Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 27 uku. 174-uku. 178 fu. 2
  • Kutoa Hotuba Bila Kutazama Sana Maandishi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoa Hotuba Bila Kutazama Sana Maandishi
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kutumia Muhtasari
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kutayarisha Hotuba za Watu Wote
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Shauku
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kutayarisha Muhtasari
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 27 uku. 174-uku. 178 fu. 2

SOMO LA 27

Kutoa Hotuba Bila Kutazama Sana Maandishi

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kuzungumza kwa njia ambayo maneno yanatoka kwa wepesi na kwa kutayarisha vizuri mawazo yako.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Njia bora ya kushika usikivu wa wasikilizaji na kuwachochea ni kwa kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi.

HUENDA ikawa umetayarisha hotuba kwa bidii na labda ina habari zenye kuarifu na sababu zinazovutia au labda unaweza kuitoa kwa ufasaha. Lakini je, kweli utafaulu ikiwa wasikilizaji si makini na wanasikia tu mambo machache hapa na pale kwa sababu akili zao zinatangatanga? Ikiwa hawawezi kusikiliza kwa makini hotuba yako, je, kweli utagusa mioyo yao?

Sababu kuu ya tatizo hilo huenda ikawa nini? Kunaweza kuwa na sababu kadhaa. Mara nyingi tatizo ni kushindwa kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi. Yaani, msemaji anatazama-tazama sana maandishi yake, au hatoi hotuba kwa njia ya maongezi. Lakini, matatizo hayo husababishwa na jinsi mtu anavyotayarisha hotuba.

Ukiandika hotuba yote kwanza kisha ujaribu kuigeuza kuwa muhtasari, haitakuwa rahisi kuitoa bila kutazama sana maandishi. Kwa nini? Kwa sababu umechagua maneno hususa unayotaka kutumia. Hata ukitumia muhtasari kutoa hotuba, utakuwa ukijaribu kukumbuka maneno ambayo ulitumia katika yale maandishi uliyotayarisha awali. Hotuba ikiandikwa, mara nyingi haitokei kwa njia ya maongezi na sentensi huwa ndefu-ndefu kuliko katika mazungumzo ya kawaida. Na jambo hilo litaonekana unapotoa hotuba.

Badala ya kuandika mambo mengi, jaribu kufanya yafuatayo: (1) Chagua kichwa kikuu na mambo makuu ya habari ambayo utatumia kufafanua kichwa hicho. Ikiwa unatoa hotuba fupi, mambo mawili makuu yanaweza kutosha. Hotuba ndefu inaweza kuwa na mambo makuu manne au matano. (2) Chini ya kila jambo kuu, chagua maandiko makuu unayotaka kutumia kulifafanua; pia andika mifano na sababu kuu ambazo unataka kutumia. (3) Fikiria jinsi ambavyo utatoa utangulizi wa hotuba hiyo. Hata unaweza kuandika sentensi moja au mbili. Pia panga umalizio wako.

Ni muhimu sana kufanya matayarisho ya kutoa hotuba. Lakini usipitie hotuba hiyo neno kwa neno na kuikariri yote. Ili kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi, unapaswa kutayarisha hasa mawazo bali si neno moja-moja. Pitia-pitia mawazo mpaka yafuatane kwa urahisi akilini mwako. Ikiwa hotuba yako inafuatana vizuri na imepangwa vizuri, basi utaweza kuitoa kwa urahisi na mawazo yatatiririka tu vizuri.

Fikiria Faida. Faida kubwa ya kuhutubu bila kutazama sana maandishi ni kwamba utazungumza kwa njia ya kawaida na utagusa mioyo ya watu kwa urahisi. Utatoa hotuba kwa shauku zaidi na kupendeza wasikilizaji zaidi.

Njia hii ya kuzungumza inakuwezesha kuwatazama wasikilizaji vizuri, na hiyo huboresha mawasiliano kati yako na wao. Inaelekea wasikilizaji wataona kwamba unafahamu sana jambo unalozungumzia na kwamba unaamini kabisa jambo unalosema ikiwa hutazami sana maandishi na kusoma kila sentensi. Kwa hiyo, kutoa hotuba kwa njia hii hufanya iwe rahisi kuzungumza kutoka moyoni, kwa njia ya maongezi, na kugusa mioyo ya wasikilizaji.

Kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi kunakuwezesha kubadilikana. Hufuati sana hotuba hiyo kiasi cha kwamba huwezi kuirekebisha. Kwa mfano, mapema siku ile ambayo una hotuba kunatokea habari inayofaa kabisa hotuba yako. Ingefaa kutaja habari hiyo, sivyo? Au labda unapotoa hotuba, unagundua kwamba kuna watoto wengi wanaoenda shuleni miongoni mwa wasikilizaji. Ingefaa sana kurekebisha mifano yako na matumizi yake ili kuwasaidia watoto hao waone jinsi hotuba yako inavyohusu maisha yao.

Faida nyingine ya kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi ni kwamba akili yako mwenyewe inachochewa. Ikiwa wasikilizaji wanathamini na ni wachangamfu, hata wewe unachangamka, kisha unafafanua zaidi mawazo yako au unachukua muda kukazia mambo fulani kwa kuyarudia. Ukitambua kwamba upendezi wa wasikilizaji unafifia, unaweza kuchukua hatua za kurekebisha hali hiyo badala ya kuhutubia watu ambao hata hawakusikilizi kwa sababu akili zao ziko mbali.

Epuka Mitego. Pia tambua kwamba kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi kuna mitego yake. Mtego mmoja ni kupitisha wakati. Ukiongeza mambo mengi mno katika hotuba, unaweza kupitisha wakati. Unaweza kurekebisha tatizo hilo kwa kuonyesha katika muhtasari wakati ambao unapasa kutumia katika kila sehemu. Kisha fuata sana wakati huo.

Mtego mwingine kwa wasemaji wazoefu ni kujitumaini kupita kiasi. Kwa kuwa wamezoea kuhutubia watu, ni rahisi kwa baadhi yao kukusanya haraka-haraka mambo fulani na kuyaingiza kwenye hotuba ili watimize wakati unaotakikana. Lakini sifa ya unyenyekevu na kule kutambua kwamba tunashiriki katika programu ya elimu ambayo Yehova mwenyewe ndiye Mwalimu Mkuu Zaidi, kunapasa kutuchochea tutimize kila mgawo kwa bidii na sala na kujitayarisha vizuri.—Isa. 30:20; Rom. 12:6-8.

Labda wasemaji wengi ambao hawana uzoefu wanaogopa kwamba watasahau mambo wanayotaka kusema wasipotazama sana maandishi. Jambo hili lisikuzuie kufanya maendeleo ya kuwa msemaji bora. Tayarisha vizuri, na mtegemee Yehova akusaidie kwa roho yake.—Yn. 14:26.

Wasemaji wengine huhangaikia sana maneno ya kutumia na kushindwa kutoa hotuba kwa njia ya mazungumzo. Ni kweli kwamba tofauti na hotuba za kusoma, huenda usitumie maneno yanayofaa zaidi au lugha sanifu zaidi unapotoa hotuba bila kutazama sana maandishi, lakini hotuba yenye kuvutia inayotolewa kwa njia ya mazungumzo hufunika kasoro hiyo. Watu huguswa moyo zaidi na maneno na sentensi wanazoelewa kwa urahisi. Ukitayarisha mawazo yako vizuri, itakuwa rahisi kutumia maneno yanayofaa bila kushika maneno hayo akilini. Na ikiwa umezoea kutumia lugha sanifu katika mazungumzo ya kawaida, itakuwa rahisi kutumia maneno yanayofaa jukwaani.

Mihtasari ya Kutumia. Ukizoea kutoa hotuba na kufanya mazoezi, unaweza kupunguza muhtasari wako uwe na maneno machache kwa kila jambo kuu la hotuba yako. Unaweza kuandika mambo hayo pamoja na maandiko unayopanga kutumia kwenye karatasi ili uweze kuyarejelea kwa urahisi. Mara nyingi utaweza kushika akilini muhtasari mfupi kwa ajili ya huduma ya shambani. Kama umefanya utafiti kuhusu jambo fulani ambalo mtazungumzia kwenye ziara ya kurudia, unaweza kuandika maandishi mafupi kwenye karatasi na kuiweka katika Biblia yako. Au unaweza tu kutumia muhtasari mmoja katika “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo” au habari zinazopatikana katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko.

Lakini, kama umepewa migawo kadhaa katika majuma machache na labda pia una migawo ya kutoa hotuba za watu wote, unaweza kuhitaji maandishi mengi. Kwa nini? Ili kujikumbusha habari hiyo kabla ya kushughulikia kila mmoja wa migawo hiyo. Hata hali ikiwa hivyo, ukitegemea sana maandishi yako ili ujue jambo la kusema unapotoa hotuba—ukitazama-tazama karibu kila sentensi—utakosa faida zinazotokana na kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi. Ukiwa na maandishi mengi, yatie alama maneno machache na maandiko ambayo utatumia ili uweze kuyarejelea kwa urahisi.

Ingawa mara nyingi msemaji mwenye uzoefu hutoa hotuba bila kutazama sana maandishi, kutumia njia nyinginezo za kutoa hotuba kunaweza kufaidi pia. Unaweza kushika akilini maneno machache ili kuyatumia kwenye utangulizi na umalizio kwa sababu sehemu hizo zinahitaji mawasiliano mazuri na wasikilizaji na pia mkazo. Inafaa kusoma tarakimu, manukuu, maandiko, na unaweza kupata matokeo mazuri ukifanya hivyo.

Wengine Wanapotaka Majibu. Nyakati nyingine sisi huulizwa maswali yanayohusu imani yetu bila kuwa na fursa ya kujitayarisha. Hali hiyo inaweza kutokea mtu anapozusha kipingamizi fulani tunapokuwa katika utumishi wa shambani. Hali kama hizo zinaweza kutokezwa pia na watu wa ukoo, kazini, au hata shuleni. Maofisa wa serikali pia huenda wakataka kujua imani yetu na juu ya maisha yetu. Maandiko yanatuhimiza hivi: “Sikuzote [mwe] tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.”—1 Pet. 3:15.

Ebu ona jinsi Petro na Yohana walivyojibu Sanhedrini ya Wayahudi katika Matendo 4:19, 20. Walitangaza msimamo wao kwa sentensi mbili tu. Walifanya hivyo kwa njia iliyofaa wale waliokuwa wakiwasikiliza—wakitaja kwamba jambo linalowakabili pia linakabili mahakama hiyo. Baadaye, Stefano aliwekelewa mashtaka bandia, akapelekwa mbele ya mahakama iyo hiyo. Soma jibu lake lenye nguvu katika Matendo 7:2-53. Alipangaje habari zake? Yeye alitaja matukio kwa kufuata utaratibu wa jinsi yalivyotokea. Alipofikia mahali panapofaa, alianza kukazia roho ya uasi ya taifa la Israeli. Akimalizia, alionyesha kwamba Sanhedrini ilionyesha roho ileile kwa kumfanya Mwana wa Mungu auawe.

Unapoitwa kwa ghafula ueleze juu ya imani yako, ni nini kinachoweza kukusaidia kufaulu? Mwige Nehemia, ambaye alisali kwa ukimya kabla ya kujibu swali la Mfalme Artashasta. (Neh. 2:4) Kisha, tayarisha haraka akilini jambo utakalosema. Tunaweza kuorodhesha hivi hatua hizo kuu: (1) Chagua jambo moja au mambo mawili ambayo unapaswa kutia ndani ya jibu lako (unaweza kuchagua jibu katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko). (2) Amua maandiko ambayo utatumia kuunga mkono mambo hayo. (3) Fikiria jinsi utakavyoanzisha mazungumzo kwa busara ili mwenye kuuliza swali aweze kusikiliza. Kisha anza kuzungumza.

Je, utakumbuka jambo la kusema ukiwa chini ya mkazo? Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Msiwe wenye kuhangaikia jinsi gani au jambo gani mtakalosema; kwa maana lile mtakalosema litapewa kwenu katika saa hiyo; kwa maana wanaosema si nyinyi tu, bali ni roho ya Baba yenu isemayo kupitia nyinyi.” (Mt. 10:19, 20) Hiyo haimaanishi kwamba utapewa kimuujiza “usemi wa hekima” kama Wakristo wa karne ya kwanza. (1 Kor. 12:8) Lakini ukitumia kwa ukawaida elimu ambayo Yehova huandalia watumishi wake katika kutaniko la Kikristo, roho takatifu itakusaidia kukumbuka mambo wakati unapohitaji kuyakumbuka.—Isa. 50:4.

Kwa kweli kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana. Ukizoea kutoa hotuba kwa njia hiyo kila wakati unapokuwa na migawo kutanikoni, basi haitakuwa vigumu kujibu maswali unayoulizwa kwa ghafula kwa sababu njia ya kujitayarisha ni ileile moja. Usiogope kutumia njia hiyo. Kujifunza kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi kutaboresha huduma yako. Na kama una pendeleo la kutoa hotuba kutanikoni, inaelekea wasikilizaji watakusikiliza kwa makini na utagusa mioyo yao.

JINSI YA KUFAULU

  • Fikiria sana faida za kutoa hotuba bila kutazama sana maandishi.

  • Badala ya kuandika hotuba yote, tayarisha muhtasari wenye mambo machache.

  • Tayarisha utoaji wako kwa kupitia akilini kila jambo kuu likiwa peke yake. Fikiria kufafanua mawazo kwa njia inayofuatana vizuri badala ya kuhangaikia mno maneno hususa utakayosema.

MAZOEZI: (1) Unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, uwe na zoea la kutia mstari maneno makuu pekee badala ya kutia sentensi nzima-nzima mstari. Jibu kwa maneno yako mwenyewe. (2) Unapotayarisha hotuba yako itakayofuata katika shule, anza kwa kukumbuka kichwa kikuu na mambo makuu mawili au matatu ambayo utatumia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki