YOELI, KITABU CHA
Kitabu cha Maandiko ya Kiebrania kilichoongozwa na roho takatifu na kilichoandikwa na “Yoeli mwana wa Pethueli.” (Yoe 1:1) Hakuna habari zozote zinazojulikana kuhusu maisha ya nabii huyo. Kwa kuwa anataja Yuda, Yerusalemu, na nyumba ya Yehova iliyokuwa huko, inaweza kusemwa kwamba alifanya kazi yake ya unabii huko Yuda na huenda aliishi Yerusalemu. (1:9, 14; 2:17, 32; 3:1, 2, 16-20) Kwa kuwa anataja “bonde la Yehoshafati” (3:2, 12) hilo likadokeza kwamba aliandika kitabu chake baada ya ushindi mkubwa wa Yehova kwa niaba ya Mfalme Yehoshafati. Lakini wakati hususa haujulikani.
Kilipoandikwa. Wasomi wanasema kwamba huenda kitabu cha Yoeli kiliandikwa kabla ya mwaka wa 800 K.W.K. hadi mwaka wa 400 K.W.K. Kuhusu maoni yanayounga mkono kwamba kitabu hicho kilikamilika mapema au baadaye kati ya miaka iliyotajwa, The International Standard Bible Encyclopædia (kilichohaririwa na James Orr, 1960, Buku la III, uku. 1690) kinasema hivi: “Wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu kitabu hicho, kwa mfano kuhusu mambo ambayo nabii huyo hakutaja au kurejelea [kutia ndani Wakaldayo, Waashuru, mfalme wa Yuda, na ufalme wa makabila kumi], na kutotajwa kwa mambo hayo ni jambo linalozua shaka kubwa.” Vivyo hivyo, haiwezi kusemwa kwa uhakika ikiwa Yoeli aliwanukuu manabii wengine au ikiwa manabii wengine walimnukuu. Mwaka hususa baada ya uhamisho wa kwenda Babiloni ungetajwa ikiwa Yoeli (2:32) angemnukuu Obadia (17). Kwa upande mwingine, si Obadia tu lakini huenda hata Amosi (linganisha Yoe 3:16 na Am 1:2), nabii wa mapema zaidi alimnukuu Yoeli. Hilo lingemaanisha kwamba Yoeli aliandika kitabu chake wakati wa Uzia (Am 1:1), huenda mwaka wa 820 K.W.K. hivi. Ingawa haiwezi kuthibitishwa, mahali ambapo kitabu cha Yoeli kinapatikana katika Maandiko ya Kiebrania yanayokubalika, yaani, katikati ya kitabu cha Hosea na Amosi panaunga mkono kwamba kitabu cha Yoeli kiliandikwa mapema karibu na mwaka uliotajwa hapo juu.
Usahihi Wake. Wayahudi hawakutilia shaka usahihi wa kitabu cha Yoeli lakini walikiorodhesha kikiwa cha pili miongoni mwa manabii “wadogo.” Pia, kinapatana kabisa na Maandiko mengine, kama inavyoonekana kupitia mambo yanayofanana kati ya kitabu cha Yoeli na vitabu vingine vya Biblia. (Linganisha Yoe 2:2 na Sef 1:14, 15; Yoe 2:4, 5, 10 na Ufu 9:2, 7-9; Yoe 2:11 na Mal 4:5; Yoe 2:12 na Yer 4:1; Yoe 2:13 na Kut 34:6, Hes 14:18, Zb 86:15, na 106:45; Yoe 2:31 na Isa 13:9, 10, Mt 24:29, 30, na Ufu 6:12-17.) Kutimia kwa unabii wa Yoeli kunatoa uthibitisho mwingine kwamba kitabu hicho ni sahihi. Kama ilivyokuwa imetabiriwa, Tiro, Ufilisti, na Edomu yalihukumiwa na Yehova. (Yoe 3:4, 19; kwa habari zaidi, ona EDOMU, WAEDOMU; UFILISTI, WAFILISTI; TIRO.) Katika siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alionyesha kwamba ulikuwa utimizo wa unabii wa Yoeli roho takatifu ya Mungu ilipomwagwa juu ya wanafunzi wa Yesu Kristo. (Yoe 2:28-32; Mdo 2:17-21) Baadaye, mtume Paulo alitumia maneno ya kinabii yaliyo kwenye Yoeli 2:32 kuwahusu Wayahudi na watu wasio Wayahudi wanaomwitia Yehova kwa imani.—Ro 10:12, 13.
[Sanduku katika ukurasa wa 86]
MAMBO MAKUU YA KITABU CHA YOELI
Unabii ulio wazi unaokazia kisasi cha Yehova na rehema zake
Huenda kiliandikwa mwaka wa 820 K.W.K. hivi, miaka tisa baada ya Uzia kuwa mfalme na labda miaka mia moja hivi baada ya ushindi mkubwa wa Yehova juu ya Moabu, Amoni, na wakaaji wa Seiri katika siku za Yehoshafati
Nzige wavamia nchi na kula kila kitu; siku ya Yehova iko karibu (1:1–2:11)
Watu watasema kuhusu tauni hiyo inayokuja kwa vizazi vingi
Mimea ya nchi itaharibiwa kabisa hivi kwamba matoleo ya nafaka na ya vinywaji yatasitishwa katika nyumba ya Yehova
Makuhani wanaambiwa waomboleze na kulilia msaada wa Yehova
Siku ya Yehova itakuwa na “jeshi lake” lenye kusababisha uharibifu
Waisraeli wanaalikwa wamrudie Yehova; roho yake itamwagwa juu yao (2:12-32)
Wakazi wa Sayuni wanaalikwa ‘warudi’ kwa Yehova; atawarudishia ufanisi wao na kuwalinda kutokana na “mkaaji wa kaskazini”
Yehova atamwaga roho yake juu ya watu wake, naye atatoa ishara mbinguni na juu ya dunia kabla ya “siku [yake] iliyo kuu na yenye kuogopesha”
Wale wanaoliitia jina la Yehova wataokolewa katika siku yake kuu
Mataifa yatahukumiwa kwenye “Bonde la Yehoshafati” (3:1-21)
Mataifa yatahukumiwa kwa kuwatesa watu wa Mungu
Mataifa yanaambiwa yajitayarishe kwa ajili ya vita dhidi ya Yehova na waje chini kwenye Bonde la Yehoshafati; hapo watakanyagwa kama zabibu ndani ya shinikizo la divai
Wakati huo Yehova atakuwa kimbilio la watu wake
Misri na Edomu yatakuwa nyika, na Yuda litakaliwa na kuzaa kwa wingi; Yehova atakaa Sayuni