BOAZI, I
(Boazi) [huenda, Katika Nguvu].
Mmiliki wa ardhi huko Bethlehemu katika jiji la Yuda, “[aliyekuwa] tajiri sana” katika karne ya 14 K.W.K. hivi. (Ru 2:1) Boazi alikuwa mwana wa Salma (Salmoni) na Rahabu, na alikuwa baba ya Obedi. (Mt 1:5) Alikuwa sehemu ya orodha ya ukoo wa Masihi, akiwa wa saba katika orodha ya wazao wa Yuda. (1Nya 2:3-11; Lu 3:32, 33) Habari kuhusu jinsi mfuatano wa matukio yasiyotarajiwa ulivyofanya Boazi awe sehemu ya ukoo wa Yesu, zimehifadhiwa kwa ajili yetu kwenye kitabu cha Ruthu.
Boazi alikuwa na mtu wa karibu wa ukoo aliyeitwa Elimeleki, ambaye, alikufa pamoja na wanawe wawili bila kuacha mzao wa kiume ili awe mrithi. Ruthu, mmoja wa wajane hao, alishikamana na Naomi, mjane wa Elimeleki. Kilikuwa kipindi cha mavuno, na “bila kutarajia” Ruthu alienda kuokota masalio katika shamba la Boazi. (Ru 2:3) Boazi alikuwa Myudea, mwabudu mwenye bidii wa Yehova. Hakuwasalimia tu wavunaji wake kwa maneno haya “Yehova na awe pamoja nanyi,” bali pia, baada ya kutambua ushikamanifu wa Ruthu kumwelekea Naomi, alimwambia hivi, “Yehova na akuthawabishe kwa yale uliyofanya, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova.” (Ru 2:4, 12) Ruthu alipomwambia mama mkwe wake mambo hayo, Naomi alisema hivi: “Na abarikiwe na Yehova . . . Yeye ni kati ya watu wanaoweza kutukomboa.” (Ru 2:20) Zaidi ya hayo, mavuno yalipoisha, Naomi alimwelezea Ruthu jinsi ya kumwambia Boazi jambo hilo. Boazi alipokuwa amelala kwenye uwanja wa kupuria, aliamka na kukuta Ruthu amelala kwenye miguu yake iliyokuwa haijafunikwa, akimwomba akomboe mashamba ya Elimeleki kupitia ndoa ya ndugu mkwe. (Ona NDOA YA NDUGU MKWE.) Ruthu angekuwa mbadala wa Naomi, ambaye alikuwa amepita umri wa kupata watoto. Bila kupoteza muda, asubuhi iliyofuata Boazi alimtafuta mtu wa karibu zaidi wa ukoo, lakini mtu huyo, ambaye Biblia inamtaja tu kuwa fulani wa fulani, alikataa kufuata mpango wa Mungu. Hata hivyo, bila kukawia Boazi alimchukua Ruthu kuwa mke wake, wakipata ruhusa kutoka kwa watu wa jijini. Alimzalia mwana aliyeitwa Obedi, babu ya Mfalme Daudi.—Ru 3:1–4:17.
Katika simulizi lote, kuanzia salamu yake yenye fadhili kwa wafanyakazi mpaka kukubali kwake jukumu la kuendeleza jina la familia ya Elimeleki, Boazi anaonekana kuwa mwanamume wa pekee—mwanamume mwenye bidii na mamlaka, akiwa na sifa ya kujizuia, imani, na utimilifu, mkarimu na mwenye fadhili, safi kiadili, na mtiifu kikamili kwa amri za Yehova katika mambo yote.