SOMO LA 71
Yehova Alimlinda Yesu
Katika nchi fulani iliyo upande wa mashariki mwa Israeli, kulikuwa na watu walioamini kwamba nyota zingeweza kuwaongoza. Pindi moja wakati wa usiku, wanaume fulani kutoka sehemu za mashariki waliona kitu kilichoonekana kama nyota yenye kung’aa ikisonga angani, na wakaifuata. “Nyota” hiyo ikawaongoza hadi Yerusalemu. Wanaume hao wakaanza kuwauliza watu hivi: ‘Yuko wapi yule mtoto ambaye atakuwa mfalme wa Wayahudi? Tumekuja kumsujudia.’
Herode, mfalme wa Yerusalemu, aliposikia kuhusu mfalme mpya, akawa na wasiwasi sana. Akawauliza wakuu wa makuhani hivi: ‘Mfalme huyo alipaswa kuzaliwa wapi?’ Wakamwambia hivi: ‘Manabii walisema kwamba angezaliwa Bethlehemu.’ Kwa hiyo, Herode akawaita wale wanaume kutoka mashariki na kuwaambia hivi: ‘Nendeni Bethlehemu mkamtafute mtoto huyo. Kisha, mrudi na kunieleza yuko wapi. Mimi pia ninataka kumsujudia.’ Lakini alikuwa akisema uwongo.
“Nyota” ile ikaanza kusonga tena. Wanaume hao wakaifuata hadi Bethlehemu. “Nyota” ile ikatua juu ya nyumba fulani na wanaume hao wakaingia ndani ya nyumba hiyo. Wakampata Yesu akiwa na Maria mama yake. Wakamsujudia mtoto huyo na kumpa zawadi za dhahabu, ubani, na manemane. Je, kweli Yehova alikuwa amewatuma wanaume hao wamtafute Yesu? Hapana.
Usiku huo, Yehova akamwambia hivi Yosefu kupitia ndoto: ‘Herode anataka kumwangamiza Yesu. Mchukue mke na mwana wako na mkimbilie Misri. Kaeni huko hadi nitakapowaambia kwamba ni salama kwenu kurudi.’ Mara moja, Yosefu na familia yake wakaenda Misri.
Yehova alikuwa amewaambia wanaume waliotoka mashariki kwamba wasirudi kwa Herode. Herode alipotambua kwamba wanaume hao hawatarudi, alikasirika sana. Kwa kuwa hangeweza kumpata Yesu, aliagiza wavulana wote waliokuwa na umri kama wa Yesu walioko Bethlehemu wauawe. Lakini Yesu alikuwa salama katika nchi ya mbali ya Misri.
Baada ya muda, Herode akafa. Yehova akamwambia Yosefu hivi: ‘Sasa ni salama kwako kurudi.’ Yosefu, Maria, na Yesu wakarudi Israeli, na kuishi katika jiji la Nazareti.
“Hivyo ndivyo neno langu linalotoka katika kinywa changu litakavyokuwa . . . , na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11