MWILI
Umbo la mwanadamu au mnyama. Neno la Kiebrania gewi·yahʹ linarejelea mwili, iwe upo hai (Mwa 47:18) au umekufa. (1Sa 31:10; Zb 110:6) Neno la Kiebrania neve·lahʹ linatokana na mzizi wa kitenzi na·velʹ (‘nyauka’; Zb 1:3) na linatafsiriwa kwa njia tofauti-tofauti kuwa “mtu aliyekufa,” “mzoga,” na “maiti.” (Hes 9:6; Law 5:2; Isa 26:19) Neno la Kiebrania kwa ajili ya nyama, ba·sarʹ, linaweza kuwakilisha mwili mzima. (Linganisha Zb 16:9, maelezo ya chini; ona NYAMA.) Kwa kawaida neno la Kigiriki soʹma linatafsiriwa “mwili” (Mt 5:29), lakini neno khros, ambalo kihalisi linamaanisha “ngozi,” limetafsiriwa kuwa “mwili” kwenye Matendo 19:12. Neno la Kigiriki ptoʹma, ambalo linatokana na mzizi wa kitenzi piʹpto (anguka), linarejelea mwili ulioanguka au “maiti.” (Mt 14:12) Aina mbalimbali za miili zimefanyizwa kwa aina tofauti-tofauti za nyama, pamoja na nguvu za uhai.—1Ko 15:39; Yak 2:26; Mwa 7:22; ona NAFSI.
Miili ya Kiroho. Kama tu kulivyo na miili ya nyama, inayoonekana na kushikika, kuna miili ya kiroho, isiyoonekana kwa macho ya kibinadamu. (1Ko 15:44) Miili ya watu wa kiroho (Mungu, Kristo, malaika) ni yenye utukufu. “Hakuna mtu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (1Yo 4:12) Mwanadamu hawezi kumwona Mungu na aendelee kuishi. (Kut 33:20) Mtume Paulo alipoona sehemu ndogo tu ya utukufu wa Yesu Kristo baada ya ufufuo Wake, alianguka chini na kupofushwa na mng’ao wa utukufu huo, akahitaji muujiza ili arudishiwe uwezo wake wa kuona. (Mdo 9:3-5, 17, 18; 26:13, 14) Isitoshe, malaika wana nguvu nyingi kuliko wanadamu. (2Pe 2:11) Wana utukufu mwingi unaong’aa na wameonekana hivyo pia katika umbo la kibinadamu. (Mt 28:2-4; Lu 2:9) Wana hao wa kiroho wa Mungu wana uwezo wa kuona unaoweza kustahimili mng’ao wa utukufu wa Mungu Mweza-Yote.—Lu 1:19.
Kwa sababu hatuwezi kumwona Mungu kwa macho ya kibinadamu, anatumia baadhi ya semi za kibinadamu ili kutusaidia tumwelewe na kumthamini. Biblia inapozungumzia kumhusu inataja kwamba ana macho (Zb 34:15; Ebr 4:13); mikono (Ayu 40:9; Yoh 12:38); miguu (Zb 18:9; Zek 14:4); moyo (Mwa 8:21; Met 27:11); vidole (Kut 31:18; Lu 11:20); pua, mianzi ya pua (Eze 8:17; Kut 15:8); na masikio (1Sa 8:21; Zb 10:17). Haimaanishi kwamba kihalisi ana viungo hivyo kama tunavyovijua. Mtume Yohana, ambaye ana tumaini la kuishi mbinguni aliwaambia hivi warithi wenzake wa tumaini la kimbingu: “Wapendwa, sasa sisi ni watoto wa Mungu, lakini bado haijafunuliwa jinsi tutakavyokuwa. Tunajua kwamba atakapofunuliwa tutakuwa kama yeye, kwa sababu tutamwona kama alivyo.” (1Yo 3:2) Mwili wao utakuwa kama ‘mwili wenye utukufu’ wa Yesu Kristo (Flp 3:21), ambaye ni “mfano wa Mungu asiyeonekana,” “mng’ao wa utukufu wa Mungu na mfano kamili wa utu wake.” (Kol 1:15; Ebr 1:3) Kwa hiyo, watapokea miili isiyoweza kuharibika, isiyoweza kufa, ambayo ni tofauti na ya wanadamu na ya malaika wote, ambao wanaweza kufa.—1Ko 15:53; 1Ti 1:17; 6:16; Mk 1:23, 24; Ebr 2:14.
Mwili wa Nyama wa Yesu. Yesu alipokuwa akianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana aliwapa mitume wake 11 waaminifu mkate usiotiwa chachu na kuwaambia: “Huu unamaanisha mwili wangu, ambao utatolewa kwa ajili yenu.” (Lu 22:19) Baadaye, mtume Petro alisema hivi: “Yeye [Yesu] mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti.”—1Pe 2:24; Ebr 10:10; ona MLO WA JIONI WA BWANA.
Ili Yesu awe “Adamu wa mwisho” (1Ko 15:45) na awe “fidia inayolingana kwa ajili ya [wanadamu] wote,” mwili wake wa nyama ulipaswa kuwa mwili halisi wa mwanadamu, na wala si mwili wa kiumbe wa roho aliyejivika mwili wa kibinadamu. (1Ti 2:5, 6; Mt 20:28) Ulipaswa kuwa mkamilifu, kwa kuwa ungetolewa dhabihu kwa Yehova Mungu kama bei ya ukombozi. (1Pe 1:18, 19; Ebr 9:14) Hakuna mwanadamu asiyekamilika ambaye angeweza kulipia bei hiyo. (Zb 49:7-9) Kwa sababu hiyo, Yesu alipokuwa akijitoa ili abatizwe na kuanza maisha yake ya kujidhabihu alimwambia hivi Baba yake: “Ulinitayarishia mwili.”—Ebr 10:5.
Mwili wa nyama wa Yesu haukuachwa uoze na kuwa mavumbi kama tu ilivyokuwa kwa mwili wa Musa na Daudi, wanaume waliotumiwa kumrejelea Kristo. (Kum 34:5, 6; Mdo 13:35, 36; 2:27, 31) Wanafunzi wake walipoenda kwenye kaburi asubuhi na mapema siku ya kwanza ya juma mwili wa Yesu haukuwepo, na vitambaa ambavyo vilikuwa vimeufunika mwili wake viliachwa kaburini, bila shaka mwili wake ulitoweka//ulisambaratika bila kuoza.—Yoh 20:2-9; Lu 24:3-6.
Baada ya Yesu kufufuliwa alionekana katika miili tofauti-tofauti. Maria alimfananisha na mtunza-bustani. (Yoh 20:14, 15) Halafu alionekana akiwa na mwili wenye alama za majeraha alipoingia kwenye chumba milango ikiwa imefungwa. (Yoh 20:24-29) Mara kadhaa alijifunua mwenyewe na kutambuliwa, si kwa mwonekano wake, bali kwa maneno na matendo yake. (Lu 24:15, 16, 30, 31, 36-45; Mt 28:16-18) Pindi moja, muujiza uliofanywa kwa mwongozo wake ulifungua macho ya wanafunzi wake nao wakamtambua. (Yoh 21:4-7, 12) Kwa kuwa Yesu alifufuliwa katika roho (1Pe 3:18), pindi fulani aliweza kujivika mwili wa kibinadamu kama malaika walivyofanya nyakati zilizopita, walipotokea kama wajumbe. (Mwa 18:2; 19:1, 12; Yos 5:13, 14; Amu 13:3, 6; Ebr 13:2) Katika kipindi cha kabla ya Gharika, malaika ambao “hawakubaki mahali pao pa kwanza bali waliacha makao yao yanayowafaa” walijivika miili ya kibinadamu na kuoa mabinti wa wanadamu. Uthibitisho kuwa wana hao wa Mungu wa kimalaika hawakuwa wanadamu halisi bali walikuwa wamejivika miili ya kibinadamu unaonyeshwa na ukweli wa kwamba Gharika haikuwaharibu malaika hao, bali walijivika miili yao ya kiroho na kurudi kwenye makao ya roho.—Yuda 6; Mwa 6:4; 1Pe 3:19, 20; 2Pe 2:4.
Matumizi ya Mfano. Yesu Kristo anatajwa akiwa Kichwa cha “kutaniko, ambalo ni mwili wake.” (Efe 1:22, 23; Kol 1:18) Mwili huo wa watu wa Kikristo hauna migawanyiko ya kitabaka, kitaifa, au vinginevyo, Wayahudi na watu wa mataifa yote wakiwakilishwa nao. (Gal 3:28; Efe 2:16; 4:4) Wote wanabatizwa kwa roho takatifu katika Kristo na katika kifo chake. Kwa hiyo, wote wanabatizwa katika mwili mmoja. (1Ko 12:13) Hivyo basi, mwili wote unamfuata kichwa, ukifa katika kifo kama chake na kupokea ufufuo kama wake.—Ro 6:3-5; ona UBATIZO (Kubatizwa Katika Kristo Yesu, Katika Kifo Chake).
Mtume Paulo alitumia mfano wa jinsi mwili wa mwanadamu unavyofanya kazi ili kuonyesha jinsi kutaniko la Kikristo linavyofanya kazi, akiwafananisha washiriki wake wanaoishi duniani wakati wowote na mwili, huku Kristo akiwa Kichwa asiyeonekana. (Ro 12:4, 5; 1Ko 12) Alikazia umuhimu wa nafasi ya kila mshiriki, ushirikiano wao, upendo na utunzaji wa kweli, na kutimizwa kwa kazi. Mungu amemweka kila mmoja katika nafasi yake katika mwili, na kupitia utendaji wa aina mbalimbali wa roho takatifu, mwili unatimiza kile kinachohitajiwa. Yesu Kristo, ambaye ni Kichwa, anapotenda kama kiunganishi, anavipa viungo vya mwili vitu wanavyohitaji kupitia “viungo na kano zake,” yaani, mipango na njia za kusambaza chakula cha kiroho pamoja na uratibu na mawasiliano, ili “mwili” ulishwe vizuri kiroho na kila kiungo kijue mgao wa kutimiza.— Kol 2:19; Efe 4:16.
Matumizi Yanayofaa ya Mwili. Mkristo anapaswa kuuthamini mwili ambao Mungu amempa na anapaswa kujipenda kufikia hatua ya kuutunza vizuri mwili wake ili aweze kuutoa ukiwa unakubalika, utumishi mtakatifu kwa Mungu. (Ro 12:1) Hilo linahusisha kutumia akili na kuutunza mwili kwa chakula na mahitaji mengine ya msingi, pamoja na usafi wa kimwili, lakini aina nyingine za utunzaji ni za muhimu zaidi. Aina hizo zinatia ndani hali ya kiroho, kuutafuta Ufalme wa Mungu na uadilifu wake, na kufuata viwango vya maadili. (Mt 6:25, 31-33; Kol 2:20-23; 3:5) Mtume Paulo anashauri hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo, lakini ujitoaji-kimungu una faida katika mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1Ti 4:8.
Mtu ambaye ni mshiriki aliyetiwa mafuta kwa roho katika kutaniko la Kikristo, mwili wa Kristo, ambaye anafanya uasherati anakiondoa kiungo cha Kristo na kukifanya kuwa kiungo cha ukahaba. Mkristo yeyote anayefanya uasherati anajiletea unajisi wa kimaadili na pia “anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” Anajiweka mwenyewe kwenye hatari kubwa ya kuondolewa kutoka katika mwili wa Kristo, usimamizi wa hekalu, na anajiweka katika hatari ya kupata magonjwa ya kufisha. (1Ko 6:13, 15-20 Met 7:1-27) Anaweza ‘kukabidhiwa na kutaniko kwa Shetani kwa ajili ya kuangamizwa kwa mwili.’—1Ko 5:5)
Wale ambao ni viungo vya mwili wa Kristo, pamoja na wengine waliojiweka wakfu ambao wanashirikiana na viungo hivyo vya mwili vilivyonunuliwa kwa roho, wanapaswa kuepuka si tu uasherati wa kimwili bali pia uasherati wa kiroho. Maandiko yanamwita mtu anayefanya urafiki na ulimwengu ‘mzinzi.’ (Yak 4:4) Yesu alisema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh 17:16) Kwa hiyo, Yesu anahakikisha kwamba wale wanaofanyiza viungo vya mwili wake ni wasafi kiadili na kiroho. (Efe 5:26, 27) Inasemwa kwamba ‘miili yao imeoshwa kwa maji safi.’ (Ebr 10:22) Hilo linapatana na yale ambayo mtume Paulo aliwaambia waume: “Vivyo hivyo, waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Mwanamume anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza, kama vile Kristo anavyolitendea kutaniko, kwa kuwa sisi ni viungo vya mwili wake. ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.’ Siri hii takatifu ni kubwa. Sasa ninazungumza kuhusu Kristo na kutaniko.”— Efe 5:28-32.
Ona sehemu za mwili chini ya majina ya kibinafsi//jina moja-moja.