Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jy sura 129 uku. 294-uku. 295 fu. 2
  • Pilato Asema: “Tazama! Mwanamume!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Pilato Asema: “Tazama! Mwanamume!
  • Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Habari Zinazolingana
  • “Tazama, Mtu Huyu!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • “Tazama, Mtu Huyu!”
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Pontio Pilato Alikuwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kutoka kwa Pilato Mpaka kwa Herode na Kurudi Tena
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
jy sura 129 uku. 294-uku. 295 fu. 2
Yesu, akiwa amevaa taji la miiba na joho la zambarau anatolewa nje na Pilato

SURA YA 129

Pilato Asema: “Tazama! Mwanamume!”

MATHAYO 27:15-17, 20-30 MARKO 15:6-19 LUKA 23:18-25 YOHANA 18:39–19:5

  • PILATO AJARIBU KUMWEKA YESU HURU

  • WAYAHUDI WAOMBA BARABA AACHILIWE

  • YESU ADHIHAKIWA NA KUTESWA

Pilato aliuambia hivi umati unaotaka Yesu auawe: “Sikupata msingi wa mashtaka yenu dhidi yake. Kwa kweli, hata Herode hakupata.” (Luka 23:14, 15) Sasa ili kujaribu kumlinda Yesu, Pilato anatumia njia nyingine, anawaambia hivi watu: “Mna desturi kwamba niwafungulie mtu siku ya Pasaka. Basi, mnataka niwafungulie Mfalme wa Wayahudi?”—Yohana 18:39.

Pilato ana habari kuhusu mfungwa anayeitwa Baraba, anayejulikana kuwa mwizi, mchochezi, na muuaji. Basi Pilato anauliza: “Mnataka niwafungulie nani, Baraba au Yesu anayeitwa Kristo?” Wakichochewa na wakuu wa makuhani, watu wanaomba Baraba afunguliwe bali si Yesu. Pilato anauliza tena: “Mnataka niwafungulie nani kati ya hawa wawili?” Umati unapaza sauti: “Baraba”!—Mathayo 27:17, 21.

Akiwa amefadhaika, Pilato anauliza: “Basi, nifanye nini na Yesu anayeitwa Kristo?” Watu wanasema kwa sauti kubwa: “Atundikwe mtini!” (Mathayo 27:22) Bila aibu, wanataka mtu asiye na hatia auawe. Pilato anawauliza: “Kwa nini? Amefanya kosa gani? Mimi sikuona jambo lolote linalofanya astahili kifo; kwa hiyo nitamwadhibu kisha nimfungue.”—Luka 23:22.

Licha ya jitihada nyingi za Pilato, umati wenye hasira unapaza sauti hivi kwa pamoja: “Atundikwe mtini!” (Mathayo 27:23) Viongozi wa kidini wameuchochea sana umati huo hivi kwamba wanataka kumwaga damu! Na si damu ya mhalifu fulani, wala muuaji fulani. Ni damu ya mtu asiye na hatia ambaye siku tano zilizopita alikaribishwa Yerusalemu kama Mfalme. Ikiwa wanafunzi wa Yesu wako hapo, wanakaa kimya na kuwa waangalifu.

Pilato anaona kwamba maombi yake yanakataliwa. Vurugu zinaanza kutokea, basi anachukua maji na kunawa mikono yake mbele ya umati. Anawaambia: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu huyu. Shauri yenu.” Ingawa hivyo, watu hawabadili mtazamo wao. Badala yake wanasema: “Damu yake na iwe juu yetu na juu ya watoto wetu.”—Mathayo 27:24, 25.

Gavana huyo anataka kuwafurahisha watu hao badala ya kufanya kile anachojua kwamba ni haki. Basi kulingana na ombi la umati, Pilato anamweka huru Baraba. Anaagiza Yesu avuliwe nguo na kisha apigwe mijeledi.

Baada ya kupigwa na kuteswa sana, wanajeshi wanampeleka Yesu kwenye jumba la gavana. Kikosi cha wanajeshi kinakusanyika na kumtendea vibaya hata zaidi. Wanasokota taji la miiba na kulikandamiza juu ya kichwa chake. Pia, wanajeshi wanaweka utete kwenye mkono wa kuume wa Yesu na kumvika vazi la zambarau, kama lile linalovaliwa na wafalme. Wanasema hivi kwa dharau: “Salamu, ewe Mfalme wa Wayahudi!” (Mathayo 27:28, 29) Zaidi ya hayo, wanamtemea mate na kumpiga makofi usoni. Wanauchukua utete alioshika mkononi, wanampiga nao kichwani, na hivyo kufanya adungwe zaidi na miiba mikali iliyo kwenye “taji” walilomvisha kichwani ili kumshushia heshima.

Yesu anajiendesha kwa heshima na uthabiti licha ya hayo yote hivi kwamba Pilato anafanya jaribio lingine la kujiondolea lawama, akisema: “Ona! Namtoa nje kwenu ili mjue kwamba sijampata na kosa lolote.” Je, Pilato anafikiri kwamba sasa akimtoa Yesu nje akiwa amechubuka na akivuja damu, umati utamhurumia? Yesu anaposimama mbele ya umati wenye hasira, Pilato anasema: “Tazama! Mwanamume!”—Yohana 19:4, 5.

Ingawa amepigwa na kuumizwa, Yesu anatenda kwa heshima na utulivu hivi kwamba hata Pilato anatambua jambo hilo, kwa kuwa maneno yake yanaonyesha heshima na huruma.

KUPIGWA MIJELEDI

Kiboko kilichotumiwa kupiga mijeledi

Dakt. William D. Edwards katika kitabu The Journal of the American Medical Association anafafanua desturi ya Waroma ya kupiga mijeledi:

“Kwa kawaida kifaa kilichotumiwa ni kiboko kifupi (flagramu au flagelamu) chenye kamba kadhaa za ngozi zenye urefu mbalimbali, kamba mojamoja au zilizosokotwa, ambazo zilifungwa vipande vidogo vya chuma au vipande vya mifupa ya kondoo vilivyoachana na vilivyokuwa na ncha kali. . . . Wanajeshi Waroma walipompiga kwa nguvu zote mfungwa mgongoni kwa kurudia rudia, vile vipande vya chuma vingesababisha michubuko yenye kina kirefu, na zile kamba za ngozi na mifupa ya kondoo ingekata ngozi na sehemu zilizo chini ya ngozi. Kisha, walipoendelea kumpiga mijeledi, majeraha yalipasuka kufikia kwenye misuli na kutokeza nyuzinyuzi zinazoning’inia za minofu inayotoka damu.”

  • Pilato anajaribuje kumweka Yesu huru na hivyo kujiondolea lawama?

  • Kupigwa mijeledi kulihusisha nini?

  • Baada ya Yesu kupigwa mijeledi, anatendewaje vibaya hata zaidi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki