Programu Inayokusaidia Kuwa Msemaji na Mwalimu Bora
UWE mchanga au mzee, uwe mwanamume au mwanamke, shule hii inaweza kukusaidia kujua kuzungumza vizuri zaidi na kuwa mwalimu bora zaidi wa Neno la Mungu.
Mwangalizi wa shule atawapa migawo wale ambao wamejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Fomu yako ya ushauri iko kwenye kurasa tatu zinazofuata. Nambari zinazotangulia kila ushauri zinaonyesha masomo yanayohusika. Masomo hayo yanafafanua jinsi unavyoweza kukuza sifa za kusema na kufundisha, na umuhimu wa kila somo. Pia kuna mwongozo mzuri wa jinsi unavyoweza kutimiza mapendekezo yanayotolewa.
Rangi zilizo kwenye fomu ya ushauri zinaonyesha mashauri yanayohusu migawo ya (1) kusoma mbele ya wasikilizaji, (2) onyesho la watu wawili au zaidi, au (3) hotuba mbele ya kutaniko. Mwangalizi wa shule atapanga sifa ambayo utafanyia kazi. Ni afadhali kufanyia kazi sifa moja kwa wakati mmoja. Utafaidika ukifanya mazoezi yanayopendekezwa mwishoni mwa sifa unayofanyia kazi. Ikionekana wazi kwamba umetimiza vizuri ushauri wa sifa unayofanyia kazi, mshauri wa shule atakupa mgawo mwingine.
Ikiwa utatoa mgawo wako kwa njia ya onyesho, unahitaji kikao. Kuna orodha ya vikao katika ukurasa wa 82, lakini unaweza kutumia vikao vingine ukitaka. Yule anayekushauri anaweza kupendekeza ujaribu kutumia kikao fulani ili upate ujuzi zaidi, au anaweza kukuruhusu uchague kikao unachotaka.
Hata kama hutayarishi migawo ya shule, kusoma kitabu hiki na kufanya mazoezi yanayoonyeshwa kunaweza kukusaidia sana kufanya maendeleo. Labda unaweza kuchunguza somo tofauti kila juma moja hivi.
Hata iwe umekuwa katika shule hii kwa muda gani au umeshiriki katika huduma ya shambani kwa muda gani, bado unaweza kufanya maendeleo zaidi. Faidika kabisa na elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.