Inakupasa Kuchagua Njia Inayofaa Sasa
1, 2. (a) Kwa habari ya ibada, Biblia inasema kutakuwa ulimwengu wa namna gani? (b) Sababu gani sasa ndio wakati wenye uharaka wa kufanya uamuzi juu ya mwendo wa mtu?
KULINGANA na mambo ya hakika yaliyo wazi, wingi wa wanadamu haumwabudu Mungu wa Biblia Takatifu. Katika historia yote iliyopita hesabu iliyo kubwa zaidi ya wakaaji wa dunia haijapata kufanya hivyo kamwe. Matengenezo ya Dini ya Jumuiya ya Wakristo yanadai kufanya hivyo. Matengenezo mengine machache ya kidini yanaweza kudai pia yanafanya hivyo kwa kufuata sehemu tu ya Biblia. Walakini yote yale yanayodai namna fulani ya dini yatakapoharibiwa au kukazwa yaache namna yao ya ibada, je! itatokeza badiliko kubwa? Au Je! ulimwengu huu utakuwa ulimwengu wa namna gani? Utakuwa namna ya ulimwengu ambao Biblia inatabiri utatokea karibuni, ulimwengu usio wa kidini utakaokuwapo kwa muda mfupi.
2 Hata hivyo, kwa wazi zaidi kuliko wakati mwingine wo wote uliopita utamwabudu “mungu wa taratibu hii ya mambo.” nayo Biblia inayomfunua “mungu huyo inasema kwamba yeye ni adui mkuu wa Yehova, Shetani Ibilisi. (2 Kor. 4:4, NW) Yesu Kristo alimwita “mkuu” au “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 16:11) Wakati, punde si punde, ulimwengu wote utakapolazimishwa kumwabudu “mungu” huyo wa uongo, mtu ambaye sasa anatishwa na wazo hilo afanyeje? Atakuwa na nguvu ya kidini kufanya jambo gani? Inashauriwa kwamba sasa ndio wakati wenye uharaka wa kufanya uamuzi!
3. Yehova alifanya uamuzi wake muda mrefu kadiri gani kabla ya kuufikiliza juu ya mataifa?
3 Yoeli 3:14 latabiri hivi: “Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno! Kwa maana siku ya [Yehova] i karibu, katika bonde la kukata maneno.” Biblia ya The Living Bible inayo maandishi kamili zaidi ya Yoeli 3:14 nayo yasema hivi: “Umati mkubwa, umati mkubwa ukingojea katika bonde la uamuzi wa kuhukumiwa kwao maangamizi! Kwa kuwa Siku ya Bwana imekaribia, katika Bonde la hukumu.” Biblia ya The Bible in Living English, ya Byington, inapaita “Bonde la Uamuzi.” Nabii Yoeli alimaliza kitabu chake wapata mwaka 820 K.W.K. Hiyo ilikuwa zaidi ya miaka 200 kabla Yehova hajafikiliza kwa halisi “uamuzi” wake juu ya mataifa ya wakati huo wa kale.
4. (a) Kwa habari hiyo, Yehova alituwekeaje mfano mzuri? (b) Baruku mwana wa Neria alituwekeaje mfano mzuri?
4 Yehova alituwekea sisi mfano mzuri. Yeye alifanya uamuzi wake kimbele na kuutangaza waziwazi. Sisi leo, tukiwa katika wakati wenye hatari pia, kila mmoja wetu apaswa kufanya uamuzi wa binafsi kabla ya msiba unaokuja wa ulimwengu. Kuwa na wazo kwamba wakati huo mtu ataweza kubadili ghafula mwendo aliodumu ndani yake na kufanya uamuzi unaofaa na hivyo kuepuka kushiriki katika msiba huo ni kujihatirisha kwa kujidanganya mwenyewe. Mtu aliye mfano mzuri aliyetenda ifaavyo miaka 18 kabla ya msiba wa mataifa yote ambao alipashwa habari zake katika mwaka 625 K.W.K. alikuwa Baruku mwana wa Neria. Mwaka 625 K.W.K. ulikuwa mwaka wa nne wa utawala wa mfalme wa tatu wa mwisho wa Yerusalemu uliohukumiwa maangamizi. Jina lake lilikuwa Yehoyakimu mwana wa Yosia. Alikalia kiti cha enzi katika mwaka 628 K.W.K., baada ya nduguye mchanga zaidi, Yehoahazi, kuondolewa juu ya kiti cha enzi na Farao Neko wa Misri na kupelekwa mpaka Misri.
5, 6. (a) Sababu gani ulikuwa mwaka wenye hatari wakati neno la Yehova kupitia kwa Yeremia lilipomjia Baruku? (b) Kulingana na Yeremia 45:1-3, Baruku alikuwa anajisikiaje?
5 Baada ya Yehoyakimu kutawala kwa miaka mitatu akiwa anatii Misri, kuhani-nabii Yeremia alipata ujumbe kutoka kwa Yehova wa kumpa mwandishi wake, Baruku mwana wa Neria. Sasa ulikuwa mwaka wa nne wa Mfalme Yehoyakimu. Huo ulikuwa mwaka wenye hatari, kwa kuwa katika mwaka huo (625 K.W.K.) Nebukadreza mwana wa Nabopolasa alipata kuwa mfalme wa Babeli. Sasa mfalme wa Yerusalemu angepaswa kupambana na mtawala wa Mamlaka ya Ulimwengu ya Tatu, Babeli, aliyeshinda Milki ya Ashuru. Ebu hapa tusome Yeremia 45:1-3:
6 “Neno hili ndilo ambalo Yeremia, nabii, alimwambia Baruku, mwana wa Neria, alipoyaandika maneno haya katika kitabu kwa kinywa cha Yeremia, mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, kusema, [Yehova], Mungu wa Israeli, akuambia wewe, Ee Baruku; Ulisema, Ole wangu! kwa maana [Yehova] ameongeza huzuni pamoja na maumivu yangu. Nimechoka kwa ajili ya kuugua kwangu, wala sioni [mahali pa kupumzika].”
7. Huenda ikawa Baruku alijisikiaje alipoona hali yenye kuharibika zaidi ya Yerusalemu, nao ujumbe wa Yeremia juu ya kuhukumiwa maangamizi uliorudiwa-rudiwa huenda ukawa ulikuwa na matokeo gani juu ya Baruku?
7 Hatujui ni muda mrefu kadiri gani Baruku alikuwa ametumikia kama mwandishi wa Yeremia kabla ya hapo, walakini alikuwa angali na angaa miaka 18 zaidi ambayo angepaswa kuwa mwenzi wa nabii huyo. “Maumivu” ambayo alipata kwa kuona hali yenye kuharibika zaidi na zaidi ya ufalme wa Yuda, hatuwezi kufahamu; lakini sasa, licha ya hayo, alipaswa kuandika ujumbe wenye kuhuzunisha kama ulivyosemwa na Yeremia. Yeye angeona kama vile Yeremia wakati nabii huyo alipoandika kitabu cha “Maombolezo” baada ya Yerusalemu kuharibiwa katika mwaka 607 K.W.K. na mfalme wa Babeli. Pengine utabiri wa Yeremia wenye kuendelea na wa kurudiwa-rudiwa juu ya kuhukumiwa maangamizi ulimchosha Baruku.
8. Sasa Yehova alimfunulia Baruku kuwa kusudi lake lilikuwa nini, walakini Baruku alikuwa akijitafutia nini?
8 Baruku hakuwa na taraja la ‘mahali pa kujipumzisha.’ Yehova aliona maelekeo ya ndani ya Baruku na kumwambia Yeremia amwarifu hivi: “[Yehova] asema hivi, Tazama, niliyoyajenga nitayabomoa, na niliyoyapanda nitayang’oa; na haya yatakuwa katika nchi yote. Je! unajitafutia mambo makuu? usiyatafute.”—Yer. 45:4, 5.
9, 10. Sababu gani Yehova alikuwa na sababu ya kutokubaliana na utafutaji wa Baruku wa “mambo makuu” yake wakati huo?
9 Ingawa Yehova hakumtajia Baruku, yeye alifahamu yale “mambo makuu” aliyokuwa akijitafutia. Kwa wazi Yehova hakuyakubali, na kwa hiyo alipaswa kuacha kuyatafuta. Sababu gani?
10 Ilikuwa kwa sababu ya kusudi la Yehova la wakati huo. Katika mwaka uo huo alikuwa amemtokeza Nebukadreza kama mfalme wa Babeli, naye huyo ndiye aliyekusudia kumtumia kama mwuaji wa watu wa Baruku. Sana sana kuanzia siku za Mfalme Daudi (1077-1037 K.W.K.), Yehova alikuwa ameusimamisha ufalme wa Israeli, walakini sasa, kupitia kwa Nebukadreza, alikuwa anakaribia kuangusha serikali hiyo ya kifalme, iendelee katika hali ya kutotenda kwa miaka 2,520, au mpaka mwaka 1914 wa karne yetu wenyewe. Huko nyuma katika mwaka 1473 K.W.K., Yehova alilipanda taifa la Israeli katika Nchi ya Ahadi, lakini sasa, baada ya zaidi ya miaka 800, alikuwa karibu kuling’oa. Nchi ya ufalme wa Yuda ingepaswa kukaa ukiwa pasipo Myahudi wala mnyama wa kufugwa kwa miaka 70. Kwa sababu ya mambo hayo yenye kukaribia, je! ulikuwa wakati unaofaa kwa mtu aliyefahamu kusudi la Yehova kama lilivyotangazwa na Yeremia awe akitafuta “mambo makuu” yake mwenyewe? Sivyo kabisa!
11. Ni jambo gani lililotegemea Baruku kufanya uchaguzi ufaao, na wakati uo huo?
11 Hiyo ndiyo sababu Yehova alimwambia aache kutafuta mambo hayo. Namna gani Baruku akiendelea kutafuta mambo ya kichoyo? Je! angeweza kuwa na upatano wa moyoni na ujumbe ambao alikuwa akitumiwa auandike na kuutangaza? Sivyo! Mtengano fulani kati yake na nabii wa Yehova, Yeremia, ungefuata. Iwapo Baruku angetaka kuendelea kuwa na upatano wa moyoni pamoja na Yeremia na ujumbe wake, basi angepaswa kuacha kujitakia makuu kwa uchoyo. Kulikuwa kungali miaka 18 ya kupita ndipo msiba uliotabiriwa ufike, na hali sasa lilikuwa jambo la lazima Baruku afanye uamuzi. Uhai wake wenyewe, ‘nafsi’ yake, ulitegemea kufanya kwake uamuzi unaofaa, ndiyo, kushikamana nao. Alipaswa kufanya jambo hilo iwapo hakutaka kuvunja uhusiano wake.
12. Kama ilivyokuwa katika habari ya Baruku, sababu gani ni jambo la hekima sasa kwetu kuacha kujitafutia wenyewe “mambo makuu” katika ulimwengu huu kwa vyo vyote?
12 Loo! namna hali yenye hatari ya Baruku inavyofanana sana na yetu sisi watu wa leo tuliopashwa habari! Sana sana ndivyo ilivyo kuanzia mwaka 1914 kuendelea, kwa kuwa tangu wakati huo Mashahidi wa Yehova wamehubiri kwamba Jumuiya ya Wakristo, mfano wa kisasa wa Yerusalemu usioaminika, itaharibiwa na aliye mkuu zaidi kuliko Nebukadreza, Mfalme wa kimbinguni anayetawala sasa, Yesu Kristo. Kwa hiyo ni jambo la upumbavu sana kwa ye yote aliye katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu kutafuta “mambo makuu” yake mwenyewe katika taratibu hii ya mambo inayovunjika-vunjika katika wakati huu wa sasa wenye hatari. Jambo hilo lingeonyesha kukosa kuthamini kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho.” Jambo hilo lingeonyesha kukosa imani na uhakika katika usahihi na wakati unaofaa wa ujumbe unaotangazwa na jamii ya Yeremia kuhusiana na kuhukumiwa maangamizi kwa hii taratibu mbovu ya mambo ya kale. Uhai wa mtu, ‘nafsi’ yake, umo hatarini! Sasa Yehova yu karibu kufanya kazi yake ya kuharibu na kung’oa, kupitia kwa wakili aliye mwenye nguvu zaidi kuliko Nebukadreza, Yesu Kristo. Je! tunataka kuangamizwa pamoja na mfano wa kisasa wa Yerusalemu wenye kuasi, Jumuiya ya Wakristo? Ikiwa sivyo, basi twapaswa kufanya uamuzi wetu maadamu wakati ungalipo kufanya yale ambayo Yehova alimwambia mwandishi wa Yeremia, Baruku, afanye, nayo hayo ni kuacha kutafuta “mambo makuu” katika ulimwengu huu.
13. Sasa ni wakati wetu kushirikiana na jamii ya Yeremia katika kufanya jambo gani?
13 Sisi mmoja mmoja na tuishi kulingana na ujumbe unaotangazwa na jamii ya Yeremia. Na tuachane na kujitakia mambo makuu ya kichoyo, kutoweka mapendo yetu juu ya mambo ya muda ya taratibu hii ya mambo iliyohukumiwa maangamizi. Jambo hilo linatutaka tushiriki kwa ujasiri pamoja na jamii ya Yeremia katika kuonya juu ya “siku ya kisasi” ya Yehova inayokuja. Huu si wakati wa kuwa na moyo uliogawanyika.—Isa. 61:1, 2.
14, 15. (a) Kama zawadi ya kutii, Baruku angepata nini kama “nyara” yake? (b) Je! ndivyo mambo yalivyokuwa?
14 Zawadi ya kufanya jambo hilo ni nini? Inaonyeshwa wazi na yale ambayo Yeremia aliambiwa amwambie Baruku “Kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili, asema [Yehova]; lakini [nafsi] yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.”—Yer. 45:5b
15 Ndivyo ilivyokuwa kweli kweli kwa Baruku. Jambo hilo linaonyesha kwamba yeye alifanya uamuzi unaofaa pasipo kuchelewa isivyofaa. Jambo hilo linahakikishwa katika sura inayotangulia, katika Yeremia 43:5-7, ambayo inaeleza juu ya yale yaliyotokea baada ya Yerusalemu kuharibiwa katika mwaka 607 K.W.K. Twasoma hivi: Wayahudi wenye kuogopa waliookoka walipokuwa wakikimbia kutoka nchi ya Yuda kwenda Misri waliwachukua “Yeremia, nabii, na Baruku, mwana wa Neria; wakaingia nchi ya Misri; maana hawakuitii sauti ya [Yehova]; wakafika hata Tahpenesi,” kaskazini mwa Misri. Hata baada ya jambo hilo Yeremia aliendelea kutabiria Wayahudi hao wasiotii.—Yer. 43:8–44:30.
16. Iwapo Baruku aliokoka mpaka wakati mfalme wa Babeli alipoipindua Misri, angeweza kutazamia jambo gani kutoka kwa mshindi huyo?
16 Wayahudi hao wenye kujitakia yao hawakuepuka utawala wa Mamlaka ya Ulimwengu ya Babeli kwa muda mrefu, kwa kuwa muda si muda Nebukadreza aliiongeza Misri katika eneo la milki yake. Iwapo Yeremia na Baruku waliokoka na kushuhudia kutwaliwa huko na Babeli, wasingepatwa na hasira ya Nebukadreza. Yeye alikuwa na sababu ya kuwakumbuka kwa fadhili. Baruku angeendelea kuwa na ‘nafsi’ yake kama nyara ili kuondolea lawama ahadi ya Yehova katika Yeremia 45: 5. Ndipo angethamini kabisa namna alivyokuwa mwenye hekima na mwenye akili nzuri kwa kuachana na mwendo wa wakati usiofaa wa kutafuta “mambo makuu” yake.
17. Twaweza kupata faida gani kutokana na utii wa Baruku kuwa mfano wa jambo la kufanya?
17 Je! sisi leo twaweza kupata faida kutokana na utii wa Baruku wa kujinyenyekeza chini ya shauri la kusahihisha la Yehova? Ndiyo! Hata tuwe tuna uhusiano wa karibu namna gani na jamii ya Yeremia, twafanya jambo linalokubaliwa na Mungu kwa kutojitwalia wenyewe “mambo makuu” wakati wa hizi siku za mwisho za Jumuiya ya Wakristo. ‘Nafsi’ yetu, uhai wetu, kama watu, ni wa thamani kubwa zaidi kuliko “mambo makuu” yaliyohukumiwa maangamizi yapite pamoja na ulimwengu huu mwovu, hivyo kumwacha kila mtu na ‘nafsi’ yake tu. Kwa hiyo kuwa hai kama ‘nafsi’ chini ya kibali ya kimungu litakuwa jambo la thamani zaidi sana kuliko kufurahia sasa kwa kitambo mambo yo yote yanayoweza kuharibika ya Jumuiya ya Wakristo na Matengenezo ya Dini yote.
KUEPUKA LAANA KWA AJILI YA KUTOTUMIA “UPANGA”
18, 19. Sababu gani “siku ya kisasi” cha Yehova haikuwa imemalizika baada ya msiba uliopata Yuda na Yerusalemu?
18 Baruku na Yeremia walihuzunika kwa ajili ya uharibifu wa Yerusalemu na kuondolewa kwa watu kutoka katika nchi hiyo. Walakini mataifa ya kipagani yaliyokuwa karibu karibu au yaliyowazunguka yalifurahi sana kwa ajili ya msiba huo uliowapata watu wa agano wa Yehova. (Zab. 83:6-8; 137:7) Bila shaka, Misri haikufurahi kabisa, kwa kuwa ilikuwa inafurahia kutiiwa na Yuda na Yerusalemu na kuwa na urafiki nazo. Pamoja na hayo, ufalme wa Yuda ulikuwa umetumika kama eneo la kukinga kati yake na mamlaka ya ulimwengu yenye kuogopesha, Babeli. Hata hivyo Misri ilikuwa imejifanyia kumbukumbu lenye sifa kwa habari ya Yuda na mji wake mkuu, Yerusalemu, ambako ‘kiti cha enzi cha Yehova’ kilikuwa kimekaliwa na wafalme wa nasaba ya kifalme ya Daudi. Chuki mbaya ya mataifa juu ya watu wa agano wa Yehova ilionekana naye, kwa kuwa ibada yake ilihusika.
19 Kwa hiyo “siku ya kisasi” ya Yehova haikuwa imepita wakati alipomtumia mfalme wa Babeli kama chombo chake cha kuupindua ufalme wa Yuda. Kikombe cha msiba wa taifa zima ambacho kilikuwa kimewekwa kwenye midomo ya Yuda na Yerusalemu kilistahili kupewa kwa mataifa hayo yenye kunia mabaya yapate kupinduliwa kama wachukiaji wa Yehova.
20. (a) Yehova alimwongoza Yeremia kwa roho afanye jambo gani kwa habari ya mataifa hayo yenye Kunia mabaya? (b) Yeremia 48:10 ilitamkwa kwa habari ya nani, na je! walijionyesha kuwa walistahili laana hiyo?
20 Kwa hiyo Yehova alimwongoza Yeremia kwa roho apate kumalizia unabii wake kwa kutabiri juu ya kupinduliwa kwa nguvu kwa mataifa maovu kama vile Misri, Ufilisti, Moabu, Amoni, Edomu, Kedari na hata Elamu. (Yer. 46:1—49:39; 25:15-33) Wababeli chini ya Mfalme Nebukadreza ndio ambao Yehova alikuwa akikusudia kutumia katika kunyanyua “upanga” wa kuua juu ya mataifa hayo yaliyomkaidi Mungu wa kweli. Kwa hiyo Yehova alimwongoza Yeremia kwa roho aseme hivi kuhusiana na mataifa hayo: “Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya [Yehova] kwa ulegevu; na alaaniwe auzuiaye upanga wake usimwage damu.” (Yer. 48:10) Wala Wababeli hao wala Mfalme Nebukadreza hawakupatwa na laana hiyo kwa kutofikiliza kikamilifu “kazi” yao waliyopewa na Mungu.
21. (a) Je! Yeremia na Baruku ‘walilaaniwa’ kwa kutotumia “upanga” wa chuma? (b) Je! Mashahidi wa Yehova ndio watakaoondolea mbali Jumuiya ya Wakristo, au ni nani atakayefanya hivyo?
21 Hata hivyo, namna gani sisi leo? Je! twaweza kuja chini ya laana kama hiyo kwa ajili ya kupuza mgawo wetu, kwa kujiepusha kwa habari ya “upanga”? Ni kweli, twafahamu kwamba wala Yeremia wala Baruku hawakunyanyua upanga wa chuma juu ya mataifa hayo adui. Huo hakuwa mgawo wao. Mgawo huo walipewa Wababeli chini ya mfalme wao aliyetawazwa karibuni, Nebukadreza. Jamii ya Yeremia ya leo ikiwa Mashahidi wa Yehova haitatumia nguvu juu ya Jumuiya ya Wakristo, mfano wa Yerusalemu yenye kuasi na milki yake. Waliokuwa washiriki wa kisiasa wa Jumuiya ya Wakristo wakati mmoja na watu wengine wasiomcha Mungu wataiharibu bila kujali hata kidogo, kama vile tu mataifa yaliyobaki yalivyokuwa na furaha kwa ajili ya kuondolewa mbali kwa Yerusalemu na ufalme wake usiwe jirani yao.—Ufu. 17:12-18.
22. Ni nani ambao hawatashiriki matumaini makubwa ya watakaoharibu Matengenezo ya Dini yote, nayo maoni yao yatakuwa nini juu ya mamlaka mpya yenye kutawala?
22 Hata hivyo, kufutiliwa mbali kwa Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyingine zote za milki ya ulimwengu ya dini ya uongo kutabakiza nini katika tamasha ya kidunia? Vikosi vya Kisiasa, visivyo vya kidini, vipate kuchukua uongozi wa mambo ya kibinadamu! Watafanya hivyo wakiwa na matumaini makubwa ya kufaulu na wakijiona kutulia kwa sababu ya kutoamrishwa tena na Matengenezo ya Dini. (Linganisha Ezekieli, sura 23.) Walakini matumaini hayo yenye kumkaidi Mungu hayatakuwa ya jamii ya Yeremia na wenzi wao wenye kumwogopa Mungu, hata ingawa wao wanaweza kuonyesha utii wa kadiri kwa mamlaka hiyo mpya yenye kutawala kama “mamlaka iliyo kuu.”—Rum. 13:1, 2.
23. Kisha ni nini kitakachofanya sehemu iliyobaki “siku ya kisasi” cha Yehova itimizwe?
23 Wakati huo “siku ya kisasi” cha Yehova itakuwa imekwisha anza, walakini haitamalizika wakati wa kuharibiwa kwa Matengenezo ya Dini, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Lazima iendelee mpaka “kisasi” kamili cha kimungu kimwagwe juu ya wapinzani wote wa enzi kuu ya ulimwenguni pote ya Yehova. Lakini kwanza watajaribu kufanya jamii ya Yeremia na wenzi wao washikamanifu wajipatanishe kabisa na taratibu hii ya mambo isiyomcha Mungu, kama vile Yohana na wafuasi wake walivyowachukua Yeremia na Baruku kifungoni na kuwaendesha kwa miguu kwa kushurutishwa mpaka Misri. Wakishindwa na jambo hilo, watashambulia kabisa waabudu hawa wa Yehova wasioridhiana (wasiogeuza nia). Kama vile vikosi vya mataifa yote vinavyoongozwa na Gogu wa nchi ya Magogu, watajaribu kuteka paradiso ya kiroho ya mabaki wa Yehova na wenzi wao wasiotengeka. Kwa njia hiyo wakijaribu kupata uongozi kamili wa ulimwengu, watajionyesha wenyewe kuwa wanastahili kuwakiwa na kisasi cha Yehova.—Eze. 38:1–39:20.
24. Kisha ni nani watakaopinga shambulio hilo, na je! wao watastahili ‘kulaaniwa’ kwa kukosa kujali au kuzuia upanga?
24 Halafu? Ufunuo 19: 11-21 unaonyesha kwamba Yesu Kristo, mshindi mkuu zaidi kuliko Mfalme Nebukadreza, atapanda farasi pamoja na majeshi ya kimalaika kupinga shambulio hilo. Wao hawatalaaniwa kwa sababu ya kutekeleza mgawo wao waliopewa na Yehova kwa kutojali. Hawatastahili kulaaniwa kwa sababu ya kuzuia “upanga” wa kuua usimwage damu ya adui. (Yer. 48:10) Watatekeleza kisasi cha Yehova juu ya mataifa yenye uadui. Kwa ajili ya kufanya jambo hilo watabarikiwa kwa ushindi wenye utukufu, hivyo kumwondolea Yehova lawama milele na milele.
25. Basi Mashahidi wa Yehova wanapaswa kumwigaje Yeremia baada ya yeye kuburutwa mpaka kwenye nchi ile aliyotabiri juu yake?
25 Tangu mwaka 1914 tumekuwa katika “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Kwa hiyo sasa jamii ya Yeremia na wenzi wao walio wakf wanapaswa kuvuta fikira za ulimwengu kwenye “upanga” wenye kutisha, chombo cha kuua ambacho Yehova atatumia wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja. (Mt. 24:21) Wanapaswa kumwiga Yeremia ambaye baada ya kuburutwa kwa nguvu toka nchi ya Yuda, alitangaza “upanga” wenye kutisha wa Mfalme Nebukadreza juu ya nchi ambayo aliburutwa mpaka huko, Misri, vilevile Ufilisti, Moabu, Amoni, Edomu na nchi nyingine adui. Hata sasa kabla ya kufyatuka kwa “dhiki kubwa” wako chini ya amri za kimungu “kutangaza . . . siku ya kisasi ya Mungu wetu” juu ya Matengenezo ya Dini na mataifa yote ya kilimwengu. (Yer. 46:1–49:39) “Kazi” yao ni kusikizisha ujumbe huu wa kuonya: “Maana ni siku ya kisasi cha [Yehova], mwaka wa malipo, ili kushindania Sayuni.”—Isa. 34:8.
26, 27. Jamii ya Yeremia inapaswa kuweka moyoni maneno gani ya Yehova aliyompa Ezekieli kama mlinzi?
26 Sasa maneno ya Yesu ya kiunabii katika Luka 21:22 yanatumika: “Kwa kuwa siku hizo ndizo za mapatilizo, ili yatimizwe yote yaliyoandikwa.” Sasa ndio wakati sana sana kwa jamii ya Yeremia kuweka moyoni maneno ambayo Yehova alimwambia Ezekieli, ambaye alianza kutabiri katika Babeli katika mwaka 613 K.W.K., miaka saba kabla ya Yeremia kupelekwa Misri bila kutaka:
27 “Bali mlinzi akiona upanga unakuja, kama hapigi tarumbeta, wala watu hawakuonywa, na upanga ukaja ukamwondoa mtu awaye yote miongoni mwao; ameondolewa huyo katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwa mlinzi huyo. Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa [nafsi] yako.”—Eze. 33:6-9; linganisha Ezekieli 9:2-10.
28. Nia ya jamii ya Yeremia na wenzi wao ni nini kwa habari ya jambo hilo, lakini ni jambo gani linaloweza kutokea, nalo hilo lingemaanisha nini kwao?
28 Jamii ya Yeremia leo na wenzi wao wenye kushirikiana nao hawana nia yo yote ya kuwa na hatia ya damu kwa njia hiyo. Walakini jambo hilo laweza kuwa hivyo. Iwapo, kwa sababu ya kuogopa wanadamu, wanaacha kuonya watu wote juu ya “upanga” wa “siku ya kisasi” ya Yehova na hivyo kushindwa kutekeleza “kazi” yao, watajifanya kuwa wenye kustahili laana. Jambo hilo lingemaanisha kwao kushindwa kuokoka, kwa sababu ya kukosa kutii.
29. Ili kuepuka kufuata njia ya watu wasiosikia baada ya Matengenezo ya Dini kuharibiwa, watu wenye kutafuta uzima wanapaswa kuchagua jambo gani sasa?
29 Wakati, katika “dhiki kubwa” inayokaribia, “upanga” wa kisasi cha kimungu utakapopiga na kuharibu Matengenezo ya Dini yote, watu ambao hawajasikiza “mlinzi” wa Yehova, jamii ya Yeremia, watakimbilia sehemu za kisiasa zilizohukumiwa maangamiza—kufanya hivyo kukimaanisha uharibifu wao hakika katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Ili kuepuka kwenda katika njia hiyo pamoja nao, njia inayofaa inahitaji kuchaguliwa sasa wakati njia ifaayo ingali wazi. Katika njia hiyo watu wenye kutafuta uzima hawatahitaji kamwe kubadili mwendo wao.
—Kutoka The Watchtower Mar. 1, 1980.
(Makala ya kumalizia katika mfululizo huu juu ya unabii wa Yeremia itachapwa baadaye.)
[Picha katika ukurasa wa 12]
“Siku ya kisasi” cha Mungu si wakati wa kujitafutia “mambo makuu”
[Picha katika ukurasa wa 15]
Tusipuze kamwe ‘kazi ya Yehova’