SIKU YA BWANA
Kipindi fulani hususa ambacho katika hicho Bwana Yesu Kristo atakamilisha na kutimiza kwa mafanikio kabisa mambo fulani yanayohusiana na kusudi la Mungu.
Katika Biblia, neno “siku” linaweza kurejelea kipindi cha wakati chenye urefu wa zaidi ya saa 24. (Mwa 2:4; Yoh 8:56; 2Pe 3:8) Uthibitisho unaotegemea muktadha unaonyesha kwamba “siku ya Bwana” inayotajwa kwenye Ufunuo 1:10 si ya urefu wa saa 24. Kwa kuwa Yohana alikuja kuwa ‘katika siku ya Bwana kwa mwongozo wa roho,’ basi siku hiyo haiwezi kuwa inarejelea siku fulani hususa ya juma. Haingekuwa lazima Yohana aongozwe na roho ili afike katika siku hususa ya juma. Kwa hiyo, “siku ya Bwana” lazima iwe wakati ujao ambapo matukio ambayo Yohana alipendelewa kuona yangetimia. Matukio hayo yanatia ndani vita vilivyotokea mbinguni na kutupwa kwa Shetani kutoka mbinguni, kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa na wafalme wa dunia na majeshi yao, Shetani kufungwa na kutiwa ndani ya abiso, kufufuliwa kwa wafu, na Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.
Muktadha unaonyesha kwamba Yesu Kristo ndiye Bwana wa “siku” hiyo. Mara tu baada ya kuingia “katika siku ya Bwana,” Yohana alisikia sauti ya Mwana wa Mungu aliyefufuliwa, wala si sauti ya Mungu Mweza-Yote. (Ufu 1:10-18) Pia, “siku ya Bwana” inayotajwa katika 1 Wakorintho 1:8; 5:5; na 2 Wakorintho 1:14 ni siku ya Yesu Kristo.