Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 5/1 kur. 14-20
  • Wapiga-Mbiu ya Ufalme Walio Watendaji Duniani Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wapiga-Mbiu ya Ufalme Walio Watendaji Duniani Pote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Kutarajia Mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi
  • Kupiga Mbiu kwa Bidii Juu ya Ufalme Uliosimamishwa
  • Kufikia Dunia Nzima Inayokaliwa
  • Kufikia Kila Mtu Kadiri Iwezekanavyo kwa Habari Njema
  • Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kuhubiri Hadharani na Kutoka Nyumba Hadi Nyumba
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 5/1 kur. 14-20

Wapiga-Mbiu ya Ufalme Walio Watendaji Duniani Pote

“Mtakuwa mashahidi wangu . . . hata mwisho wa nchi.”—MATENDO 1:8.

1. Yesu alisema wafuasi wake wangepiga mbiu ya ujumbe gani katika siku zetu?

ALIPOKUWA akieleza juu ya kazi ambayo Yehova alimtuma Mwana wake aifanye duniani, Yesu alisema hivi: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Vilevile, alipokuwa akisema juu ya kazi ambayo wanafunzi wake wangefanya duniani wakati ambapo angerudi akiwa na mamlaka ya kifalme, Yesu alisema hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

2. (a) Kwa nini ni muhimu sana kwamba ujumbe wa Ufalme utangazwe kwa eneo kubwa? (b) Sisi sote twapaswa kujiuliza swali gani?

2 Kwa nini habari juu ya Ufalme wa Mungu ni za maana sana? Kwa nini Ufalme unahitaji kutangazwa sana hivyo? Ni kwa sababu Ufalme wa Kimesiya ndio utakaotetea enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova. (1 Wakorintho 15:24-28) Kupitia huo, Yehova atatekeleza hukumu dhidi ya mfumo wa mambo uliopo wa kishetani na kutimiza ahadi yake ya kubariki familia zote za dunia. (Mwanzo 22:17, 18; Danieli 2:44) Kwa kufanya ushahidi utolewe juu ya Ufalme, Yehova amewapata wale ambao baadaye amewapaka kuwa warithi-washirika na Mwana wake. Kupitia kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme, kazi ya kugawanya inatimizwa leo pia. (Mathayo 25:31-33) Yehova ataka watu wa mataifa yote wajulishwe kuhusu kusudi lake. Yeye awataka wao wawe na fursa ya kuchagua uhai wakiwa raia wa Ufalme wake. (Yohana 3:16; Matendo 13:47) Je! unashiriki kikamili katika kupiga mbiu ya Ufalme huo?

Kwa Kutarajia Mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi

3. (a) Kwa kufaa, C. T. Russell alisema juu ya habari gani katika ziara ya mapema ya kupanga vikundi kwa ajili ya funzo la Biblia? (b) Wanafunzi wa Biblia hao wa mapema waling’amua nini kuhusu umaana wa Ufalme wa Mungu maishani mwao?

3 Huko nyuma katika 1880, Charles Taze Russell, mhariri wa kwanza wa gazeti Mnara wa Mlinzi, alifunga safari kupitia kaskazini-mashariki mwa United States ili kutia moyo kuundwa kwa vikundi kwa ajili ya funzo la Biblia. Kwa kufaa, kichwa alichozungumzia kilikuwa “Mambo Yahusuyo Ufalme wa Mungu.” Kama ilivyoonyeshwa katika matoleo ya mapema ya Mnara wa Mlinzi, Wanafunzi wa Biblia (kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) waling’amua kwamba kama wangestahili kushiriki katika Ufalme wa Mungu, basi ni lazima waweke masilahi ya Ufalme kwanza, wakitumia kwa furaha maisha zao, uwezo wao, na mali zao katika utumishi wa ufalme huo. Kila kitu kingine maishani kilichukua nafasi ya pili. (Mathayo 13:44-46) Daraka lao lilitia ndani kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu kwa wengine. (Isaya 61:1, 2) Walifanya hivyo kwa kadiri gani kabla ya mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi katika 1914?

4. Kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia kiligawanya fasihi za Biblia kwa kadiri gani kabla ya 1914?

4 Kuanzia miaka ya 1870 hadi kufikia 1914, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wachache kwa kulinganisha. Kufikia 1914, ni watu wapatao 5,100 tu waliokuwa wenye bidii katika kushiriki kutoa ushahidi hadharani. Lakini huo ulikuwa ushahidi wenye kutokeza kama nini! Katika 1881, miaka miwili tu baada ya kuchapishwa kwa Mnara wa Mlinzi kwa mara ya kwanza, wao walianza kugawanya kichapo Food for Thinking Christians chenye kurasa 162. Katika muda wa miezi michache, waligawanya nakala 1,200,000. Katika miaka michache, makumi ya mamilioni ya trakti zilikuwa zikigawanywa kila mwaka katika lugha nyingi.

5. Makolpota walikuwa nani, nao walikuwa na roho ya aina gani?

5 Pia kuanzia 1881, wengine walijitolea kuwa waeneza-evanjeli makolpota. Hao walikuwa watangulizi wa mapainia (waeneza-evanjeli wa wakati wote) wa leo. Baadhi ya makolpota, wakisafiri kwa miguu au kwa baiskeli, walitoa ushahidi binafsi katika karibu kila sehemu ya nchi walikoishi. Wengine walifikia mashamba ya kigeni na walikuwa wa kwanza kupeleka habari njema kwenye nchi kama vile Finland, Barbados, na Burma (ambayo sasa ni Myanmari). Wao walionyesha bidii ya kazi ya mishonari kama ile ya Yesu Kristo na mitume wake.—Luka 4:43; Warumi 15:23-25.

6. (a) Safari za Ndugu Russell za kueneza kweli ya Biblia zilienea kadiri gani? (b) Ni jambo jipi jingine lililofanywa ili kuendeleza kuhubiriwa kwa habari njema katika mashamba ya kigeni kabla ya mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi?

6 Ndugu Russell mwenyewe alisafiri mbali ili kueneza kweli. Alienda Kanada mara kwa mara; alihutubu katika Panama, Jamaika, na Kyuba; alifunga safari nyingi za Ulaya; akazunguka dunia katika safari ya kueneza evanjeli. Yeye pia aliwatuma watu wengine waanzishe na kuongoza kazi ya kuhubiri habari njema katika mashamba ya kigeni. Adolf Weber alitumwa Ulaya katika miaka ya katikati ya 1890, na huduma yake ilienea kutoka Uswisi hadi Ufaransa, Italia, Ujerumani, na Ubelgiji. E. J. Coward alitumwa kwenye eneo la Karibea. Robert Hollister alipewa mgawo wa kwenda nchi za Mashariki katika 1912. Huko, trakti za pekee zilitayarishwa katika lugha kumi, na mamilioni ya nakala hizo zilienezwa na wenyeji kotekote India, Uchina, Japani, na Korea. Kama ungaliishi wakati huo, je, moyo wako ungalikusukuma ujitahidi sana kufikia wengine katika jumuiya yako na hata watu wa mbali kwa habari njema?

7. (a) Magazeti ya habari yalitumiwaje kuongeza ushahidi? (b) “Photo-Drama of Creation,” ilikuwa nini, na ni watu wangapi walioiona kwa mwaka mmoja tu?

7 Nyakati za Wasio Wayahudi zilipokaribia mwisho wazo, hotuba za Biblia za Ndugu Russell zilichapishwa katika magazeti ya habari. Hotuba hizo zilikazia hasa kusudi la Mungu na uhakika wa kutimizwa kwalo badala ya kukazia mwaka 1914. Magazeti ya habari yapatayo 2,000 kwa wakati mmoja, yakifikia wasomaji 15,000,000, yalichapisha hotuba hizo kwa ukawaida. Kisha, mwaka 1914 ulipoanza, Sosaiti ilianza kuonyesha umma sinema ya “PhotoDrama of Creation” (Drama-Picha ya Uumbaji). Hiyo ilitoa kweli za Biblia kuanzia uumbaji hadi kufikia Mileani (Miaka Elfu) katika maonyesho manne ya muda wa saa 2. Katika muda wa mwaka mmoja tu, watazamaji zaidi ya milioni tisa katika Amerika Kaskazini, Ulaya, Australia, na New Zealand walikuwa wameiona.

8. Kufikia 1914, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamefikia nchi ngapi kwa habari njema?

8 Kulingana na rekodi zinazopatikana, kufikia sehemu ya mwisho ya 1914, kikundi hicho cha waeneza-evanjeli wenye bidii kilikuwa kimeeneza kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu katika nchi 68.a Lakini huo ulikuwa mwanzo tu!

Kupiga Mbiu kwa Bidii Juu ya Ufalme Uliosimamishwa

9. Kwenye mikusanyiko ya Cedar Point, kazi ya kutoa ushahidi juu ya Ufalme ilichochewaje kwa njia ya kipekee?

9 Wanafunzi wa Biblia walipokusanyika Cedar Point, Ohio, mnamo 1919, J. F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Society, alitangaza hivi: “Kazi yetu ilikuwa na ingali ni kutangaza ufalme wa Mesiya wenye utukufu.” Kwenye mkusanyiko wa pili katika Cedar Point, mnamo 1922, Ndugu Rutherford alikazia kwamba kwenye mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi, katika 1914, ‘Mfalme wa utukufu alikuwa amechukua mamlaka kuu na alikuwa ameanza kutawala.’ Kisha akauliza wasikilizaji wake moja kwa moja hivi, akisema: “Je! mnaamini kwamba Mfalme wa utukufu ameanza kutawala? Basi rudini shambani, Enyi wana wa Mungu aliye juu zaidi! . . . Tangazeni ujumbe kwa mapana na marefu. Ni lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku iliyo kuu kuliko zote. Tazameni, Mfalme atawala! Nyinyi ni watangazaji wake.”

10, 11. Redio, magari ya kutoa sauti, na mabango vilitumiwaje kwa matokeo ili kufikia watu na kweli ya Ufalme?

10 Zaidi ya miaka 70 imepita tangu mikusanyiko hiyo ya Cedar Point ifanywe—karibu miaka 80 tangu Yehova aanze kutawala kupitia utawala wa Kimesiya wa Mwana wake. Mashahidi wa Yehova wametimiza kwa kadiri gani hasa ile kazi waliyopewa katika Neno la Mungu? Wewe binafsi unashiriki kwa kadiri gani katika kazi hiyo?

11 Mapema katika miaka ya 1920, redio ilikuja kuwa chombo ambacho kingeweza kutumiwa kutangaza kwa upana zaidi ujumbe wa Ufalme. Katika miaka ya 1930, hotuba za mkusanyiko zilizozungumzia Ufalme kuwa tumaini la ulimwengu zilitangazwa na stesheni nyingi za redio au kwa sawia na kwa simu zilizozunguka dunia nzima. Magari yenye vikuza-sauti pia yalitumiwa kuchezesha katika sehemu za umma hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Kisha, mnamo 1936, katika Glasgow, Scotland, ndugu zetu walianza kuvaa mabango walipoandamana kupitia sehemu za biashara ili kutangaza hotuba za watu wote. Hizo zote zilikuwa njia zenye mafanikio za kutoa ushahidi kwa watu wengi wakati tulipokuwa wachache.

12. Kama Maandiko yaonyeshavyo, ni ipi mojapo njia zenye matokeo zaidi kwetu sisi mmoja-mmoja kutoa ushahidi?

12 Bila shaka, Maandiko yasema waziwazi kwamba tukiwa Wakristo, sisi mmoja-mmoja tuna daraka la kutoa ushahidi. Hatuwezi tu kuacha makala za magazeti ya habari na matangazo ya redio yafanye kazi hiyo. Maelfu ya Wakristo waaminifu-washikamanifu—wanaume, wanawake, na vijana—wamekubali daraka hilo. Matokeo ni kwamba, kuhubiri nyumba kwa nyumba kumekuwa alama ya kutambulisha Mashahidi wa Yehova.—Matendo 5:42; 20:20.

Kufikia Dunia Nzima Inayokaliwa

13, 14. (a) Kwa nini Mashahidi wengine huhamia miji mingine, hata kuhamia nchi nyingine, ili kuendeleza huduma yao? (b) Hangaiko la upendo kwa watu wa nchi ya nyumbani limesaidiaje kueneza habari njema?

13 Wakijua kwamba ni lazima ujumbe wa Ufalme uhubiriwe katika dunia nzima inayokaliwa, baadhi ya Mashahidi wa Yehova wamefikiria kwa uzito jambo wawezalo kufanya binafsi ili kufikia maeneo yaliyo mbali na jumuiya zao.

14 Watu wengi wamejifunza kweli baada ya kuhamia mbali na nchi zao. Ingawa huenda ikawa wao walihama ili wapate vitu vya kimwili, wamepata jambo jingine lililo la thamani zaidi, na wengine wao wamehisi tamaa ya kurudi nchi zao au jumuiya zao ili kutangaza kweli. Hivyo, mapema katika karne hii, kazi ya kuhubiri habari njema ilipanuka hadi Skandinevia, Ugiriki, Italia, nchi za Ulaya Mashariki, na maeneo mengine mengi. Hata sasa, katika miaka ya 1990, ujumbe wa Ufalme unaenea kwa njia iyo hiyo.

15. Katika miaka ya 1920 na 1930, watu fulani wenye mtazamo kama ule unaoonyeshwa kwenye Isaya 6:8 walitimiza mambo gani?

15 Kwa kutumia shauri la Neno la Mungu maishani mwao, wengine wameweza kujitoa kwa ajili ya utumishi katika nchi ambazo hawakupata kuishi zamani. W. R. Brown (aliyeitwa mara nyingi “Bible Brown”) alikuwa mmoja wao. Katika 1923, alitoka Trinidad kwenda Afrika Magharibi ili kuendeleza kazi ya kueneza evanjeli. Katika miaka ya 1930, Frank na Gray Smith, Robert Nisbet, na David Norman walikuwa miongoni mwa wale waliopeleka ujumbe wa Ufalme kwenye pwani ya mashariki ya Afrika. Wengine walisaidia kukuza shamba la Amerika Kusini. Katika miaka ya mapema ya 1920, George Young, Mkanada, alishiriki kazi hiyo katika Argentina, Brazili, Bolivia, Chile, na Peru. Juan Muñiz, aliyekuwa ametumikia katika Uhispania, aliendelea kuhubiri katika Argentina, Chile, Paraguay, na Uruguay. Hao wote walikuwa na roho kama ile ionyeshwayo kwenye Isaya 6:8: “Mimi hapa, nitume mimi.”

16. Mbali na miji, kazi ya kutoa ushahidi ilikuwa ikifanywa wapi kwingine katika miaka ya kabla ya vita?

16 Kazi ya kuhubiri habari njema ilikuwa ikifikia hata maeneo ya mbali. Mashua zilizoendeshwa na Mashahidi zilikuwa zikizuru bandari zote za Newfoundland, pwani ya Norway hadi Arktiki, visiwa vya Pasifiki, na bandari za Asia ya Kusini-Mashariki.

17. (a) Kufikia 1935, Mashahidi walikuwa wamefikia nchi ngapi? (b) Kwa nini kazi haikuwa imemalizika kufikia wakati huo?

17 Kwa kushangaza, kufikia mwaka 1935, Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye shughuli wakihubiri katika nchi 115, na walikuwa tayari wamefikia nchi nyinginezo 34 ama kupitia safari za kutoa ushahidi ama kwa fasihi zilizopelekwa kwa posta. Hata hivyo, kazi haikuwa imemalizika. Mwaka huo Yehova alifungua macho yao waone kusudi lake la kukusanya “mkutano mkubwa” ambao ungeokoka na kuingia moja kwa moja ndani ya ulimwengu wake mpya. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Kungali kulikuwa na kazi nyingi ya kufanywa ya kutoa ushahidi!

18. Katika kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme, Shule ya Gileadi na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma zimetimiza mafungu gani?

18 Hata wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokumba dunia na kulipokuwa na marufuku kwa fasihi au utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika makumi ya nchi, Watchtower Bible School of Gilead ilifunguliwa ili kuwazoeza wale waliotazamia kuwa wamishonari ili watimize kazi nyingine kubwa zaidi ya kupiga mbiu kwa mataifa mengi. Kufikia sasa, wahitimu wa Gileadi wametumika katika nchi zaidi ya 200. Wao wamefanya kazi zaidi ya kuangusha tu fasihi na kusonga mbele. Wao wameongoza mafunzo ya Biblia, wakapanga makutaniko kitengenezo, na kuwazoeza watu waweze kuchukua madaraka ya kitheokrasi. Hivi karibuni zaidi, wazee na watumishi wa huduma ambao wamehitimu kutoka Shule ya Mazoezi ya Kihuduma pia wamesaidia kujazia mahitaji muhimu kwa habari ya kazi hiyo katika mabara sita. Msingi imara umewekwa kwa ajili ya ukuzi wenye kuendelea.—Linganisha 2 Timotheo 2:2.

19. Watumishi wa Yehova wameitikia kwa kadiri gani ule mwaliko wa kutumikia katika maeneo mengine yenye uhitaji zaidi?

19 Je! wengine wangeweza kusaidia kushughulikia baadhi ya maeneo yasiyofanyiwa kazi? Katika 1957, kwenye mikusanyiko ulimwenguni pote, watu mmoja-mmoja na familia—Mashahidi wa Yehova wakomavu—walitiwa moyo kufikiria kuhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi ili waishi huko na kuendelea na huduma yao. Mwaliko ulikuwa kama ule uliotolewa na Mungu kwa mtume Paulo, aliyeona katika mwono fulani mtu aliyemhimiza hivi: “Vuka, uje Makedonia utusaidie.” (Matendo 16:9, 10) Wengine walihama wakati wa miaka ya 1950, wengine walihama baadaye. Mashahidi wapatao elfu moja walihamia Ailandi na Kolombia; mamia walihamia sehemu nyinginezo. Makumi ya maelfu walihamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi katika nchi yao wenyewe.—Zaburi 110:3.

20. (a) Tangu 1935, nini kimefanywa kwa utimizo wa unabii wa Yesu kwenye Mathayo 24:14? (b) Katika miaka michache iliyopita, kazi imehimizwaje?

20 Kwa baraka ya Yehova kwa watu wake, kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme yaendelea kusonga mbele kwa kasi sana. Tangu 1935 idadi ya wahubiri imeongezeka kwa karibu mara themanini, na kiwango cha ongezeko la mapainia kimeshinda kile cha ongezeko la idadi ya wahubiri kwa asilimia 60. Mpango wa funzo la Biblia nyumbani ulianzishwa katika miaka ya 1930. Sasa kuna wastani wa mafunzo zaidi ya milioni nne na nusu yanayoongozwa kila mwezi. Tangu 1935 na kuendelea muda wa saa bilioni 15 umetumiwa kwa kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme. Habari njema sasa inahubiriwa kwa ukawaida katika nchi 231. Maeneo katika Ulaya Mashariki na Afrika yalipofunguka kwa ajili ya kuhubiri habari njema kwa uhuru zaidi, mikusanyiko ya kimataifa imetumiwa kwa mafanikio ili kutangaza ujumbe wa Ufalme waziwazi kwa umma. Kama vile Yehova alivyoahidi muda mrefu uliopita, kwenye Isaya 60:22, kwa kweli yeye ‘anaihimiza kazi kwa wakati wake.’ Tuna pendeleo tukufu kama nini la kushiriki katika kazi hiyo!

Kufikia Kila Mtu Kadiri Iwezekanavyo kwa Habari Njema

21, 22. Twaweza kufanya nini sisi binafsi ili tuwe Mashahidi wenye matokeo zaidi popote pale tunapotumikia?

21 Bwana hajasema kwamba kazi imeisha. Maelfu mengi ya watu wangali wanajiunga na ibada ya kweli. Kwa hiyo swali lazuka, Je! twafanya yote iwezekanavyo ili tutumie vizuri ule muda ambao subira ya Yehova imeruhusu kwa kazi hii?—2 Petro 3:15.

22 Si kila mtu awezaye kuhamia eneo lisilofanyiwa kazi mara nyingi. Lakini je, unatumia kikamili zile fursa unazopata? Je! wewe hutoa ushahidi kwa wafanyakazi wenzako? kwa walimu na wanafunzi wenzako? Je! umebadilika kupatana na hali zinazobadilika katika eneo lako? Ikiwa kwa sababu za kikazi, watu wachache sana hupatikana nyumbani wakati wa mchana, je, umebadili ratiba yako ili uwatembelee jioni? Ikiwa majengo hayafikiwi na wageni wasiotarajiwa, je, unatoa ushahidi kupitia simu au barua? Je! unafuatia wale wanaoonyesha kupendezwa na kujitolea kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani? Je! unatimiza huduma yako kikamili?—Linganisha Matendo 20:21; 2 Timotheo 4:5.

23. Yehova aonapo kazi tunayofanya katika utumishi wake, ni jambo gani lapasa lionekane wazi kwa habari yetu?

23 Sisi sote na tufanye huduma yetu kwa njia ionyeshayo Yehova kwa wazi kwamba kwa kweli sisi twathamini pendeleo tukufu la kuwa Mashahidi wake katika nyakati hizi zenye umaana sana. Na liwe pendeleo letu kujionea kwa macho Yehova atekelezapo hukumu dhidi ya mfumo wa kale wenye ufisadi na kuleta Utawala mtukufu wa Yesu Kristo wa Mileani!

[Maelezo ya Chini]

a Zikihesabiwa kulingana na jinsi dunia ilivyokuwa imegawanywa katika miaka ya mapema ya 1990.

Kwa Kupitia

◻ Kwa nini ni muhimu sana kuhubiri ujumbe wa Ufalme?

◻ Habari njema zilihubiriwa kwa kadiri gani kufikia 1914?

◻ Ushahidi umetolewa sana kadiri gani tangu kusimamishwa kwa Ufalme?

◻ Ni nini kiwezacho kufanya sehemu yetu ya huduma iwe yenye matokeo zaidi?

[Sanduku katika ukurasa wa 16, 17]

MASHAHIDI WA YEHOVA—Wapiga-Mbiu ya Ufalme wa Mungu

Kwenye mamia ya mikusanyiko iliyofanywa ulimwenguni pote katika kipindi cha 1993 na 1994, kulikuwa na tangazo la kutolewa kwa kitabu kipya chenye kichwa Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom (Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu ya Ufalme wa Mungu). Hiyo ni historia ya Mashahidi wa Yehova ya kuarifu zaidi na yenye habari nyingi zaidi. Hicho ni kitabu chenye kurasa 752, chenye vielezi vinavyovutia sana, na kina picha zaidi ya elfu moja zilizokusanywa kutoka nchi mbalimbali 96. Tayari kilikuwa kimechapishwa katika lugha 25 kufikia mwisho wa 1993 na kinaendelea kutafsiriwa katika lugha nyingine zaidi.

Kwa nini kitabu hiki kimekuja kwa wakati ufaao? Katika miaka ya karibuni, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wamekuwa Mashahidi wa Yehova. Hao wote wapaswa wajue vizuri historia ya tengenezo wanaloshirikiana nalo. Na zaidi, kuhubiri kwao na njia yao ya ibada imevuka mipaka ya vikundi vya kitaifa na vya kijamii ulimwenguni pote na imekubaliwa na wote wachanga kwa wazee, watu wa kila tabaka la kiuchumi na kielimu. Matokeo ni kwamba watu wengi wanaoona mambo yanayoendelea wana maswali juu ya Mashahidi—juu ya chanzo chao, historia yao, tengenezo lao, makusudi yao, na vilevile itikadi zao. Wengine wameandika juu yao, ingawa si kwa kuwaonea nyakati zote. Hata hivyo, hakuna mtu yeyote ajuaye historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi ya Mashahidi wenyewe. Wahariri wa kitabu hicho wamejitahidi kutoa historia hiyo kwa njia ya kweli na unyoofu. Kwa kufanya hivyo, pia wameandika juu ya utimizo wa mpaka sasa wa sehemu muhimu sana wa ishara ya kuwapo kwa Kristo ambayo imerekodiwa kwenye Mathayo 24:14, na wameiandika kwa undani sana hivi kwamba habari hizo zingeweza kutolewa tu na wale ambao wamejihusisha sana katika kazi hiyo iliyotabiriwa.

Kitabu hiki kimegawanywa katika kata kuu saba:

Kata ya 1: Sehemu hii inachunguza vyanzo vya historia ya Mashahidi wa Yehova. Yatia ndani pitio la unyoofu na lenye kuarifu la historia yao ya kisasa kuanzia 1870 hadi 1992.

Kata ya 2: Ina pitio lenye kufunua mambo mengi juu ya maendeleo ya usitawi wa itikadi zinazotofautisha Mashahidi wa Yehova na vikundi vingine vya kidini.

Kata ya 3: Sehemu hii ya kitabu yachunguza usitawi wa muundo wa tengenezo lao. Yataja mambo ya kupendeza juu ya mikutano ya kutaniko na mikusanyiko yao, na vilevile jinsi wanavyojenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko yaliyo makubwa, na vifaa vya kuchapishia fasihi za Biblia. Yaonyesha bidii ambayo Mashahidi wa Yehova hutia katika kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu na upendo unaodhihirika wanaposhughulikiana katika nyakati za matatizo.

Kata ya 4: Utapata hapo mambo mengi yenye kuvutia juu ya jinsi kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu imefikia nchi kubwa-kubwa na visiwa vya mbali duniani kote. Ebu wazia—kuhubiri katika nchi 43 mwaka wa 1914, lakini katika nchi 229 kufikia 1992! Maono ya wale ambao wameshiriki katika upanuzi huo wa duniani kote yanachangamsha moyo sana.

Kata ya 5: Kutimiza kazi hiyo yote ya kupiga mbiu ya Ufalme kumetaka kusitawishwa kwa vifaa vya kimataifa vya kuchapa Biblia kutia na fasihi za Biblia katika lugha zaidi ya mia mbili. Hapo utajifunza juu ya sehemu hiyo ya kazi yao.

Kata ya 6: Mashahidi wamekabili majaribu pia—baadhi yayo yakisababishwa na kutokamilika kwa kibinadamu, mengine kwa sababu ya ndugu bandia, na mengine zaidi kwa sababu ya mnyanyaso wa moja kwa moja. Neno la Mungu lilionya kwamba hali ingekuwa hivyo. (Luka 17:1; 2 Timotheo 3:12; 1 Petro 4:12; 2 Petro 2:1, 2) Kata hiyo ya kitabu yasimulia waziwazi yale ambayo yametukia hasa na jinsi imani ya Mashahidi wa Yehova imewawezesha washinde.

Kata ya 7: Kwa kumalizia, kitabu hicho chazungumzia kwa nini Mashahidi wa Yehova wamesadiki kabisa kwamba kwa kweli tengenezo lao linaongozwa na Mungu. Pia chazungumzia kwa nini wanahisi ni jambo la lazima wafulize kulinda kitengenezo na wakiwa mtu mmoja-mmoja.

Kwa kuongezea mambo yaliyotajwa, buku hilo linalovutia latia ndani pia sehemu yenye kurasa 50 iliyo nzuri na yenye kuarifu sana ya picha za rangi, zikionyesha makao makuu ya ulimwengu na pia ofisi za tawi zinazotumiwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.

Kama hujakisoma bado, utanufaika sana kwa kupata na kusoma nakala ya kichapo hiki chenye kuvutia sana.

Maelezo Kutoka kwa Baadhi ya Watu Ambao Wamekisoma

Wale ambao tayari wamekisoma kitabu hicho wanaitikiaje? Hapa pana wachache:

“Nimetoka tu kumaliza kusoma masimulizi haya yaliyo halisi na yenye kuvutia ya Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom. Ni tengenezo lenye uaminifu-mshikamanifu na lenye unyenyekevu kwa kweli pekee ndilo liwezalo kuandika kweli kwa njia ya waziwazi, moyo mkuu, na kwa njia yenye kugusa hisia sana hivyo.”

“Ni kama kusoma kitabu cha Matendo, kikifuatia haki na unyoofu.”

“Ni kichapo kipya chenye kushangaza kama nini! . . . Ni kitabu bora sana cha kihistoria.”

Baada ya kusoma karibu nusu ya kitabu hiki, mtu mmoja aliandika hivi: “Nilishangaa sana, nikaduwaa, nami nikakaribia kutoa machozi. . . . Kwa miaka yangu yote, hakuna kichapo kingine ambacho kimegusa moyo sana kuliko hicho.”

“Mimi hujawa na furaha sana kila pindi nifikiripo jinsi kitabu hiki kitakavyoimarisha imani ya wachanga na vilevile wapya wanaoingia katika tengenezo leo.”

“Nimethamini kweli nyakati zote, lakini kukisoma kitabu hiki kumenifungua macho na kunisaidia kutambua kuliko wakati mwingine wowote kwamba roho takatifu ya Yehova inategemeza hayo yote.”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Watu wengi walifikiwa na ujumbe wa Ufalme hata Mashahidi walipokuwa wachache

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki