Je, Tutahitaji Majeshi Sikuzote?
MAJESHI yametumia sehemu kubwa ya mali za binadamu na kumharibia mwanadamu furaha nyingi. Kwa hiyo watu fulani wameuliza, ‘Je, wanadamu waweza kufanikiwa wakati wowote kuwa na aina ya usalama wa ulimwengu ambao hauruhusu majeshi kuwako?’ Kwa vile sasa silaha zenye uharibifu mkubwa zimefanya kuwe na uwezekano wa uhai wote kutoweka kabisa, hilo swali lawa lenye hima. Je, ni jambo halisi jinsi gani kutumainia kuwa na ulimwengu usio na majeshi?
Vielelezo vingi huthibitisha kwamba, wakati ambapo mahusiano mazuri ya kimataifa hutokeza hali ya uhakika, huenda yakaongoza kwenye kupunguzwa kwa silaha. Kwa mfano, urafiki wa kawaida kati ya Kanada na Marekani, umemaanisha kwamba mpaka kati yao wenye urefu wa kilometa 5,000, umekuwa bila ulinzi wa majeshi kwa zaidi ya karne moja na nusu. Kama vile mataifa mengine mengi, Norway na Sweden zimefanikiwa kuwa na upatano kama huo. Je, upatano kati ya mataifa yote waweza kufanikiwa kuleta ulimwengu usio na majeshi? Kwa sababu ya machukizo ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, hilo wazo lilipata kupendwa kwa njia isiyo na kifani.
Amani ilipofanywa mwaka wa 1918, mojawapo ya makusudi ya mapatano ya amani ya Versailles lilikuwa “kuwezesha kuanzishwa kwa upunguzaji wa silaha wa ujumla wa mataifa yote.” Wakati wa miaka iliyofuata, upinzani-vita ukawa wenye kupendwa sana. Wapinzani-vita fulani walidhani kwamba vita ilikuwa jambo lililo baya zaidi liwezalo kulipata taifa na kwa hiyo ni mbaya zaidi ya kushindwa. Wapinzani wa wapinzani-vita hawakukubaliana na hilo, wakitoa hoja kwamba kwa karne kadhaa zilizopita, Wayahudi katika maeneo makubwa hawakukinza kwa silaha washambuliaji, hata hivyo majaribio yenye ukatili ya kuwaangamiza kabisa yaliendelea. Waafrika walikuwa na fursa ndogo ya kukinza wale waliowapeleka mabara ya Amerika, na hata hivyo, walitendwa kikatili kwa karne nyingi.
Hata hivyo, kwa sababu ya kuzuka kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, wapinzani-vita wengi walikata kauli kwamba nchi zahitaji ulinzi. Kwa hiyo, Umoja wa Mataifa ulipoanzishwa baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, mkazo ulikuwa mdogo juu ya kupunguzwa kwa silaha, ukaongezwa juu ya ushirikiano wa kimataifa ili kuzuia uchokozi. Washiriki walitumaini kwamba usalama ulioandaliwa ungeyapa mataifa uhakika wa kupunguza silaha.
Tatizo jingine lilipata kuwa wazi zaidi. Mara nyingi jitihada za taifa fulani za kujifanya salama zilifanya mataifa jirani zake yahisi kuwa bila usalama. Duru hiyo ya matukio iliongoza kwenye shindano la silaha. Lakini majuzi mahusiano yaliyoboreka kati ya mataifa makubwa yameimarisha tumaini la kupunguza silaha. Hata hivyo, tangu wakati huo, Vita ya Ghuba na machafuko yaliyokuwa katika Yugoslavia ya zamani yamevunja matumaini ya wengi juu ya kupunguzwa kwa silaha. Miaka ipatayo mitano iliyopita, gazeti la Time lilieleza hivi: “Ingawa vita baridi imekwisha, ulimwengu umekuwa pahali penye hatari iliyoongezeka, badala ya kuwa salama zaidi.”
Tamaa ya Kuwa na “Polisi” wa Tufeni Pote
Watazamaji wengi hukata kauli kwamba wanadamu wahitaji serikali moja ya ulimwengu yenye jeshi lenye nguvu za kutosha kumlinda kila mtu. Kwa kuwa wala shirika la Umoja wa Mataifa wala serikali za kijeshi zenye kuongoza haziwezi kufanya hivyo, wengine huhisi kwamba kuna tumaini dogo kwa wakati ujao. Lakini ikiwa umeikubali Biblia kuwa Neno la Mungu, huenda ikawa umeuliza kama Mungu Mweza Yote atatosheleza uhitaji huo wa hima.
Je, Yule ambaye Biblia humwita “Mungu wa upendo na amani” angetumia uwezo wa kijeshi ili kutekeleza haki? Ikiwa ndivyo, ni jeshi gani? Majeshi mengi ya leo hudai kuwa na utegemezo wa Mungu, lakini je, wao kwa kweli wanatekeleza mapenzi ya Mungu? Au je, Mungu ana njia nyingine ya kuingilia kati na kuandaa amani na usalama?—2 Wakorintho 13:11.
Mungu Mweza Yote alishughulika na uasi wa kwanza kwa kuwafukuza Adamu na Hawa kutoka Edeni na kusimamisha makerubi ili kuwazuia wasirudi. Pia alitangaza kusudi lake la kuponda uasi wote dhidi ya enzi kuu yake. (Mwanzo 3:15) Je, huenda hilo likahusisha Mungu kutumia jeshi fulani?
Biblia husema juu ya pindi ambapo Mungu alitumia majeshi ili kutekeleza hukumu zake. Kwa mfano, falme katika nchi ya Kanaani zilizoea ngono pamoja na wanyama, kudhabihu watoto, na shughuli za vita zenye ukatili mwingi. Mungu aliagiza waharibiwe kabisa, akatumia jeshi la Yoshua kutekeleza hiyo hukumu. (Kumbukumbu la Torati 7:1, 2) Vivyo hivyo, jeshi la Mfalme Daudi lilitekeleza hukumu ya Mungu dhidi ya Wafilisti ukiwa mfano wa jinsi ambavyo Mungu ataharibu uovu wote siku yake ya mwisho ya hukumu.
Matukio hayo yalikuwa yenye kufundisha. Yehova alionyesha kwamba aweza kutumia jeshi kuwatolea watu wake usalama. Kwa kweli, Yehova ana jeshi la namna ya pekee ambalo litashughulika na uasi mkubwa wa ulimwengu dhidi ya utawala wake.
“Yehova wa Majeshi”
Biblia hutumia usemi “Yehova wa majeshi” zaidi ya mara 250. Huo husema kimsingi warejezea cheo cha Mungu akiwa kamanda wa majeshi mengi sana ya malaika. Pindi moja nabii Mikaya aliwaambia Wafalme Ahabu na Yehoshafati hivi: “Nalimwona BWANA ameketi katika kiti chake cha enzi, na jeshi lote la mbinguni wamesimama upande wa mkono wake wa kuume na wa kushoto.” (1 Wafalme 22:19) Ni majeshi ya malaika yanayorejezewa hapa. Yehova aliyatumia majeshi hayo kulinda watu wake. Jiji la Dothani lilipozingirwa, mtumishi wa Elisha alikata tumaini. Hata hivyo, ili kumtumainisha, Mungu alimwonyesha kimuujiza jeshi lake la viumbe-roho. “BWANA akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto.”—2 Wafalme 6:15-17.
Je, matukio kama hayo yamaanisha kwamba Mungu huyaunga mkono majeshi leo? Huenda majeshi fulani ya Jumuiya ya Kikristo yakadai kuwa ya Mungu. Wengi wamewaomba makasisi wayabariki. Lakini mara nyingi majeshi ya Jumuiya ya Wakristo hupigana vita yenyewe na dhidi ya waamini wenzao. Vita viwili vya ulimwengu vya karne hii vilianza kati ya majeshi yaliyodai kuwa ya Kikristo. Hiyo haiwezi kuwa kazi ya Mungu. (1 Yohana 4:20) Ingawa huenda majeshi hayo yakadai kwamba yapigania amani, je, Yesu aliwaagiza wafuasi wake wayapange majeshi kama hayo katika jaribio la kuzuia kuvurugwa kwa amani duniani?
Kuvunjwa kwa amani kukubwa kulitokea wakati ambapo kikundi chenye ghasia kilichokuwa na silaha kilimkamata Yesu katika bustani ambako alikuwa amekuwa akiomba pamoja na wanafunzi wake. Mmoja wa wanafunzi hao alimpiga kwa upanga mwanamume fulani aliyekuwa katika kikundi hicho chenye ghasia. Yesu alitumia hiyo pindi kueleza kanuni fulani ya maana. Alisema hivi: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga. Au wafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika?” Yesu alikuwa na jeshi kubwa sana lililo chini ya usimamizi wake, lakini Petro hakuwa ameandikishwa kuwa askari katika jeshi hilo, wala hakuna binadamu mwingine yeyote ambaye ameandikishwa. Badala ya hivyo, Petro na wafuasi wale wengine wa Yesu waliitwa wawe “wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19; 26:47-53) Saa chache baadaye, Yesu alielewesha jambo hilo wazi kwa Pilato. Alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangalipigana ili nisikabidhiwe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Tofauti na ufalme wa Daudi uliosimamishwa duniani, Ufalme ambao Mungu amempa Yesu uko mbinguni na utaleta amani duniani.
Majeshi ya Mungu Yaingia Vitani
Karibuni majeshi ya Mungu yatachukua hatua. Kikifafanua kabiliano lenye uhasama lililoko mbele, kitabu Ufunuo chamwita Yesu “Neno la Mungu.” Twasoma hivi: “Majeshi yaliyokuwa mbinguni yalikuwa yakimfuata juu ya farasi weupe, nayo yalikuwa yamevikwa kitani nyeupe, safi, bora. Na kutoka kinywani mwake hutokeza upanga mrefu mkali, ili apate kupiga mataifa kwa huo.” Biblia husema kwamba kabiliano hilo lenye uhasama litatokeza mwisho wa “wafalme wa dunia na majeshi yao.” Kwa habari ya wengine ambao hushindwa kuonyesha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Mungu, unabii waongeza kusema hivi: “Wale wengine wakauawa kabisa kwa upanga mrefu wa yeye aketiye juu ya farasi.” Hata Shetani Ibilisi atawekwa katika hali ya kutotenda. Hilo kwa kweli litawezesha kuwe na ulimwengu wa amani bila majeshi.—Ufunuo 19:11-21; 20:1-3.
Ebu Wazia Ulimwengu Bila Vita
Je, waweza kuwazia ulimwengu ulio salama sana hivi kwamba majeshi hayahitajiwi? Zaburi fulani ya Biblia husema hivi: “Njoni myatazame matendo ya BWANA, jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:8, 9.
Hicho kitakuwa kitulizo kilichoje! Ebu wazia uwezekano wa kuwa na jamii ya kibinadamu ikiwa imefunguliwa kutoka mzigo wenye kulemea na wenye kuumiza wa kulipia majeshi na vifaa vyake! Watu wataweza kuelekeza nishati zao kwenye kuboresha hali za kuishi kwa ajili ya kila mtu, kwenye kusafisha dunia na kuipanda mimea tena. Kutakuwa fursa mpya za kubuni vitu ambavyo kikweli vitakuwa vyenye manufaa kwa wanadamu.
Ahadi hii itakuwa na utimizo wa ulimwenguni pote: “Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako.” (Isaya 60:18) Mamilioni ya wakimbizi wenye kukata tumaini hawatamiminika tena kamwe kutoka katika kanda za vita, wakiwa wamelazimishwa kuacha nyumba zao na mali na kwenda kuishi katika kambi za taabu. Watu hawatawaombolezea tena kamwe wapendwa waliouawa au kuharibiwa viungo katika mapambano kati ya mataifa. Mfalme wa kimbingu wa Yehova ataleta amani ya ulimwengu yenye kudumu. “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu.”—Zaburi 72:7, 14.
Maisha yatakuwa yenye kupendeza hata zaidi miongoni mwa watu ambao wamejifunza si kuchukia bali kuziiga njia za Mungu za upendo. Neno la Mungu latabiri hivi: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Itakuwaje kuishi miongoni mwa watu wamjuao na kumpenda Yehova? Kitabu hichohicho chaendelea kutabiri hivi: “Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”—Isaya 11:9; 32:17, 18.
Watu ambao imani yao imejengwa juu ya ujuzi wa Biblia hufahamu kwamba majeshi ya Mungu yako tayari kuwaondoa maadui wote wa amani kutoka duniani. Ujuzi huo huwapa uhakika wa kutenda kupatana na yale Biblia isemayo ‘yatatukia katika siku za mwisho.’ Yaani: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:2-4.
Watu kutoka mataifa mengi ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova tayari hujiepusha na ‘kujifunza vita.’ Wameweka uhakika wao katika ulinzi wa majeshi ya Mungu ya kimbingu. Kwa kujifunza Biblia pamoja nao, wewe pia waweza kusitawisha uhakika kama huo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]
Picha ya Hifadhi za Nyaraka za Kitaifa ya Marekani