Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 10 uku. 115-uku. 117 fu. 4
  • Shauku

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shauku
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Fundisha kwa Shauku
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2021
  • Kuwaelimisha Wasikilizaji
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Shauku
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Kutoa Hotuba Bila Kutazama Sana Maandishi
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 10 uku. 115-uku. 117 fu. 4

SOMO LA 10

Shauku

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kutoa hotuba kwa uchangamfu ili kuonyesha jinsi unavyohisi kuhusu yale unayosema.

KWA NINI NI MUHIMU?

Shauku itasaidia wasikilizaji waendelee kukusikiliza; pia inaweza kuwachochea. Ukitoa hotuba kwa shauku, wasikilizaji pia watakuwa na shauku.

SHAUKU husaidia kuchangamsha hotuba. Ingawa ni muhimu kutoa hotuba yenye kuarifu, hotuba yenye uchangamfu na shauku ndiyo husaidia kuvuta usikivu wa wasikilizaji. Hata wewe unaweza kukuza sifa ya shauku haidhuru malezi yako au utu wako.

Zungumza kwa Hisia. Yesu alipokuwa akizungumza na mwanamke fulani wa Samaria, alisema kwamba wale wanaomwabudu Yehova ni sharti wamwabudu “kwa roho na kweli.” (Yn. 4:24) Ni lazima ibada yao ichochewe na mioyo yenye uthamini na pia ipatane na kweli zilizo katika Neno la Mungu. Mtu anapokuwa na uthamini wa kadiri hiyo, mazungumzo yake yataonyesha jambo hilo. Anakuwa na hamu ya kuwaambia wengine mambo ambayo Yehova ametuandalia kwa upendo. Uso wake, ishara zake, na sauti yake itaonyesha jinsi anavyohisi hasa.

Basi, inakuwaje kwamba msemaji anayeamini mambo anayosema na anayempenda Yehova akose shauku anapotoa hotuba? Haitoshi tu kutayarisha mambo atakayosema. Ni lazima hotuba atakayotoa imwingie kabisa, atie moyo wake wote ndani yake. Tuseme ana mgawo wa kutoa hotuba inayohusu dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Anapotoa hotuba hiyo, mbali na kuzingatia tu habari zinazohusika, ni lazima athamini kabisa jinsi dhabihu ya fidia ya Yesu inavyomfaidi na inavyowafaidi wasikilizaji. Anahitaji kukumbuka uthamini wake kwa Yehova Mungu na Kristo Yesu kwa kufanya uandalizi huo mzuri ajabu. Anahitaji kufikiria jinsi ambavyo dhabihu ya fidia imetokeza tumaini zuri ajabu la maisha kwa wanadamu—furaha ya milele na afya kamili katika dunia iliyorudishwa kuwa paradiso! Kwa hiyo, anahitaji kutia moyo wake katika hotuba hiyo.

Biblia inasema hivi kuhusu mwandishi Ezra aliyekuwa pia mwalimu katika Israeli: ‘Alikuwa ameutayarisha moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha katika Israeli.’ (Ezra 7:10) Mbali na kutayarisha mambo tutakayosema, tutayarishe mioyo yetu, ili sisi pia tutoe hotuba kutoka moyoni. Kuzungumza hivyo juu ya kweli kutoka moyoni kunaweza kuwasaidia sana wale tunaozungumza nao waipende kweli sana.

Wafikirie Wasikilizaji. Jambo jingine kuu linalosaidia kuonyesha shauku ni kusadiki kwamba wasikilizaji wanahitaji kujua mambo unayosema. Hiyo inamaanisha kwamba unapotayarisha hotuba, mbali na kukusanya habari zinazofaa, sali ili Yehova akupe mwongozo wa kutumia habari hizo ili zifaidi wasikilizaji. (Zab. 32:8; Mt. 7:7, 8) Chunguza uone ni kwa nini wasikilizaji wanahitaji kusikia hotuba hiyo? Hotuba hiyo itawafaidije? Na unaweza kuitoa kwa njia gani ili waithamini?

Tayarisha hotuba hiyo mpaka ujisikie una msisimko wa kutaka kuitoa. Si lazima iwe na mambo mapya, lakini uitoe kwa njia tofauti. Ni lazima uwe na shauku ikiwa umetayarisha hotuba ambayo kwa kweli itawasaidia wasikilizaji waimarishe uhusiano wao na Yehova, wathamini maandalizi yake, wakabiliane kwa mafanikio na mikazo ya maisha katika mfumo huu wa kale, au kuwasaidia wawe na matokeo mazuri katika huduma.

Vipi ikiwa una mgawo wa kusoma mbele ya watu? Ili uweze kusoma kwa shauku, unahitaji kufanya zaidi ya kutamka tu maneno kwa usahihi na kusoma vizuri mafungu-mafungu ya maneno. Chunguza habari hiyo. Kama ni mgawo wa kusoma Biblia, fanya utafiti kuhusu sehemu unayosoma. Hakikisha kwamba kwa ujumla unaielewa. Fikiria jinsi usomaji huo unavyokufaidi na jinsi unavyofaidi wasikilizaji, na usome ukiwa na hamu ya kufanya wasikilizaji waone faida hiyo.

Je, unajitayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani? Pitia habari ambayo utazungumzia na maandiko utakayotumia. Pia fikiria mambo yanayohangaisha watu. Kumekuwa na visa gani katika habari? Watu wana matatizo gani? Unapokuwa tayari kuonyesha watu kwamba Neno la Mungu lina masuluhisho kwa matatizo yanayowahangaisha, unakuwa na hamu ya kuhubiri, na shauku hutokea yenyewe tu.

Onyesha Shauku kwa Kutoa Hotuba kwa Uchangamfu. Shauku hudhihirishwa zaidi na uchangamfu wa hotuba. Uso wako uonyeshe shauku hiyo. Ni lazima wasikilizaji waone unasadiki mambo unayosema, bila kushikilia mambo kishupavu.

Usawaziko unahitajika. Kuna watu ambao wana mwelekeo wa kusisimukia kila jambo. Huenda wakahitaji kusaidiwa kutambua kwamba mtu anapoonyesha shauku au hisia kupita kiasi, wasikilizaji huanza kumfikiria badala ya kufikiria ujumbe wake. Kwa upande mwingine, watu wenye haya wanahitaji kutiwa moyo kuonyesha shauku zaidi.

Shauku ni sifa inayoshika wengine kwa urahisi. Ikiwa una mawasiliano mazuri na wasikilizaji na unatoa hotuba kwa shauku, wasikilizaji pia watakuwa na shauku. Apolo alizungumza kwa uchangamfu, na ilisemekana yeye ni msemaji mwenye ufasaha. Ukiwaka roho ya Mungu, hotuba yako changamfu itachochea wasikilizaji.—Mdo. 18:24, 25; Rom. 12:11.

Shauku Ifae Habari. Jihadhari usiwe na shauku kupita kiasi katika hotuba yote hivi kwamba inachosha wasikilizaji. Watakuwa wamechoka kiasi cha kwamba hawatasikia hata ukiwahimiza wafuate maagizo unayotoa. Jambo hilo linaonyesha kwamba kuna uhitaji wa kutayarisha habari inayoweza kutolewa kwa njia mbalimbali. Jaribu sana usianze kutoa hotuba kwa njia inayoonyesha kutojali. Ukichagua kwa uangalifu habari utakazotoa, utapendezwa sana nazo. Lakini kwa kawaida mambo fulani huhitaji kutolewa kwa shauku zaidi kuliko mengine, lakini yote yanapaswa kutolewa kwa ustadi na kwa shauku ya kadiri tofauti-tofauti katika hotuba yote.

Hasa mambo makuu yanapaswa kutolewa kwa shauku. Ni lazima hotuba yako iwe na vilele vinavyoitegemeza. Kwa kuwa vilele hivyo ni upeo wa hotuba yako, mara nyingi ni mambo unayokusudia yachochee wasikilizaji. Baada ya kuwasadikisha wasikilizaji, unahitaji kuwachochea, ukiwaonyesha faida za kutumia maishani mambo unayosema. Shauku itakusaidia kufikia mioyo ya wasikilizaji. Usilazimishe uchangamfu katika hotuba. Lazima kuwe na sababu ya kufanya iwe changamfu, na hiyo inategemea habari ambayo umetayarisha.

JINSI YA KUKUZA SHAUKU

  • Mbali na kutayarisha mambo utakayosema, tayarisha moyo wako; ili uhusishe hisia zako.

  • Fikiria sana jinsi ambavyo mambo utakayozungumzia yatafaidi wasikilizaji.

  • Tambua sehemu ambazo zinahitaji shauku ya kipekee.

  • Uwe mchangamfu kabisa unapotoa hotuba. Hakikisha uso wako unaonyesha jinsi unavyohisi. Ongea kwa nguvu na kwa bidii.

MAZOEZI: Chunguza Yoshua sura ya 1 na ya 2, ukiangalia sehemu inayofaa kusomwa kwa shauku na jinsi inavyopasa kusomwa kwa shauku. Fanya mazoezi ya kuisoma kwa sauti kwa shauku inayofaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki