Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jr sura 2 kur. 14-31
  • Kutumikia Katika “Siku za Mwisho”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumikia Katika “Siku za Mwisho”
  • Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIKU ZA YEREMIA
  • MABADILIKO YA KIDINI
  • “UANDIKE . . . MANENO YOTE”
  • KUINUKA KWA TAIFA LA BABILONI
  • SIKU ZA MWISHO ZA UTAWALA WA KINASABA
  • UTENDAJI WA MABAKI WA YUDA
  • Kitabu Cha Biblia Namba 26—Yeremia
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Yeremia Nabii wa Hukumu za Mungu Asiyependwa na Wengi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Utachagua Marafiki wa Aina Gani?
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Nimeyatia Maneno Yangu Katika Kinywa Chako”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
Pata Habari Zaidi
Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
jr sura 2 kur. 14-31

SURA YA PILI

Kutumikia Katika “Siku za Mwisho”

1, 2. (a) Yeremia aliona nini katika maono, na maono hayo yalihusiana jinsi gani na mgawo wake? (b) Kwani nini tupendezwe na ujumbe wa Yeremia?

“UNAONA nini?” Mungu akamuuliza Yeremia aliyekuwa ametoka tu kupata mgawo wa kuwa nabii. Yeremia akajibu: “Ninaona chungu cha kupikia chenye mdomo mpana ambacho kinapuliziwa, na mdomo wake umeinama kutoka kaskazini.” Maono hayo yalikuwa ishara ya ujumbe ambao Yeremia alipaswa kutangaza. (Soma Yeremia 1:13-16.) Chungu hicho cha mfano kilikuwa kikipuliziwa, si ili kipoe, bali kuzidisha moto ulio chini yake. Yehova alikuwa akitangaza kwamba msiba utamwagika kutoka katika chungu hicho juu ya nchi ya Yuda kwa sababu ya uasi. Kwa nini mdomo wa chungu hicho ulikuwa umeinama kuelekea kusini? Msiba ungetoka kaskazini. Nchi ya Yuda ingeshambuliwa na Babiloni iliyokuwa upande wa kaskazini. Na ndivyo ilivyokuwa. Katika kipindi alichotumikia akiwa nabii, Yeremia alishuhudia chungu hicho kikimwagika mara kadhaa hadi jiji la Yerusalemu lilipoharibiwa mwishowe.

2 Jiji la Babiloni halipo tena, hata hivyo, kuna sababu nzuri ya kupendezwa na ujumbe wa kinabii wa Yeremia. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho,” wakati ambapo watu wengi wanadai kuwa Wakristo; ijapokuwa wao na makanisa yao hawana kibali cha Mungu. (Yer. 23:20) Kwa upande mwingine, kama Yeremia, tunahubiri ujumbe wa hukumu na wenye tumaini pia.

Picha katika ukurasa wa 14

3. (a) Kitabu cha Yeremia kimeandikwa kwa mpangilio gani? (b)  Ni habari gani inayozungumziwa katika sura hii?

3 Yamkini, kuelekea mwishoni mwa utumishi wake, Yeremia hakurekodi matukio yaliyokuwa yakitendeka, badala yake alimtumia mwandishi kuyaandika. (Yer. 25:1-3; 36:1, 4, 32) Masimulizi katika kitabu hicho hayafuatani kulingana na tarehe badala yake yamepangwa kulingana na habari inayozungumziwa. Hivyo basi, huenda ukafaidika kwa kupata muhtasari wa matukio yanayosimuliwa katika vitabu hivyo kulingana na wakati ambapo yalitukia. Ona chati kwenye ukurasa wa 19. Kujua mfalme aliyekuwa akitawala Yuda, wakati alipokuwa akitawala, na hata yaliyokuwa yakitendeka ndani na nje ya Yuda wakati huo, kwaweza kukusaidia kuelewa vizuri zaidi yale ambayo Yeremia alisema au kufanya. Kwa kufanya hivyo, utafaidika hata zaidi kutokana na ujumbe wa Mungu kwa watu Wake uliotangazwa na Yeremia.

SIKU ZA YEREMIA

4-6. Kabla ya Yeremia kuwa nabii, watu wa Mungu walikuwa katika hali gani?

4 Yeremia alikuwa nabii katika kipindi chenye msukosuko. Kulikuwa na uadui kati ya Ashuru, Babiloni, na Misri. Miaka 93 hivi kabla ya Yeremia kuwa nabii, Ashuru ilishinda ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi na kuondosha wengi wa wakaaji wake. Wakati huo, Yehova alilinda Yerusalemu na mfalme Hezekia mwaminifu kutoka mikononi mwa Ashuru kwa kuwaua askari 185,000. (2 Fal. 19:32-36) Mmoja kati ya wana wa Hezekia ni Manase. Inaonekana Yeremia alizaliwa wakati wa utawala wa Manase wa miaka 55, wakati ambapo Yuda ilikuwa chini ya Ashuru.—2 Nya. 33:10, 11.

5 Kulingana na Wafalme wa Kwanza na Wafalme wa Pili, vitabu vilivyoandikwa na Yeremia, Manase alijenga upya mahali pa juu ambapo baba yake alikuwa ameharibu. Manase alijenga madhabahu kwa ajili ya Baali na majeshi ya mbinguni, hata ndani ya hekalu la Yehova. Alimwaga damu ya watu wengi wasio na hatia. Isitoshe, alimtoa mwana wake kuwa dhabihu ya kuteketezwa kwa mungu wa uwongo. Kwa ujumla, “alifanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.” Kwa sababu ya uovu wote huo, Mungu alitangaza kwamba Yerusalemu na Yuda yatapata msiba, kama vile Samaria na Israeli. (2 Fal. 21:1-6, 12-16) Baada ya kifo cha Manase, mwana wake, Amoni, aliendeleza ibada ya sanamu ambayo baba yake alikuwa ameanzisha. Hata hivyo, muda si muda mambo yalibadilika. Miaka miwili tu baadaye, Amoni aliuawa, na mwaka wa 659 K.W.K., mwana wake Yosia, mwenye umri wa miaka minane akaanza kutawala.

6 Katika wa miaka 31 ya utawala wa Yosia, ukuu wa Babiloni ulianza kupita ule wa Ashuru. Yosia aliuona huo kuwa wakati unaofaa kukomboa Yuda kutoka mikononi mwa utawala wa kigeni. Tofauti na baba na babu yake, Yosia alimtumikia Yehova kwa uaminifu na kuanzisha mabadiliko makubwa ya kidini. (2 Fal. 21:19–22:2) Katika mwaka wa 12 wa utawala wake, Yosia aliondolea mbali mahali pa juu, miti mitakatifu, na sanamu za dini ya uwongo kotekote katika eneo lote la ufalme wake na kuagiza hekalu la Yehova lifanyiwe marekebisho. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:1-8.) Katika mwaka wa 13 wa utawala wa Yosia (647 K.W.K.), ndipo Yeremia alipopewa mgawo wa kuwa nabii wa Mungu.

Ungeuona namna gani mgawo wa kuwa nabii katika siku za Yeremia?

7, 8. (a) Ni kwa njia gani utawala wa Mfalme Yosia ulikuwa tofauti na utawala wa Manase na Amoni? (b) Yosia alikuwa mtu wa aina gani? (Ona sanduku katika ukurasa wa 20.)

7 Hekalu lilipokuwa likirekebishwa, katika mwaka wa 18 wa utawala wa mfalme Yosia, kuhani mkuu alikipata “kile kitabu chenyewe cha sheria.” Mwandishi akamsomea mfalme kitabu hicho. Yosia akatambua makosa ya watu wake, akatafuta mwongozo wa Yehova kupitia nabii Hulda, na kuwasihi watu washike amri za Mungu. Hulda alimfahamisha Yosia kwamba Yehova ataleta “msiba” juu ya Yudea kwa sababu ya kukosa uaminifu. Hata hivyo, kwa sababu Yosia alikuwa na maoni mazuri kuhusu ibada safi, msiba haungekuja wakati wake.—2 Fal. 22:8, 14-20.

Chati katika ukurasa wa 19

8 Mfalme Yosia alianzisha tena jitihada zake za kuondolea mbali ibada yoyote ya sanamu iliyokuwa imebaki. Akiwa na bidii hiyo alienda mpaka eneo lililokuwa la ufalme wa kaskazini wa Israeli, ili kuharibu mahali pa juu na madhabahu ya Betheli. Pia, alifanya mipango kwa ajili ya sherehe kubwa ya Pasaka. (2 Fal. 23:4-25) Haikosi hatua hiyo ilimfurahisha sana Yeremia! Hata hivyo, haikuwa rahisi kwa watu kubadili njia zao. Manase na Amoni walikuwa wameanzisha ibada ya sanamu yenye kuchukiza, kwa hiyo, hali ya kiroho ya watu ilikuwa imezorota sana. Licha ya mabadiliko ambayo Yosia alikuwa amefanya, Mungu alisema kupitia Yeremia kwamba bado kuna miungu mingi Yudea. Watu walioishi siku za Yeremia walikuwa kama mke mwasherati, walikuwa wamemwacha Yehova na kufanya ukahaba na miungu ya kigeni. Yeremia aliwaambia: “Mmeweka madhabahu nyingi kama barabara za Yerusalemu kwa ajili ya kile kitu cha aibu, madhabahu za kumfukizia Baali moshi wa dhabihu.”—Soma Yeremia 11:1-3, 13.

9. Ni mambo gani yaliyohusisha mataifa mengine yaliyotokea katika miaka ya mwishomwisho ya utawala wa Yosia?

9 Ujumbe wa Yeremia haukuwabadili Wayahudi wala mataifa yaliyokuwa yaking’ang’ania kuwa na mamlaka katika eneo hilo. Mwaka wa 632 K.W.K., majeshi ya Wababiloni na Wamedi yaliteka Ninawi, mji mkuu wa Ashuru. Miaka mitatu baadaye, Farao Neko wa Misri aliongoza majeshi yake upande wa kaskazini kwenda kuwasaidia Waashuru waliokuwa taabani. Kwa sababu zisizojulikana, Yosia alijaribu kuyazuia majeshi ya Misri yalipokuwa Megido, hata hivyo, aliumizwa vibaya sana, naye akafa. (2 Nya. 35:20-24) Tukio hilo lenye kuhuzunisha lingeleta mabadiliko gani ya kisiasa na kidini katika taifa la Yuda? Ni hali gani ngumu ambazo Yeremia angekabili?

MABADILIKO YA KIDINI

10. (a) Hali zilizokuwapo baada ya kifo cha Yosia zinalingana jinsi gani na siku zetu? (b) Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kuchunguza maisha ya Yeremia?

10 Wazia jinsi Yeremia alivyohisi aliposikia kwamba Yosia amekufa! Akiwa na huzuni nyingi, aliimba nyimbo za maombolezo. (2 Nya. 35:25) Tayari hali ilikuwa ngumu katika taifa la Yuda. Isitoshe, kulikuwa na mizozo kati ya mataifa mbalimbali. Misri, Ashuru, na Babiloni yalikuwa yaking’ang’ania eneo hilo. Mazingira ya ibada katika Yuda yalikuwa yamebadilika baada ya kifo cha Yosia. Huo ndio uliokuwa mwisho wa utawala uliomfaa Yeremia na kazi yake ya kutoa unabii, na mwanzo wa utawala mkatili. Wengi kati ya ndugu zetu wamejikuta katika hali kama hizo leo. Wamepoteza ghafula uhuru wa ibada waliokuwa nao na kujikuta chini ya marufuku na mateso. Hatujui ni wangapi kati yetu watajikuta katika hali kama hizo. Tunaweza kufanya nini tukijikuta katika hali kama hizo? Ni nini kinachoweza kutusaidia kudumisha utimilifu wetu? Tunapotafakari maswali hayo, tutatiwa moyo kwa kufikiria hali ngumu ambazo Yeremia alikabili.

YOSIA—MFALME MZURI WA MWISHO KUTAWALA YUDA

Picha katika ukurasa wa 20

Yosia alianza kutawala Yuda akiwa na umri wa miaka nane, baada ya baba yake, Amoni, kufa. Alipokuwa na umri wa miaka 15, alianza kumtafuta Mungu na “kutembea katika njia yote ya Daudi babu yake.” Alipokuwa na umri wa miaka 19, alianza kusafisha Yuda na Israeli na kuondoa mahali pa ibada yao ya uwongo na kuziharibu sanamu zao. Akiwa na umri wa miaka 25, alianza kurekebisha hekalu la Yehova.—2 Fal. 21:19–22:2; 2 Nya. 34:2-8.

Kitabu cha Sheria, huenda ni kile kilichoandikwa na Musa mwenyewe, kilipatikana wakati hekalu lilipokuwa likirekebishwa, nacho kikasomwa mbele ya Yosia. Mfalme huyo alijinyenyekeza, akayararua mavazi yake, na kulia. Yosia alipanga makuhani, Walawi, na watu wake wote, wakubwa kwa wadogo, wasikilize kitabu hicho kikisomwa. Masimulizi yanasema kwamba mfalme huyo alifanya agano “ili kumfuata Yehova na kushika amri zake . . . kwa moyo wake wote na kwa nafsi yake yote.” Kisha, Yosia akachukua hatua kubwa hata zaidi kukomesha ibada ya uwongo. Pia, mfalme alimfanyia Yehova Pasaka kubwa, ambayo haikuwa na kifani tangu siku za Samweli.—2 Nya. 34:14–35:19.

11. Mambo yalikuwaje Yuda baada ya Yosia kufa?

11 Wakaaji wa Yuda walimtawaza Yehoahazi, mwana wa Yosia, awe mfalme huko Yerusalemu. Yehoahazi, aliyekuwa pia akiitwa Shalumu, alitawala kwa miezi mitatu tu. Farao Neko aliporudi kusini baada ya kupigana na Wababiloni, alimwondoa mamlakani mfalme huyo mpya na kumpeleka Misri, naye Yeremia akatangaza kwamba Yehoahazi “hatarudi hapo tena.” (Yer. 22:10-12; 2 Nya. 36:1-4) Kisha Neko akamtawaza Yehoyakimu, mwana mwingine wa Yosia. Yehoyakimu hakufuata mfano mzuri wa baba yake. Badala ya kuendeleza mabadiliko yaliyoanzishwa na baba yake, alikuwa mwabudu-sanamu.—Soma 2 Wafalme 23:36, 37.

12, 13. (a) Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu, mazingira ya ibada yalikuwaje? (b) Viongozi wa dini ya Kiyahudi walimtendea Yeremia namna gani?

12 Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu, Yehova alimwagiza Yeremia aende hekaluni na kuwashutumu Wayudea kwa sababu ya uovu wao. Walikuwa wakiliona hekalu la Yehova kama hirizi ambayo ingewalinda. Hata hivyo, ikiwa hawangeacha “wizi, uuaji na uzinzi na kuapa kwa uwongo na kumfukizia Baali moshi wa dhabihu na kuifuata miungu mingine,” Yehova angeliacha hekalu lake pamoja na wanafiki waliokuwa wakiabudia humo, kama vile alivyoiacha maskani iliyokuwa Shilo wakati wa Kuhani Mkuu, Eli. Nchi ya Yuda “itakuwa mahali palipofanywa ukiwa.” (Yer. 7:1-15, 34; 26:1-6)a Yeremia alihitaji uhodari ili kutangaza ujumbe huo! Huenda alihitaji kufanya hivyo mbele ya watu wenye vyeo. Ndugu na dada fulani leo wamehisi kwamba wanahitaji moyo mkuu ili kuhubiri barabarani au kuwahubiria matajiri au watu wenye vyeo. Hata hivyo, tuna hakika kwamba Mungu anatutegemeza, kama vile alivyomtegemeza Yeremia.—Ebr. 10:39; 13:6.

Picha katika ukurasa wa

13 Katika mazingira hayo ya kidini na kisiasa, viongozi wa dini wangeitikia jinsi gani ujumbe wa Yeremia? Kulingana na masimulizi ya nabii huyo, “makuhani na manabii na watu wote [wakanikamata], wakisema: ‘Hakika utakufa.’” Wakiwa na hasira, walisema: “Mtu huyu anastahili hukumu ya kifo.” (Soma Yeremia 26:8-11.) Hata hivyo, wapinzani wa Yeremia hawakushinda. Yehova alimkomboa. Naye Yeremia hakubabaishwa na vitisho wala idadi ya wapinzani wake. Wewe pia unaweza kufuata mfano wake.

Hali wakati wa utawala wa Manase, Amoni, na Yosia zilikuwa tofauti jinsi gani? Unaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yeremia alivyoutekeleza mgawo wake mgumu?

“UANDIKE . . . MANENO YOTE”

14, 15. (a) Yeremia na mwandishi wake, Baruku walianza kazi gani katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu? (b) Yehoyakimu alikuwa mtu wa aina gani? (Ona sanduku katika ukurasa wa 25.)

14 Katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu, Yehova alimwagiza Yeremia aandike maneno yote ambayo alikuwa amemwambia tangu siku za Yosia. Yeremia alimtumia mwandishi wake, Baruku kuandika maneno yote ambayo Mungu alikuwa amemwambia kwa miaka 23 iliyotangulia. Ujumbe wake wa hukumu ulihusu wafalme na falme 20 hivi. Yeremia alimwagiza Baruku asome kwa sauti kitabu hicho cha kukunjwa katika nyumba ya Yehova. Kwa nini? “Labda wale wa nyumba ya Yuda watausikiliza msiba wote ninaofikiria kuwatendea,” Yehova akasema, “kusudi warudi, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya, na ili mimi kwa kweli nisamehe kosa lao na dhambi yao.”—Yer. 25:1-3; 36:1-3.

15 Ofisa mmoja wa makao ya mfalme alipomsomea Yehoyakimu kitabu hicho, mfalme alikirarua-rarua na kukiteketeza. Kisha akaagiza Yeremia na Baruku waletwe mbele yake. “Lakini Yehova akaendelea kuwaficha.” (Soma Yeremia 36:21-26.) Kwa sababu ya maoni mabaya sana ya Yehoyakimu, Yehova alimtumia nabii wake kutangaza kwamba mfalme huyo “atazikwa kwa maziko ya punda-dume.” ‘Atakokotwa na kutupwa, nje ya malango ya Yerusalemu.’ (Yer. 22:13-19) Je, ndivyo ambavyo ingekuwa au Yeremia alikuwa akitilia chumvi?

16. Yeremia alitangaza ujumbe gani wenye kutia moyo?

16 Ijapokuwa alikuwa akitangaza ujumbe wa hukumu, Yeremia hakuwa mtabiri-maangamizi. Alitangaza pia ujumbe wenye tumaini. Yehova angekomboa mabaki ya Waisraeli kutoka mikononi mwa adui zao na kuwarudisha katika nchi yao, ambapo wangeishi salama. Mungu angeanzisha ‘agano jipya linalodumu mpaka wakati usio na kipimo’ pamoja na watu wake na kuandika sheria yake katika moyo wao. Angewasamehe makosa yao naye hangekumbuka kamwe dhambi zao. Isitoshe, mzao wa Daudi angetenda “haki na uadilifu katika nchi.” (Yer. 31:7-9; 32:37-41; 33:15) Unabii huo ungetimizwa miaka na karne nyingi baadaye, kufikia siku zetu. Unabii huo pia unatupa tumaini la wakati ujao ulio bora. Hata hivyo, katika siku za Yeremia, adui za Yuda waliendelea kupigania eneo hilo.—Soma Yeremia 31:31, 33, 34; Waebrania 8:7-9; 10:14-18.

KUINUKA KWA TAIFA LA BABILONI

17, 18. Ni mambo gani yaliyohusisha mataifa kadhaa yaliyotokea katika miaka ya mwisho-mwisho ya utawala wa Yehoyakimu na Sedekia?

17 Mwaka wa 625 K.W.K., Wababiloni na Wamisri walipigana vita vya kukata maneno huko Karkemishi, karibu na Mto Efrati, kilomita 600 hivi kaskazini mwa Yerusalemu. Mfalme Nebukadneza aliyashinda majeshi ya Farao Neko, na kukomesha mamlaka ambayo Misri ilikuwa nayo katika eneo hilo. (Yer. 46:2) Nebukadneza akaanza kutawala Yuda, naye Yehoyakimu akawa kibaraka wake. Hata hivyo, baada ya miaka mitatu, Yehoyakimu akaasi. (2 Fal. 24:1, 2) Kisha, Nebukadneza na jeshi lake wakavamia Yuda mwaka wa 618 K.W.K. na kuzingira Yerusalemu. Huo ulikuwa wakati mgumu sana, hata kwa Yeremia. Inaelekea Yehoyakimu aliuawa wakati huo.b Mwana wake Yehoyakini alisalimu amri kwa Wababiloni baada ya kutawala Yuda kwa miezi mitatu tu. Nebukadneza alipora mali ya Yerusalemu na kuwapeleka uhamishoni Yehoyakini, watu wa familia ya mfalme, wenye vyeo katika Yuda, wenye nguvu, na mafundi. Danieli, Hanania, Mishaeli, na Azaria walikuwa kati ya watu hao waliotekwa.—2 Fal. 24:10-16; Dan. 1:1-7.

18 Kisha, Nebukadneza akamtawaza Sedekia, mwana mwingine wa Yosia, awe mfalme wa Yuda. Ndiye aliyekuwa mfalme wa mwisho wa Yuda. Utawala wake ulikoma mwaka wa 607 K.W.K., Yerusalemu na hekalu lake lilipoharibiwa. (2 Fal. 24:17) Hata hivyo, kwa miaka 11 ambayo Sedekia alitawala, kulikuwa na misukosuko mingi ya kijamii na kisiasa katika taifa la Yuda. Yeremia alihitaji kumtumaini Yehova kabisa.

YEHOYAKIMU​—MFALME AMBAYE ALIMUUA NABII WA YEHOVA

Picha katika ukurasa wa 25

Yehoyakimu alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala Yuda, naye alitawala kwa miaka 11 hivi. Muhtasari wa mambo aliyofanya unapatikana katika 2 Mambo ya Nyakati 36:5-8 ambapo tunasoma kwamba alifanya si mabaya tu, bali “machukizo.” Yehoyakimu aliyapuuza maonyo ya Yeremia, naye akatawala kwa njia isiyo ya haki, unyang’anyi, na uuaji. Nabii Uriya alipotoa ujumbe uliofanana na wa Yeremia, Yehoyakimu aliagiza auawe. Inaonekana kwamba mfalme Yehoyakimu alikufa wakati mji wa Yerusalemu ulipozingirwa.—Yer. 22:17-19; 26:20-23.

19. Katika siku za Yeremia, watu waliuitikia ujumbe wake jinsi gani, nasi tunaweza kujifunza nini?

19 Wazia hali ya Yeremia. Tangu siku za Yosia, Yeremia alikuwa amejionea misukosuko ya kisiasa na kuzorota kwa hali ya kiroho kati ya watu wa Mungu. Hata hivyo, alijua kwamba mambo yangezidi kuwa mabaya. Watu wa kwao walimwambia: “Usitoe unabii katika jina la Yehova, usije ukafa mkononi mwetu.” (Yer. 11:21) Hata baada ya kuona unabii wa Yeremia ukitimia, Wayahudi walisema: “Kuhusu lile neno ambalo umetuambia katika jina la Yehova, sisi hatutakusikiliza.” (Yer. 44:16) Hata hivyo, maisha ya watu yalikuwa hatarini, kama ilivyo leo. Leo pia, tunatangaza ujumbe wa Yehova. Kwa hiyo, kuchunguza jinsi Yehova alivyomlinda nabii wake katika kipindi kilichotangulia kuanguka kwa Yerusalemu kunaweza kutusaidia kuwa na bidii zaidi katika huduma.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na Yeremia wakati wa utawala wa Yehoyakimu? Yeremia alitoa unabii gani ambao unatimia wakati wetu?

SIKU ZA MWISHO ZA UTAWALA WA KINASABA

20. Kwa nini wakati wa utawala wa Sedekia ulikuwa kipindi kigumu katika mgawo wa Yeremia? (Ona sanduku katika ukurasa wa 29.)

20 Huenda kipindi kigumu zaidi katika mgawo wa Yeremia kilikuwa wakati wa utawala wa Sedekia. Kama wengi waliomtangulia, Sedekia ‘aliendelea kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’ (Yer. 52:1, 2) Alikuwa mfalme kibaraka wa Wababiloni, naye Nebukadneza alimwapisha kwa jina la Yehova kwamba atajitiisha kwa mfalme wa Babiloni. Licha ya kufanya hivyo, mwishowe Sedekia aliasi. Nao adui za Yeremia walikuwa wakimshinikiza ajiunge na waasi.—2 Nya. 36:13; Eze. 17:12, 13.

21-23. (a) Taifa la Yuda lilikuwa limegawanyika katika pande gani mbili wakati wa utawala wa Sedekia? (b) Yeremia alitendewa jinsi gani kwa sababu ya msimamo wake, nasi tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kutafakari juu ya hali yake?

21 Inaonekana kwamba, mapema katika utawala wa Sedekia, wafalme wa Edomu, Moabu, Amoni, Tiro, na Sidoni, walituma wajumbe Yerusalemu. Labda lengo lao lilikuwa kumshawishi Sedekia ajiunge nao dhidi ya Nebukadneza. Hata hivyo, Yeremia alimsihi Sedekia ajitiishe kwa Babiloni. Yeremia aliwapa wajumbe hao nira ili kuonyesha kwamba mataifa yao pia yanapaswa kuwatumikia Wababiloni. (Yer. 27:1-3, 14)c Ujumbe huo wa Yeremia haukuwafurahisha, naye Hanania alifanya mambo yawe magumu hata zaidi. Hanania alikuwa nabii wa uwongo ambaye alidai katika jina la Mungu kwamba nira ya Wababiloni itavunjwa. Hata hivyo, Yehova alitangaza kupitia Yeremia kwamba mlaghai huyo, Hanania, atakufa kabla ya mwaka kwisha. Hivyo ndivyo ilivyokuwa.—Yer. 28:1-3, 16, 17.

22 Taifa la Yuda lilikuwa limegawanyika katika pande mbili, wale waliokuwa tayari kujitiisha kwa Babiloni na wale waliokuwa wakichochea uasi. Mwaka wa 609 K.W.K., Sedekia aliasi kwa kutafuta usaidizi wa jeshi la Misri. Yeremia alilazimika kukabiliana na mchafuko uliosababishwa na watu waliokuwa wakiunga mkono maasi. (Yer. 52:3; Eze. 17:15) Nebukadneza pamoja na jeshi lake walirudi Yuda ili kuzima ghasia hizo, akayapiga na kuyashinda majiji yote ya Yuda na kuuzingira tena mji wa Yerusalemu. Wakati huo, Yeremia alitangaza kwamba Yerusalemu litaanguka mikononi mwa Wababiloni. Wowote ambao watabaki jijini watauawa. Nao wale ambao watakaoenda kwa Wakaldayo wataokoka.—Soma Yeremia 21:8-10; 52:4.

23 Wakuu wa Yuda walidai kwamba Yeremia anaunga mkono Babiloni. Aliposema ukweli wa mambo, wakuu wa Yuda walimpiga na kumtia kizuizini. (Yer. 37:13-15) Hata hivyo, Yeremia hakupunguza uzito wa ujumbe wa Yehova. Kwa hiyo, wakuu wakamchochea Sedekia amuue Yeremia. Wakamtupa Yeremia ndani ya tangi ambalo halikuwa na maji ambamo angeweza kuangamia kwenye matope. Hata hivyo, aliokolewa na Ebed-meleki, Mwethiopia aliyekuwa mtumishi katika nyumba ya mfalme. (Yer. 38:4-13) Leo pia, watumishi wa Yehova hujikuta hatarini kwa sababu ya kukataa kuunga mkono mizozo ya kisiasa. Bila shaka, kutafakari mambo yaliyompata Yeremia kunaweza kukupa nguvu za kukabili majaribu na kuyashinda.

SEDEKIA​—MFALME WA MWISHO KUTAWALA YUDA

Picha katika ukurasa wa 29

Sedekia alikuwa mtawala mwoga, asiye na msimamo, na asiyejiamini ambaye alipelekwa huku na huku na wakuu wake. Wababiloni walipozingira Yerusalemu kwa mara ya mwisho, Sedekia alitafuta mwongozo wa Mungu kupitia Yeremia. Lakini mfalme huyo hakufuata mwongozo huo alipoambiwa ajiuzulu. Kwa kuwa Sedekia hakupendezwa na ujumbe wa Yeremia, alimtia kizuizini. (Yer. 21:1-9; 32:1-5) Hata hivyo, mfalme aliendelea kutafuta kisiri ushauri kutoka kwa Yeremia, akihofia kuwakera wakuu wa Yuda. Walipotaka kumwua Yeremia, Sedekia alikubali kwa woga, akisema: “Yuko mikononi mwenu. Kwa maana hakuna jambo lolote ambalo mfalme anaweza kuwazuia ninyi.” Yeremia alipoponyoka tisho la kifo, mfalme alitafuta ushauri kutoka kwake tena na kukubali kwamba aliogopa eti akimtii Mungu, atatendewa isivyofaa na watu.—Yer. 37:15-17; 38:4, 5, 14-19, 24-26.

Hata hivyo, Sedekia “hakujinyenyekeza kwa ajili ya nabii Yeremia . . . , naye akaendelea kuifanya shingo yake kuwa ngumu na kuufanya moyo wake kuwa mgumu ili asirudi kwa Yehova.”—2 Nya. 36:12, 13; Eze. 21:25.

24. Mwaka wa 607 K.W.K. kulikuwa na matukio gani?

24 Hatimaye, mwaka wa 607 K.W.K., Wababiloni walibomoa kuta za Yerusalemu na kuliangusha jiji hilo. Jeshi la Nebukadneza likateketeza hekalu la Yehova, likabomoa kuta za jiji, na kuwaua watu wenye vyeo wa Yuda. Sedekia alijaribu kukimbia, lakini akakamatwa na kutiwa mikononi mwa Wababiloni. Wana wake wakauawa mbele ya macho yake, kisha Nebukadneza akaagiza apofushwe, afungwe kwa pingu, na kupelekwa Babiloni. (Yer. 39:1-7) Ndiyo, unabii wa Yeremia kuhusu Yuda na Yerusalemu ulitimia. Badala ya kushangilia, Yeremia aliomboleza kwa sababu ya msiba uliowakumba watu wa taifa lake. Tunaweza kuona hisia zake katika kitabu cha Maombolezo. Utaguswa moyo sana kwa kusoma kitabu hicho.

UTENDAJI WA MABAKI WA YUDA

25, 26. (a) Baada ya Yerusalemu kuanguka, ni matukio gani yaliyofuata? (b) Watu waliitikia jinsi gani ujumbe wa Yeremia baada ya Yerusalemu kuanguka?

25 Yote hayo yalipokuwa yakitendeka Yeremia alikuwa wapi? Wakuu wa Yerusalemu walikuwa wamemfunga gerezani, lakini Wababiloni walipofika walimtendea kwa fadhili na kumfugua. Baadaye, Yeremia alikuwa kati ya Wayahudi fulani waliokuwa wakipelekwa uhamishoni, lakini akaachiliwa. Bado alikuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, kati ya wale waliobaki. Nebukadneza alimchagua Gedalia kuwa gavana, naye akawaahidi Wayudea kuishi kwa amani ikiwa tu watamtumikia yeye, mfalme wa Babiloni. Hata hivyo, Wayahudi fulani wenye kinyongo wakamuua Gedalia. (Yer. 39:13, 14; 40:1-7; 41:2) Yeremia aliwasihi Wayudea waliobaki waendelee kukaa katika nchi hiyo na wasimwogope mfalme wa Babiloni. Hata hivyo, viongozi wao, walidai kwamba Yeremia ni mwongo, nao wakamchukua Yeremia na Baruku kwa lazima na kukimbilia Misri. Hata hivyo, Yeremia alikuwa ametabiri kwamba Nebukadneza atashambulia na kutiisha Misri na kwamba wakimbizi wa Yudea wangekumbwa na msiba.—Yer. 42:9-11; 43:1-11; 44:11-13.

26 Kwa mara nyingine tena watu hawakutaka kumsikiliza Yeremia, nabii wa kweli wa Mungu. Kwa nini? “Tangu tulipoacha kumfukizia ‘malkia wa mbingu’ moshi wa dhabihu na kummiminia matoleo ya kinywaji,” wakasema, “tumekosa kila kitu, nasi tumemalizika kwa upanga na kwa njaa.” (Yer. 44:16, 18) Hali ya kiroho ya watu wa siku za Yeremia ilikuwa yenye kusikitisha kama nini! Kwa upande mwingine, tunatiwa moyo kama nini kujua kwamba mtu asiye mkamilifu anaweza kuwa mwaminifu kwa Yehova hata akiwa katikati ya watu wasio waaminifu!

27. Tunajua nini kuhusu miaka ya mwisho-mwisho ya kazi ya Yeremia akiwa nabii?

27 Tukio la mwisho ambalo Yeremia aliandika juu yake ni kule kufunguliwa kwa Yehoyakini kutoka mikononi mwa Evil-merodaki aliyetawala baada ya Nebukadneza. Hilo lilitukia mwaka wa 580 K.W.K. (Yer. 52:31-34) Kufikia wakati huo, Yeremia alikuwa na umri wa miaka 90 hivi. Hatuna habari zenye kutegemeka kuhusu mwisho wa maisha yake. Yawezekana kwamba aliishi miaka yake ya mwisho-mwisho nchini Misri na kufa huko akiwa amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka 67 hivi. Alitumikia wakati ambapo watu wengi walikuwa wakimwabudu Mungu wa kweli, na pia wakati ambapo uasi imani ulikuwa umeenea sana. Watu fulani wanaomwogopa Mungu walimsikiliza. Hata hivyo, walio wengi waliukataa ujumbe wake, hata wakamtendea kikatili. Je, hilo linamaanisha kwamba Yeremia alifanya kazi bure? Sivyo hata kidogo! Tangu mwanzo, Yehova alimwambia: “Hakika watapigana nawe, lakini hawatakushinda, kwa maana ‘Mimi niko pamoja nawe.’” (Yer. 1:19) Kazi yetu leo tukiwa Mashahidi wa Yehova ni kama ya Yeremia. Kwa hiyo, tunaweza kutazamia watu waitikie vivyo hivyo. (Soma Mathayo 10:16-22) Hivyo basi, tunaweza kujifunza mambo gani kutoka kwa Yeremia, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu huduma yetu? Acheni tufikirie maswali hayo.

Sedekia na watu wa taifa lake waliokataa ujumbe wa Yeremia walipatwa na nini? Unamwonaje Yeremia?

a Watu fulani wanaamini kwamba masimulizi ya Yeremia 7:1-15 na Yeremia 26:1-6 yanazungumzia kisa kilekile kwa sababu ya ulinganifu uliopo.

b Kulingana na Danieli 1:1, 2, Yehoyakimu alitiwa mkononi mwa Nebukadneza katika mwaka wa tatu wa kuwa kwake kibaraka. Huenda hilo likamaanisha kwamba mfalme huyo alikufa wakati wa mazingiwa, ambayo hatimaye yalifanikiwa. Inawezekana kwamba, kama mwanahistoria Yosefo alivyoandika, Nebukadneza alimuua Yehoyakimu na kuagiza mwili wake utupwe nje ya kuta za Yerusalemu bila kuzikwa. Hata hivyo, Biblia haisemi lolote kuhusu jambo hilo.—Yer. 22:18, 19; 36:30.

c Huenda kutajwa kwa Yehoyakimu katika Yeremia 27:1 ni kosa la unakili kwa sababu mstari wa 3 na wa 12 unazungumza kuhusu Sedekia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki