SURA YA TISA
Epuka “Kujitafutia Makuu”
1, 2. (a) Baruku alikuwa na tatizo gani katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu? (b) Yehova alimsaidia Baruku jinsi gani?
BARUKU, mwandishi mwaminifu wa Yeremia, alikuwa amechoka. Ulikuwa mwaka wa nne wa utawala wa mfalme mwovu Yehoyakimu, mwaka wa 625 K.W.K. hivi. Yeremia alimwagiza Baruku aandike maneno yote ambayo Yehova alisema kuhusu Yerusalemu na Yuda katika kipindi cha miaka 23, tangu mwanzo wa utume wa Yeremia hadi wakati huo. (Yer. 25:1-3; 36:1, 2) Baruku hakuwasomea Wayahudi maneno hayo wakati huo. Alipaswa kuyasoma mwaka uliofuata. (Yer. 36:9, 10) Lakini je, kuna jambo lililokuwa likimsumbua Baruku?
2 “Ole wangu, sasa,” akaomboleza Baruku, “kwa maana Yehova ameongeza huzuni juu ya maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kuugua kwangu.” Huenda nyakati nyingine wewe pia umeomboleza hivyo, iwe ni kwa sauti au moyoni. Vyovyote vile, Yehova alikuwa akisikiliza. Mungu, anayeichunguza mioyo ya wanadamu, alijua kilichokuwa kinamhangaisha Baruku, naye akamtumia Yeremia kumrekebisha kwa fadhili. (Soma Yeremia 45:1-5.) Hata hivyo, huenda ukajiuliza ni kwa nini Baruku alikuwa amechoka hivyo. Je, ni kwa sababu ya mgawo wake au mazingira ya kazi yake? Hisia hizo zilitoka moyoni. Wajua, Baruku alikuwa ‘anajitafutia makuu.’ Makuu gani? Yehova alimhakikishia nini ikiwa angekubali shauri na mwongozo wake? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyompata Baruku?
“MAKUU” HAYO YALIKUWA NINI?
3. Ni nini kilichokuwa kiini cha tatizo la kiroho la Baruku?
3 Haikosi Baruku alijua “makuu” hayo yalikuwa nini. Mwandishi huyo alitambua kwamba macho ya Mungu “yako juu ya njia za mwanadamu, naye huziona hatua zake zote.” (Ayu. 34:21) Sababu iliyomfanya Baruku ahisi kwamba hana “mahali pa kupumzika” alipokuwa akiandika maneno ya kinabii ya Yeremia haikuwa mgawo wenyewe. Badala yake ni maoni yake mwenyewe kuhusu mambo aliyoyaona kuwa makuu—yale yaliyokuwa moyoni mwake. Kwa sababu ya kujishughulisha sana akijitafutia “makuu,” Baruku alikosa kutambua mambo yaliyo ya maana zaidi, yaani, kufanya mapenzi ya Mungu. (Flp. 1:10) Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatoa maana halisi ya kitenzi kilichotumiwa inaposema “unaendelea kujitafutia.” Kwa hiyo, halikuwa wazo la muda tu. Tayari Baruku alikuwa akijitafutia “makuu” Yehova alipomwonya aache kufanya hivyo. Ingawa mwandishi huyo mwaminifu wa Yeremia alikuwa akifanya mapenzi ya Mungu, wakati huohuo alikuwa anatamani kujitafutia “makuu.”
4, 5. Kwa nini yawezekana kwamba “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia yalitia ndani sifa na umashuhuri, na kwa nini onyo la Yehova lilifaa?
4 Yawezekana kwamba mojawapo ya mambo yaliyokuwa yakimhangaisha Baruku ni kupata sifa na umashuhuri. Ingawa Baruku alikuwa akinakili ujumbe wa Yeremia, huenda hakuwa mwandishi wake wa kibinafsi. Katika Yeremia 36:32, Baruku anaitwa “mwandishi.” Wachimbuzi wa vitu vya kale wamefukua vitu vinavyodokeza kwamba alikuwa ofisa mkuu katika makao ya mfalme. Mwingine aliyekuwa na cheo hicho ni “Elishama mwandishi,” anayetajwa kati ya wakuu wa Yuda. Kwa hiyo huenda Baruku angeweza kuingia katika “chumba cha kulia chakula cha mwandishi” katika “nyumba ya mfalme” akiwa mfanyakazi-mwenzi wa Elishama. (Yer. 36:11, 12, 14) Hivyo basi, yawezekana kwamba Baruku alikuwa ofisa mwenye elimu katika nyumba ya mfalme. Ndugu yake, Seraya, alikuwa msimamizi wa makao ya Mfalme Sedekia, naye aliandamana na mfalme katika ziara muhimu kule Babiloni. (Soma Yeremia 51:59.) Akiwa msimamizi wa makao, yaelekea Seraya ndiye aliyekuwa akisimamia mahali pa kulala pa mfalme na vitu alivyohitaji akiwa safarini. Bila shaka, hicho kilikuwa cheo cha juu.
5 Basi inaeleweka ni kwa nini mtu mwenye cheo kama yeye angeweza kuchoshwa na kazi ya kuandika ujumbe wenye shutuma mmoja baada ya mwingine, dhidi ya Yuda. Isitoshe, kumuunga mkono nabii wa Mungu, kungeweza kuhatarisha cheo na kazi ya Baruku. Pia fikiria matokeo yangekuwa nini ikiwa Yehova angebomoa kile ambacho alikuwa amekijenga kama tunavyosoma katika Yeremia 45:4. Huenda “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia, iwe ni umashuhuri zaidi katika makao ya mfalme au utajiri, yangekuwa ubatili. Ikiwa Baruku alikuwa anatafuta cheo katika mfumo wa Kiyahudi wa wakati huo uliokuwa umehukumiwa, basi Mungu alikuwa na sababu nzuri ya kumzuia.
6, 7. Ikiwa “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia ni vitu vya kimwili, ni mambo gani tunayoweza kufikiria kwa uzito?
6 Kwa upande mwingine, huenda “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia yalikuwa utajiri. Mataifa yaliyokuwa jirani ya Yuda yalitegemea sana vitu vya kimwili na utajiri. Taifa la Moabu lilitegemea ‘kazi na hazina zake.’ Ndivyo na taifa la Amoni pia. Yeremia akiongozwa na Yehova alifananisha Babiloni na mwanamke “mwenye hazina nyingi.” (Yer. 48:1, 7; 49:1, 4; 51:1, 13) Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mungu aliyashutumu mataifa hayo.
7 Hivyo basi, ikiwa Baruku alikuwa akitafuta vitu vya kimwili na utajiri, inaeleweka ni kwa nini Yehova alimwonya asifanye hivyo. Mungu ‘aliponyoosha mkono wake juu’ ya Wayahudi, nyumba zao na mashamba yao yalitekwa na adui zao. (Yer. 6:12; 20:5) Tuseme ungekuwa unaishi Yerusalemu katika siku za Baruku. Wengi wa wakaaji—kutia ndani wakuu, makuhani, na mfalme mwenyewe—wanataka kupigana dhidi ya Wababiloni wanaovamia. Hata hivyo, ulisikia ujumbe wa Yeremia: “Mtumikieni mfalme wa Babiloni, mwendelee kuishi.” (Yer. 27:12, 17) Je, ingekuwa rahisi kwako kutii agizo hilo la Mungu ikiwa ungekuwa na vitu vingi jijini humo? Je, maoni yako kuelekea vitu hivyo yangekuchochea kutii onyo la Yeremia au ungefuatana na umati? Vitu vyote vyenye thamani vya Yuda na Yerusalemu, kutia ndani vitu vilivyokuwa hekaluni, viliporwa na kupelekwa Babiloni. Hivyo, kufuatilia vitu vya kimwili kungekuwa kazi bure. (Yer. 27:21, 22) Tunaweza kujifunza lolote kutokana na jambo hilo?
Yehova alirekebisha jinsi gani mtazamo wa Baruku wa kujitafutia “makuu”? kwa nini kukubali kurekebishwa na Mungu ni jambo la hekima?
“NITAKUPA WEWE NAFSI YAKO KUWA NYARA”
8, 9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba halikuwa jambo dogo kwa Baruku kupokea nafsi yake kama nyara?
8 Sasa fikiria jambo hili: Baruku angepata nini kwa kutii agizo la Mungu? Nafsi yake! Alihakikishiwa ataipata ikiwa “nyara.” (Soma Yeremia 45:5.) Ni watu wachache waliokoka. Akina nani? Wale tu waliotii agizo la Mungu ya kwamba wajisalimishe, au kujitia mikononi mwa Wakaldayo. (Yer. 21:9; 38:2) Hata hivyo, huenda wengine wakauliza, ‘Yaani, hilo tu ndilo walilopata kwa kutii?’
9 Wazia mambo yalivyokuwa Yerusalemu lilipozingirwa na Wababiloni. Ni kana kwamba Yerusalemu lilikuwa likiteketea polepole. Kwa upande mwingine, tofauti na Yerusalemu, ni kana kwamba Sodoma liliangamizwa kwa dakika moja. Twaweza kusema kwamba watu hawakuteseka sana wakati wa uharibifu wa Sodoma. (Omb. 4:6) Baruku aliandika unabii uliotabiri kwamba wakaaji wa Yerusalemu wangekufa kwa upanga, njaa, au tauni. Yaelekea alishuhudia utimizo wa unabii huo. Jijini Yerusalemu chakula kilikuwa haba. Lilikuwa jambo lenye kutisha kama nini kuwaona akina mama, ambao kiasili ni wenye “huruma,” wakiwatokosa na kuwala watoto wao wenyewe! (Omb. 2:20; 4:10; Yer. 19:9) Hata hivyo, Baruku aliokoka. Bila shaka, katika kipindi hicho chenye kufadhaisha kwelikweli, uhai wenyewe ulikuwa kama nyara, au zawadi wanayotunukiwa askari walioshinda vitani. Ni wazi kwamba Baruku alikubali na kufuata shauri la Mungu la kutojitafutia “makuu.” Na kuokoka kwake ni uthibitisho wa kutosha kwamba alipata kibali cha Yehova.—Yer. 43:5-7.
JE, UTATAFUTA “MAKUU”?
10, 11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi ya Baruku leo, na hata katika maisha yetu binafsi?
10 Ingawa Baruku alikuwa akifanya mapenzi ya Mungu kwa bidii, kwa muda fulani alipambana na tamaa ya kutaka “makuu.” Yehova alimwonya kuhusu hatari ya kufanya hivyo, naye akaokoka msiba wa kiroho na wa kimwili. Kama Baruku, je, tunaweza kujaribiwa na labda hata kulemewa na tamaa za moyo wetu, hata tunapoendelea kumtumikia Yehova kwa bidii?
11 Huenda Baruku alitamani sana kujijengea jina. Wazia akijiuliza: ‘Nitapoteza kazi yangu ya “mwandishi”? Nitapandishwa cheo?’ Namna gani sisi leo? Jiulize: ‘Ninajitakia “makuu” moyoni mwangu, labda mafanikio katika kazi ya kimwili sasa hivi au baada ya muda usio mrefu?’ Vijana Wakristo wanaweza kujiuliza, ‘Tarajio la kupata umashuhuri na pesa nyingi kutokana na masomo kunaweza kunishawishi kujitafutia “makuu”?’
12. Ndugu mmoja alimtafutia Yehova makuu jinsi gani, nawe unauonaje uamuzi wake?
12 Ndugu ambaye sasa anatumikia katika makao makuu alipata fursa ya kulipiwa masomo ya chuo kikuu alipokuwa na umri wa miaka 15. Mwalimu wake alisikitika sana kijana huyo alipoukataa msaada huo na badala yake akaamua kufanya upainia. Hata hivyo, kupenda kwake kujifunza hakukuishia hapo. Baadaye akawa mmishonari katika kisiwa fulani cha mbali. Akiwa huko akaanza kujifunza lugha inayozungumzwa na watu wapatao 10,000. Hakukuwa na kamusi katika lugha hiyo, kwa hiyo akajitungia orodha yake mwenyewe ya maneno. Mwishowe akaijua vizuri lugha hiyo naye akapewa mgawo wa kutafsiri baadhi ya vitabu vyetu. Baadaye, orodha ya maneno aliyotunga ilitumiwa kuwa msingi wa kamusi ya kwanza katika lugha hiyo. Pindi moja aliuambia umati mkubwa katika kusanyiko moja la wilaya: “Kama ningekubali elimu ya chuo kikuu, mafanikio yoyote ambayo ningepata yangeniletea utukufu mimi mwenyewe. Lakini kama ilivyo leo, sina vyeti vyovyote vya kielimu. Kwa hiyo, sipati sifa kwa sababu ya mambo ambayo nimetimiza. Sifa zote zinamwendea Yehova.” (Met. 25:27) Unauonaje uamuzi aliofanya alipokuwa na umri wa miaka 15? Kwa miaka mingi amefurahia mapendeleo mengi kati ya watu wa Mungu. Namna gani wewe, ungependa kutumia vipawa vyako jinsi gani? Badala ya kujitafutia utukufu, umeazimia kutumia vipawa vyako kumsifu Yehova?
13. Kwa nini wazazi fulani wanapaswa kutafakari hali ambayo Baruku alikabili?
13 Tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu hili: kutafuta “makuu” kwa ajili ya au kupitia watu tunaowapenda na ambao tunaweza kuwashawishi. Yaelekea umeona jinsi wazazi walimwengu wanavyojitahidi kufanya wawezayo ili mtoto wao afanikiwe zaidi maishani kuliko wao au awe mtu ambaye wanaweza kujisifia. Labda umesikia wengine wakisema: “Sitaki ataabike kama vile ambavyo nimetaabika” au “Nataka mtoto wangu aende chuo kikuu ili awe na maisha mazuri.” Huenda wazazi Wakristo pia wakawa na maoni kama hayo. Ni kweli kwamba huenda mtu akasema, ‘Sijitafutii makuu.’ Hata hivyo, je, anaweza kuwa anajitafutia makuu kupitia mtu mwingine, labda mwana au binti yake? Kama vile huenda Baruku alitamani kupata makuu kupitia cheo au kazi yake, huenda moyoni mzazi akajitafutia makuu kupitia mafanikio ya mtoto wake. Hata hivyo, je, “mchunguzaji wa mioyo” hatatambua hilo, kama alivyofanya katika kisa cha Baruku? (Met. 17:3) Kama alivyofanya Daudi, tunapaswa kumwomba Mungu achunguze hisia zetu za ndani kabisa. (Soma Zaburi 26:2; Yeremia 17:9, 10.) Yehova anaweza kutumia njia mbalimbali, kutia ndani habari ambazo tumezungumzia kuhusu Baruku, ili kutuonya kuhusu hatari ya kujitafutia “makuu.”
Huenda Baruku alikuwa akijitafutia “makuu” kwa njia gani? Nawe unaweza kujifunza nini?
MTEGO WA “VITU VYENYE THAMANI”
14, 15. Utajiri unaweza kuwa “makuu” kwetu jinsi gani?
14 Fikiria uwezekano wa kwamba “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia ni utajiri. Kama ilivyotajwa, ikiwa Baruku angehangaikia sana mali yake huko Yuda, huenda haingekuwa rahisi kwake kutii onyo la Mungu la kujitia mikononi mwa Wakaldayo. Huenda umeona kwamba mara nyingi tajiri hutegemea ‘vitu vyake vyenye thamani,’ lakini kulingana na Biblia ulinzi huo upo “katika mawazo yake.” (Met. 18:11) Watumishi wote wa Yehova wanaweza kufaidika kwa kujikumbusha maoni yenye usawaziko kuhusu vitu vya kimwili yanayopatikana katika Neno la Mungu. (Soma Methali 11:4.) Hata hivyo, huenda wengine wakauliza, ‘Kuna ubaya gani wa kufurahia kwa kiasi fulani vitu vya ulimwengu?’
15 Kupenda mali kunaweza kumfanya Mkristo aanze kutamani vitu ambavyo ni sehemu ya mfumo wa mambo unaopita. Yeremia na Baruku hawakufanya hivyo. Miaka mingi baadaye, Yesu aliwapa onyo watu ambao wangekuwapo siku ambayo “Mwana wa binadamu atafunuliwa.” Yesu aliwaambia: “Mkumbukeni mke wa Loti.” Leo, Wakristo wanaweza kufaidika kutokana na onyo kama hilo: ‘Mkumbukeni Yeremia na Baruku.’ (Luka 17:30-33) Tukipenda sana vitu vya kimwili, itakuwa vigumu kwetu kutii maneno ya Yesu. Hata hivyo, usisahau kwamba kwa kutii onyo la Mungu, Baruku aliendelea kuishi.
16. Simulia kisa kinachoonyesha kwamba watumishi wa Mungu walikuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili.
16 Fikiria hali ya ndugu zetu nchini Rumania wakati wa utawala wa Kikomunisti. Maofisa wa serikali walipokuwa wakipekua nyumba za Mashahidi, nyakati nyingine walinyakua mali zao, hasa vitu ambavyo wangeweza kuviuza. (Omb. 5:2) Ndugu na dada wengi katika enzi hizo walikuwa tayari kupoteza mali zao. Baadhi yao walilazimika kuacha vitu na mali zao walipohamishiwa kwingineko; hata hivyo, waliendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova. Ukijikuta katika hali kama hiyo, utaruhusu kupenda vitu vya kimwili kukuzuie kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu?—2 Tim. 3:11.
17. Huenda Yeremia na Baruku walitegemezwa jinsi gani na watumishi wengine wa siku zao?
17 Yaelekea Yeremia na Baruku walitegemezwa na watumishi wengine wa siku zao. Sefania alitoa unabii wakati wa utawala wa Yosia, Yeremia akiwa nabii. Yeremia angeyaonaje maneno ya Sefania 1:18? (Soma.) Labda Yeremia alizungumza na Baruku kuhusu ujumbe huo uliopuliziwa na Mungu. Nabii mwingine aliyeishi wakati huo ni Ezekieli, ambaye alichukuliwa mateka na kupelekwa Babiloni mwaka wa 617 K.W.K. Ujumbe wake uliwahusu moja kwa moja Wayahudi waliorudi katika nchi yao, hivyo, inawezekana Yeremia alipata kujua mambo ambayo Ezekieli alisema au kutenda na huenda Ezekieli pia alipata kujua mambo ambayo Yeremia alisema au kutenda. Ujumbe wa Ezekieli unatia ndani maneno yaliyo katika Ezekieli 7:19. (Soma.) Kama vile Yeremia na Baruku wangeweza kufaidika na maneno hayo yaliyoongozwa na roho, sisi pia tunaweza kufaidika. Watu wataita miungu yao iwaokoe katika siku ya Yehova. Hata hivyo, miungu yao wala pesa zao hazitawaokoa.—Yer. 2:28.
UTAIPATA ‘NAFSI YAKO KAMA NYARA’?
18. Tungependa kuipata “nafsi” ya nani kama nyara, nasi tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?
18 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova ametuahidi “nafsi” yetu kama nyara. Hata watumishi wake wachache wakifa kwa sababu ya mateso yanayoweza kutokea wakati wa “dhiki kuu” pembe za kisiasa za yule mnyama-mwitu zitakapogeukia dini, waaminifu hao hawatakuwa wamepoteza chochote. “Nafsi” yao imehakikishiwa kuishi tena na kufurahia “uzima ulio wa kweli” katika ulimwengu mpya. (Ufu. 7:14, 15; 1 Tim. 6:19) Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba wengi kati ya watumishi wa Mungu watakaokuwa waaminifu wakati huo wataokoka dhiki kuu. Unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atakapoleta msiba dhidi ya mataifa, hakuna mwaminifu atakayekuwa kati ya “wale waliouawa na Yehova.”—Yer. 25:32, 33.
Chagua kile ambacho kwa kweli ni chenye thamani (Linganisha ukurasa wa 46.)
19. Masimulizi ya Yeremia na Baruku yameimarisha jinsi gani azimio lako la kuepuka kujitafutia “makuu”?
19 Huenda wengine wakazindushwa na wazo la kwamba labda wataokoka na “nafsi” yao tu ikiwa kama nyara. Hata hivyo hilo halipaswi kuwavunja moyo. Kumbuka kwamba watu wa Yerusalemu walipokuwa wakifa kutokana na njaa, Yehova alimhifadhi hai Yeremia. Jinsi gani? Mfalme Sedekia alimtia Yeremia kifungoni katika Ua wa Walinzi na kuagiza apewe “mkate wa mviringo kila siku kutoka kwenye barabara ya waokaji, mpaka mkate wote ulipokwisha jijini.” (Yer. 37:21) Na Yeremia akaokoka! Yehova anaweza kutumia njia yoyote ile kuwategemeza watu wake. Vyovyote vile, atawategemeza hakika, kwa kuwa tumaini lao la kuishi milele limehakikishwa. Baruku aliokoka uharibifu wa Yerusalemu kwa kutojitafutia “makuu.” Sisi nasi, tunaweza kutazamia kuokoka Har–Magedoni na kumsifu Yehova tukiwa na “nafsi” zetu kama nyara tunayoweza kufurahia milele.
Kwa nini ni jambo la hekima leo kutojitafutia “makuu,” badala yake tutazamie kuipata “nafsi” yetu ikiwa kama nyara?