Kutoka Kwenye Ghorofa Ndefu za Jiji Hadi Kwenye Nyika ya Tundra Endeeni Watu
WALA mvua wala theluji wala mvua ya mawe wala mbwa-mwitu wala simba wa milimani, wala eneo lenye wakazi wenye uhasama halingeweza kupunguza roho yao ya kuazimia. Kwa kasi yenye kushangaza, walikimbia kwa farasi kuvuka kilometa 3,000 za mbuga iliyo wazi, mito yenye kwenda kasi, na mabonde yenye kina ili kupeleka barua za hima hadi Pwani ya Magharibi. Hao walikuwa nani?
Walikuwa vijana wapanda-farasi jasiri wa mfumo wa kupeleka barua kwa farasi.a Ni nini kilichochochea roho hiyo ya azimio lenye nguvu ya vijana hao? Labda ule ugumu, ile hatari, na ule uradhi wa kufikisha barua. Kwa kupendeza, kila mpanda-farasi alibeba Biblia katika mifuko ya matandiko ya farasi pamoja na ile barua muhimu.
Zaidi ya karne moja baadaye, roho kubwa zaidi ya azimio, shauku, na ujitoaji waonyeshwa na wapiga-mbiu wa Ufalme zaidi ya 113,000 waliojitoa kotekote katika Kanada. Wao huchochewa na nini? Kumpenda Mungu na jirani huwachochea kupeleka kweli ya Ufalme kwa kutumia vichapo na kwa kutumia mdomo. Kweli hiyo yenye kutoa uhai ni ya hima zaidi kuliko barua yoyote iliyopelekwa kwa kutumia mfumo wa kupeleka barua kwa farasi. Ndiyo, ni ule ujumbe wa Ufalme wenye thamani wa Biblia Takatifu, kitabu kilekile kilichopatikana katika mfuko wa tandiko la farasi wa wapeleka-barua waliopanda farasi.—Mithali 2:21, 22; Isaya 2:2-4; 61:2; Mathayo 22:37-39; 24:14.
Kuchochewa na Upendo kwa Yehova na kwa Watu
Mashahidi wa Yehova hupenda kuzungumza na watu juu ya Ufalme. Utawaona wakifanya hivyo katika ghorofa ndefu za jiji, katika jumuiya za mbali sana za tundra, katika vituo vya ndege, barabarani na mahali penginepo pa watu wote, na kwenye simu. Kwa nini wafanye hivyo katika maeneo hayo tofauti-tofauti?
Mitindo-maisha ambayo imeletwa na hali za kiuchumi na za idadi ya watu imefanya iwe vigumu sana kupata watu nyumbani. Katika visa vingi, mume na mke hufanya kazi ili kutunza mahitaji ya kimsingi ya lazima ya familia, mara nyingi wakipuuza mahitaji ya kiroho. Katikati ya misongo na mikazo hiyo, wao wahitaji sana ujumbe wenye tumaini unaochangamsha moyo. Mashahidi wa Yehova huitikia kwa kuterema. Wakitumia busara na fadhili, wao hutokeza fursa za kuwapelekea habari njema watu wa namna zote katika njia yenye kuvutia na yenye kuamsha fikira.—1 Timotheo 2:3, 4.
Katika Lugha Nyingine: Yesu alipowaamuru wafuasi wake ‘waende wakafanye wanafunzi,’ aliruhusu kuwe na uchukuaji wa hatua ya kwanza na kuazimia katika kuwapelekea watu wa lugha zote ujumbe wenye tumaini. (Mathayo 28:19) Kama vile ilivyo katika nchi nyingi, Kanada imekuwa jamii ya kimataifa, na wapiga-mbiu wa Ufalme wamebadilikana ili wafaane na hali kwa kujifunza lugha mpya mbalimbali.
Kwa mfano, wenzi wa ndoa, ambao ni wahudumu wa wakati wote katika Edmonton, Alberta, waliona uhitaji wa kuwafikia watu wa jiji waliozungumza lugha ya Kichina ya Mandarin. Hata hivyo, hao wenzi wa ndoa walihitaji kwanza wajifunze hiyo lugha, kwa hiyo wakawasiliana na mwanafunzi wa chuo kikuu aliyezungumza lugha ya Mandarin. Alikubali kuwafundisha hiyo lugha na wakati uleule kujifunza kweli za Biblia kutoka kwao. Ni hali iliyofaa kama nini! Kwa muda wa miezi 24 wapiga-mbiu hao wawili wa Ufalme wenye kujitoa walifikia hatua ya kufundisha katika lugha ya Mandarin. Wakati huohuo, mwalimu/mwanafunzi wao akafikia hatua ya ubatizo wa Kikristo.
Mambo yaliyoonwa kama hayo yaendelea kuonewa shangwe katika majiji mengine huku wapiga-mbiu wa Ufalme, wenye kuchochewa na upendo, wakijifunza lugha kama Kipoland, Kirusi, Kivietnam.
Barabarani: Kama wale wapeleka-barua kwa farasi wa karne iliyopita ambao walisafiri peke yao, baadhi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika eneo la ndani la British Columbia husafiri peke yao kwa lori. Kiasi kikubwa cha wakati wao hutumiwa katika kazi yao ya kimwili ya kuendesha malori yenye nguvu ya kubebea magogo kupitia vichakani hadi kwenye viwanda vya kupasulia mbao. Hilo huhitaji kuwasiliana daima na madereva wengine kwa redio iitwayo CB (bendi ya raia), wakiwasiliana kuhusu mtiririko wa magari na hatari za barabara.
Kwa ubuni, wapiga-mbiu hao wa Ufalme hutumia redio zao za CB kwa njia ya pekee. Wao huanzisha mazungumzo kwenye CB kwa kuzungumzia habari za wakati huo. Kisha wao hurejezea Biblia kwa ustadi. Katika kisa kimoja dereva mwenzi aliitikia yale isemayo Biblia juu ya tumaini la wafu. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Kifo cha dereva mwenzake katika aksidenti ya barabara kuu kilimsumbua sana. Alikubali kwa shukrani funzo la Biblia na sasa aweza kusikiwa akipiga mbiu juu ya habari njema kwa wafanyakazi wenzake na marafiki. Kuongezea furaha yake, funzo la Biblia lilianzishwa pamoja na mjane wa rafiki yake aliyekufa. Ni thawabu iliyoje kwa kuchukua hatua ya kwanza ya kutoa ujumbe wa kweli wenye kutoa uhai katika njia hiyo isiyo ya kawaida!
Kwa Ndege: Kwa habari ya kutoa ujumbe wa kweli wenye thamani, wapiga-mbiu wa Ufalme wenye bidii huenda palipo na watu, ‘wakiingia vijiji’ kwa ndege ndogo. (Mathayo 10:11, 12) Muda fulani uliopita, vikundi viwili vyenye kusukumwa na bidii ya kutangaza habari njema na vyenye kujigharamia, viliruka kwa ndege hadi vikawafikia watu waliotawanyika wa lile eneo kubwa sana la nyika ya tundra. Kila kikundi kiliruka kwa ndege umbali wa kilometa 3,000 na kutua katika jumuiya 14 tofauti, umbali wa kilometa 250 kutoka Mzingo Aktiki. Wapiga-mbiu hao wasiochoka waliendelea kwa siku saba kamili ili kuwafikia watu waliotengwa na umbali mkubwa.
Je, jitihada hizo zote zilifaa? Ebu fikiria matokeo chanya ambayo ujumbe wa Biblia ulikuwa nayo juu ya jumuiya hizo. Hao wahudumu wenye kuzuru walitosheleza uhitaji muhimu wa kiroho walipoeleza kusudi la Yehova la kuwa na dunia iliyo paradiso hivi karibuni. (Mathayo 5:3) Muda mrefu baada ya waleta-ujumbe kuondoka, hao watu wenye mioyo ya haki wataweza kusoma kutoka katika Biblia na misaada ya kujifunzia Biblia 542 na magazeti 3,000 waliyoangushiwa.—Linganisha Matendo 12:24.
Kwa Simu: Maelfu ya wakaaji wa jijini huishi katika ghorofa ndefu ambazo zina mfumo wa usalama wa hali ya juu. Hata hivyo, wapiga-mbiu wa Ufalme waliojitoa wakfu husonga mbele kwa bidii na busara. Je, wao huwezaje kwenda mahali ambapo watu hao wako? Ingawa kuwasiliana uso kwa uso kwapendelewa zaidi, mara nyingi kifaa cha kuwasiliana kwenye sebule ya hivyo vyumba hutumiwa kwa mafanikio. Wakati ambapo hilo haliwezekani, wao huwapigia watu simu.
Asubuhi moja, mwanamke mwenye umri mkubwa zaidi alijibu simu. Baada ya salamu fupi ya upole, aliulizwa kama alifikiri kungekuwa na wakati ambapo watu wangeweza kutembea barabarani usiku wakiwa salama. Maandiko yalisomwa kumtumainisha kwamba amani ingekuwa nyingi wakati ujao. (Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Alikubali kuwa na mazungumzo ya simu wakati uleule juma lililofuata, ili kuzungumza juu ya kwa nini twaweza kuamini ahadi za Mungu. Baada ya kujifunza Biblia kupitia simu kwa muda wa mwezi mmoja, wakisoma mafungu kutoka katika kifaa cha kujifunzia Biblia na kuuliza maswali yafaayo, mpiga-mbiu huyo wa Ufalme alisifiwa na huyo mwanamke kwa kumhubiria mambo tofauti-tofauti kila juma. Wakati ulikuwa umefika wa kumfafanulia kitabu cha funzo na kumtolea nakala yake binafsi. Mipango ilifanywa wakati huo ili wote wawili wakutane kibinafsi. Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova wameonyesha upendo wao kwa watu, na watu wanaitikia, wakitambua kwamba Yehova yuko pamoja na wahubiri hao Wakristo.—Linganisha 1 Wakorintho 14:25.
Kwa Vichapo: Katika wilaya ya Quebec yenye watu wengi wazungumzao Kifaransa, wapiga-mbiu wa Ufalme pia wanaenda palipo na watu. Mhudumu mmoja asafiriye alisema hivi: “Kwa miaka kadhaa ndugu walihisi kwamba hawakuwa wakifanya maendeleo yoyote kwa sababu ya upinzani mkali wa kanisa. Lakini kupitia kazi ambayo ndugu huifanya bila kuchoka, na kurudia kwao tena na tena, Biblia ambayo ilikuwa kitabu kisichojulikana na wengi, kilichosomwa tu na wachache, sasa yapatikana katika nyumba nyingi.”
Matokeo yenye kusisimua yaonewa shangwe huku waeneza-evanjeli wapya wakija kutoka tabaka zote za jamii ya Quebec, kutia na jumuiya ya kitiba. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa daktari mmoja. Mke wake, ambaye mwenyewe ni mpiga-mbiu wa Ufalme, angezungumza naye mara nyingi juu ya tumaini la Biblia. Mzee wa kutaniko aliyekuwa chonjo alichukua hatua ya kwanza kumwalika huyo daktari kwenye mkutano wa kutaniko wakati ambapo ile broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? ilikuwa ikisomwa. Alikuja na hata kushiriki. Akiwa amevutiwa na ubora na kina cha kiroho cha hayo mazungumzo alikubali kuwa na funzo la Biblia lake mwenyewe binafsi. Sasa yeye ni mpiga-mbiu wa Ufalme.
Kutumia magazeti kwa matokeo, kumetimiza fungu kubwa katika kuvutia watu kwenye Biblia. Mtu huwa hajui kamwe ni makala ipi itakayokuwa kichocheo cha kumvuta mtu kwenye kweli. Mpiga-mbiu mmoja wa Ufalme alimtolea toleo la Amkeni! jirani ambaye hakutaka kusikiliza ujumbe lakini aliyependezwa na ulimwengu wa wadudu. Picha iliyokuwa katika makala ya “Chagas’ Disease—A Kiss of Death” (“Maradhi ya Chagas—Busu la Kifo”) katika Amkeni! la Novemba 22, 1992 (la Kiingereza), ilimpendeza sana. Akivutiwa na yale aliyosoma, aliomba aletewe magazeti zaidi. Funzo la Biblia lilianzishwa, na katika kipindi cha miezi sita, alikuwa akiwatolea wengine ushahidi.
Kwenda Sehemu za Watu Wote: Sheria ya Kanada hutoa uhuru wa kusema katika sehemu za watu wote, kama vile nyanja za ndege. Kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Halifax, wapiga-mbiu wa Ufalme huwafikia kwa busara wasafiri walio kati ya safari za ndege, wakiwashirikisha katika mazungumzo. Maswali yenye kuongoza yafaayo huulizwa ili kuelekeza mazungumzo kwenye Biblia. Kwa kuwa wao hubeba Biblia yenye ukubwa wa kutoshea mfukoni na vichapo, waweza kuitikia mahitaji ya kiroho. Madaktari-wapasuaji, wanasayansi, wanasheria, marubani, makasisi, polisi, dereva wa teksi, wahandisi, walimu, wafanyakazi wa kijeshi, na wanasiasa kutoka nchi za kigeni ni miongoni mwa wale ambao wamesikia ujumbe wa Ufalme katika njia hiyo na wamezipeleka mbegu za kweli na kuzifanya zimee katika sehemu za mbali sana.—Wakolosai 1:6.
Mapema asubuhi moja kwenye uwanja wa ndege, mwanamume fulani alikubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kisha akasema hivi kwa sauti ya chini: “Ah, si Mashahidi wa Yehova!” Kwa nini aliitikia hivyo? Mwanamume huyo alikuwa Mwislamu mchaji aliyekuwa ametoka tu kusali katika kikanisa cha huo uwanja wa ndege. Alikuwa ametoka kumwomba Mungu amwonyeshe hekima, ufahamu wenye kina, na kweli. Wazo la kwamba Mashahidi wa Yehova ndio waliokuwa jibu la papo hapo kwa sala yake, kwa wazi lilimshangaza.
Kwa kweli, wapiga-mbiu wa Ufalme wenye ujasiri katika Kanada hawaruhusu chochote kizuie utoaji wao wa ujumbe wenye thamani wa Ufalme. Hawaruhusu wala lugha za kigeni, barabara za udongo zenye mawemawe, jumuiya zinazoishi mbali sana, wala majengo ya jiji yenye usalama wa hali ya juu, yawazuie. Wameazimia kuupeleka ujumbe wa Mungu wa uhai kwa watafutao kweli walio na mioyo ya haki. Wakiwa pamoja na ndugu zao wa ulimwenguni pote ambao ni wafanyakazi wenzi, wao hutii bila ubinafsi amri ya Yesu ya ‘kwenda kufanya wanafunzi.’—Mathayo 28:19.
[Maelezo ya Chini]
a Mfumo wa kupeleka barua kwa farasi ulikuwa utumishi wa kupeleka barua katika Marekani uliokuwako kwa kipindi kifupi cha miezi 18 kuanzia mwaka wa 1860 hadi wa 1861.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Wapiga-Mbiu wa Ufalme Wenye Mafanikio Watumia Simu
Baadhi yao wamesema hivi: “Halo. Jina langu ni [sema jina]. Nimekuwa nikizungumza kifupi na watu katika jengo lenu juu ya jinsi ambavyo amani yaweza kupatikana. Je, unafikiri kuna wakati wowote ambapo kutaweza kuwa na amani duniani pote? [Ruhusu jibu.] Usiwe na wasiwasi, sifanyi ukaguzi wala siuzi kitu chochote. Badala ya hivyo, nimekuwa nikishiriki wazo kutoka katika Maandiko Matakatifu kwamba, Mungu kwa kweli ataleta amani.” Kisha hayo maongezi yaweza kuendelezwa kuwa mazungumzo mafupi ya Kimaandiko.
Wengine wamesema hivi: “Habari ya jioni. Jina langu ni [sema jina]. Mimi ni mjitoleaji katika eneo letu. Nimekuwa nikipata maoni ya watu mmoja-mmoja wanaoishi katika jengo lenu. Wengi wahangaikia usalama wa kibinafsi kwa sababu ya jeuri na uhalifu wenye kuongezeka sana katika eneo lenu. Je, hilo ni jambo ambalo hukusumbua? [Ruhusu jibu.] Je, unafikiri kwamba kutakuwa na wakati wowote ambapo ulimwengu mzima utahisi ukiwa salama?” Ruhusu jibu, na uendelee na ujumbe wa Kimaandiko.