemia 7:5) Kuandikwa katika rejesta kulimaanisha kwamba mtu yu hai, kwa sababu alipokufa, jina lake liliondolewa. Katika sehemu nyinginezo za Biblia, twasoma juu ya rejesta ya kitamathali, au kitabu, chenye majina ya wale ambao Yehova huwapa thawabu ya uhai. Ijapokuwa kuna masharti ya kuandikwa majina katika kitabu hicho, kwa kuwa Yehova aweza ‘kufuta’ majina. (Kutoka 32:32, 33; Zaburi 69:28) Basi, maneno ya Isaya yadokeza onyo linalofaa kuzingatiwa—wenye kurudi waweza kuendelea kuishi katika nchi yao iliyorudishwa maadamu wadumisha utakatifu machoni pa Mungu.

16. (a) Yehova alitaka nini kwa wale alioruhusu kurejea Yuda mwaka wa 537 K.W.K.? (b) Kwa nini yaweza kusemwa kuwa rehema ya Yehova juu ya mabaki watiwa-mafuta na “kondoo wengine” haikuwa ya bure?

16 Mwaka wa 537 K.W.K., mabaki waliorudi Yerusalemu walifanya hivyo kwa nia njema—kuirudisha ibada ya kweli. Mtu yeyote aliyechafuliwa kwa mazoea ya dini ya kipagani au kwa mwenendo usio safi ambao Isaya alikuwa amekataza kwa dhati hakuwa na haki ya kurudi. (Isaya 1:15-17) Wale ambao Yehova aliona kuwa watakatifu ndio pekee wangeweza kurejea Yuda. (Isaya 35:8) Vivyo hivyo, tangu kuachiliwa kwao kutoka katika utekwa wa kiroho mwaka wa 1919, mabaki watiwa-mafuta, ambao sasa mamilioni ya “kondoo wengine” wamejiunga nao—wale walio na tumaini la uhai udumuo milele duniani—wamejitahidi kabisa kuwa watakatifu machoni pa Mungu. (Yohana 10:16) Wameondolea mbali mafundisho na mazoea ya Kibabiloni kwao. Wakiwa watu mmoja-mmoja, wao hujitahidi kushikamana na viwango vya Mungu vya maadili. (1 Petro 1:14-16) Rehema ya Yehova kwao haikuwa ya bure.

17. Yehova huandika majina ya nani katika “kitabu [chake] cha uhai,” nasi twapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Kumbuka kwamba Yehova aliwaona wale waliokuwa watakatifu nchini Israeli naye ‘akayaandika majina yao kwa ajili ya uhai.’ Leo pia, Yehova huona jitihada zetu za kuwa safi katika akili na mwili ‘tutoapo miili yetu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.’ (Waroma 12:1) Naye Mungu huwarekodi wote wanaofuata mwendo huo wa maisha katika “kitabu [chake] cha uhai”—rekodi ya kitamathali yenye majina ya wale wanaotarajia kupata uhai udumuo milele, huko mbinguni au hapa duniani. (Wafilipi 4:3; Malaki 3:16) Basi, na tufanye kila tuwezalo ili kudumisha utakatifu machoni pa Mungu, ndipo twaweza kudumisha majina yetu katika “kitabu” hicho chenye thamani.—Ufunuo 3:5.

Ahadi ya Utunzaji Wenye Upendo

18, 19. Kulingana na Isaya 4:4, 5, ni utakasaji gani atakaotekeleza Yehova, nao utatimizwaje?

18 Kisha Isaya aonyesha jinsi wakazi wa nchi iliyorudishwa watakavyokuwa watakatifu na baraka watakazopata. Asema: “Hapo Bwana atakapokuwa ameuosha uchafu wa hao binti za Sayuni na kuisafisha damu ya Yerusalemu kati yake, kwa roho ya hukumu na kwa roho ya kuteketeza. Tena juu ya makao yote ya mlima Sayuni, na juu ya makusanyiko yake, BWANA ataumba wingu na moshi wakati wa mchana, na mwangaza wa miali ya moto wakati wa usiku; kwa maana juu ya utukufu wote itatandazwa Sitara.”—Isaya 4:4, 5.

19 Hapo mwanzoni Isaya aliwakemea “binti za Sayuni,” ambao ufisadi wao wa kiadili ulifichwa ndani ya mapambo yao ya kujionyesha. Pia alifichua hatia ya damu ya watu hao kwa jumla, akiwasihi wajioshe. (Isaya 1:15, 16; 3:16-23) Ingawa hivyo, hapo yeye atazamia wakati Mungu mwenyewe atakapokuwa “ameuosha uchafu,” au takataka ya kiadili, na “kufuta madoa ya damu.” (Isaya 4:4, BHN) Utakasaji huo utatekelezwaje? Kwa “roho ya hukumu” na kwa “roho ya kuteketeza.” Uharibifu wa Yerusalemu unaokuja na uhamisho huko Babiloni zitakuwa mfoko wa hukumu za Mungu na hasira kali yake juu ya taifa lisilo safi. Mabaki wanaookoka majanga hayo na kurudi nyumbani watakuwa wamenyenyekezwa, wamesafishwa. Hiyo ndiyo sababu watakuwa watakatifu kwa Yehova na kupata rehema.—Linganisha Malaki 3:2, 3.

20. (a) Semi “wingu,” “moshi,” na “miali ya moto” zatukumbusha nini? (b) Kwa nini haitawabidi wahamishwa hao waliotakaswa kuogopa?

20 Yehova, kupitia Isaya, aahidi kwamba atawatunza kwa upendo mabaki hao waliotakaswa. Semi “wingu,” “moshi,” na “miali ya moto” zatukumbusha jinsi Yehova alivyowatunza Waisraeli baada ya kuondoka Misri. “Nguzo ya moto na ya wingu” iliwalinda dhidi ya Wamisri waliokuwa wakiwaandama; hiyo pia iliwaongoza nyikani. (Kutoka 13:21, 22; 14:19, 20, 24) Yehova alipojidhihirisha katika Mlima Sinai, mlima huo “wote pia u[li]toa moshi.” (Kutoka 19:18) Basi, haitawabidi wahamishwa hao waliotakaswa kuogopa. Yehova atakuwa Mlinzi wao. Atakuwa pamoja nao wakusanyikapo katika makao yao wenyewe au wakusanyikapo kwenye mikusanyiko mitakatifu.

21, 22. (a) Mara nyingi hema, au kibanda, ilijengwa kwa kusudi gani? (b) Ni tazamio gani liko mbele ya mabaki waliotakaswa?

21 Isaya amalizia ufafanuzi wake juu ya ulinzi wa Mungu kwa kukazia fikira maisha ya kila siku. Aandika: “Kutakuwa na hema kuwa uvuli wakati wa mchana kwa sababu ya hari, na kuwa mahali pa kukimbilia na kujificha wakati wa tufani na mvua.” (Isaya 4:6, Chapa ya 1989) Mara nyingi hema, au kibanda, ilijengwa katika shamba la mizabibu au uwanjani ili kuandaa uvuli kutoka kwa jua kali la msimu wa ukame na kutoka kwa baridi na dhoruba za msimu wa mvua.—Linganisha Yona 4:5.

22 Wakabilipo joto kali la mnyanyaso na dhoruba za upinzani, mabaki waliotakaswa wataona kuwa Yehova ndiye Chanzo chao cha ulinzi, usalama, na kimbilio. (Zaburi 91:1, 2; 121:5) Kwa hiyo tazamio zuri lawekwa mbele yao: Wakiachilia mbali itikadi na mazoea yao yasiyo safi ya Babiloni, wakubali utakasaji wa hukumu ya Yehova, na kujitahidi kudumisha utakatifu, watadumu salama, kana kwamba wamo ndani ya “hema” la ulinzi wa Mungu.

23. Kwa nini Yehova amewabariki mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao?

23 Ona kwamba utakasaji huja kwanza, kisha baraka. Hali imekuwa vivyo hivyo leo. Huko nyuma mwaka wa 1919, mabaki watiwa-mafuta walikubali kwa unyenyekevu kutakaswa, na Yehova ‘akauosha’ uchafu wao. Tangu hapo, “umati mkubwa” wa kondoo wengine pia wamekubali kutakaswa na Yehova. (Ufunuo 7:9) Wakiwa wametakaswa hivyo, mabaki na waandamani wao wamebarikiwa—Yehova amewatunza kwa ulinzi wake. Yeye hazuii kimwujiza joto kali la mnyanyaso au dhoruba za upinzani zisiwalemee. Lakini yeye huwalinda, kana kwamba anapiga ‘hema kuwa uvuli na kuwa mahali pa kukimbilia na kujificha wakati wa tufani na mvua.’ Jinsi gani?

24. Ikoje dhahiri kwamba Yehova amewabariki watu wake wakiwa tengenezo?

24 Fikiria hili: Baadhi ya serikali zenye uwezo zaidi katika historia zimepiga marufuku kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova au zimejaribu kuwaangamiza kabisa. Ingawa hivyo, Mashahidi wamedumu imara nao wameendelea kuhubiri bila kuacha! Kwa nini mataifa yenye uweza yameshindwa kukomesha utendaji wa kikundi kidogo hicho cha watu na kinachoonekana kuwa hakina ulinzi? Ni kwa sababu Yehova amewaweka watumishi wake walio safi katika “hema” la ulinzi ambalo hakuna mwanadamu yeyote awezaye kuling’oa!

25. Yehova kuwa Mlinzi wetu kwamaanisha nini kwetu mmoja-mmoja?

25 Namna gani sisi mmoja-mmoja? Yehova kuwa Mlinzi wetu hakumaanishi kwamba twaishi maisha yasiyo na matatizo yoyote katika mfumo huu wa mambo. Wakristo waaminifu wengi hukabili majanga, kama vile umaskini, misiba ya asili, vita, ugonjwa, na kifo. Tukabilipo taabu kama hizo, na tusisahau kamwe kuwa Mungu wetu yu nasi. Yeye hutulinda kiroho, akituandalia tunayohitaji—kutia ndani “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—ili tuvumilie majaribu kwa uaminifu. (2 Wakorintho 4:7) Tukiwa na usalama mbele yake, hatuhitaji kuogopa. Kwani, maadamu twafanya yote tuwezayo ili kudumisha utakatifu wetu machoni pake, chochote “hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu.”—Waroma 8:38, 39.

[Maelezo ya Chini]

a Wasomi fulani hudokeza kuwa usemi ‘chipukizi la Yehova’ humrejezea kwa njia isiyo ya moja kwa moja, Mesiya ambaye hangetokea kabla ya kurudishwa kwa Yerusalemu. Katika Targum za Kiaramu, fungu hilo lasimuliwa hivi kwa maneno mengine: “Mesiya [Kristo] wa Yehova.” Kwa kupendeza, baadaye Yeremia alitumia neno hilohilo la Kiebrania (tseʹmach) anapozungumza juu ya Mesiya akiwa kama “chipukizi la haki” analochipushiwa Daudi.—Yeremia 23:5; 33:15.

b “Walioponyoka” walitia ndani baadhi ya wale waliozaliwa uhamishoni. Hao wangeonwa kuwa ‘wameponyoka,’ kwa maana hawangalizaliwa kamwe ikiwa babu zao hawangaliokoka uharibifu.—Ezra 9:13-15; linganisha Waebrania 7:9, 10.

[Picha katika ukurasa wa 63]

Dhoruba ya hukumu ya Mungu yaja juu ya Yuda

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki