Kutoa Ushahidi kwa Simu —Njia ya Kufikia Wengi
1 Katika miji na majiji makubwa ya Afrika Mashariki, kuwasiliana kwa simu kumekuwa njia ya maisha. Na kama ilivyoelezwa katika Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1987, kutumia simu katika kuhubiri habari njema ni njia yenye kupendeza na yenye matokeo ya kutoa ushahidi.
2 Mashahidi wengi zaidi wanakuwa stadi katika sehemu hii ya huduma. Kupitia hiyo tunafikia watu ambao hatuwezi kuwakuta katika utumishi wa nyumba kwa nyumba. Kutoa ushahidi kwa simu kunapofanywa kwa hekima, na fadhili, busara, na ustadi, wengine wamepata maitikio yenye kupendeza.
3 Wakati uliopita Sosaiti imetia moyo wale ambao wamefungiwa nyumbani mwao, iwe ni kwa muda au wakati wote kwa sababu ya ugonjwa au kasoro ya kimwili, watumie ifaavyo simu. Wale wanaojipata katika hali kama hiyo wanapaswa kuendeleza kazi hii nzuri. Pia, ripoti zimepokewa kwamba akina ndugu na dada kadhaa, kutia ndani mapainia wa kawaida na wasaidizi, wametumia ushahidi wa simu kuwa kifaa cha huduma yao ya kawaida ya mlango kwa mlango. Hapa pana madokezo machache:
4 Jinsi ya Kutayarisha: Ongea na wengine ambao wanafurahia pendeleo hili la utumishi na upate mashauri. Uwe chanya sikuzote. Mwone Yehova kuwa chanzo cha uwezo na nguvu zako, na utafute mwongozo wake kupitia sala. (Zab. 27:14; Flp. 4:13) Panga kuweka moyo wako wote kwa utendaji huu, kama ilivyo na njia nyingine za kutoa ushahidi.—Linganisha Marko 12:33.
5 Maarifa yamethibisha kwamba kuketi kwenye dawati au meza kwaweza kuwa msaada. Kuketi kwenye kiti kilicho wima hufanya mtu afikiri vizuri na kukaza fikira. Toa vifaa vyote vya kutoa ushahidi ambavyo huenda ukavitumia—trakti, fasihi inayotolewa karibuni, magazeti ya karibuni au nakala za zamani zenye kupendeza, Biblia, kitabu Kutoa Sababu, mwaliko wenye saa hususa za mkutano na mahali pa Jumba la Ufalme, kalamu au penseli, na rekodi ya nyumba kwa nyumba. Uwe na fasihi yako ikiwa tayari, labda hata ikiwa imefunguliwa kwenye makala hususa. Jizoeze utoaji wako kikamili. Kumbuka kwamba kusudi lako la kupiga simu ni kutoa ushahidi na kupanga ziara na mtu huyo upesi iwezekanavyo.
6 Kupiga Simu Kwenyewe: Starehe. Ongea kwa njia yako ya kawaida. Sauti changamfu, yenye kupendeza yahitajiwa kwa ajili ya matokeo mazuri ya ushahidi wa simu. Tabasamu ya uso wako itaonyeshwa kwa namna ya sauti yako. Ongea polepole na waziwazi, ukitumia sauti ya kiasi. Uwe mwenye busara, subira, na mwenye urafiki. Usiogope kukataliwa. Kubali uhakika wa kwamba huenda watu wasipendezwe na ujumbe wako. Ione kuwa sawa na huduma yako ya kawaida ya mlango kwa mlango.
7 Katika utangulizi wako, sema jina lako kamili. Matangulizi mengi katika kitabu Kutoa Sababu yanaweza kusomwa neno kwa neno katika njia ya mazungumzo. Tumia Biblia mapema katika mazungumzo. Kufikia mahali fulani katika mazungumzo, kwa wakati unaofaa taja kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mruhusu mwenye nyumba ashiriki katika mazungumzo. Usisite kusikiliza ikiwa mtu anataka kushiriki anayofikiri. Mshukuru kwa ajili ya maelezo yake na maoni yake. Uwe tayari kumpongeza. Hata hivyo, ikiwa mtu huyo anaanza kuongea zaidi au kutoa hoja, komesha simu kwa njia ya busara. Roho ya Mungu na iongoze jitihada zako na kukusaidia utafute-tafute wale ambao mioyo yao ni minyoofu kumwelekea.
8 Inafaa umalizie mazungumzo kuliko kumwacha mwenye nyumba afanye hivyo. Unaweza kufanya hivyo kwa kumwalika mtu huyo kwa hotuba ya watu wote kwenye Jumba la Ufalme, ukimpatia mahali na saa za mikutano. Unaweza kumuuliza pia ikiwa angependa kutembelewa nyumbani kwake ili uongee naye zaidi juu ya jambo lililozungumzwa. Inawezekana hata kumweleza juu ya fasihi kwa matokeo katika simu. Magazeti yaweza kutolewa na lengo la kuanzisha kazi ya kupelekea watu magazeti kwa ukawaida.
9 Yesu Kristo aliamuru wanafunzi wake wajitahidi kueneza kazi ya kutoa ushahidi “hata mwisho wa nchi.” (Mdo. 1:8) Katika maeneo mengine, kutimiza amri hii kwaweza kufanywa kupitia ushahidi wa simu. Ndugu ambao wamefuata madokezo hayo wametiwa moyo sana na matokeo yayo. Wameona kutoa ushahidi kwa simu kuwa njia ya kipekee ya ‘kuitukuza huduma iliyo yao.’ (Rum. 11:13) Na ufurahie shangwe hiyohiyo kupitia ushahidi wa simu.