Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 3 kur. 21-27
  • “Wakajazwa Roho Takatifu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Wakajazwa Roho Takatifu”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Walikuwa Pamoja Mahali Palepale” (Mdo. 2:1-4)
  • “Kila Mmoja Wao Aliwasikia . . . Katika Lugha Yake Mwenyewe” (Mdo. 2:5-13)
  • “Petro Akasimama” (Mdo. 2:14-37)
  • “Kila Mmoja Wenu Abatizwe” (Mdo. 2:38-47)
  • Petro Ahubiri Wakati wa Pentekoste
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Ukristo Waenea Miongoni mwa Wayahudi wa Karne Ya Kwanza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Mashahidi wa Kikristo wa Yehova Katika Karne ya Kwanza
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 3 kur. 21-27

SURA YA 3

“Wakajazwa Roho Takatifu”

Matokeo ya kumiminwa kwa roho takatifu siku ya Pentekoste

Matendo 2:1-47

1. Eleza hali ilivyokuwa wakati wa Sherehe ya Pentekoste.

KUNA msisimuko mwingi katika jiji la Yerusalemu.a Moshi unapaa kutoka katika madhabahu ya hekalu huku Walawi wakiimba Haleli (Zaburi 113 hadi 118). Huenda kikundi kimoja kiliimba huku kingine kikiitikia. Kuna watu wengi barabarani. Wametoka sehemu za mbali sana kama vile Elamu, Mesopotamia, Kapadokia, Ponto, Misri, na Roma.b Wamekuja kwa kusudi gani? Ili kusherehekea Pentekoste, ambayo pia inaitwa “siku ya mavuno ya kwanza yaliyokomaa.” (Hes. 28:26) Sherehe hii hufanywa mara moja kila mwaka mwishoni mwa mavuno ya shayiri, kabla ya mavuno ya ngano kuanza. Ni siku ya shangwe sana.

Ramani inayoonyesha maeneo waliyotoka wale waliohubiriwa habari njema katika Pentekoste 33 W.K. 1. Mikoa: Libya, Misri, Ethiopia, Bithinia, Ponto, Kapadokia, Yudea, Mesopotamia, Babilonia, Elamu, Umedi, na Parthia. 2. Miji: Roma, Aleksandria, Memfisi, Antiokia (ya Siria), Yerusalemu, na Babiloni. 3. Bahari: Bahari ya Mediterania, Bahari Nyeusi, Bahari Nyekundu, Bahari ya Kaspian, na Ghuba ya Uajemi.

YERUSALEMU—CHIMBUKO LA DINI YA KIYAHUDI

Mambo mengi yanayotajwa katika sura za mwanzoni za kitabu cha Matendo yanatendeka Yerusalemu. Jiji hilo liko kwenye milima ya Yudea, kilomita 55 hivi upande wa mashariki mwa Bahari ya Mediterania. Katika mwaka wa 1070 K.W.K., Mfalme Daudi alishambulia na kuteka ngome iliyokuwa juu ya Mlima Sayuni, nalo jiji hilo ambalo lilizunguka mlima huo likaja kuwa jiji kuu la taifa la kale la Israeli.

Karibu na Mlima Sayuni, kuna Mlima Moria, ambao kulingana na mapokeo ya Wayahudi, Abrahamu alijaribu kumtoa Isaka kuwa dhabihu, miaka 1,900 hivi kabla ya matukio yanayosimuliwa katika kitabu cha Matendo. Mlima Moria ulikuja kuwa sehemu ya jiji hilo, Sulemani alipojenga hekalu la kwanza la Yehova juu ya mlima huo. Hekalu hilo likawa kituo cha ibada na shughuli mbalimbali za Wayahudi.

Wayahudi waliomwogopa Mungu kutoka sehemu mbalimbali duniani walikwenda katika hekalu la Yehova ili kutoa dhabihu, kuabudu, na kuadhimisha sherehe za kila mwaka. Walikuwa wakitii amri hii ya Mungu: “Mara tatu kwa mwaka, wanaume wenu wote wanapaswa kwenda mbele za Yehova Mungu wenu mahali atakapochagua.” (Kum. 16:16) Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi iliyokuwa pia baraza lililosimamia mambo ya kitaifa, ilikuwa katika jiji hilo la Yerusalemu.

2. Ni mambo gani yenye kushangaza yanayotokea siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K.?

2 Saa tatu hivi asubuhi, mwaka wa 33 W.K., jambo fulani la ajabu latokea, ambalo litawashangaza watu kwa karne nyingi zijayo. Ghafla kukatokea “kelele kutoka mbinguni, kama ya upepo wenye nguvu unaovuma.” (Mdo 2:2) Mvumo huo waijaza nyumba ambapo wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikuwa wamekusanyika. Kisha, jambo la kushangaza latokea. Ndimi, kama za moto, zaonekana. Wanafunzi hao wakaona ndimi kama za moto zikitua juu ya kila mmoja wao.c Ndipo, wanafunzi hao ‘wakajazwa roho takatifu’ na kuanza kusema katika lugha mbalimbali! Wanafunzi wanapotoka tu katika nyumba hiyo, watu kutoka sehemu mbalimbali walio katika barabara za Yerusalemu wanashangaa sana! Kila mtu anawasikia wanafunzi hao “wakiongea katika lugha yake mwenyewe.”​—Mdo. 2:1-6.

3. (a) Kwa nini Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. inaweza kuitwa tukio muhimu sana katika ibada ya kweli? (b) Kuna uhusiano gani kati ya hotuba ya Petro na zile “funguo za Ufalme”?

3 Masimulizi hayo yenye kusisimua yanahusu tukio muhimu sana katika ibada ya kweli—kuanzishwa kwa taifa la Israeli la kiroho, kutaniko la Wakristo watiwa mafuta. (Gal. 6:16) Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika. Petro anapotoa hotuba yake mbele ya umati uliokusanyika siku hiyo, anatumia ufunguo wa kwanza kati ya zile ‘funguo tatu za Ufalme.’ Kila moja ya funguo hizo ingefungulia kikundi fulani cha watu mapendeleo ya pekee. (Mt. 16:18, 19) Ufunguo huo wa kwanza uliwawezesha Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani kukubali habari njema na kutiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu.d Wangeweza kuwa sehemu ya Israeli la kiroho, na hivyo, kuwa na tumaini la kutawala wakiwa wafalme na makuhani katika Ufalme wa Kimasihi. (Ufu. 5:9, 10) Kisha, Wasamaria na baadaye watu wa mataifa wangepata pendeleo hilo pia. Leo, Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo muhimu ya siku ya Pentekoste?

“Walikuwa Pamoja Mahali Palepale” (Mdo. 2:1-4)

4. Eleza jinsi kutaniko la Kikristo lilivyoanza na kuendelea mpaka leo hii.

4 Kutaniko la kwanza la Kikristo lilianza likiwa na wanafunzi 120 hivi ambao “walikuwa pamoja mahali palepale,” katika chumba cha juu. Wote walikuwa wametiwa mafuta na roho takatifu. (Mdo. 2:1) Kufikia mwishoni mwa siku hiyo, washiriki waliobatizwa wa kutaniko hilo walikuwa elfu kadhaa. Huo ulikuwa mwanzo tu wa tengenezo ambalo linaendelea kukua hadi leo! Katika kutaniko la Kikristo leo, wanaume na wanawake wanaomwogopa Mungu, wanahubiri “habari njema ya Ufalme” katika “dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote” kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo.​—Mt. 24:14.

5. Ni baraka gani zinazotokana na kushirikiana na kutaniko la Kikristo?

5 Kutaniko la Kikristo lingewaimarisha kiroho washiriki wake, watiwa mafuta, na baadaye “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Paulo alithamini jinsi washiriki wa kutaniko wanavyotegemezana alipowaandikia Wakristo huko Roma: “Ninatamani kuwaona ninyi ili niwape zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au badala yake, tutiane moyo, kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia.”​—Rom. 1:11, 12.

Roma—jiji Kuu La Milki Ya Roma

Kipindi ambacho kinazungumziwa katika kitabu cha Matendo, Roma lilikuwa jiji kubwa zaidi na muhimu kisiasa katika ulimwengu wa wakati huo. Lilikuwa jiji kuu la milki ambayo wakati huo ilitawala nchi nyingi kuanzia Uingereza mpaka Afrika Kaskazini na toka Bahari ya Atlantiki mpaka Ghuba ya Uajemi.

Katika jiji la Roma kulikuwa na tamaduni, jamii, lugha, na ushirikina kutoka nchi mbalimbali. Kwa kuwa kulikuwa na barabara nzuri, jiji hilo lilipata wageni wengi na bidhaa nyingi kutoka katika kila pembe ya milki hiyo. Meli za biashara zilizokuwa na shehena ya vyakula na bidhaa nyingine za starehe zilitia nanga katika bandari ya Ostia na kupakua shehena hizo.

Kufikia karne ya kwanza W.K., zaidi ya watu milioni moja walikuwa wakiishi Roma. Huenda nusu yao walikuwa watumwa—wahalifu, watoto waliouzwa au kuachwa na wazazi wao, na wafungwa waliotekwa nyara na majeshi ya Roma. Baadhi ya watu walioletwa Roma wakiwa watumwa walikuwa Wayahudi kutoka Yerusalemu waliokamatwa baada ya jiji lao kushindwa vitani na Jenerali Mroma, Pompey, mwaka wa 63 K.W.K.

Wengi kati ya wale ambao hawakuwa watumwa walikuwa maskini sana na waliishi katika nyumba za ghorofa zilizojengwa kwa ajili ya maskini waliotegemea misaada kutoka serikalini. Hata hivyo, watawala wa milki hiyo walijenga majengo ya kifahari na ya kipekee sana yaliyofanya jiji hilo liwe lenye kupendeza. Baadhi ya majengo hayo ni yale majumba ya maonyesho na viwanja vya michezo. Majengo hayo yalitumiwa kwa ajili ya tamasha, mapigano yenye jeuri, na mashindano ya magari ya farasi ili kuwatumbuiza wakaaji wa Roma bila malipo yoyote.

6, 7. Kutaniko la Kikristo leo linatimizaje kazi ya kuwahubiria watu wa mataifa yote?

6 Leo, kutaniko la Kikristo linatimiza mambo yaleyale yaliyotimizwa na kutaniko la karne ya kwanza. Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi yenye kusisimua licha ya upinzani ambao wangepata. Aliwaagiza hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”​—Mt. 28:19, 20.

7 Yehova analitumia kutaniko la Kikristo kutimiza kazi hiyo leo. Si rahisi kuwahubiria watu wanaozungumza lugha tofauti. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wamechapisha machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 1,000. Ikiwa unahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na unashiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, una kila sababu ya kushangilia. Wewe ni mmoja wa watu wachache duniani ambao wana pendeleo la kutoa ushahidi kamili kuhusu jina la Yehova!

8. Kushirikiana na kutaniko la Kikristo kunatusaidiaje?

8 Ili kutusaidia kuendelea kuwa na shangwe katika nyakati hizi za hatari, Yehova Mungu ametupatia ushirika wa ulimwenguni pote wa akina ndugu. Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Yehova ameandaa kutaniko la Kikristo ili tutiane moyo. Shirikiana kwa ukaribu pamoja na ndugu na dada zako wa kiroho. Usiache kamwe kuhudhuria mikutano ya Kikristo!

“Kila Mmoja Wao Aliwasikia . . . Katika Lugha Yake Mwenyewe” (Mdo. 2:5-13)

Wanafunzi wa Yesu wakiwahubiria Wayahudi na wageuzwa imani kwenye mtaa wenye shughuli nyingi.

“Tunawasikia wakisema katika lugha zetu kuhusu mambo makuu ya Mungu.”—Matendo 2:11

9, 10. Wahubiri fulani wamefanya jitihada gani ili kuwahubiria watu wanaozungumza lugha nyingine?

9 Wazia msisimuko waliokuwa nao Wayahudi na wageuzwa imani katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Yaelekea wengi wao walijua Kigiriki au Kiebrania, lugha kuu za wakati huo. Lakini sasa “kila mmoja wao aliwasikia [wanafunzi] wakiongea katika lugha yake mwenyewe.” (Mdo. 2:6) Bila shaka hisia za watu hao zilichochewa sana waliposikia habari njema katika lugha zao wenyewe. Ijapokuwa Wakristo leo hawana uwezo wa kimuujiza wa kuzungumza lugha za kigeni, wengi wamejitolea kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa watu wa mataifa yote. Wamefanya hivyo jinsi gani? Baadhi yao wamejifunza lugha nyingine ili watumikie katika kutaniko la lugha ya kigeni lililo karibu au hata kuhamia nchi nyingine. Mara nyingi wahubiri hao wameona kwamba watu huvutiwa sana wanapoona jinsi wanavyojitahidi kuzungumza lugha zao.

10 Kwa mfano, Christine na Mashahidi wengine saba walijifunza Kigujarati. Siku moja alimsalimu mfanyakazi mwenzake Mgujarati, kwa Kigujarati. Mwanamke huyo alivutiwa sana, akataka kujua kwa nini Christine anajifunza lugha ngumu kama Kigujarati. Christine alitumia nafasi hiyo kumhubiria. Mwanamke huyo alimwambia Christine: “Lazima ujumbe wenu ni wa muhimu sana.”

11. Tunawezaje kujitayarisha kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa watu wanaozungumza lugha nyingine?

11 Bila shaka, si kila mtu anayeweza kujifunza lugha nyingine. Hata hivyo, tunaweza kuwa tayari kuwahubiria watu wanaozungumza lugha nyingine. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kujifunza salamu rahisi katika lugha zinazotumiwa kwa ukawaida katika eneo lenu kwa kutumia programu ya JW Language®. Pia, unaweza kujifunza maneno machache ya lugha hiyo yatakayokusaidia kuchochea upendezi wa watu wanaozungumza lugha hiyo. Waelekeze kwenye tovuti ya jw.org, na unaweza kuwaonyesha video na machapisho mbalimbali yanayopatikana katika lugha yao. Kwa kutumia vifaa kama hivyo katika huduma yetu, tunaweza kupata shangwe kama ile waliyoipata ndugu katika karne ya kwanza, watu wa mataifa mbalimbali waliposhangaa kusikia habari njema “kila mmoja . . . katika lugha yake mwenyewe.”

Wayahudi Nchini Misri Na Mesopotamia

Kitabu fulani kinasema hivi: “Katika maeneo ya Mesopotamia, Umedi na Babilonia kulikuwa na watu waliotoka katika familia za ufalme wa makabila kumi [ya Israeli], na ufalme wa Yuda, waliohamishiwa huko na Wasiria na Wababiloni.” (The History of the Jewish People in the Age of Jesus Christ—175 B.C.–A.D. 135) Kulingana na Ezra 2:64, Waisraeli waliorudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. kutoka uhamishoni Babiloni walikuwa 42,360. Flavio Yosefu anasema kwamba katika karne ya kwanza W.K., idadi ya Wayahudi waliokuwa “wakiishi Babilonia” ilikuwa makumi ya maelfu. Katika karne ya tatu mpaka ya tano W.K., jamii hizo ziliandika kitabu kinachoitwa Talmud ya Babiloni.

Kuna hati zinazothibitisha kwamba Wayahudi waliishi Misri angalau kuanzia karne ya sita K.W.K. Wakati huo Yeremia alituma ujumbe kwa Wayahudi walioishi katika sehemu mbalimbali za Misri, kutia ndani Memfisi. (Yer. 44:1, maelezo ya chini) Kuna uwezekano kwamba watu wengi walihamia Misri wakati wa utawala wa Ugiriki. Mwanahistoria Yosefu anasema kwamba Wayahudi walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuishi Aleksandria. Baada ya muda, walimiliki sehemu kubwa ya jiji hilo. Katika karne ya kwanza W.K., Philo mwandishi Myahudi, alidai kwamba Wayahudi milioni moja hivi walikuwa wakiishi katika maeneo mbalimbali nchini Misri, “kuanzia Libya hadi Ethiopia.”

“Petro Akasimama” (Mdo. 2:14-37)

12. (a) Nabii Yoeli alirejelea matukio ya Pentekoste jinsi gani? (b) Kwa nini watu wa karne ya kwanza walitazamia utimizo wa unabii wa Yoeli?

12 “Petro akasimama” ili kuzungumza na umati huo wa watu kutoka mataifa mbalimbali. (Mdo. 2:14) Alieleza kwamba Mungu alikuwa amewapa uwezo wa kimuujiza wa kusema katika lugha mbalimbali ili kutimiza unabii wa Yoeli unaosema: “Nitaimimina roho yangu juu ya kila aina ya mwili.” (Yoe. 2:28) Kabla ya kurudi mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Nitamwomba Baba naye atawapa msaidizi mwingine.” Yesu alisema msaidizi huyo ni “roho.”​—Yoh. 14:16, 17.

13, 14. Petro alifanya nini ili kuichochea mioyo ya wasikilizaji wake, nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?

13 Petro alimalizia hotuba yake kwa maneno haya ya moja kwa moja: “Nyumba yote ya Israeli na ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo, Yesu huyu ambaye ninyi mlimuua kwenye mti.” (Mdo. 2:36) Ijapokuwa wengi kati ya watu waliokuwa wakimsikiliza Petro hawakuwapo Yesu alipouawa juu ya mti wa mateso, taifa lote lilikuwa na hatia. Hata hivyo, Petro alizungumza na Wayahudi wenzake kwa heshima naye alijali hisia zao. Kusudi la Petro lilikuwa kuwachochea wasikilizaji wake watubu bali si kuwashutumu. Je, umati uliokuwa ukimsikiliza ulikasirishwa na maneno ya Petro? Hapana. Badala yake, watu hao “walichomwa moyoni.” Wakauliza: “Tufanye nini?” Yaelekea njia ya Petro ya kuzungumza nao kwa heshima ilimsaidia kuifikia mioyo ya wengi, hata wakachochewa kutubu.​—Mdo. 2:37.

14 Sisi pia, tunaweza kufanya kama Petro. Tunapohubiri, hatuhitaji kupinga kila jambo lisilopatana na Maandiko ambalo huenda mwenye nyumba akasema. Badala yake, ingefaa kuzungumzia mambo tunayoweza kukubaliana. Tukishakubaliana na wasikilizaji wetu, kwa busara tunaweza kuwasaidia kuona maoni ya Neno la Mungu. Mara nyingi, kweli za Biblia zinapozungumziwa kwa njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu wanaweza kukubali ujumbe wetu.

Ukristo Katika Mkoa Wa Ponto

Kati ya watu waliosikiliza hotuba ya Petro siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walikuwa Wayahudi kutoka Ponto, wilaya iliyo kaskazini mwa Asia Ndogo. (Mdo. 2:9) Kwa kuwa wale ambao Petro aliwatumia barua yake ya kwanza walitia ndani waamini “waliotawanyika” katika mkoa wa Ponto, inaonekana kwamba baadhi ya Wayahudi walirudi na habari njema nyumbani kwao.g (1  Pet. 1:1) Aliandika kwamba Wakristo hao walikuwa ‘wamehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali’ kwa sababu ya imani yao. (1 Pet. 1:6) Huenda majaribu hayo yalitia ndani upinzani na mateso.

Majaribu mengine yaliyowapata Wakristo huko Ponto yanarejelewa kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika mawasiliano kati ya Plini Mdogo, aliyekuwa gavana wa jimbo la Bithinia na Ponto, na Maliki Trajani. Akiandika kutoka Ponto karibu mwaka wa 112 W.K., Plini alisema kwamba kila mtu, haidhuru jinsia yake, umri wake, au cheo chake angeweza “kuambukizwa” Ukristo. Plini aliwapa wale waliokuwa Wakristo nafasi ya kukana imani yao la sivyo, wauawe. Yeyote aliyemlaani Kristo au kusali kwa miungu au kwa sanamu ya Trajani, aliachiliwa huru. Plini alikiri kwamba hayo ni mambo ambayo “Wakristo wa kweli hawangeweza kufanya.”

g Maneno yanayotafsiriwa “waliotawanyika” ni tafsiri ya neno la Kigiriki Di·a·spo·raʹ linalorejelea Wayahudi waliokuwa wametawanyika katika mataifa mengine. Maneno hayo yanadokeza kwamba wengi wa wageuzwa imani wa kwanza walitoka katika jamii za Wayahudi.

“Kila Mmoja Wenu Abatizwe” (Mdo. 2:38-47)

15. (a) Petro alisema nini, na watu waliitikiaje? (b) Iliwezekanaje kwamba maelfu ya watu waliosikia habari njema walistahili kubatizwa siku hiyohiyo?

15 Katika siku hiyo yenye kusisimua ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Petro aliwaambia hivi Wayahudi na wageuzwa imani: “Tubuni, na kila mmoja wenu abatizwe.” (Mdo. 2:38) Kisha watu 3,000 hivi wakabatizwa, huenda katika vidimbwi vilivyokuwa Yerusalemu au karibu na jiji hilo.e Je, watu hao walichukua hatua hiyo bila kufikiri? Je, hilo linamaanisha kwamba wanafunzi wa Biblia na watoto ambao wazazi wao ni Wakristo wakimbilie kubatizwa kabla ya kuwa tayari? Hapana. Kumbuka, Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani waliobatizwa siku hiyo walikuwa wamejifunza Neno la Mungu, na taifa lao lilikuwa wakfu kwa Yehova. Isitoshe, tayari walikuwa na bidii, walikuwa wakifunga safari ndefu kwenda kuhudhuria sherehe hiyo ya kila mwaka. Baada ya kukubali kweli muhimu kuhusu jukumu la Yesu Kristo katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, walikuwa tayari kuendelea kumtumikia Mungu—lakini sasa wakiwa wafuasi waliobatizwa wa Kristo.

Wageuzwa Imani Ni Nani?

“Wayahudi na pia wageuzwa imani” walimsikiliza Petro akihubiri katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K.​—Matendo 2:10.

Nikolao ambaye alikuwa mmoja wa wanaume waliowekwa rasmi juu ya ‘kazi muhimu’ ya kugawa chakula kila siku, anatajwa kuwa “mgeuzwa-imani wa Antiokia.” (Matendo 6:3-5) Wageuzwa imani walikuwa watu wa mataifa mengine, wasio Wayahudi, ambao walijiunga na dini ya Kiyahudi. Walionwa kuwa Wayahudi, kwa sababu walimkubali Mungu wa Israeli na kuikubali Sheria ya Waisraeli, walikataa miungu mingine yote, (wanaume) walitahiriwa, nao walijiunga na taifa la Israeli.

Baada ya Wayahudi kutoka uhamishoni Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., wengi wao waliishi mbali na nchi ya Israeli lakini waliendelea kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi. Hivyo, watu wengi katika maeneo ya Mashariki ya Kati na hata mbali zaidi wakaifahamu dini ya Kiyahudi. Waandikaji wa zamani, kama vile, Horace na Seneca, wanaeleza kwamba watu wengi wa nchi mbalimbali waliovutiwa na Wayahudi na imani zao, walijiunga nao na kuwa wageuzwa imani.

16. Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha jinsi gani roho ya kujidhabihu?

16 Bila shaka, Yehova alibariki kikundi hicho. Masimulizi hayo yanasema: “Wale wote ambao sasa walikuwa waamini walikusanyika pamoja na wakashirikiana katika mambo yote, nao walikuwa wakiuza mali zao na vitu walivyomiliki na kuwagawia wote pesa walizopata, kulingana na uhitaji wa kila mtu.”f (Mdo. 2:44, 45) Kwa hakika, Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuiga roho hiyo ya kujidhabihu kwa upendo.

17. Ili mtu astahili kubatizwa anapaswa kufanya nini?

17 Ili mtu ajiweke wakfu na kubatizwa lazima atimize matakwa fulani muhimu ya Kimaandiko. Lazima ajifunze Neno la Mungu. (Yoh. 17:3) Anahitaji kuwa na imani, atubu mwenendo wake wa zamani, na kujuta kikweli. (Mdo. 3:19) Kisha, lazima ageuke, au abadili mwenendo wake, na kuanza kufanya kazi nzuri zinazopatana na mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:2; Efe. 4:23, 24) Baada ya kutimiza hatua hizo zote, anajiweka wakfu kwa Mungu katika sala na kubatizwa.​—Mt. 16:24; 1 Pet. 3:21.

18. Wanafunzi waliobatizwa wa Kristo wana pendeleo gani?

18 Je, wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo, uliyejiweka wakfu na kubatizwa? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuthamini sana pendeleo hilo. Kama wanafunzi wa karne ya kwanza waliojazwa roho takatifu, wewe pia unaweza kutoa ushahidi kamili na kufanya mapenzi ya Yehova!

a Ona sanduku lenye kichwa “Yerusalemu—Chimbuko la Dini ya Kiyahudi.”

b Ona sanduku lenye kichwa “Roma—Jiji Kuu la Milki ya Roma,” “Wayahudi Nchini Misri na Mesopotamia,”; na pia “Ukristo Katika Mkoa wa Ponto,”.

c “Ndimi” hizo hazikuwa za moto halisi, bali “kama za moto,” yaani, ziling’aa na kuonekana kama ndimi za moto juu ya kila mwanafunzi.

d Ona sanduku “Wageuzwa Imani Ni Nani?”.

e Agosti 7, 1993, katika kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova huko Kiev, Ukrainia, watu 7,402 walibatizwa katika vidimbwi sita. Ubatizo huo ulichukua muda wa saa mbili na robo.

f Mpango huo wa muda ulitosheleza uhitaji uliotokea kwa kuwa wageni walibaki Yerusalemu ili kujifunza mengi zaidi kuhusu imani hiyo mpya. Huo ulikuwa mpango wa hiari wa mtu kutoa mali yake, ili vitu vyote vitumiwe kwa ushirika. Haukuwa sera ya ujamaa.​—Mdo. 5:1-4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki