Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 8 uku. 107-uku. 110 fu. 2
  • Kiasi Kinachofaa cha Sauti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kiasi Kinachofaa cha Sauti
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Ubadilifu wa Sauti
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Ubadilifu wa Sauti
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Maswali Ambayo Wazazi Huuliza
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kuwatazama Wasikilizaji
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 8 uku. 107-uku. 110 fu. 2

SOMO LA 8

Kiasi Kinachofaa cha Sauti

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kuzungumza kwa sauti ya kutosha au mkazo wa kutosha. Ili ujue kiasi kinachofaa cha sauti, fikiria (1) idadi ya wale wanaokusikiliza na pia ufikirie wao ni watu wa aina gani, (2) kelele zinazokengeusha, (3) habari unayozungumzia, na (4) kusudi lako.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Ikiwa wengine hawakusikii vizuri, akili zao zinaweza kutangatanga, na huenda wasielewe mambo unayosema. Ukizungumza kwa sauti kubwa sana, unaweza kuudhi watu—na hata wanaweza kufikiri huna heshima.

IKIWA msemaji anaongea kwa sauti ya chini, baadhi ya wasikilizaji wanaweza kuanza kusinzia. Ikiwa mhubiri anazungumza kwa sauti ya chini sana katika huduma ya shambani, huenda mwenye nyumba asimsikilize. Na ikiwa wasikilizaji wanatoa maelezo kwa sauti ya chini katika mikutano, wengine hawatapata kitia-moyo kinachohitajika. (Ebr. 10:24, 25) Kwa upande mwingine, msemaji akiinua sauti yake wakati usiofaa, wasikilizaji wanaweza kushangaa na hata kuudhika.—Mit. 27:14.

Wafikirie Wale Wanaokusikiliza. Je, unazungumza na mtu mmoja? familia? kikundi kinachokutana kwa ajili ya huduma ya shambani? kutaniko zima? au unazungumza mbele ya kusanyiko kubwa? Ni wazi kwamba kiasi cha sauti kinachofaa hali moja huenda kisifae hali nyingine.

Katika pindi kadhaa, watumishi wa Mungu wamehutubia umati. Katika siku za Solomoni, vikuza-sauti havikuwako wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu la Yerusalemu. Kwa hiyo Solomoni alisimama jukwaani akabariki watu “kwa sauti kuu.” (1 Fal. 8:55; 2 Nya. 6:13) Karne nyingi baadaye, baada ya kumwagwa kwa roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K., umati ulizingira kikundi cha Wakristo katika Yerusalemu. Watu wengine walipendezwa lakini wengine waliwadhihaki Wakristo hao. Petro alitumia hekima, “akasimama . . . na kuinua sauti yake.” (Mdo. 2:14) Akatoa ushahidi wenye nguvu sana.

Unaweza kutambuaje kama kiasi cha sauti yako kinafaa? Mojawapo ya njia bora za kutambua jambo hilo ni jinsi wasikilizaji wanavyoitikia. Ukiona baadhi ya wasikilizaji waking’ang’ana kukusikiliza, jaribu kuinua sauti yako.

Iwe tunazungumza na mtu mmoja au tunazungumza mbele ya kikundi, ni vizuri kufikiria wasikilizaji. Ikiwa kuna mmoja ambaye hasikii vizuri, huenda ukahitaji kuinua sauti yako. Lakini labda watu wenye umri mkubwa ambao huenda wasiitikie upesi wasifurahi ukizungumza kwa sauti ya juu sana. Kupiga kelele hata kunaweza kuonwa kuwa kukosa adabu. Katika jamii fulani-fulani kuongea kwa sauti kubwa sana huonwa kuwa ishara ya kukasirika au kukosa subira.

Fikiria Kelele Zinazokengeusha. Unapokuwa katika huduma ya shambani, kiasi cha sauti yako hutegemea hali unazopata. Huenda kuna kelele za magari, watoto, mbwa wanaobweka, mdundo wa juu wa muziki, au televisheni iliyowashwa kwa sauti ya juu. Kwa upande mwingine, katika maeneo ambamo nyumba ziko karibu-karibu, mwenye nyumba anaweza kuaibika ukizungumza kwa sauti ya juu hivi kwamba hata majirani wanakusikia.

Akina ndugu ambao hutoa hotuba kutanikoni au kwenye makusanyiko pia hulazimika kukabili hali tofauti-tofauti. Kuzungumza na watu kule nje ni tofauti na kutoa hotuba katika jumba lenye vikuza-sauti vinavyofaa. Katika Amerika Kusini mishonari wawili walishiriki kutoa hotuba ya watu wote katika baraza ya nyumba ya mtu mmoja aliyependezwa. Hotuba ilipokuwa ikitolewa, fataki zilikuwa zikilipuliwa katika uwanja fulani uliokuwa karibu, na jogoo mmoja alikuwa akiwika bila kukoma!

Kitu chochote kinaweza kutukia unapoendelea kutoa hotuba na huenda ukahitaji kutua kidogo mpaka kelele hiyo ipungue au unaweza kuinua sauti yako. Kwa mfano, ikiwa mikutano inafanywa katika jengo lenye paa ya mabati, mvua kubwa inaweza kufanya wasikilizaji wasimsikie msemaji. Mtoto anayelia au kelele zinazosababishwa na watu wanaofika wakiwa wamechelewa zinaweza kukuvuruga. Jifunze kukabiliana na kelele hizo zinazokengeusha ili wasikilizaji wafaidike kabisa na hotuba yako.

Vikuza-sauti vinaweza kusaidia ikiwa vinapatikana, lakini bado msemaji anahitaji kuinua sauti yake kulingana na hali. Katika maeneo mengine ambamo umeme hupotea-potea, wasemaji hulazimika kuendelea kuongea bila kutumia maikrofoni.

Fikiria Habari Unayozungumzia. Kiasi cha sauti yako pia hutegemea habari unayozungumzia katika hotuba yako. Ikiwa jambo unalosema linahitaji mkazo, usilidhoofishe kwa kuongea kwa sauti dhaifu mno. Kwa mfano, unaposoma mashutumu makali katika Maandiko, sauti yako inapasa kuwa na nguvu kuliko sauti unayotumia kusoma shauri linalohusu kuonyesha upendo. Fanya kiasi cha sauti yako kifae habari unayozungumzia, lakini ujihadhari usipite kiasi na kujielekezea fikira.

Fikiria Kusudi Lako. Ukitaka kuchochea wasikilizaji watie bidii katika utendaji, huenda ukahitaji kutumia sauti yenye nguvu kwa kiasi fulani. Ukitaka kubadili fikira zao, usitumie sauti kubwa kupita kiasi. Kama unajaribu kuwafariji, mara nyingi ni afadhali kutumia sauti ya upole.

Kutumia Vizuri Sauti ya Juu. Unapojaribu kuita mtu ambaye ana shughuli, kwa kawaida inafaa kuinua sauti. Wazazi wanajua jambo hili na basi wao huwaita watoto wao kwa sauti kubwa wakati ukifika wa kuacha kucheza na kurudi nyumbani. Pia mwenyekiti anaweza kuhitajika kuinua sauti anapotaka watu wawe makini kutanikoni au kusanyikoni. Wahubiri wanapokuwa katika huduma ya shambani, wanaweza kusalimiana kwa sauti na watu ambao wanaendelea na shughuli zao nje.

Hata baada ya kuvuta fikira za mtu, ni muhimu uendelee kutumia kiasi kinachofaa cha sauti. Sauti ya chini sana inaweza kufanya wengine wadhani mwenye kuongea hajajitayarisha vizuri au hasadiki mambo anayosema.

Ukitoa amri kwa sauti kubwa, watu wanaweza kuchochewa kuchukua hatua. (Mdo. 14:9, 10) Hali kadhalika, amri inayotolewa kwa sauti kuu inaweza kuepusha msiba. Kule Filipi, mlinzi mmoja wa jela karibu ajiue kwa sababu alidhani wafungwa aliokuwa akilinda wametoroka. ‘Paulo akapaaza sauti kubwa, akisema: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!”’ Kwa njia hiyo waliepusha msiba kwa kumzuia mlinzi huyo asijiue. Kisha Paulo na Sila wakamhubiria mlinzi huyo na jamaa yake, wote wakakubali kweli.—Mdo. 16:27-33.

Jinsi ya Kuboresha Kiasi cha Sauti Yako. Wengine wanahitaji kujitahidi sana kujifunza kutumia kiasi kinachofaa cha sauti. Mtu anaweza kuongea kwa sauti ya chini kwa sababu ana sauti ndogo. Lakini, akitia bidii anaweza kufanya maendeleo, hata ingawa bado hawezi kuongea kwa sauti yenye nguvu. Fikiria jinsi unavyopumua na jinsi unavyokaa. Fanya mazoezi ya kuketi vizuri na kusimama vizuri. Sogeza nyuma mabega yako kisha uvute pumzi nyingi. Hakikisha unajaza sehemu za chini za mapafu yako hewa. Ukitumia vizuri hewa hiyo, unaweza kudhibiti kiasi cha sauti yako unapoongea.

Wengine wana tatizo la kusema kwa sauti kubwa sana. Labda wamezoea tabia hiyo kwa sababu ya kufanya kazi sehemu za nje au katika mazingira yenye kelele nyingi. Kwa upande mwingine, labda walilelewa katika mazingira ambamo kila mtu alikuwa akipiga kelele na kukatiza-katiza mazungumzo. Na basi wanadhani kwamba njia ya pekee ya kushiriki katika mazungumzo ni kuongea kwa sauti ya juu kuliko wengine wote. Lakini wanapoendelea kutii shauri la Biblia la kujivika “shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu,” wao watarekebisha kiasi cha sauti yao wanapoongea na wengine.—Kol. 3:12.

Mambo yatakayokusaidia kuzungumza kwa kiasi kinachofaa cha sauti ni matayarisho mazuri, uzoefu unaopata kwa kushiriki kwa ukawaida katika utumishi wa shambani, na sala kwa Yehova. Iwe unatoa hotuba jukwaani au unaongea na mtu katika huduma ya shambani, jaribu kufikiria jinsi mambo unayosema yanavyoweza kuwasaidia watu.—Mit. 18:21.

WAKATI AMBAPO SAUTI YA JUU INAWEZA KUHITAJIKA

  • Unapotaka kundi la watu liwe makini.

  • Kunapokuwa na kelele.

  • Unapotaka usikilizwe unaposema jambo muhimu sana.

  • Unapotaka kufanya watu wachukue hatua fulani.

  • Unapoita mtu au kikundi fulani cha watu.

JINSI YA KUFANYA MAENDELEO

  • Tazama jinsi watu unaoongea nao wanavyoitikia; tumia kiasi kinachofaa cha sauti ili waweze kusikia kwa njia inayofaa.

  • Jifunze kujaza sehemu za chini za mapafu yako hewa.

MAZOEZI: Kwanza soma Matendo 19:23-41 kimoyo-kimoyo ukifikiria hali ya mistari hiyo kama inavyoonyeshwa na masimulizi na muktadha. Tambua yule anayeongea na pia roho inayoonyeshwa. Sasa soma kila sehemu kwa sauti inayofaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki