Neno la Mungu Li Hai
Kristo Anarudi Namna Gani?
YESU KRISTO alihitaji kufa ili atoe uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe ukombozi kwetu. Wakati mmoja alieleza hivi: “Chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Baada ya kutupa sisi mwili wake, je! angeuchukua tena wakati wo wote? Je! Yesu atarudi akiwa mwanadamu?
Biblia inasema kwamba Kristo anarudi katika utukufu pamoja na malaika wote, na kwamba ‘anaketi katika kiti cha utukufu wake.’ (Mathayo 25:31) Kama Yesu angekuja na kuketi akiwa mwanadamu juu ya kiti cha kifalme cha kidunia, cheo chake kingekuwa chini ya kile cha malaika. Lakini yeye anakuja akiwa ndiye mwana mwenye nguvu na utukufu mwingi kuliko wana hao wote wa kiroho wa Mungu, na kwa hiyo haonekani, sawa na vile wao wasivyoonekana.—Wafilipi 2:8-11.
Hata hivyo kuna watu wengi wanaoamini kwamba Kristo alienda mbinguni akiwa na mwili wake wenye nyama, na kwamba atarudi akiwa na mwili wenye nyama na damu. Wanaonyesha uhakika wa kwamba zaidi ya mara moja Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake akiwa na mwili wenye nyama ili kuwaonyesha kwamba alikuwa hai. Wakati mmoja Yesu alimwagiza mtume Tomaso atie mkono wake ndani ya tundu lililokuwa karibu na ubavu wake ili Tomaso aamini kwamba kweli alikuwa amefufuliwa. (Yohana 20:24-27) Je! hiyo haionyeshi kwamba Yesu alifufuliwa kwa wafu akiwa na mwili ule ule uliopigiliwa misumari kwenye mti?
Hapana, kwa maana alilofanya Yesu ni kuvaa tu mwili wenye nyama, kama vile malaika walivyokuwa wamefanya zamani. Ili kusadikisha Tomaso yeye ni nani, alitumia mwili fulani wenye matundu ya majeraha. Alionekana kuwa mwanadamu kabisa, mwenye kuweza kula na kunywa, sawa na wale malaika ambao Abrahamu alikuwa amekaribisha wakati mmoja na kuwafurahisha.—Mwanzo 18:8.
Ingawa Yesu alimtokea Tomaso akiwa na mwili wenye kufanana na ule aliouawa akiwa nao, alivaa pia miili mbalimbali alipokuwa akiwatokea wafuasi wake. Ndiyo sababu Mariamu Magdalene alifikiri safari moja kwamba Yesu alikuwa ni mtunza-bustani. Nyakati nyingine wanafunzi wa Yesu hawakumtambua mara ya kwanza. Nyakati hizo si sura yake ya kibinafsi iliyosaidia kumtambulisha, bali ni neno au tendo fulani walilolitambua.—Yohana 20:14-16; 21:6, 7; Luka 24:30, 31.
Fikiria njia ambayo katika hiyo Yesu aliwaacha mitume wake akiwa safarini kwenda mbinguni. Biblia inasema: “Walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao.” (Matendo 1:9) Kwa hiyo Yesu alipoanza kwenda angani, wingu lilimfunika akaachwa kuonwa na macho halisi ya mitume wake. Basi, Yesu huyo mwenye kwenda zake aliacha kuonekana nao. Wao wasingeweza kumwona. Alienda mbinguni akiwa na mwili wa kiroho. (1 Petro 3:18) Malaika waliokuwako wakati huo waliwaambia mitume hivi: “Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.” (Matendo 1:11) Basi hata kurudi kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana, akiwa na mwili wa kiroho.