SURA YA 25
Ninaweza Kuwa na Furaha Katika Familia ya Mzazi Mmoja?
“Watoto katika familia zilizo na wazazi wawili wana vyumba vya kulala nao hununua nguo mpya. Lakini mimi sina chumba changu mwenyewe; nami sina nguo ninazotaka. Mama husema kwamba hana pesa. Kwa kuwa mimi hufanya kazi nyingi nyumbani mama akiwa kazini, mimi hujiona kama mfanyakazi wa nyumbani—badala ya kuwa nikifurahia maisha kama watoto wengine.”—Shalonda, mwenye umri wa miaka 13.
BILA shaka, familia ilikusudiwa iwe na wazazi wawili. Baba na mama, wakiwa pamoja, wanaweza kutoa mwongozo, ulinzi, na utegemezo. “Wawili ni bora kuliko mmoja,” yasema Biblia, “kwa sababu wakiwa pamoja waweza kufanya kazi kwa matokeo zaidi.”—Mhubiri 4:9, Today’s English Version.
Hata hivyo, familia za wazazi wawili leo ni kama wanyama walio katika hatari ya kutoweka. Kwa mfano, zaidi ya nusu ya watoto nchini Marekani, wataishi angalau kwa muda fulani na mzazi mmoja kabla ya kufikia umri wa miaka 18.
Ijapokuwa kuna familia nyingi za mzazi mmoja, bado vijana wengi walio katika familia hizo huaibikia hali yao. Wengine hulemewa na mikazo na matatizo yanayowapata. Ikiwa familia yenu ni ya mzazi mmoja, ni mikazo gani unayopata? Kwenye nafasi iliyo hapa chini, andiko tatizo linalokusumbua zaidi.
․․․․․
Kwa kuwa hupati upendo na utunzaji wa yule mzazi mwingine, je, inamaanisha kwamba hutawahi kuwa na furaha maishani? Sivyo hata kidogo! Mengi yanategemea maoni yako. Andiko la Methali 15:15 linasema: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” Kama methali hiyo inavyodokeza, mara nyingi hali ya moyoni ya mtu inategemea mtazamo wake bali si hali zake maishani. Unaweza kufanya nini ili uwe “mchangamfu moyoni” licha ya hali zako maishani?
Ondolea Mbali Hisia Zisizofaa
Kwanza, jaribu kutoruhusu mambo ambayo wengine wanasema yakufanye uvunjike moyo. Kwa mfano, walimu fulani husema bila kufikiri mambo yenye kuvunja moyo kuhusu wanafunzi kutoka katika familia ya mzazi mmoja. Wengine hata huamini kwamba tabia yoyote mbaya inatokana na malezi mabaya. Lakini jiulize: ‘Je, wanaosema mambo hayo wananijua vizuri mimi na familia yetu? Au wanaropoka tu mambo ambayo wamesikia wengine wakisema kuhusu familia za mzazi mmoja?’
Kumbuka kwamba maneno “mvulana asiye na baba” yanapatikana mara nyingi katika Maandiko. Maneno hayo hayatumiwi kamwe kwa njia yenye kushusha heshima. Katika karibu masimulizi yote hayo, Yehova anaonyesha hangaiko la pekee kuelekea watoto wanaolelewa katika familia ya mzazi mmoja.a
Kwa upande mwingine huenda watu ambao hawana nia mbaya wakawa waangalifu kupita kiasi wanapozungumza na wewe. Kwa mfano, huenda wakaepuka kutumia maneno kama vile “baba,” “ndoa,” “talaka,” au “kifo,” wakiogopa kwamba maneno hayo huenda yakakuudhi au kukuaibisha. Je, mambo kama hayo yanakusumbua? Ikiwa ndivyo, basi waambie kwa busara kwamba hawahitaji kuwa waangalifu kupita kiasi wanapozungumza nawe. Tony mwenye umri wa miaka 14, hakumjua baba yake mzazi. Anasema kwamba watu fulani husita kutumia maneno fulani wanapozungumza naye. Hata hivyo, Tony mwenyewe huyatumia maneno hayo anapozungumza nao. Anasema: “Ninataka wajue kwamba sionei aibu hali yangu.”
Epuka Kusema “Laiti”
Ni kawaida kuhuzunika na kusononeka ikiwa wazazi wako wametalikiana au mzazi wako mpendwa anapokufa. Hata hivyo, mwishowe unahitaji kukubali ukweli wa mambo. Biblia inatoa shauri hili: “Usiseme: ‘Kwa nini siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’” (Mhubiri 7:10) Kuhusiana na hilo, Sarah mwenye umri wa miaka 13, ambaye wazazi wake walitalikiana alipokuwa na miaka 10, anapendekeza hivi: “Usisononeke daima, huku ukisema ‘laiti,’ au kuhisi una matatizo kwa sababu unatoka katika familia ya mzazi mmoja, au kwamba watoto wengine walio na wazazi wote wawili wanaishi raha mustarehe.” Hilo ni shauri zuri. Kwa kuwa, hata familia za wazazi wawili zina matatizo yake pia.
Kwa nini usiione familia yenu kama timu ya wapiga-makasia katika mashua? Ni kweli kwamba mashua inahitaji idadi kamili ya wapiga-makasia. Katika familia ya mzazi mmoja, mmoja wa wapiga-makasia anakosekana, kwa hiyo, waliobaki wanahitaji kufanya kazi kwa bidii zaidi. Je, inamaanisha kwamba familia hiyo haiwezi kufaulu? Hapana! Waliobaki wakishirikiana pamoja, mashua hiyo inaweza kuendelea kuelea mpaka mwisho wa safari.
Je, Unatimiza Sehemu Yako?
Ni nini hasa unachoweza kufanya ili kuhakikisha kwamba, pamoja na wengine katika familia yenu, unatimiza sehemu yako? Fikiria madokezo matatu yafuatayo:
Jifunze kutumia pesa kwa uangalifu. Familia nyingi za mzazi mmoja zina matatizo ya pesa. Unaweza kufanya nini ili kusaidia? Tony, aliyetajwa mapema, anasema: “Watoto shuleni kwetu huwalazimisha wazazi wao wawanunulie viatu na nguo za bei ghali. Ama sivyo, hawaendi shuleni. Sina nguo za bei ghali, hata hivyo, nguo zangu ni nadhifu na safi, nami huzitunza vizuri. Mama yangu anafanya kila awezalo; singependa kufanya maisha yawe magumu kwake.” Ukiongeza bidii, unaweza kumwiga mtume Paulo, aliyesema: “Nimejifunza kuridhika na vitu nilivyo navyo. . . . Nimejizoeza kuridhika katika kila hali na mahali.”—Wafilipi 4:11, 12, BHN.
Njia nyingine ya kutumia pesa kwa uangalifu ni kutumia kwa hekima vitu ulivyo navyo. (Yohana 6:12) Kijana Rodney anasema: “Mimi hujitahidi kuwa mwangalifu nisiharibu au kuvunja vitu nyumbani, kwa kuwa pesa zitahitajika ili kuvirekebisha au kununua vingine. Mimi huzima umeme iwapo hautumiki. Hilo hupunguza gharama ya umeme tunaotumia.”
Chukua hatua. Wazazi wengi katika familia ya mzazi mmoja huogopa kuweka sheria za nyumbani au kuwaomba watoto wao wasaidie kufanya kazi za nyumbani. Kwa nini? Wengine huhisi kwamba wanahitaji kujazia nafasi ya mzazi ambaye hayuko kwa kutowalemea watoto wao kwa kuwapa kazi nyingi. Huenda wakasema: ‘Ninataka watoto wangu wafurahie maisha kama watoto wengine.’
Kwa hiyo, huenda ukafurahia hali hiyo na kuketi kitako tu. Lakini kufanya hivyo ni kumwongezea mzigo mzazi wako. Mbona usijitolee kusaidia katika kazi za nyumbani? Ona kile ambacho Tony alijitolea kufanya. Anasema: “Mama yangu anafanya kazi hospitalini na nguo zake za kazi zinahitaji kupigwa pasi. Hivyo, mimi humpigia pasi.” Je, hiyo si kazi ya wanawake? “Wengine wanafikiri hivyo,” anasema Tony. “Lakini ninamsaidia mama yangu, kwa hiyo mimi huifanya.”
Onyesha shukrani. Mbali na kusaidia, unaweza pia kumtia moyo mzazi wako kwa kumshukuru. Mzazi mmoja asiye na mwenzi aliandika: “Mara nyingi, ninapokuwa nimevunjika moyo au kuudhika kwa sababu ya tatizo fulani kazini—ninaporudi nyumbani, ninakuta binti yangu amepanga meza na kuanza kutayarisha chakula cha jioni.” Kisha anaongeza: “Mwanangu hunikumbatia.” Anahisije? Anasema: “Ninakuwa na furaha tena.”
Andika hapa mambo unayohitaji kufanyia kazi kati ya madokezo hayo matatu. ․․․․․
Kuishi katika familia ya mzazi mmoja kunakupa nafasi ya kukuza sifa kama vile huruma, ukarimu, na kutegemeka. Pia, Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Nawe utakuwa na furaha kubwa zaidi ukijitolea kumsaidia mzazi wako.
Ni kweli kwamba mara kwa mara huenda ukatamani kwamba yule mzazi mwingine angekuwako. Hata hivyo, unaweza kujifunza kufanya yote uwezayo katika hali zako. Ndivyo alivyoona msichana anayeitwa Nia. Anasema: “Baada ya baba yangu kufa, mtu fulani aliniambia ‘maisha yako hayategemei hali zako bali hutegemea mtazamo wako,’ na mpaka leo nakumbuka maneno yake. Yananikumbusha kwamba naweza kuwa na furaha licha ya hali zangu.” Unaweza kuwa na mtazamo kama huo. Kumbuka kwamba si hali zako zinazofanya uwe na furaha bali ni maoni yako na jinsi unavyotenda ukiwa katika hali hizo.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 4
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, ona Kumbukumbu la Torati 24:19-21 na Zaburi 68:5.
MAANDIKO MUHIMU
“Pasiwe na mtu anayetafuta faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake.”—Wafilipi 2:4, BHN.
PENDEKEZO
Ikiwa unaona kwamba una majukumu mengi kupita uwezo wako, mweleze mzazi wako kwa busara ajaribu mambo yafuatayo:
● Atengeneze orodha inayoonyesha kazi zote ambazo kila mmoja katika familia anapaswa kufanya.
● Ikihitajika, wengine wenye uwezo katika familia wanaweza kugawiwa kazi zinazowalemea washiriki fulani.
JE, WAJUA . . .?
Kutimiza majukumu mbalimbali nyumbani kunaweza kukusaidia kukomaa haraka kuliko watoto walio katika familia zenye wazazi wawili ambao mara nyingi hawapewi majukumu yoyote.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nitazuia hisia zisizofaa kwa ․․․․․
Ikiwa watu ninaochangamana nao huumia hisia kwa urahisi, nitasema ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini watu fulani huwabagua watoto wanaotoka katika familia za mzazi mmoja?
● Kwa nini huenda wazazi wako wakasita kukuomba usaidie kufanya kazi fulani za nyumbani?
● Unaweza kumwonyesha jinsi gani mzazi wako kwamba unamthamini?
Blabu katika ukurasa wa 211]
‘‘Tangu wazazi wangu watalikiane, mimi na mama hupata muda mwingi wa kuzungumza; tumekuwa na uhusiano wa karibu sana.’’—Melanie
[Picha katika ukurasa wa 210, 211]
Familia ya mzazi mmoja ni kama mashua inayokosa mmoja wa wapiga-makasia—wale wengine watalazimika kuongeza bidii, hata hivyo, wanaweza kufanikiwa wakifanya kazi bega kwa bega