KUTOWEZA KUFA
Neno la Kigiriki a·tha·na·siʹa limeundwa kwa kiambishi a kinachokanusha muundo wa neno linalotafsiriwa “kifo” (thaʹna·tos). Hivyo, maana ya msingi ni ‘kutoweza kufa,’ na inarejelea ubora wa uhai ambao unafurahiwa, kutokuwa na mwisho kwa uhai huo na kutoharibika kwake. (1Ko 15:53, 54; 1Ti 6:16) Neno la Kigiriki a·phthar·siʹa, linalomaanisha “kutoweza kuharibika,” linarejelea uhai usioweza kudhoofika au kuharibika, ule unaodumu milele.—Ro 2:7; 1Ko 15:42, 50, 53; Efe 6:24; 2Ti 1:10.
Maneno “asiyeweza kufa” au “kutoweza kufa” hayapatikani katika Maandiko ya Kiebrania, hata hivyo, Maandiko hayo yanaonyesha kwamba, Yehova Mungu, akiwa chanzo cha uhai wote, hawezi kupatwa na kifo, hivyo, hawezi kufa. (Zb 36:7, 9; 90:1, 2; Hab 1:12) Pia, ukweli huo umeonyeshwa wazi na mtume Mkristo Paulo alipomrejelea Mungu kama “Mfalme wa umilele, asiyeweza kuharibika.”—1Ti 1:17.
Vilevile, kama makala NAFSI inavyoonyesha, Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha wazi kwamba mwanadamu hakuumbwa akiwa asiyeweza kufa. Mara nyingi nafsi (Kiebr., neʹphesh) ya mwanadamu inatajwa kuwa inakufa, inaenda kaburini, na inaharibiwa. (Mwa 17:14; Yos 10:32; Ayu 33:22; Zb 22:29; 78:50; Eze 18:4, 20) Hali kadhalika, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanapatana na yanataja kuhusu kufa kwa nafsi (Kigr., psy·kheʹ). (Mt 26:38; Mk 3:4; Mdo 3:23; Yak 5:20; Ufu 8:9; 16:3) Hivyo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hayapingani au kutofautiana na fundisho lililoongozwa na roho la Maandiko ya Kiebrania kwamba mwanadamu, nafsi ya mwanadamu, hufa, inaweza kufa. Ingawa hivyo, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanafunua kusudi la Mungu la kuwapa baadhi ya watumishi wake uhai usioweza kufa.
Yesu anawezaje kuwa “yeye peke yake asiyeweza kufa”?
Mtu wa kwanza kutajwa kwenye Biblia kwamba amezawadiwa kutoweza kufa ni Yesu Kristo. Ukweli wa kwamba Yesu hakuwa na uhai usioweza kufa kabla ya kufufuliwa na Mungu unaonekana katika maneno ya mtume Paulo yaliyoongozwa na roho kwenye Waroma 6:9: “Kristo, kwa kuwa sasa amefufuliwa kutoka kwa wafu, hatakufa tena; kifo si bwana juu yake tena.” (Linganisha Ufu 1:17, 18.) Kwa sababu hiyo, andiko la 1 Timotheo 6:15, 16 linapotaja kwamba Yesu ni “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” linaonyesha kwamba yeye ni tofauti na wafalme na mabwana wengine wote kwa kuwa ni “yeye peke yake asiyeweza kufa.” Wafalme na mabwana wengine, kwa kuwa hawana uhai usioweza kufa, wanakufa, kama tu makuhani wakuu wa Israeli walivyokufa. Hata hivyo, Yesu aliyetukuzwa, aliyechaguliwa na Mungu kuwa Kuhani Mkuu kwa mfano wa Melkizedeki, ana “uzima usioweza kuharibika.”—Ebr 7:15-17, 23-25.
Neno hili “usioweza kuharibika” linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki a·ka·taʹly·tos, ambalo kihalisi linamaanisha “usio na kikomo.” (Ebr 7:16, UV) Neno hilo ni muunganiko wa kiambishi a kinachokanusha maneno mengine yanayohusiana na “kuangushwa chini,” kama maneno ya Yesu yanayohusiana na kuangushwa chini kwa mawe ya hekalu la Yerusalemu (Mt 24:1, 2), na pia kwenye maneno ya Paulo kuhusiana na kuvunjwa kwa “hema” la kidunia la Wakristo, yaani, kuharibiwa kwa maisha yao ya kidunia katika miili ya kibinadamu. (2Ko 5:1) Kwa hiyo, uhai usioweza kufa ambao Yesu alipewa alipofufuliwa si tu wa milele lakini hauwezi kudhoofika wala kuisha na hauwezi kuharibika.
Watawala Wenzi Kupewa Kutoweza Kufa. Wakristo watiwa-mafuta waliochaguliwa ili kutawala pamoja na Kristo mbinguni (1Pe 1:3, 4), wameahidiwa kushiriki pamoja na Kristo katika mfano wa ufufuo wake. (Ro 6:5) Hivyo, kama katika kisa cha Yesu aliye Bwana na Kichwa chao, wale waliotiwa mafuta katika kutaniko la Kikristo wanapokufa wakiwa waaminifu wanafufuliwa wakiwa viumbe wa kiroho wasioweza kufa, ili ‘huu unaoweza kufa uvae kutoweza kufa.’ (1Ko 15:50-54) Kama Yesu, kutoweza kufa katika kisa chao hakumaanishi tu uhai wa milele, au uhuru kutokana na kifo. Kunamaanisha kwamba wao pia wanapewa “nguvu za uzima usioweza kuharibika” wakiwa watawala wenzi pamoja na Kristo na hilo linaonekana katika maneno ya mtume Paulo kuhusiana na hali ya kutoweza kuharibika na kutoweza kufa wanayopokea. (1Ko 15:42-49) “Kifo cha pili hakina mamlaka” juu yao.—Ufu 20:6; ona KUTOWEZA KUHARIBIKA.
Ni jambo la pekee sana kwa warithi wa Ufalme kupewa kutoweza kufa, kwa kuzingatia ukweli huu kwamba hata malaika wa Mungu, licha ya kwamba wana miili ya kiroho na si ya nyama, wanatajwa kuwa wanaweza kufa. Uhakika wa kwamba malaika wanaweza kufa unaonekana katika hukumu ya kifo ambayo amepewa mwana wa kiroho aliyekuja kuwa Mpinzani wa Mungu, au Shetani, na pia hukumu dhidi ya malaika wengine waliofuata mwenendo wa kishetani na “hawakubaki mahali pao pa kwanza bali waliacha makao yao yanayowafaa.” (Yud 6; Mt 25:41; Ufu 20:10, 14) Kwa hiyo, kupewa “uzima usioweza kuharibika” (Ebr 7:16) au “uzima usio na kikomo” kwa Wakristo ambao wamepata pendeleo la kutawala na Mwana wa Mungu katika Ufalme wa mbinguni kunaonyesha kwa njia ya pekee uhakika ambao Mungu anao kuwaelekea.—Ona MBINGU (Njia ya kuingia katika maisha\uhai ya mbinguni); UHAI.