YEHOVA WA MAJESHI
Maneno hayo au yanayofanana na hayo yanapatikana zaidi ya mara 270 kwenye Maandiko, na yanatokana na maneno ya Kiebrania Yeho·wahʼ tseva·ʼohthʼ. Yanapatikana mara nyingi zaidi katika vitabu vya unabii kama vile Isaya, Yeremia, na Zekaria. Waliponukuu au kurejezea unabii, Paulo na Yakobo walitumia maneno yanayofanana na hayo (yaliyotoholewa kutoka Kiebrania kwenda Kigiriki) kwenye maandishi yao.—Ro 9:29; Yak 5:4; linganisha Isa 1:9.
Kimsingi, neno la Kiebrania tsa·vaʼʼ (umoja; wingi wake ni, tseva·ʼohthʼ) linamaanisha jeshi halisi la wanajeshi au kikosi cha wanajeshi, kama ilivyo katika Mwanzo 21:22; Kumbukumbu la Torati 20:9, na maandiko mengine. Hata hivyo, neno hilo linatumiwa pia katika njia ya mfano, kama vile “mbingu na dunia na jeshi lake lote likakamilika,” au “jua na mwezi na nyota—jeshi lote la mbinguni.” (Mwa 2:1, maelezo ya chini; Kum 4:19) Neno la wingi (tseva·ʼohthʼ) linatumiwa mara kadhaa kurejelea majeshi ya Israeli kwa mfano katika Zaburi 44:9; 60:10. Baadhi ya wasomi wanaamini kwamba neno “majeshi” katika usemi “Yehova wa majeshi” linarejelea si majeshi ya malaika tu, bali pia jeshi la Israeli na vitu vya angani visivyo hai. Hata hivyo, inaonekana kwamba neno “majeshi” kimsingi linarejelea hasa majeshi ya malaika.
Yoshua alipomwona malaika karibu na Yeriko alimuuliza ikiwa alikuwa upande wa Israeli au upande wa adui zao, malaika huyo alimjibu hivi, “Hapana, mimi ni mkuu wa jeshi la Yehova.” (Yos 5:13-15) Nabii Mikaya alimwambia Mfalme Ahabu na Mfalme Yehoshafati hivi, “Nilimwona Yehova akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme na jeshi lote la mbinguni likiwa limesimama kando yake, upande wake wa kulia na upande wake wa kushoto,” bila shaka akimaanisha wana wa kiroho wa Yehova. (1Fa 22:19-21) Maneno “Yehova wa majeshi” yanafaa kwa kuwa majeshi ya malaika yamepangwa katika vikundi vya makerubi, maserafi na malaika (Isa 6:2, 3; Mwa 3:24; Ufu 5:11) na makundi hayo yamepangwa kwa utaratibu, hivi kwamba Yesu Kristo alisema angeweza kuomba “vikosi zaidi ya 12 vya malaika.” (Mt 26:53) Hezekia alipomsihi Yehova amsaidie, alimwita “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, unayeketi kwenye kiti cha ufalme juu ya makerubi,” huenda akirejelea sanduku la agano na makerubi waliokuwa juu ya kifuniko chake, waliowakilisha kiti cha ufalme cha Yehova kilicho mbinguni. (Isa 37:16; linganisha 1Sa 4:4; 2Sa 6:2) Mtumishi wa Elisha aliyekuwa akiogopa alifarijika alipoona kimuujiza eneo lenye milima iliyozunguka jiji alimoishi Elisha likiwa “limejaa farasi na magari ya vita ya moto,” yaliyokuwa sehemu ya majeshi ya Yehova ya malaika.—2Fa 6:15-17.
Hivyo, maneno “Yehova wa majeshi” yanaonyesha nguvu, nguvu alizo nazo Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu mzima anayeongoza jeshi kubwa la viumbe wa roho. (Zb 103:20, 21; 148:1, 2; Isa 1:24; Yer 32:17,?18) Jambo hilo linawafanya watumishi wa Yehova wamheshimu sana na kumstaajabia na wakati huohuo wanafarijika na kutiwa moyo. Akiwa peke yake na bila msaada wa jeshi lolote hapa duniani, Daudi alipigana na Goliathi, jitu la Ufilisti, “kwa jina la Yehova wa majeshi, Mungu wa vikosi vya Israeli.” (1Sa 17:45) Wanapokabili vita halisi na pia majaribu mengine yoyote, au pindi muhimu, watu wa Mungu wakiwa kikundi au mtu binafsi wanaweza kupata ujasiri na tumaini wanapotambua ukuu wa enzi kuu ya Yehova unaoonyeshwa na jinsi anavyoongoza majeshi yenye nguvu yanayomtumikia mbinguni. (1Sa 1:9-11; 2Sa 6:18; 7:25-29) Manabii walipotumia maneno “Yehova wa majeshi” waliwahakikishia wale waliosikiliza unabii huo kwamba utatimia.