Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kr sura 12 kur. 118-131
  • Tengenezo Linalomtumikia “Mungu wa Amani”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tengenezo Linalomtumikia “Mungu wa Amani”
  • Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Nitaweka Amani Kuwa Waangalizi Wako”
  • Jinsi Kristo Anavyoliongoza Kutaniko
  • “Kuwa Vielelezo kwa Kundi”
  • Jinsi Wazee Wanavyolichunga Kundi la Mungu Leo
  • Usimamizi Ulioboreshwa Unaimarisha Umoja Miongoni mwa Watu wa Mungu
  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Waangalizi Wanaochunga Kundi
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kundi la Kikristo na Utendaji Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Ufalme wa Mungu Unatawala!
kr sura 12 kur. 118-131

SURA YA 12

Tengenezo Linalomtumikia “Mungu wa Amani”

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Yehova anawapanga watu wake kitengenezo hatua kwa hatua

1, 2. Gazeti Zion’s Watch Tower lilifanyiwa marekebisho gani mnamo Januari 1895, na akina ndugu waliitikiaje badiliko hilo?

MWANAFUNZI wa Biblia mwenye bidii, John A. Bohnet, alifurahi sana alipopata gazeti Zion’s Watch Tower la Januari 1895. Gazeti hilo lilikuwa na jalada jipya kabisa—picha ya mnara mrefu wa taa ukiangaza anga lenye giza kwenye bahari iliyochafuka. Tangazo lililochapishwa katika gazeti hilo kuhusu muundo huo mpya lilikuwa na kichwa “Sura Yetu Mpya.”

2 Ndugu Bohnet alivutiwa sana na jalada hilo hivi kwamba alimwandikia barua Ndugu Russell. Aliandika hivi: “Ninafurahi kuona gazeti Mnara wa Mlinzi likipendeza sana. Ni maridadi sana.” Mwanafunzi mwingine mwaminifu wa Biblia, John H. Brown aliandika hivi kuhusu jalada hilo: “Linavutia sana. Mnara huo unasimama kwenye msingi imara huku mawimbi na dhoruba zikiupiga.” Jalada hilo jipya lilikuwa ndilo badiliko la kwanza ambalo ndugu zetu waliona mwaka huo—lakini huo ulikuwa mwanzo tu. Mwezi wa Novemba, walifahamishwa kuhusu badiliko lingine kubwa. Kwa kupendeza, lilihusu tena bahari yenye dhoruba.

3, 4. Ni tatizo gani lililozungumziwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1895, na ni badiliko gani kubwa lilitangazwa?

3 Makala ndefu iliyochapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1895, lilifunua wazi tatizo lililokuwa kama mawimbi yenye dhoruba ambalo lilikuwa likivuruga amani ya shirika, au tengenezo, la Wanafunzi wa Biblia. Akina ndugu walikuwa wakizozana kuhusu ni nani aliyepaswa kuwa kiongozi wa kutaniko. Ili kuwasaidia akina ndugu kujua walichohitaji kufanya ili kutatua roho hiyo ya ushindani inayosababisha migawanyiko, makala hiyo ilifananisha tengenezo na meli. Kisha ikakubali waziwazi kwamba ndugu waliokuwa wakiongoza hawakuwa wamelitayarisha tengenezo lililo kama meli kustahimili dhoruba kali. Walipaswa kufanya nini?

4 Makala hiyo ilisema kwamba nahodha mzuri huhakikisha kwamba meli ina vitu vinavyoweza kutumiwa kuokoa uhai na mabaharia wako tayari kufunga milango ya kushukia ndani ya meli wanapoona dhoruba ikija. Vivyo hivyo, ndugu waliokuwa wakiongoza katika tengenezo walipaswa kuhakikisha kwamba makutaniko yote yametayarishwa kukabiliana na hali zilizo kama dhoruba kali. Ili kutimiza hilo, makala hiyo ilitangaza badiliko kubwa sana. Iliagiza kwamba “katika kila kutaniko, wazee wachaguliwe” haraka iwezekanavyo ili “‘wasimamie’ kundi.”—Mdo. 20:28.

5. (a) Kwa nini mpango wa kwanza wa kuwa na wazee ulikuwa hatua muhimu? (b) Tutazungumzia maswali gani?

5 Mpango huo wa kwanza wa kuwa na wazee ulikuwa hatua muhimu katika kuanzishwa kwa utaratibu uliopaswa kufuatwa kutanikoni. Uliwasaidia ndugu zetu kukabiliana na misukosuko iliyosababishwa na Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kwa makumi ya miaka iliyofuata, marekebisho mengine ya kitengenezo yaliwasaidia watu wa Mungu kumtumikia Yehova vizuri zaidi. Ni unabii gani wa Biblia uliotabiri kuhusu marekebisho hayo? Ni mabadiliko gani ya kitengenezo ambayo umejionea? Yamekunufaishaje?

“Nitaweka Amani Kuwa Waangalizi Wako”

6, 7. (a) Andiko la Isaya 60:17 linamaanisha nini? (b) Kutajwa kwa “waangalizi” na “wagawa-kazi” kunaonyesha nini?

6 Kama tulivyozungumzia katika Sura ya 9, Isaya alitabiri kwamba Yehova angewabariki watu wake kwa kufanya idadi yao iongezeke. (Isa. 60:22) Hata hivyo, Yehova aliahidi kufanya mengi zaidi. Katika unabii huohuo, alisema hivi: “Badala ya shaba nitaingiza dhahabu, na badala ya chuma nitaingiza fedha, na badala ya miti, shaba, na badala ya mawe, chuma; nami nitaweka amani kuwa waangalizi wako na uadilifu kuwa wagawa-kazi wako.” (Isa. 60:17) Unabii huo unamaanisha nini? Unatuhusuje leo?

Kitu kibaya hakibadilishwi kwa kitu kizuri, bali kitu kizuri kinabadilishwa kwa kitu kizuri zaidi

7 Unabii wa Isaya unasema kwamba kitu kimoja kingebadilishwa kwa kingine. Lakini ona kwamba kitu kibaya hakibadilishwi kwa kitu kizuri, bali kitu kizuri kinabadilishwa kwa kitu kizuri zaidi. Kubadilisha fedha kwa dhahabu ni maendeleo, na ndivyo ilivyo na vitu vingine vinavyotajwa katika unabii huo. Hivyo, kupitia unabii huo, Yehova alitabiri kwamba hali ya watu wake ingeboreshwa hatua kwa hatua. Unabii huo unazungumzia maendeleo ya aina gani? Kwa kutaja “waangalizi” na “wagawa-kazi,” Yehova alionyesha maendeleo ya hatua kwa hatua kuhusiana na jinsi ambavyo watu wake wangepangwa kitengenezo na kutunzwa.

8. (a) Ni nani anayeleta maendeleo yanayotajwa katika unabii wa Isaya? (b) Tunanufaikaje na maendeleo hayo? (Ona pia sanduku “Alikubali kwa Unyenyekevu Kurekebishwa.”)

8 Ni nani anayeleta maendeleo hayo ya kitengenezo? Yehova anasema: “Nitaingiza dhahabu, . . . nitaingiza fedha, . . . nami nitaweka amani.” Kwa kweli, maendeleo ya utaratibu unaofuatwa kutanikoni hayaletwi na jitihada za wanadamu, bali na Yehova mwenyewe. Na tangu Yesu awekwe rasmi kuwa Mfalme, Yehova ameleta maendeleo hayo kupitia Mwana wake. Tunanufaikaje na mabadiliko hayo? Andiko hilohilo linasema kwamba maendeleo hayo yataleta “amani” na “uadilifu.” Tunapokubali mwongozo wa Mungu na kufanya marekebisho, tunakuwa na amani miongoni mwetu na kupenda uadilifu kunatuchochea kumtumikia Yehova, ambaye mtume Paulo alimtaja kuwa “Mungu wa amani.”—Flp. 4:9.

9. Ni msingi gani unaofaa ili kuwe na utaratibu na umoja katika kutaniko, na kwa nini?

9 Paulo pia aliandika hivi kumhusu Yehova: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” (1 Kor. 14:33) Ona kwamba Paulo hakutofautisha machafuko na utaratibu, bali aliyatofautisha na amani. Kwa nini? Fikiria hili: Utaratibu peke yake hauleti hali zenye amani. Kwa mfano, huenda wanajeshi wakawa wamepangwa kwa utaratibu wakielekea vitani, lakini hawaendi kufanya amani bali kupigana vita. Hivyo, tukiwa Wakristo, tunataka kukumbuka jambo hili muhimu: Utaratibu wowote usio na msingi wa amani utavurugika punde si punde. Tofauti na hilo, amani kutoka kwa Mungu hufanya kuwe na utaratibu unaodumu. Kwa hiyo, tunashukuru sana kwamba tengenezo letu linaongozwa na kusafishwa na “Mungu anayetoa amani”! (Rom. 15:33) Amani kutoka kwa Mungu ndio msingi wa utaratibu mzuri na umoja tunaofurahia na kuthamini sana katika makutaniko yetu ulimwenguni pote.—Zab. 29:11.

10. (a) Ni mabadiliko gani yaliyotokea katika tengenezo letu miaka ya mapema? (Ona sanduku “Jinsi Utaratibu wa Usimamizi Ulivyoboreshwa.”) (b) Tutachunguza maswali gani sasa?

10 Sanduku “Jinsi Utaratibu wa Usimamizi Ulivyoboreshwa” linatueleza kifupi mabadiliko yenye manufaa na yaliyofanywa kwa utaratibu katika tengenezo letu katika miaka ya mapema. Hata hivyo, akimtumia Mfalme wetu Yesu, Yehova amebadilishaje ‘shaba kuwa dhahabu’ katika miaka ya hivi karibuni? Marekebisho hayo katika usimamizi yameimarishaje amani na umoja katika makutaniko ulimwenguni pote? Yanakusaidiaje wewe binafsi kumtumikia “Mungu wa amani”?

Jinsi Kristo Anavyoliongoza Kutaniko

11. (a) Kuchunguza Maandiko kulileta badiliko gani katika uelewaji wetu? (b) Ndugu wa baraza linaloongoza waliazimia kufanya nini?

11 Kuanzia mwaka wa 1964 hadi mwaka wa 1971, baraza linaloongoza lilisimamia mradi mkubwa wa kujifunza Biblia ambao ulichunguza habari nyingi kutia ndani jinsi ambavyo kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza liliendeshwa.a Kuhusu utaratibu wa tengenezo, uchunguzi huo ulionyesha kwamba makutaniko ya karne ya kwanza yalisimamiwa na mabaraza ya wazee badala ya kusimamiwa na mzee au mwangalizi mmoja tu. (Soma Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 4:14.) Jambo hilo lilipoeleweka vizuri, baraza linaloongoza lilitambua kwamba Mfalme wao, Yesu, alikuwa akiwaongoza wafanye mabadiliko katika utaratibu wa kitengenezo wa watu wa Mungu—na ndugu wa baraza linaloongoza waliazimia kufuata mwongozo wa Mfalme. Walifanya marekebisho mara moja ili tengenezo lifuate kwa ukamili mpango unaotajwa katika Maandiko wa kuwaweka rasmi wazee. Ni marekebisho gani ambayo yalifanywa katika miaka ya mapema ya 1970.

ALIKUBALI KWA UNYENYEKEVU KUREKEBISHWA

CHAPA ya Kifini ya gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1916, ilikuwa na barua ambayo Ndugu Russell aliwaandikia ndugu wachache huko Skandinavia, kutia ndani Ndugu Kaarlo Harteva. Ndugu Russell aliwaandikia hivi: “Tunawatia moyo ninyi nyote, ndugu zetu wapendwa katika imani, mrudi kwenye kweli na mfanye kazi inayopaswa kufanywa.” Kwa nini Ndugu Russell aliwasihi hivyo?

Kaarlo Harteva

Kaarlo Harteva

Ndugu Harteva, ambaye alizaliwa mwaka wa 1882, alikuwa miongoni mwa Wanafunzi wa kwanza wa Biblia nchini Finland. Alibatizwa Aprili 1910, na mnamo Agosti 1912, Ndugu Russell alimwagiza achapishe gazeti Mnara wa Mlinzi katika Kifini. Mambo yalienda vizuri hadi Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipotokea. Ndugu Harteva aliandika hivi katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1914: “Kwa sababu ya hali ngumu ya kiuchumi, . . . hatuwezi kuahidi kwamba Mnara wa Mlinzi litakuwa na kurasa zilezile au litachapishwa mara zilezile mwaka huu.” Hata hivyo, katika mwaka wa 1915, ili kuchangisha pesa, Ndugu Harteva na wengine walianzisha shirika lililoitwa Ararat, ambalo lilianza kuchapisha gazeti lililoitwa kwa jina la shirika hilo.

Kwa kuwa Ndugu Harteva alijishughulisha sana na shirika hilo jipya na gazeti lake, ndugu mwingine alianza kuwa mhariri wa gazeti Mnara wa Mlinzi la Kifini. Gazeti Ararat lilichapisha makala za Biblia na pia makala nyingine kama vile kuhusu tiba za asili na kuhusu lugha ya Esperanto iliyokuwa imevumbuliwa karibuni. Muda si muda, gazeti hilo jipya liliwakengeusha akina ndugu kutoka kwenye mafundisho ya kweli yaliyo wazi. Mambo yalipofikia hapo, Ndugu Russell alianza kuhangaikia hali ya kiroho ya ndugu hao na akamsihi Ndugu Harteva na wengine ‘warudi kwenye kweli.’

Ndugu Harteva aliitikiaje? Alichapisha barua ya Ndugu Russell pamoja na jibu alilompa katika gazeti Ararat. Ndugu Harteva aliomba msamaha na kusema: “Nitafanya kila niwezalo kurekebisha mambo.” Muda mfupi baadaye, katika toleo la mwisho la gazeti Ararat, Ndugu Harteva aliomba tena msamaha kwa kuwachanganya wasomaji, kisha akasema: “Nitajaribu kuwa mwangalifu sana na mambo yote yanayohusiana na kweli tuliyo nayo leo.” Tofauti na baadhi ya wazee wenye kiburi waliochaguliwa kwa njia ya kura siku hizo, kwa unyenyekevu, Kaarlo Harteva alikubali kurekebishwa.

Baadaye, Ndugu Harteva aliwekwa tena kuwa mhariri wa gazeti Mnara wa Mlinzi la Kifini na pia kuwa mwangalizi wa tawi. Aliendelea na majukumu hayo hadi mwaka wa 1950. Alimaliza mwendo wake wa kidunia mwaka wa 1957, akiwa mwaminifu kwa Yehova na kwa ile kweli. Kwa kweli, wale wanaokubali kwa unyenyekevu kurekebishwa na Mfalme wao, Yesu, wanasafishwa na hupokea baraka za Yehova.

12. (a) Ni rekebisho gani lilifanywa kwenye baraza linaloongoza? (b) Fafanua jinsi ambavyo Baraza Linaloongoza limepangwa kitengenezo leo. (Ona sanduku “Jinsi Baraza Linaloongoza Linavyoshughulikia Mambo ya Ufalme,” ukurasa wa 130.)

12 Rekebisho la kwanza lilihusu baraza linaloongoza. Kabla ya wakati huo, kikundi hicho cha ndugu watiwa-mafuta kilifanyizwa na washiriki saba wa baraza la waelekezi la shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Hata hivyo, katika mwaka wa 1971, idadi ya washiriki wa baraza linaloongoza iliongezeka kutoka 7 hadi 11 na hawakuhusianishwa tena na baraza la waelekezi. Kwa kuwa hakuna mshiriki wa baraza linaloongoza aliye na cheo cha juu kuliko mwingine, walianza kupokezana zamu ya kuwa mwenyekiti kila mwaka kwa kufuata majina yao kialfabeti.

13. (a) Ni mpango gani uliokuwa ukifuatwa kwa miaka 40? (b) Baraza Linaloongoza lilifanya nini katika mwaka wa 1972?

13 Rekebisho lililofuata liliathiri makutaniko yote. Katika njia gani? Kuanzia mwaka wa 1932 hadi mwaka wa 1972, kutaniko lilikuwa likisimamiwa na ndugu mmoja tu. Kabla ya mwaka wa 1936, ndugu huyo aliyewekwa rasmi aliitwa mkurugenzi wa utumishi. Kuanzia mwaka huo na kuendelea, jina hilo lilibadilishwa na kuwa mtumishi wa kutaniko, na kisha mwangalizi wa kutaniko. Ndugu hao waliowekwa rasmi walihangaikia sana hali ya kiroho ya kundi. Kwa kawaida mwangalizi wa kutaniko alifanya maamuzi yaliyohusu kutaniko bila kuwasiliana na watumishi wengine wa kutaniko. Hata hivyo, katika mwaka wa 1972, Baraza Linaloongoza lilifanya matayarisho kwa ajili ya badiliko la kihistoria. Badiliko hilo lilihusisha nini?

14. (a) Ni mpango gani mpya ulianza kufuatwa kuanzia Oktoba 1, 1972? (b) Mratibu wa baraza la wazee anafuata jinsi gani shauri linalopatikana kwenye Wafilipi 2:3?

14 Badala ya kuwa na ndugu mmoja tu aliyetumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko, sasa kutaniko lingesimamiwa na baraza la wazee ambalo lingefanyizwa na ndugu ambao tayari walikuwa wametimiza matakwa ya Kimaandiko na kuwekwa rasmi kitheokrasi kuwa wazee Wakristo. Mpango huo mpya wa wazee ulianza kufuatwa Oktoba 1, 1972. Leo, mratibu wa baraza la wazee hajioni kuwa muhimu kuliko wazee wengine, bali anajiona kuwa “aliye mdogo zaidi.” (Luka 9:48) Ndugu hao wanyenyekevu ni baraka kubwa sana kwa undugu wa ulimwenguni pote!—Flp. 2:3.

Ni wazi kwamba kwa hekima Mfalme wetu amewapa wafuasi wake wachungaji wanaohitajika kwa wakati unaofaa

15. (a) Mpango wa kuwa na baraza la wazee kutanikoni umekuwa na faida gani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Mfalme wetu alitenda kwa hekima?

15 Mpango wa baraza la wazee kugawana majukumu ya kutaniko umeleta maendeleo makubwa. Chunguza faida hizi tatu: Kwanza kabisa, mpango huo huwasaidia wazee wote, hata iwe wana majukumu mazito kadiri gani kutanikoni, kutambua kwamba Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko. (Efe. 5:23) Pili, kama Methali 15:22 inavyosema: “Katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Wazee wanaposhauriana kuhusu mambo yanayoathiri hali njema ya kiroho ya kutaniko na kufikiria madokezo ya kila mmoja wao, hilo linawasaidia kufikia uamuzi unaopatana na kanuni za Biblia. (Met. 27:17) Yehova hubariki maamuzi hayo, na hivyo yanafanikiwa. Tatu, kuwa na ndugu wengi ambao wanatumikia wakiwa wazee kumesaidia tengenezo liweze kutosheleza uhitaji unaozidi kuongezeka wa kuwa na ndugu wa kusimamia na kuchunga makutaniko. (Isa. 60:3-5) Hebu wazia—idadi ya makutaniko ulimwenguni pote iliongezeka kutoka zaidi ya makutaniko 27,000 katika mwaka wa 1971 hadi zaidi ya makutaniko 113,000 katika mwaka wa 2013! Ni wazi kwamba kwa hekima Mfalme wetu amewapa wafuasi wake wachungaji wanaohitajika kwa wakati unaofaa.—Mika 5:5.

JINSI UTARATIBU WA USIMAMIZI ULIVYOBORESHWA

  • 1881—Ili Wanafunzi wa Biblia wanaoishi katika eneo moja waweze kuwasiliana, Ndugu Russell anawaomba wale wanaofanya mikutano kwa ukawaida wajulishe ofisi ya Watch Tower mahali wanapokutana.

  • 1895—Makutaniko yote yanaagizwa yachague miongoni mwao wale wanaoweza kutumikia wakiwa wazee.

  • 1919—Mkurugenzi wa utumishi anawekwa rasmi na ofisi ya tawi katika kila kutaniko. Majukumu yake yanatia ndani kupanga kazi ya kuhubiri na kuwatia moyo wahubiri washiriki katika huduma ya shambani. Wazee fulani katika kutaniko hawaungi mkono mpango wa kuwa na mkurugenzi wa utumishi.

  • 1932—Mpango wa kuwachagua wazee kila mwaka kwa kupiga kura unaondolewa. Badala yake, kutaniko linachagua halmashauri ya utumishi inayofanyizwa na ndugu ambao huhubiri kwa bidii na wanaishi kupatana na jina jipya, Mashahidi wa Yehova. Mzee mmoja kati ya wale waliochaguliwa na kutaniko anawekwa rasmi na Sosaiti au ofisi ya tawi kuwa mkurugenzi wa utumishi.

  • 1937—Ndugu ambao ni sehemu ya ule umati mkubwa wanaweza kutumikia pamoja na ndugu waliotiwa mafuta katika halmashauri za utumishi.

  • 1938—Makutaniko yanaombwa kuunga mkono azimio la kwamba watumishi wote kutanikoni wawekwe rasmi kwa njia ya kitheokrasi. Huo ndio mwisho wa kuwachagua wazee makutanikoni kwa kupiga kura.

Ili kujifunza mengi kuhusu mabadiliko makubwa yaliyohusiana na utaratibu wa kitengenezo, ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 204-235.

Mkutano wa kila mwaka wa kuchagua wazee wa makutaniko katika miaka ya 1920

“Tulipiga kura ya kuwachagua wazee kwa kuinua mkono wa kulia. Kisha ndugu angehesabu kura hizo.”—Dada Rose Swingle, Chicago, Illinois, Marekani

“Kuwa Vielelezo kwa Kundi”

16. (a) Wazee wana jukumu gani? (b) Wanafunzi wa Biblia walilionaje himizo la Yesu kwamba ‘wachunge kondoo’?

16 Katika siku za mapema za Wanafunzi wa Biblia, tayari wazee walielewa kwamba walikuwa na jukumu la kuwasaidia waamini wenzao kuendelea kuwa watumishi wa Mungu. (Soma Wagalatia 6:10.) Katika mwaka wa 1908, makala moja katika gazeti Mnara wa Mlinzi ilizungumzia himizo hili la Yesu: “Chunga kondoo wangu wadogo.” (Yoh. 21:15-17) Makala hiyo iliwaambia hivi wazee: “Ni muhimu sana kwamba utume ambao Bwana ametupatia kuhusiana na kondoo uchukue mahali muhimu maishani mwetu, ili tuliheshimu inavyofaa pendeleo kubwa la kulisha na kutunza wafuasi wa Bwana.” Katika mwaka wa 1925, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikazia tena umuhimu wa wazee kutumikia wakiwa wachungaji kwa kuwakumbusha hivi: “Kanisa la Mungu ni mali yake, . . . na atawatoza hesabu wote walio na pendeleo la kuwatumikia ndugu zao.”

17. Waangalizi wamesaidiwaje kuwa wachungaji wenye ustadi?

17 Tengenezo la Yehova limewasaidiaje wazee kubadili ustadi wao wa uchungaji kutoka ‘chuma na kuwa fedha’? Kwa kuandaa programu za kuwazoeza. Katika mwaka wa 1959, Shule ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya waangalizi ilifanywa kwa mara ya kwanza. Somo moja lilikuwa na kichwa, “Kuhangaikia Mahitaji ya Mtu Mmoja-Mmoja.” Ndugu hao wenye majukumu walitiwa moyo “wawe na ratiba ya kuwatembelea wahubiri katika nyumba zao.” Somo hilo lilizungumzia njia mbalimbali ambazo wachungaji wangetumia ili kufanya ziara hizo ziwe zenye kujenga. Katika mwaka wa 1966, Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanyiwa marekebisho ilianza. Somo moja lilizungumzia “Umuhimu wa Kazi ya Uchungaji.” Somo hilo lilizungumzia jambo gani kuu? Wale wanaoongoza “wanapaswa kuwatunza kwa upendo kondoo wa Mungu, lakini hawapaswi kupuuza familia zao na huduma ya shambani.” Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na shule nyingi kwa ajili ya wazee. Mazoezi hayo yanayoendelea ambayo yameandaliwa na tengenezo la Yehova yamekuwa na matokeo gani? Leo, kutaniko la Kikristo lina maelfu ya ndugu ambao wanatumikia wakiwa wachungaji wa kiroho.

Darasa la Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Ufilipino katika mwaka wa 1966

Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Filipino, 1966

18. (a) Wazee wamekabidhiwa jukumu gani zito? (b) Kwa nini Yehova na Yesu wanawapenda wazee wanaofanya kazi kwa bidii?

18 Mpango wa kuwa na wazee Wakristo umewekwa na Yehova kupitia Mfalme wetu, Yesu, ili watimize mgawo mzito. Mgawo gani? Mgawo wa kuwaongoza kondoo wa Mungu katika kipindi hatari zaidi katika historia. (Efe. 4:11, 12; 2 Tim. 3:1) Yehova na Yesu wanawapenda sana wazee wanaofanya kazi kwa bidii kwa sababu ndugu hao wanatii himizo hili la Kimaandiko: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu . . . kwa kupenda . . .  kwa hamu . . . , [na] kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:2, 3) Acheni tuchunguze njia mbili kati ya njia nyingi ambazo wachungaji Wakristo wanakuwa vielelezo kwa kundi na kuchangia sana amani na shangwe katika kutaniko.

“TULISHANGAA”

WENZI fulani wa ndoa ambao ni wamishonari barani Asia walitumwa kwenye kutaniko ambalo halikuwa na ongezeko kwa miaka mingi. Waliona kwamba akina ndugu walikuwa na upendo lakini hawakufuata maagizo ya tengenezo. Baada ya kusitawisha urafiki pamoja na wahubiri hao, ndugu huyo mmishonari alianza hatua kwa hatua kusaidia kutaniko hilo lifuate utaratibu uleule wa kitengenezo unaofuatwa na watu wa Yehova ulimwenguni pote. Matokeo yalikuwa nini? Katika kipindi cha miaka miwili, idadi ya wanaohudhuria mikutano iliongezeka mara mbili, wapya wakaanza kuhubiri, na watu zaidi ya 20 wakabatizwa. Wenzi hao wanasema hivi: “Tulishangaa. Yehova alitubariki sana! Kuona matokeo ya kufuata maagizo ya tengenezo la Mungu kumefanya wote katika kutaniko wawe na shangwe.”

Jinsi Wazee Wanavyolichunga Kundi la Mungu Leo

19. Tunahisije wazee wanapoandamana nasi katika huduma?

19 Kwanza, wazee hufanya kazi pamoja na washiriki wa kutaniko. Luka, mwandikaji wa Injili alisema hivi kumhusu Yesu: ‘Alisafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu. Na wale kumi na wawili walikuwa pamoja naye.’ (Luka 8:1) Kama vile Yesu alivyohubiri pamoja na mitume wake, leo wazee ambao ni mfano mzuri hufanya kazi bega kwa bega na waamini wenzao katika kazi ya kuhubiri. Wanatambua kwamba kwa kufanya hivyo, wanachangia roho nzuri katika kutaniko. Washiriki wa kutaniko wanahisije kuhusu wazee hao? Jeannine, dada mwenye umri unaokaribia miaka 90 anasema: “Kuhubiri pamoja na mzee hunipa fursa ya kuzungumza naye na kumfahamu vizuri.” Steven, ndugu mwenye umri wa miaka 30 na kitu, anasema: “Ninapohubiri mlango kwa mlango pamoja na mzee, ninahisi kwamba anataka kunisaidia. Ninafurahi sana anaponisaidia.”

Mchungani akimpata kondoo aliyepotea katika usiku wenye dhoruba

Kama vile mchungaji anavyomtafuta kondoo aliyepotea, ndivyo wazee wanavyojitahidi kuwatafuta wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko

20, 21. Wazee wanawezaje kumwiga mchungaji anayetajwa katika mfano wa Yesu? Toa mfano. (Ona pia sanduku “Ziara za Kila Juma Zenye Matokeo.”)

20 Pili, tengenezo la Yehova limewazoeza wazee wajue jinsi wanavyoweza kuwasaidia wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko. (Ebr. 12:12) Kwa nini wazee wanapaswa kuwasaidia watu hao walio dhaifu kiroho, na wanaweza kufanya hivyo jinsi gani? Jibu linapatikana katika mfano wa Yesu wa mchungaji na kondoo aliyepotea. (Soma Luka 15:4-7.) Mchungaji huyo anapogundua kwamba kondoo mmoja hayupo, anamtafuta kwa bidii kana kwamba ana kondoo huyo mmoja tu. Wazee Wakristo leo wanaigaje mfano uliowekwa na mchungaji huyo? Kama vile mchungaji anavyomwona kondoo aliyepotea kuwa mwenye thamani, ndivyo wazee wanavyowaona kuwa wenye thamani wale ambao wameacha kushirikiana na watu wa Mungu. Hawapaswi kuona jitihada zao za kumtafuta kondoo aliyepotea na kumsaidia kuwa ni kupoteza wakati. Isitoshe, kama vile mchungaji ‘anavyoenda kumtafuta aliyepotea mpaka ampate,’ wazee huchukua hatua ya kuwatafuta na kuwasaidia wale walio dhaifu.

21 Mchungaji anayetajwa katika mfano wa Yesu anafanya nini anapompata kondoo? Anamwinua kwa wororo na “kumweka juu ya mabega yake,” na kumrudisha kwenye kundi. Vivyo hivyo, maneno ya mzee yenye kutia moyo yanaweza kumwinua kwa wororo ndugu aliye dhaifu kiroho na kumsaidia arudi kutanikoni. Ilikuwa hivyo kwa Victor, ndugu anayeishi barani Afrika ambaye aliacha kushirikiana na kutaniko. Anasema: “Katika kipindi cha miaka minane nilipokuwa sishirikiani na kutaniko, wazee walijaribu tena na tena kunisaidia.” Ni nini hasa kilichomgusa moyo? Anaeleza hivi: “Siku moja, John, mzee ambaye tulihudhuria pamoja Shule ya Utumishi wa Painia, alikuja kunitembelea na akanionyesha picha tulizopigwa katika shule hiyo. Zilinifanya nikumbuke mambo mengi yenye kupendeza hivi kwamba nilianza kutamani shangwe niliyokuwa nayo nilipokuwa nikimtumikia Yehova.” Muda mfupi baada ya John kumtembelea, Victor alirudi kutanikoni. Leo anatumikia tena akiwa painia. Kwa kweli, wazee Wakristo wanaotujali huchangia sana shangwe yetu.—2 Kor. 1:24.b

Ndugu wawili Wakristo wakimtembelea ndugu mzee asiyetenda

ZIARA ZA KILA JUMA ZENYE MATOKEO

WAKIWA wamechochewa na tamaa ya kuwasaidia kondoo waliopotea, wazee wa kutaniko moja nchini Marekani walizungumzia hatua ambazo wangeweza kuchukua ili kuwasaidia wahubiri walioacha kushirikiana na kutaniko. Waligundua kwamba watu 30 hivi ambao walikuwa wameacha kumtumikia Yehova miaka mingi iliyopita walikuwa bado wanaishi katika eneo la kutaniko hilo. Wengi wao walikuwa wamezeeka.

Alfredo, mzee katika kutaniko hilo alipata orodha ya majina ya ndugu hao na akaanza kuwatembelea. Anasema hivi: “Kila Ijumaa asubuhi, mimi hubisha mlango wa mhubiri asiyetenda.” Mhubiri huyo anapofungua mlango, Alfredo huzungumza naye kwa njia yenye kustarehesha na kumwambia jinsi anavyomjali. Yeye humwambia ndugu au dada huyo kwamba kutaniko halijasahau kazi yake nzuri ambayo alifanya kwa ajili ya Ufalme wa Yehova. Alfredo anasema, “Nilipomwambia ndugu fulani mzee asiyetenda saa alizohubiri na magazeti aliyowaachia watu katika ripoti yake ya mwisho ya utumishi ya mwaka wa 1976, alilengwalengwa na machozi.” Alfredo pia huwasomea wale anaowatembelea andiko la Luka 15:4-7, 10, kisha anawauliza, “Inakuwaje kondoo aliyepotea anaporudi kwenye kutaniko? Yehova, Yesu, na malaika hushangilia—hebu wazia hilo!”

Kwa miaka miwili sasa, Alfredo amekuwa akiwasaidia wale wasiotenda. Jitihada zake zenye subira zimekuwa na matokeo gani? Amepata shangwe ya kuwasaidia ndugu wawili waanze tena kushirikiana na kutaniko. Sasa wanahudhuria kwa ukawaida mikutano ya Jumapili. Anasema hivi huku akitabasamu: “Walipoingia Jumba la Ufalme, nilitokwa na machozi.” Anaongezea hivi: “Ingawa ndugu hao wasiotenda wameanza kuhudhuria mikutano, bado ninawatembelea kila Ijumaa kwa sababu wao huniambia kwamba wao hutazamia kwa hamu sana ziara hizo za kila juma. Nami nahisi vivyo hivyo!

Usimamizi Ulioboreshwa Unaimarisha Umoja Miongoni mwa Watu wa Mungu

22. Sifa ya uadilifu na amani huimarishaje umoja wa kutaniko la Kikristo? (Ona pia sanduku “Tulishangaa.”)

22 Kama ilivyotajwa awali, Yehova alitabiri kwamba uadilifu na amani zitaendelea kuongezeka miongoni mwa watu wa Mungu. (Isa. 60:17) Sifa hizo mbili huimarisha umoja katika makutaniko. Katika njia zipi? Kuhusiana na uadilifu, “Mungu . . . ni Yehova mmoja.” (Kum. 6:4) Viwango vyake vya uadilifu havitofautiani kati ya makutaniko ya nchi moja na nyingine. Ana viwango vilevile vya mema na mabaya, na “makutaniko yote ya watakatifu” yanafuata viwango hivyo. (1 Kor. 14:33) Kwa hiyo, kutaniko litasitawi ikiwa tu viwango vya Mungu vinafuatwa. Kuhusu amani, Mfalme wetu anataka tufurahie amani katika kutaniko na pia tuwe watu “wanaofanya amani.” (Mt. 5:9) Kwa hiyo, ‘tunafuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani.’ Tunachukua hatua ya kwanza kusuluhisha hali ya kutoelewana ambayo huenda ikatokea miongoni mwetu. (Rom. 14:19) Kwa kufanya hivyo, tunachangia amani na pia umoja katika kutaniko letu.—Isa. 60:18.

23. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunafurahia nini leo?

23 Huko nyuma mnamo Novemba 1895, gazeti Mnara wa Mlinzi lilipotangaza kwa mara ya kwanza mpango wa kuwa na wazee, ndugu wenye madaraka walieleza tamaa yao ya kutoka moyoni. Ni tamaa gani hiyo? Walitamani na kusali kwamba mpango huo mpya wa kitengenezo ungewasaidia watu wa Mungu “wafikie haraka umoja wa imani.” Tunapotafakari mambo ambayo yametokea makumi ya miaka iliyopita, tunashukuru kwamba marekebisho ya hatua kwa hatua kuhusu usimamizi ambayo Yehova amefanya kupitia Mfalme wetu yameimarisha umoja wetu katika ibada. (Zab. 99:4) Matokeo ni kwamba leo watu wote wa Yehova ulimwenguni pote wanashangilia ‘tunapotembea katika roho ileile,’ tunapofuata “hatua zilezile,” na kumtumikia “Mungu wa amani” “bega kwa bega.”—2 Kor. 12:18; soma Sefania 3:9.

a Matokeo ya uchunguzi huo wa kina yalichapishwa katika kitabu cha marejeo Aid to Bible Understanding.

b Ona makala “Wazee Wakristo Ni ‘Wafanyakazi Wenzi kwa Shangwe Yetu’” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 2013, ukurasa wa 27-31.

Ufalme Ni Halisi Kwako Kadiri Gani?

  • Ufalme umeleta maendeleo gani ya kitengenezo?

  • Marekebisho ya usimamizi katika kutaniko yamekusaidiaje kumtumikia “Mungu wa amani”?

  • Ni maneno na matendo gani ya mzee ambayo yameongeza shangwe yako?

  • Wewe binafsi unaweza kuchangiaje amani na umoja wa kutaniko?

Mkutano wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova

Kushoto kwenda Kulia: Gerrit Lösch, Geoffrey Jackson, Samuel Herd, Guy Pierce, Mark Sanderson, David Splane, Anthony Morris III, Stephen Lett

JINSI BARAZA LINALOONGOZA LINAVYOSHUGHULIKIA MAMBO YA UFALME

BARAZA LINALOONGOZA la Mashahidi wa Yehova linafanyizwa na ndugu watiwa-mafuta ambao ni watumishi wa Yehova Mungu. Wakiwa kikundi, wanafanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Wana jukumu la kuandaa chakula cha kiroho, kutoa mwongozo, na kuwahimiza Mashahidi wa Yehova washiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme duniani pote.—Mt. 24:14, 45-47.

Mikutano ya Baraza Linaloongoza inafanywa kila juma, kwa kawaida siku ya Jumatano. Mikutano hiyo inawawezesha ndugu hao kufanya kazi pamoja kwa umoja. (Zab. 133:1) Washiriki wa Baraza Linaloongoza wanatumikia pia katika halmashauri mbalimbali. Ili kushughulikia mambo ya Ufalme, kila halmashauri inasimamia utendaji fulani. Yafuatayo ni majukumu yao kwa ufupi.

Ndugu Wakristo wakishirikiana katika juhudu za kutunza ndugu zao Wakristo
  • Halmashauri ya Waratibu

    Ndugu wanaotumikia katika halmashauri hii wanasimamia mambo ya kisheria na pia vyombo vya habari inapohitajika kutoa habari sahihi kuhusu imani yetu. Pia wanashughulikia misiba, mateso, na mambo mengine ya dharura yanayowakumba ndugu zetu ulimwenguni pote.

  • Washiriki wa familia ya Betheli wakifanya migawo mbalimbali
  • Halmashauri ya Wafanyakazi

    Halmashauri hii imepewa daraka la kusimamia mipango ya kushughulikia hali ya kimwili na ya kiroho ya washiriki wa familia ya Betheli duniani pote na kuwasaidia. Inasimamia kazi ya kuwachagua na kuwaalika washiriki wapya wa familia za Betheli na kushughulikia masuala yanayohusu utumishi wao wa Betheli.

  • Mwanabetheli akisaidia katiak kuchapisha na kusafirisha machapisho ya Biblia
  • Halmashauri ya Uchapishaji

    Ndugu wanaotumikia katika halmashauri hii wanasimamia uchapishaji na usafirishaji wa machapisho ya Biblia ulimwenguni pote. Wanasimamia mashine za kuchapisha na majengo yanayomilikiwa na kuendeshwa na mashirika mbalimbali yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova, na pia ujenzi unaofanywa ulimwenguni pote, kutia ndani ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Wanapanga jinsi michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya Ufalme inavyoweza kutumiwa kwa njia nzuri zaidi.

  • Ndugu Mkristo akitayarisha vitu vya kufanyia utafiti mezani
  • Halmashauri ya Utumishi

    Washiriki wa halmashauri hii wanasimamia kazi yote ya kuhubiri na masuala yanayohusu makutaniko, wahubiri, mapainia, wazee, waangalizi wanaosafiri, na wamishonari. Mbali na mambo mengine mengi, wanasimamia pia utendaji wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali. Wanasimamia pia kazi ya kutayarisha Huduma Yetu ya Ufalme.

  • Ndugu Mkristo wakitoa hotuba jukwaani
  • Halmashauri ya Ufundishaji

    Halmashauri hii inasimamia programu za ufundishaji katika makusanyiko yote na mikutano ya kutaniko. Inasimamia pia Shule ya Gileadi, Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Shule ya Utumishi wa Painia, na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na shule nyingine. Kwa kuongezea, halmashauri hii inasimamia utayarishaji wa rekodi za sauti na video.

  • Mifumo mbalimbali ya machapisho, kutia ndani tovuti ya jw.org
  • Halmashauri ya Uandikaji

    Ndugu wanaotumikia katika halmashauri hii wanasimamia utayarishaji wa chakula cha kiroho kupitia machapisho na kupitia njia za kielektroniki kwa ajili ya waamini wenzao na watu wote. Halmashauri hii pia husimamia Tovuti ya tengenezo na pia kazi ya kutafsiri duniani kote. Isitoshe, halmashauri hii hujibu maswali yanayoulizwa kuhusu maana ya maandiko fulani na mambo ambayo yametajwa katika machapisho yetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki