Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • od sura 16 kur. 162-168
  • Undugu Wenye Umoja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Undugu Wenye Umoja
  • Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUBADILI MTAZAMO
  • KUDUMISHA UMOJA WETU WA ULIMWENGUNI POTE
  • KUTUNZANA
  • WAMECHAGULIWA ILI KUFANYA MAPENZI YA YEHOVA
  • Je, Unawaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Msingi wa Ulimwengu Mpya Sasa Unafanyizwa
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • “Nanyi Nyote Ni Ndugu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Tumikieni Yehova kwa Upatano Mmoja
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
od sura 16 kur. 162-168

SURA YA 16

Undugu Wenye Umoja

YEHOVA MUNGU alishughulika na Waisraeli kwa miaka 1,500 hivi wakiwa taifa lake. Baadaye, Yehova ‘alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Mdo. 15:14) Watu kwa ajili ya jina la Yehova wangekuwa mashahidi wake, nao wangefikiri na kutenda kwa umoja popote walipo duniani. Kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake ingetokeza kukusanywa kwa watu kwa ajili ya jina la Mungu. Aliwaagiza hivi: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”—Mt. 28:19, 20.

Wewe ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wenye umoja ambao hawatenganishwi na tofauti za kitaifa, kikabila, au kiuchumi

2 Umekuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo kwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Wewe ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wenye umoja ambao hawatenganishwi na tofauti za kitaifa, kikabila, au kiuchumi. (Zab. 133:1) Kwa sababu hiyo, unawapenda na kuwaheshimu ndugu zako Wakristo kutanikoni. Huenda zamani usingeweza kushirikiana na baadhi yao kwa sababu ya tofauti za kijamii, kitaifa, au kielimu. Mmeunganishwa kwa upendo wa kindugu ulio imara na wenye nguvu kuliko uhusiano mwingine wowote wa kijamii, wa kidini, au wa familia.—Marko 10:29, 30; Kol. 3:14; 1 Pet. 1:22.

KUBADILI MTAZAMO

3 Ikiwa wengine wanaona ni vigumu kushinda ubaguzi wa rangi, wa kisiasa, wa kitabaka, au ubaguzi wa aina nyingine yoyote, wanaweza kuwafikiria Wakristo Wayahudi wa karne ya kwanza, ambao walihitaji kufanya juu chini ili waache kuwabagua watu wengine ambao hawakuwa wa dini ya Kiyahudi. Petro alipoagizwa aende nyumbani kwa Kornelio, ofisa wa jeshi wa kikosi cha Roma, Yehova alimtayarisha Petro kwa ajili ya mgawo huo kwa njia ya fadhili.—Matendo sura ya 10.

4 Katika maono, Petro aliambiwa achinje na kula wanyama fulani waliokuwa najisi kulingana na desturi za Wayahudi. Petro alipokataa, sauti kutoka mbinguni ilimwambia: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” (Mdo. 10:15) Mungu alihitaji kuingilia kati ili Petro abadili mtazamo wake kuhusu mgawo ambao angepewa wa kwenda kumtembelea mtu wa mataifa. Alipotii mwelekezo wa Yehova, Petro aliwatangazia hivi wale waliokusanyika: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine, lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi. Basi nilipoitwa nilikuja bila kupinga.” (Mdo. 10:28, 29) Baadaye, Petro alijionea uthibitisho wa kwamba Yehova alikuwa amemkubali Kornelio na watu wa nyumbani mwake.

5 Sauli wa Tarso, Farisayo mwenye elimu ya juu, alihitaji kujinyenyekeza ili kushirikiana na watu wa jamii ambayo hapo zamani hangekubali kushirikiana nao. Hata alihitaji kukubali mwongozo kutoka kwao. (Mdo. 4:13; Gal. 1:13-20; Flp. 3:4-11) Ni wazi kwamba watu kama vile Sergio Paulo, Dionisio, Damari, Filemoni, Onesimo, na wengine walihitaji kubadili kabisa mtazamo wao walipokubali habari njema na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Mdo. 13:6-12; 17:22, 33, 34; Flm. 8-20.

KUDUMISHA UMOJA WETU WA ULIMWENGUNI POTE

6 Bila shaka upendo wa ndugu na dada katika kutaniko lenu ulikusaidia umkaribie Yehova na tengenezo lake. Uliona alama ya pekee ya upendo na umoja ambayo inawatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, kama alivyosema: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:34, 35) Ulimthamini zaidi Yehova na tengenezo lake ulipotambua kwamba upendo unaoonyeshwa kutanikoni ni kionjo tu cha upendo unaoonyeshwa na ushirika wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova. Unajionea utimizo wa unabii wa Biblia wa kukusanywa kwa watu katika siku za mwisho ili wamwabudu Yehova kwa amani na umoja.—Mika 4:1-5.

7 Kwa kuwa kuna mambo mengi leo yanayosababisha migawanyiko, ni nani angefikiri kwamba ingewezekana kuwaunganisha watu “kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha”? (Ufu. 7:9) Fikiria tofauti zilizopo kati ya jamii ya watu wenye elimu ya kisasa na wale wanaoshikilia desturi za kale za kikabila. Hebu fikiria mizozo ya kidini kati ya watu wa kabila na taifa moja. Kwa sababu ya uzalendo, watu wamegawanyika zaidi kisiasa kuliko wakati mwingine wowote. Pia, unapofikiria tofauti kubwa za kiuchumi na mambo mengine mengi yanayosababisha migawanyiko, kuwaunganisha watu wa mataifa, lugha, vikundi, na tabaka mbalimbali katika kifungo kisichoweza kuvunjika cha upendo na amani, ni muujiza ambao unaweza kufanywa tu na Mungu Mweza-Yote.—Zek. 4:6.

8 Lakini umoja huo ni halisi, na ulipojiweka wakfu na kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, ulijiunga na undugu huo. Ili ufaidike na umoja huo, una jukumu la kuudumisha. Unaweza kufanya hivyo kwa kutii maneno ya mtume Paulo katika Wagalatia 6:10: “Tukiwa bado na nafasi, acheni tuwatendee watu wote mema, na hasa wale ambao ni ndugu zetu katika imani.” Pia, tunafuata ushauri huu: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” (Flp. 2:3, 4) Maadamu tunajizoeza kuwaona ndugu na dada zetu kama Yehova anavyowaona, wala si kulingana na wanavyoonekana kwa nje, tutaendelea kufurahia uhusiano wenye amani pamoja nao.—Efe. 4:23, 24.

KUTUNZANA

9 Kama mtume Paulo alivyofafanua, wote kutanikoni hawana mgawanyiko, bali ni viungo vya mwili mmoja vinavyotunzana kwa njia ileile. (1 Kor. 12:14-26) Huenda tukawa mbali sana na baadhi ya ndugu zetu, lakini bado tunawahangaikia. Baadhi ya ndugu zetu wakiteswa, sisi huhuzunika sana. Ikiwa baadhi ya akina ndugu wana uhitaji fulani au wamekumbwa na msiba, vita, au mizozo ya kikabila, sisi sote hujitahidi sana kutafuta njia za kuwasaidia kiroho na vilevile kimwili.—2 Kor. 1:8-11.

10 Kila siku sisi sote tunapaswa kusali kwa ajili ya ndugu zetu. Kuna ndugu wanaoshawishiwa kufanya mambo mabaya. Huenda mateso ya baadhi ya ndugu zetu yanajulikana. Hata hivyo huenda tusijue upinzani ambao wengine wanakabili kila siku kutoka kwa wafanyakazi wenzao na familia zilizogawanyika kidini. (Mt. 10:35, 36; 1 The. 2:14) Sote tunahangaishwa na hali hizo kwa sababu sisi ni undugu wa ulimwenguni pote. (1 Pet. 5:9) Pia, miongoni mwetu tuna wale wanaofanya utumishi wa Yehova kwa bidii, wakiongoza katika kazi ya kuhubiri na kusimamia makutaniko. Na kuna wale wanaosimamia kazi ya ulimwenguni pote. Wote wanahitaji sala zetu, na kupitia sala, tunaonyesha kwamba tunawajali na kuwapenda ndugu zetu kikweli hata wakati ambapo hakuna lolote ambalo sisi wenyewe tunaweza kufanya ili kuwasaidia.—Efe. 1:16; 1 The. 1:2, 3; 5:25.

11 Kwa sababu ya misukosuko ya siku hizi za mwisho, watu wa Yehova wanapaswa kuwa tayari kusaidiana. Wakati mwingine, majanga kama vile matetemeko ya nchi na mafuriko yanapotokea, huenda tukahitaji kukusanya na kutuma misaada mingi ya kimwili. Wakristo wa karne ya kwanza waliweka mfano mzuri katika jambo hilo. Wakikumbuka ushauri wa Yesu, wanafunzi huko Antiokia walifurahi kutuma msaada kwa ndugu zao waliokuwa Yudea. (Mdo. 11:27-30; 20:35) Baadaye, mtume Paulo aliwatia moyo Wakorintho waunge mkono mipango ya kutoa msaada kwa utaratibu. (2 Kor. 9:1-15) Leo, ndugu zetu wanapopatwa na hali ngumu na kuhitaji msaada, tengenezo na Wakristo mmoja-mmoja hutenda haraka na kuandaa msaada unaohitajika.

WAMECHAGULIWA ILI KUFANYA MAPENZI YA YEHOVA

12 Undugu wetu wenye umoja wa ulimwenguni pote umepangwa ili kufanya mapenzi ya Yehova. Wakati huu, mapenzi yake ni kwamba habari njema ya Ufalme ihubiriwe katika dunia yote ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote. (Mt. 24:14) Tunapofanya kazi hiyo, ni mapenzi ya Yehova kwamba sikuzote mwenendo wetu upatane na viwango vyake vya juu vya maadili. (1 Pet. 1:14-16) Ili kutimiza kazi ya Yehova, sote tunapaswa kuwa tayari kujitiisha kila mmoja kwa mwenzake na kuunga mkono kazi ya kuhubiri habari njema. (Efe. 5:21) Huu si wakati wa kutafuta mapendezi yetu bali ni wakati wa kujitahidi kabisa kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwetu. (Mt. 6:33) Tunapozingatia jambo hilo na kufanya kazi pamoja  kwa umoja kwa ajili ya habari njema, tunaridhika na kupata shangwe sasa na kutazamia baraka za milele.

13 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi ni watu wa pekee, watu waliochaguliwa kutoka kwa wanadamu wengine wakiwa watu safi ili tumtumikie Mungu wetu kwa bidii. (Tito 2:14) Ibada yetu kwa Yehova inatufanya tuwe tofauti. Mbali na kufanya kazi bega kwa bega na ndugu zetu duniani pote, tunazungumza lugha moja ya kweli na kutenda kupatana na kweli tunayozungumza. Hilo lilitabiriwa Yehova alipotangaza hivi kupitia nabii Sefania: “Nitabadili lugha ya mataifa iwe lugha safi, ili wote waweze kuliitia jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.

14 Kisha, kupitia roho takatifu, Yehova alimwongoza Sefania kufafanua undugu wa ulimwenguni pote ambao ni halisi leo: “Waisraeli watakaobaki hawatatenda mambo yasiyo ya uadilifu; hawatasema uwongo, wala hawatakuwa na ndimi za udanganyifu vinywani mwao; watakula na kulala, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.” (Sef. 3:13) Baada ya kuelewa Neno la Yehova la kweli, kufanya upya akili zetu, na kupatanisha maisha yetu na viwango vya Yehova, tunaweza kufanya kazi kwa umoja. Tunatimiza mambo ambayo wale walio na mtazamo wa kimwili wanafikiri kwamba haiwezekani kuyatimiza. Kwa kweli, sisi ni watu tofauti, watu wa Mungu, tunaomletea heshima duniani pote.—Mika 2:12.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki