Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 8 kur. 77-86
  • “Nilitumwa Kufanya Hivyo”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nilitumwa Kufanya Hivyo”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Yesu Alihubiri?
  • Habari Ambayo Yesu Alihubiri
  • Jinsi Yesu Alivyoiona Huduma Yake
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • “Niliweka Kiolezo kwa Ajili Yenu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Twazoezwa Kutoa Ushahidi Kamili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Nifuateni, Nami Nitawafanya Kuwa Wavuvi Watu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 8 kur. 77-86

Sura ya 8

“Nilitumwa Kufanya Hivyo”

1-4. (a) Yesu anamfundisha mwanamke Msamaria kwa ustadi jinsi gani, na anapata matokeo gani? (b) Mitume wake wana maoni gani juu ya jambo hilo?

YESU na mitume wake wamekuwa wakitembea kwa muda fulani. Wanaelekea kaskazini, kutoka Yudea kwenda Galilaya. Njia fupi zaidi, inayochukua siku tatu hivi, inapitia Samaria. Saa sita hivi mchana, wanakaribia jiji dogo linaloitwa Sikari ambapo wanapumzika.

Picha katika ukurasa mzima wa 78

2 Mitume wake wanapoenda kununua chakula, Yesu anapumzika kando ya kisima kilicho nje ya jiji hilo. Mwanamke fulani anakuja kuchota maji. Ikiwa Yesu angetaka, angempuuza kwa kuwa “amechoka kwa sababu ya safari hiyo.” (Yohana 4:6) Ingeeleweka ikiwa Yesu angempuuza mwanamke huyo Msamaria na kuendelea na shughuli zake. Kama tulivyoona katika Sura ya 4 ya kitabu hiki, mwanamke huyo angetazamia mtu yeyote ambaye ni Myahudi ampuuze. Hata hivyo, Yesu anaanzisha mazungumzo pamoja naye.

3 Anaanza kwa mfano unaohusu maisha ya kila siku ya mwanamke huyo. Anazungumzia jambo ambalo mwanamke huyo anafanya sasa hivi. Amekuja kuchota maji, naye Yesu anazungumza kuhusu maji ya uzima yatakayomaliza kiu yake ya kiroho. Mara kwa mara mwanamke huyo anataja mambo yanayoweza kutokeza mabishano.a Kwa busara, Yesu anaepuka mambo hayo na kuzungumzia habari aliyokuwa nayo akilini. Anakazia mambo ya kiroho, yale yanayohusu ibada safi na Yehova Mungu. Maneno yake yana matokeo sana, kwa maana mwanamke huyo anawasimulia watu wa jiji hilo, nao pia wanataka kumsikiliza Yesu.—Yohana 4:3-42.

4 Mitume wanaporudi, wana maoni gani kuhusu ushahidi wa pekee ambao Yesu anatoa? Hawachangamki hata kidogo. Wanashangaa kumwona Yesu akizungumza na mwanamke huyo, na inaonekana kwamba hawaongei na mwanamke huyo hata kidogo. Mwanamke huyo anapoondoka, wanamsihi Yesu tena na tena ale chakula ambacho wameleta. Hata hivyo, Yesu anawaambia: “Nina chakula ambacho hamkijui.” Wanashangaa! Mwanzoni, wanafikiri kwamba Yesu anazungumzia chakula cha kimwili. Kisha, anaeleza hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:32, 34) Hivyo, Yesu anawafundisha kwamba anaiona kazi yake kuu maishani kuwa jambo la maana kuliko kula. Anataka wawe na maoni hayohayo kuhusu kazi hiyo. Ni kazi gani hiyo?

5. Ni kazi gani kuu ambayo Yesu alifanya maishani, na tutachunguza nini katika sura hii?

5 Pindi moja Yesu alisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Yesu alitumwa kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wa Mungu.b Wafuasi wa Yesu leo wanafanya kazi hiyohiyo. Basi tuchunguze kwa nini Yesu alihubiri, habari alizohubiri, na jinsi alivyoiona kazi yake.

Kwa Nini Yesu Alihubiri?

6, 7. Yesu alitaka kila “mfundishaji wa watu wote” awe na maoni gani kuhusu kuwaeleza wengine habari njema? Toa mfano.

6 Acheni tuone jinsi Yesu alivyoziona kweli alizofundisha; kisha tutazungumzia maoni yake kuelekea watu aliowafundisha. Yesu alitumia mfano ulio wazi kuonyesha maoni yake kuhusu kueleza wengine kweli ambazo Yehova alimfundisha. Alisema hivi: “Kila mfundishaji wa watu wote, anapofundishwa kuhusiana na ufalme wa mbinguni, ni kama mtu, mwenye nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na vya zamani.” (Mathayo 13:52) Kwa nini mwenye nyumba katika mfano huo anatoa vitu katika hazina yake?

7 Kusudi la mwenye nyumba huyo si kuonyesha tu mali yake kama Mfalme Hezekia wa kale alivyofanya na kujiletea matatizo. (2 Wafalme 20:13-20) Basi, nia yake ni nini? Fikiria mfano huu: Tuseme umeenda kumtembelea mwalimu unayempenda nyumbani kwake. Anafungua kisanduku cha meza na kutoa barua mbili, moja imezeeka na kubadilika rangi, na nyingine ni ya karibuni. Alizipokea kutoka kwa baba yake, moja ilitumwa zamani sana mwalimu huyo alipokuwa kijana mdogo tu, na ile nyingine ilitumwa hivi karibuni. Kwa uchangamfu, anakueleza jinsi anavyothamini barua hizo na jinsi ambavyo mashauri yaliyomo yamebadili maisha yake na kwamba yanaweza kukusaidia. Ni wazi kwamba mwalimu huyo anathamini sana barua hizo. (Luka 6:45) Anakuonyesha barua hizo, si ili kujivuna au kujifaidi kwa njia fulani, bali ili kukufaidi na kukuonyesha kwamba ni zenye thamani.

8. Kwa nini tuna sababu nzuri ya kuziona kweli tunazojifunza katika Neno la Mungu kuwa hazina?

8 Yesu, Mwalimu Mkuu, alikuwa na nia hiyohiyo alipowaeleza wengine kweli kumhusu Mungu. Aliziona kweli hizo kuwa zenye thamani sana. Alizipenda, naye alitamani kuwaambia wengine. Alitaka “kila mfundishaji wa watu wote,” yaani, wafuasi wake wote, wawe na maoni kama yake. Je, tuna maoni kama hayo? Tuna sababu nzuri ya kupenda kila kweli tunayojifunza katika Neno la Mungu. Tunathamini kweli zenye thamani, iwe ni mafundisho ambayo tumeamini kwa muda mrefu au yale yaliyorekebishwa hivi karibuni. Kwa kuzungumza kwa uchangamfu na kuendelea kupenda mambo ambayo Yehova ametufundisha, tunaonyesha upendo huo, kama Yesu.

9. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu watu aliowafundisha? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuiga maoni yake kuelekea watu?

9 Kama tutakavyozungumzia kwa undani katika Sehemu ya 3, Yesu aliwapenda pia watu aliowafundisha. Ilitabiriwa kwamba Masihi “atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini.” (Zaburi 72:13) Kwa kweli, Yesu aliwahangaikia watu. Alihangaikia fikira na mitazamo yao; alihangaikia mizigo iliyowalemea na mambo yaliyowazuia wasielewe kweli. (Mathayo 11:28; 16:13; 23:13, 15) Kwa mfano, mkumbuke yule mwanamke Msamaria. Bila shaka, alivutiwa sana kwa kuwa Yesu alipendezwa naye. Utambuzi ambao Yesu alikuwa nao kuhusu maisha ya mwanamke huyo ulimchochea mwanamke huyo kumkubali kuwa nabii na kuwaambia wengine juu ya Yesu. (Yohana 4:16-19, 39) Ni kweli kwamba wafuasi wa Yesu leo hawawezi kusoma mioyo ya watu wanaowahubiria. Hata hivyo, tunaweza kupendezwa na watu kama Yesu alivyofanya; tunaweza kuwaonyesha kwamba tunawahangaikia; na tunaweza kuchagua maneno yatakayofaa mapendezi, matatizo, na mahitaji yao.

Habari Ambayo Yesu Alihubiri

10, 11. (a) Yesu alihubiri nini? (b) Kwa nini Ufalme wa Mungu ulihitajiwa?

10 Yesu alihubiri nini? Ikiwa ungetafuta jibu kwa kuchunguza mafundisho ya dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo, unaweza kukata kauli kwamba alitangaza injili fulani ya kijamii, yaani, kutumia kanuni za Kikristo ili kutatua matatizo ya kibinadamu. Au unaweza kufikiri kwamba aliunga mkono mabadiliko ya kisiasa au alikazia kwamba lazima kila mtu aokoke. Hata hivyo, kama tulivyoona, Yesu alisema hivi waziwazi: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu.” Hilo lilimaanisha nini?

11 Kumbuka, Yesu alikuwa mbinguni wakati Shetani alipotokeza shaka kwa mara ya kwanza kuhusu haki ya Yehova ya kutawala. Haikosi Yesu aliumia sana kumwona Baba yake mwadilifu akichongewa na kushtakiwa kuwa Mtawala asiyetenda kwa haki, ambaye anawanyima viumbe Wake mema! Lazima Mwana wa Mungu alihuzunika sana wakati Adamu na Hawa, waliokuja kuwa wazazi wa wanadamu wote, walipouamini uchongezi wa Shetani! Mwana huyo aliona kwamba familia ya wanadamu imerithi dhambi na kifo kwa sababu ya uasi huo. (Waroma 5:12) Ingawa hivyo, alifurahi kama nini kujua kwamba siku moja Baba yake atanyoosha mambo!

12, 13. Ufalme wa Mungu utaondoa mambo gani yasiyo ya haki, na Yesu alionyesha jinsi gani kwamba Ufalme ndicho kilichokuwa kichwa kikuu cha mahubiri yake?

12 Ni suala gani kuu lililohitaji kutatuliwa? Jina takatifu la Yehova lilihitaji kutakaswa, kuondolewa shutuma zote za Shetani na wote wanaomuunga mkono. Haki ya enzi kuu ya Yehova, njia yake ya kutawala, ilihitaji kutetewa. Yesu alielewa masuala hayo kuliko mwanadamu mwingine yeyote. Katika sala ya mfano, aliwafundisha wafuasi wake waombe kwanza jina la Baba yake litakaswe, kisha Ufalme wa Baba yake uje, halafu mapenzi ya Mungu yatendeke duniani. (Mathayo 6:9, 10) Hivi karibuni Ufalme wa Mungu, Kristo Yesu akiwa Mtawala, utaondolea mbali mfumo mfisadi wa Shetani na kuthibitisha utawala wenye uadilifu wa Yehova.—Danieli 2:44.

13 Ufalme huo ulikuwa kichwa kikuu cha huduma ya Yesu. Maneno yake yote na matendo yake yote yalionyesha wazi maana ya Ufalme huo na jinsi utakavyotimiza kusudi la Yehova. Yesu hakuruhusu jambo lolote limkengeushe aache kazi yake ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wakati huo, kulikuwa na matatizo ya kijamii na ukosefu mwingi wa haki, lakini alikazia fikira habari aliyohubiri na kazi yake. Kwa kuwa Yesu aliendelea kukazia fikira mambo hayo, je, hilo linamaanisha kwamba alikuwa na maoni finyu na kwamba alifundisha kwa njia isiyovutia na yenye kuwachosha watu? Sivyo hata kidogo!

14, 15. (a) Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “mkuu kuliko Sulemani”? (b) Tunaweza kumwiga Yesu kwa njia gani tunapohubiri?

14 Kama tutakavyoona katika sehemu hii yote, Yesu alifanya mafundisho yake yavutie na yapendeze. Maneno yake yaligusa mioyo ya watu. Huenda hilo likatukumbusha Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyetafuta maneno yenye kupendeza na maneno sahihi ya kweli ili kueleza mambo ambayo Yehova alimwongoza kuyaandika. (Mhubiri 12:10) Yehova alimpa mtu huyo asiye mkamilifu “ukunjufu wa moyo” uliomwezesha kuzungumza kuhusu mambo mengi, kutia ndani ndege, samaki, miti, na wanyama. Watu walitoka mbali kumsikia Sulemani akizungumza. (1 Wafalme 4:29-34) Hata hivyo, Yesu alikuwa “mkuu kuliko Sulemani.” (Mathayo 12:42) Alimzidi Sulemani kwa hekima na “ukunjufu wa moyo.” Yesu alipokuwa akiwafundisha watu, alitumia ujuzi wake mwingi wa Neno la Mungu na vilevile mambo mengi aliyojua kuhusu ndege, wanyama, samaki, ukulima, hali ya hewa, matukio ya karibuni, historia, na hali za kijamii. Lakini Yesu hakutumia ujuzi wake kujionyesha. Ujumbe wake ulikuwa rahisi na wazi. Haishangazi kwamba watu walifurahia kusikia akizungumza!—Marko 12:37; Luka 19:48.

15 Leo, Wakristo wanajaribu kufuata mfano wa Yesu. Hatuna hekima na ujuzi mwingi kama wake, lakini sisi sote tuna kiasi fulani cha ujuzi na uzoefu ambao tunaweza kutumia tunapowafundisha wengine kweli za Neno la Mungu. Kwa mfano, wazazi wanaweza kutumia uzoefu wao wa kuwalea watoto kuonyesha kwamba Yehova anawapenda watoto Wake. Wengine wanaweza kutumia mifano kutokana na kazi yao ya kimwili, shule, au ujuzi wao kuhusu watu na matukio ya karibuni. Wakati huohuo, tunaepuka jambo lolote linaloweza kuwakengeusha watu wasisikilize habari njema ya Ufalme wa Mungu.—1 Timotheo 4:16.

Jinsi Yesu Alivyoiona Huduma Yake

16, 17. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu huduma yake? (b) Ni kwa njia gani Yesu alionyesha kwamba jambo kuu maishani mwake lilikuwa huduma yake?

16 Yesu aliiona huduma yake kuwa hazina yenye thamani. Alifurahia kuwasaidia watu wamjue Baba yake wa mbinguni vizuri, bila kuwavuruga akili kwa mafundisho na mapokeo ya wanadamu. Yesu alipenda kuwasaidia watu wawe na uhusiano mzuri pamoja na Yehova na wawe na tumaini la uzima wa milele. Alipenda kuwapelekea watu habari njema yenye kufariji na kuchangamsha moyo. Ni nini kinachoonyesha hilo? Ona njia tatu.

17 Kwanza, Yesu alifanya huduma kuwa jambo kuu maishani mwake. Kazi yake kuu maishani ilikuwa kuzungumza kuhusu Ufalme. Hiyo ndiyo sababu Yesu alitenda kwa hekima kwa kuishi maisha rahisi, kama tulivyoona katika Sura ya 5. Kama alivyowashauri wengine, alikazia fikira jambo la maana zaidi. Hakukengeushwa na vitu vingi ambavyo angehitaji kulipia, kutunza, kurekebisha, au kubadili baada ya muda. Aliishi maisha rahisi ili asikengeushwe kutoka kwa huduma yake.—Mathayo 6:22; 8:20.

18. Ni katika njia gani Yesu alijitoa kabisa kutimiza huduma yake?

18 Pili, Yesu alijitoa kabisa kutimiza huduma yake. Alitumia nguvu nyingi katika huduma, akitembea kilomita nyingi nchini Palestina, huku akitafuta watu ambao angeweza kuwahubiria habari njema. Alizungumza nao nyumbani mwao, katika viwanja vya watu wote, sokoni, na mahali palipokuwa na watu wengi. Alizungumza nao hata alipohitaji kupumzika, kula, kunywa maji, au kustarehe pamoja na rafiki zake wa karibu. Hata alipokuwa akifa, aliendelea kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu!—Luka 23:39-43.

19, 20. Ni kwa njia gani Yesu alionyesha kwamba kazi ya kuhubiri inahitaji kufanywa haraka?

19 Tatu, Yesu aliona kwamba huduma yake ilipaswa kufanywa haraka. Kumbuka alipozungumza na yule mwanamke Msamaria kwenye kisima nje ya jiji la Sikari. Inaonekana kwamba mitume wa Yesu hawakuona uharaka wa kuwaeleza wengine habari njema katika pindi hiyo. Yesu aliwaambia hivi: “Je, ninyi hamsemi kwamba bado kuna miezi minne kabla ya mavuno kuja? Tazama! Ninawaambia ninyi: Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.”—Yohana 4:35.

20 Mfano huo wa Yesu ulitegemea majira ya wakati huo. Inaonekana kwamba ulikuwa mwezi wa Kislevu unaolingana na Novemba/Desemba (Mwezi wa 11/Mwezi wa 12). Shayiri ingevunwa miezi minne baadaye, karibu na wakati wa Pasaka, Nisani 14. Kwa hiyo, wakulima hawakuona uharaka wa kuvuna wakati huo. Bado kulikuwa na wakati wa kutosha. Namna gani kukusanywa kwa watu? Wengi walikuwa tayari kusikia, kujifunza, kuwa wanafunzi wa Kristo na kuwa na tumaini zuri ajabu ambalo Yehova aliwaahidi. Ni kana kwamba Yesu alitazama mashamba hayo ya mfano na kuyaona kuwa meupe huku nafaka zilizoiva zikipeperushwa na upepo mwanana, kuonyesha ziko tayari kuvunwa.c Wakati wa mavuno ulikuwa umefika, nayo kazi hiyo ilipaswa kufanywa haraka! Hiyo ndiyo sababu wakati watu wa jiji fulani walipotaka Yesu aendelee kukaa kwao, alisema hivi: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.”—Luka 4:43.

21. Tunaweza kumwiga Yesu kwa njia gani?

21 Tunaweza kumwiga Yesu katika njia zote tatu ambazo tumezungumzia. Tunaweza kufanya huduma ya Kikristo iwe jambo kuu maishani mwetu. Hata ingawa labda tuna madaraka ya familia na shughuli nyinginezo za maisha, tunaweza kuonyesha kwamba tunatanguliza huduma yetu kwa kuifanya kwa bidii na kwa ukawaida kama Yesu. (Mathayo 6:33; 1 Timotheo 5:8) Tunaweza kujitoa kabisa katika huduma, tukitumia wakati, nguvu, na mali yetu ili kuitimiza. (Luka 13:24) Nasi tunaweza kukumbuka sikuzote kwamba kazi yetu inahitaji kufanywa haraka. (2 Timotheo 4:2) Tunahitaji kutumia kila nafasi kuhubiri!

22. Ni nini kitakachozungumziwa katika sura inayofuata?

22 Pia, Yesu alionyesha kwamba anatambua kuwa kazi hiyo inahitaji kufanywa haraka kwa kuhakikisha ingeendelea baada ya kifo chake. Aliwaagiza wafuasi wake wafanye kazi ya kuhubiri na kufundisha. Kazi hiyo itazungumziwa katika sura inayofuata.

a Kwa mfano, mwanamke huyo anapotaka kujua kwa nini Myahudi anazungumza na Msamaria, anataja ugomvi ambao umekuwako kwa karne nyingi kati ya watu wa jamii hizo mbili. (Yohana 4:9) Pia, anakazia kwamba wao ni wazao wa Yakobo, jambo ambalo Wayahudi wa wakati huo wanapinga vikali. (Yohana 4:12) Wayahudi wanawaita Wasamaria, Wakutha, ili kukazia kwamba wametokana na jamii ya kigeni.

b Kuhubiri ni kutangaza au kueneza habari fulani. Kufundisha kuna maana hiyo pia, lakini kunatia ndani kueleza habari kwa mapana na marefu. Kufundisha kuzuri kunahusisha kutafuta njia za kufikia mioyo ili kuwachochea wanafunzi kutenda mambo wanayosikia.

c Kuhusiana na mstari huo, kitabu kimoja kinasema: “Nafaka zinapoiva, rangi yake ya kijani hubadilika kuwa manjano, kuonyesha kwamba ziko tayari kuvunwa.”

Unaweza Kumfuata Yesu Jinsi Gani?

  • Sala na matendo yetu yanaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunaelewa kuwa tunahitaji kutimiza huduma yetu haraka?—Mathayo 9:35-38.

  • Tukitambua kwamba bidii yetu katika huduma inapungua, kuwa na maoni kama ya Yesu kutatuchochea jinsi gani?—Marko 1:35-39.

  • Tunapohubiri, tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu watu wa hali ya chini, walioonewa, au wanaodharauliwa?—Luka 18:35–19:10.

  • Kwa nini hatupaswi kupunguza bidii yetu watu wasipopendezwa au wanapotupinga kwa ukali?—Yohana 7:32-52.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki