SALA
Kuzungumza kwa njia ya ibada na Mungu wa kweli, au miungu ya uwongo. Mazungumzo pamoja na Mungu hayamaanishi sala sikuzote, kama inavyoonekana wakati wa hukumu ya Edeni au katika kisa cha Kaini. (Mwa 3:8-13; 4:9-14) Kusali kunahusisha, kumtumaini, kumheshimu, kumtegemea, na kujitoa kabisa kwa yule anayeelekezewa sala. Maneno mbalimbali ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayohusiana na sala yanawasilisha wazo la kuomba, kusihi, kutoa dua, kuomba kibali, kuuliza, na vilevile kusifu, kushukuru, na kubariki.
Bila shaka, sihi na dua zinaweza kutolewa kumwelekea mwanadamu, na nyakati nyingine maneno ya lugha za awali yalitumiwa katika muktadha huo (Mwa 44:18; 50:17; Mdo 25:11), lakini neno “sala,” linapotumiwa kuhusiana na dini, halitumiwi katika maana hiyo. Mtu anaweza “kumsihi” au “kumwomba” mtu mwingine afanye jambo fulani, lakini anapofanya hivyo hatamwona kama Mungu wake. Kwa mfano, hatafanya hivyo kimyakimya au ikiwa mtu anayeombwa hayupo mahali hapo, kama watu wanavyofanya wanapotoa sala kwa Mungu.
“Msikiaji wa Sala.” Biblia nzima inatoa uthibitisho kwamba sala zinapaswa kutolewa kwa Yehova tu (Zb 5:1, 2; Mt 6:9), na kwamba yeye ni “Msikiaji wa sala” (Zb 65:2; 66:19) na ana uwezo wa kutenda kwa niaba ya wale wanaosali kwake. (Mk 11:24; Efe 3:20) Kusali kwa miungu ya uwongo na kutumia sanamu ni upumbavu, kwa kuwa sanamu hazina uwezo wa kusikia au kutenda, na zinawakilisha miungu ambayo haiwezi kamwe kulinganishwa na Mungu wa kweli. (Amu 10:11-16; Zb 115:4, 6; Isa 45:20; 46:1, 2, 6, 7) Jaribio lililofanywa kwenye Mlima Karmeli lililofunua nani aliye Mungu kati ya Baali na Yehova, lilionyesha jinsi ilivyo upumbavu kusali kwa miungu ya uwongo.—1Fa 18:21-39; linganisha Amu 6:28-32.
Ingawa baadhi ya watu wanadai kwamba ni sawa kutoa sala kwa watu wengine, kama vile Mwana wa Mungu, uthibitisho unaonyesha jambo tofauti kabisa na hilo. Ni kweli kwamba kuna visa vichache ambapo watu walizungumza na Yesu Kristo akiwa mbinguni. Stefano alipokuwa karibu kufa, aliomba hivi kwa Yesu: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.” (Mdo 7:59) Hata hivyo, muktadha unaonyesha sababu. Wakati huo Stefano aliona maono ya “Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu,” na kwa sababu alihisi kana kwamba Yesu alikuwa pamoja naye, alijihisi huru kujieleza kwa yule ambaye alitambua kuwa ndiye kichwa cha kutaniko la Kikristo. (Mdo 7:55, 56; Kol 1:18) Vivyo hivyo, mwishoni mwa Ufunuo, mtume Yohana anasema, “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” (Ufu 22:20) Lakini kwa mara nyingine muktadha unaonyesha kwamba katika maono (Ufu 1:10; 4:1, 2), Yohana alikuwa akimsikiliza Yesu akizungumza kuhusu kuja kwake wakati ujao na hivyo Yohana alitamani sana wakati huo ufike hivi kwamba akasema maneno hayo kuhusu kuja kwa Yesu. (Ufu 22:16, 20) Katika visa vyote viwili, kisa cha Stefano na Yohana, hali inatofautiana kidogo na mazungumzo ambayo Yohana alikuwa nayo na kiumbe wa roho mbinguni katika maono haya ya Ufunuo. (Ufu 7:13, 14; linganisha Mdo 22:6-22.) Hakuna jambo linaloonyesha kwamba wanafunzi Wakristo walijieleza kwa Yesu kwa njia hiyo walipokabili hali tofauti-tofauti baada ya yeye kwenda mbinguni. Hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu.”—Flp 4:6.
Makala KUMKARIBIA MUNGU inazungumzia cheo cha Kristo Yesu, akiwa yule ambaye sala zinapaswa kutolewa kupitia kwake. Kupitia damu ya Yesu iliyotolewa kuwa dhabihu kwa Mungu, “tuna ujasiri wa njia ya kuingia katika mahali patakatifu,” yaani, ujasiri wa kuzungumza na Mungu katika sala, tukimkaribia “tukiwa na mioyo minyoofu na imani kamili.” (Ebr 10:19-22) Hivyo, Yesu Kristo pekee ndiye “njia” ya kupatanishwa na Mungu na ya kumfikia Mungu katika sala.—Yoh 14:6; 15:16; 16:23, 24; 1Ko 1:2; Efe 2:18; ona YESU KRISTO (Cheo Chake Muhimu Katika Kusudi la Mungu).
Wale Wanaosikilizwa na Mungu. “Watu wa kila aina” wanaweza kumwendea “Msikiaji wa sala,” Yehova Mungu. (Zb 65:2; Mdo 15:17) Hata Waisraeli walipokuwa ‘mali binafsi’ ya Mungu, yaani, watu waliofanya agano pamoja naye, watu wa mataifa mengine wangeweza kumwendea Yehova katika sala kwa kutambua kwamba Waisraeli walikuwa watu walioteuliwa na Mungu na kwamba hekalu lililokuwa Yerusalemu lilikuwa mahali pake palipochaguliwa kwa ajili ya kutoa dhabihu. (Kum 9:29; 2Nya 6:32, 33; linganisha Isa 19:22.) Baadaye, kupitia kifo cha Kristo, tofauti kati ya Wayahudi na watu wasio Wayahudi iliondolewa kwa umilele wote. (Efe 2:11-16) Akiwa nyumbani mwa Mwitalia aliyeitwa Kornelio, Petro alitambua kwamba “Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Mdo 10:34, 35) Kwa hiyo, jambo linalozingatiwa ni hali ya moyo wa mtu na jambo ambalo moyo wake unamchochea kufanya. (Zb 119:145; Omb 3:41) Wale wanaoshika amri za Mungu na kufanya “mambo yanayopendeza machoni pake” wana uhakika kwamba “masikio” yake yanawasikiliza.—1Yo 3:22; Zb 10:17; Met 15:8; 1Pe 3:12.
Kinyume chake, wale wanaodharau Neno la Mungu na sheria yake, wanaomwaga damu na kutenda mambo mengine maovu, hawasikilizwi na Mungu, sala zao ni “chukizo” kwake. (Met 15:29; 28:9; Isa 1:15; Mik 3:4) Sala za watu wa aina hiyo zinaweza “kuwa dhambi.” (Zb 109:3-7) Kwa sababu ya kutenda kwa kimbelembele na kwa uasi, Mfalme Sauli alipoteza kibali cha Mungu, na “ingawa Sauli alikuwa akimwomba Yehova ushauri, Yehova hakumjibu kamwe, iwe ni katika ndoto au kwa Urimu au kupitia manabii.” (1Sa 28:6) Yesu alisema kwamba watu wanafiki wanaotaka uadilifu wao uonekane na watu, wanaposali “wanapata thawabu yao kikamili”—kutoka kwa wanadamu, bali si kutoka kwa Mungu. (Mt 6:5) Mafarisayo walijionyesha kuwa waadilifu na walitoa sala ndefu, walijisifu kwamba maadili yao yalikuwa ya kiwango cha juu, hata hivyo walikataliwa na Mungu kwa unafiki wao. (Mk 12:40; Lu 18:10-14) Ingawa walimkaribia Mungu kwa midomo yao, mioyo yao ilikuwa mbali sana na Mungu na Neno lake la kweli.—Mt 15:3-9; linganisha Isa 58:1-9.
Ni lazima mtu awe na imani kwa Mungu na kwamba yeye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii” (Ebr 11:6), na amkaribie akiwa na “imani kamili.” (Ebr 10:22, 38, 39) Ni muhimu kwa mtu kutambua kwamba yeye si mkamilifu, na ikiwa ametenda dhambi nzito, ni lazima ‘atafute kibali cha Yehova’ (1Sa 13:12; Da 9:13) kwanza kwa kuufanya moyo wake uwe laini kwa kutubu kutoka moyoni kwa unyoofu na kwa unyenyekevu na aonyeshe kwamba anajutia jambo alilofanya. (2Nya 34:26-28; Zb 51:16, 17; 119:58) Kisha Mungu anaweza kukubali sihi zake, akamsamehe, na kumsikiliza (2Fa 13:4; 2Nya 7:13, 14; 33:10-13; Yak 4:8-10); na hataendelea kuhisi kana kwamba Mungu ‘ameziba kwa wingu njia ya kumkaribia, ili sala yake isipenye.’ (Omb 3:40-44) Ingawa huenda Mungu asikatae kabisa kumsikiliza mtu, sala zake zinaweza ‘kuzuiwa’ ikiwa anakataa kufuata ushauri wa Mungu. (1Pe 3:7) Wale wanaotaka kusamehewa lazima wao pia wawasamehe wengine.—Mt 6:14, 15; Mk 11:25; Lu 11:4.
Ni mambo gani yanayofaa kutajwa katika sala?
Kimsingi sala inahusisha kuungama, (2Nya 30:22), maombi au dua (Ebr 5:7), sifa na shukrani (Zb 34:1; 92:1), na nadhiri (1Sa 1:11; Mhu 5:2-6). Inaonekana kwamba sala ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake ilikuwa ya kielelezo, au mfano wa kuiga, kwa sababu baadaye, sala ambazo Yesu mwenyewe alitoa, na pia zilizotolewa na wanafunzi wake, hazikuwa na maneno hususa yaliyo katika sala ya kielelezo. (Mt 6:9-13) Maneno ya kwanza ya sala hiyo yanakazia mambo ya msingi yaliyo muhimu sana, kutakaswa kwa jina la Yehova, ambalo lilianza kuchafuliwa uasi ulipotokea Edeni, na vilevile kufunuliwa kwa mapenzi ya Mungu kupita Ufalme ulioahidiwa, ambao Masihi, ule uzao ulioahidiwa ndiye atakayekuwa Mfalme wa Ufalme huo. (Mwa 3:15; ona YEHOVA [Enzi Kuu Itatetewa na Jina Kutakaswa].) Ili kutoa sala kama hiyo ni lazima mtu anayesali aunge mkono kikamili upande wa Mungu katika suala linalohusu haki ya Yehova ya kutawala.
Mfano wa Yesu katika Luka 19:11-27 unaonyesha kwamba ‘kuja kwa Ufalme’ kunamaanisha Ufalme huo utakuja kutekeleza hukumu, kuwaangamiza wapinzani wote, na kuleta kitulizo kwa wale wote wanaotumaini. (Linganisha Ufu 16:14-16; 19:11-21.) Maneno “mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni,” kimsingi hayamaanishi wanadamu wafanye mapenzi ya Mungu, badala yake yanamaanisha Mungu achukue hatua ili kutimiza mapenzi yake kuelekea dunia na wanadamu, na hivyo kuonyesha nguvu zake za kutimiza kusudi lake lililofunuliwa. Bila shaka yule anayesali anaonyesha pia kwamba anapenda na atajitiisha kwa mapenzi hayo. (Mt 6:10; linganisha Mt 26:39.) Mtu anapoomba mkate wake wa kila siku, msamaha, ulinzi kutokana na majaribu, na ukombozi kutoka kwa yule mwovu anaonyesha kwamba anatamani kuendelea kuwa na kibali cha Mungu. Anasali hivyo kwa niaba ya wengine wote walio na imani kama yake, si kwa ajili yake peke yake.—Linganisha Kol 4:12.
Mambo hayo yaliyo katika sala ya kielelezo yana umuhimu mkubwa kwa watu wote wenye imani na yanaonyesha uhitaji wao kwa ujumla. Mistari hiyo inaonyesha kwamba kuna mambo mengine yanayoweza kumhangaisha mtu, iwe ni kwa kadiri kubwa au ndogo yanayosababishwa na hali au tukio fulani, na ni mambo yanayofaa pia kutajwa katika sala. Ingawa mambo hayo hayajatajwa kihususa katika sala ya kielelezo ya Yesu, bado yanahusiana na mambo yaliyotajwa katika sala hiyo. Hivyo basi, sala za kibinafsi zinaweza kugusa kila sehemu ya maisha ya mtu.—Yoh 16:23, 24; Flp 4:6; 1Pe 5:7.
Sote tunajitahidi kuongezea ujuzi wetu, uelewaji, na hekima (Zb 119:33, 34; Yak 1:5); hata hivyo huenda wengine wakahitaji mambo hayo kwa njia ya pekee. Huenda wakamwomba Mungu awape mwongozo kuhusu maamuzi ya kihukumu, kama Musa alivyofanya (Kut 18:19, 26; linganisha Hes 9:6-9; 27:1-11; Kum 17:8-13), au wanapomweka mtu rasmi awe na mapendeleo ya pekee miongoni mwa watu wa Mungu. (Hes 27:15-18; Lu 6:12, 13; Mdo 1:24, 25; 6:5, 6) Wanaweza kuomba uwezo na hekima ya kutimiza migawo ya pekee au ili wakabiliane na majaribu au hatari fulani. (Mwa 32:9-12; Lu 3:21; Mt 26:36-44) Sababu zao za kumbariki na kumshukuru Mungu zinaweza kutofautiana kulingana na mambo waliyopitia maishani.—1Ko 7:7; 12:6, 7; 1Th 5:18.
Kwenye 1 Timotheo 2:1, 2, mtume Paulo anataja sala zinazotolewa “kwa ajili ya watu wa namna zote, kutia ndani wafalme na wote wenye vyeo vya juu.” Katika usiku wake wa mwisho hapa duniani, Yesu alisema katika sala kwamba haombi kwa ajili ya ulimwengu, bali kuhusu wale ambao Mungu alikuwa amempa, na kwamba hawakuwa sehemu ya ulimwengu na ulimwengu umewachukia. (Yoh 17:9, 14) Kwa sababu hiyo, inaonekana kwamba kuna mipaka inapohusu sala ya Mkristo kwa ajili ya wakuu wa ulimwengu. Maneno ya mtume Paulo yanaendelea kufunua kwamba sala kama hizo lazima zitolewe kwa ajili ya watu wa Mungu, “ili tuendelee kuishi kwa amani na utulivu na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.” (1Ti 2:2) Mifano ya awali inaonyesha hivyo: Nehemia alisali Mungu amfanye Mfalme Artashasta ‘amhurumie’ (Ne 1:11; linganisha Mwa 43:14), na Yehova aliwaagiza Waisraeli ‘watafute amani kwa ajili ya jiji la Babiloni’ ambamo walipelekwa uhamishoni, na wasali kwa ajili ya jiji hilo, “kwa maana jiji hilo likiwa na amani mtakuwa na amani.” (Yer 29:7) Vivyo hivyo, Wakristo walisali kuhusu vitisho kutoka kwa watawala wa siku zao (Mdo 4:23-30), na hapana shaka kwamba sala zilizotolewa kwa niaba ya Petro aliyekuwa amefungwa gerezani zilihusisha kusali maofisa wenye mamlaka wamwachilie huru. (Mdo 12:5) Walitenda kupatana na ushauri wa Kristo kwa kusali kwa ajili ya wale waliokuwa wakiwatesa.—Mt 5:44; linganisha Mdo 26:28, 29; Ro 10:1-3.
Tangu zamani, watu walimshukuru Mungu kwa ajili ya maandalizi kama vile chakula. (Kum 8:10-18; ona pia Mt 14:19; Mdo 27:35; 1Ko 10:30, 31.) Hata hivyo, tunapaswa kuonyesha kwamba tunathamini wema wa Mungu katika “kila jambo,” si kuhusu baraka za kimwili pekee.—1Th 5:17, 18; Efe 5:19, 20.
Kimsingi, ujuzi alio nao mtu kuhusu mapenzi ya Mungu ndio ambao huamua mambo atakayotaja katika sala zake, kwa sababu lazima atambue kwamba ili sala yake ijibiwe lazima impendeze Mungu. Mtu anayesali anajua kwamba waovu na wale wanaopuuza Neno la Mungu hawana kibali cha Mungu, hivyo hawezi kuomba mambo ambayo ni kinyume na uadilifu na kinyume na mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa, kutia ndani mafundisho ya Mwana wake na ya wanafunzi wake walioongozwa na roho ya Mungu. (Yoh 15:7, 16) Hivyo kuomba “jambo lolote” (Yoh 16:23) hakupaswi kueleweka kwa njia isiyofaa. Ni wazi kwamba “jambo lolote” halihusishi mambo ambayo mtu anajua au ana sababu ya kuamini kwamba hayatampendeza Mungu. Yohana anasema hivi: “Huu ndio uhakika tulio nao kwake, kwamba tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1Yo 5:14; linganisha Yak 4:15.) Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Wawili kati yenu duniani wakikubaliana kuomba jambo lolote muhimu, litatendeka kwa ajili yao kwa sababu ya Baba yangu aliye mbinguni.” (Mt 18:19) Ingawa vitu vya kimwili kama vile chakula ni mambo yanayofaa kutajwa katika sala, tamaa ya vitu vya kimwili na ya mambo makuu haifai kama andiko la Mathayo 6:19-34; na 1 Yohana 2:15-17 linavyoonyesha. Pia, sala zinazotolewa kwa niaba ya watu waliokataliwa na Mungu haziwezi kusikilizwa.—Yer 7:16; 11:14.
Waroma 8:26, 27 inaonyesha kwamba Mkristo akiwa katika hali fulani huenda asijue la kusema katika sala; hata hivyo Mungu anaelewa “kuugua” kwake kusikotamkwa. Mtume huyo anaonyesha hilo linawezekana kupitia roho takatifu ya Mungu, au nguvu yake ya utendaji. Tunapaswa kukumbuka kwamba Maandiko yameongozwa na roho hiyo ya Mungu. (2Ti 3:16, 17; 2Pe 1:21) Maandiko hayo yanatia ndani unabii uliohusisha matukio yaliyofanana na hali ambazo zingewapata watumishi wake katika nyakati za baadaye na yanaonyesha jinsi ambavyo Mungu angewaongoza watumishi wake na kuwapa msaada wanaohitaji. (Ro 15:4; 1Pe 1:6-12) Huenda Mkristo asitambue, mpaka baada ya kupokea, kwamba jambo ambalo huenda aliomba (ingawa labda hakujua jinsi ya kujieleza) tayari lilikuwa limeandikwa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho.—Linganisha 1Ko 2:9, 10.
Majibu ya Sala. Ingawa zamani Mungu aliwasiliana moja kwa moja na watu fulani, halikuwa jambo la kawaida, na mara nyingi alifanya hivyo kupitia wawakilishi wa pekee, kama vile Abrahamu na Musa. (Mwa 15:1-5; Kut 3:11-15; linganisha Kut 20:19.) Hata alipofanya hivyo, maneno yake yaliwasilishwa kupitia malaika, isipokuwa wakati alipozungumza na Mwana wake alipokuwa hapa duniani au alipozungumza kumhusu. (Linganisha Kut 3:2, 4; Gal 3:19.) Kwa ujumla watu walishtuka sana malaika waliojivika mwili wa kibinadamu walipowasilisha kibinafsi ujumbe wa Mungu, kwa kuwa hilo halikuwa jambo la kawaida. (Amu 6:22; Lu 1:11, 12, 26-30) Hivyo, katika visa vingi sala nyingi zilijibiwa kupitia manabii au kwa kupokea kilichoombwa au kukataliwa kwa ombi la mtu. Mara nyingi jibu la Yehova lilionekana wazi, kama wakati alipowakomboa watumishi wake kutoka kwa adui (2Nya 20:1-12, 21-24) au alipoandaa mahitaji yao ya kimwili kulipokuwa na uhaba mkubwa. (Kut 15:22-25) Hata hivyo, majibu ya sala zilizotolewa mara nyingi hayakuonekana waziwazi sana, kwa kuwa yalihusiana na kuimarishwa kiadili na kupata uelewaji, mambo ambayo yangemsaidia mtu kushikamana na uadilifu na kutimiza mgawo wake aliopewa na Mungu. (2Ti 4:17) Majibu ya sala za Mkristo yalihusu mambo ya kiroho, hayakuhusisha mambo yenye kustaajabisha kama yale ambayo Mungu alifanya nyakati za kale, lakini bado yalikuwa muhimu.—Mt 9:36-38; Kol 1:9; Ebr 13:18; Yak 5:13.
Sala zinazokubalika lazima zitolewe kwa anayestahili, Yehova Mungu; lazima zihusu mambo yanayofaa, mambo yanayopatana na makusudi ya Mungu yaliyofunuliwa; lazima zitolewe kwa njia inayofaa, kupitia njia iliyowekwa na Mungu, yaani, Kristo Yesu; na kwa nia inayofaa na moyo safi. (Linganisha Yak 4:3-6.) Pamoja na mambo hayo yote, tunahitaji kuendelea kusali bila kuchoka. Yesu alisema ‘tuendelee kuomba, kutafuta, na kupiga hodi,’ bila kuchoka. (Lu 11:5-10; 18:1-7) Yesu aliuliza ikiwa ‘atakapofika’ wakati ujao, je, atakuta mtu yeyote duniani anayeamini kwamba sala hufanya kazi? (Lu 18:8) Kama Maandiko yanavyoonyesha wazi, inapoonekana kana kwamba Mungu anachelewa kujibu baadhi ya sala si kwa sababu ameshindwa au hataki kufanya hivyo. (Mt 7:9-11; Yak 1:5, 17) Katika visa vingine, lazima jibu lisubiri ‘ratiba’ ya Mungu. (Lu 18:7; 1Pe 5:6; 2Pe 3:9; Ufu 6:9-11) Hata hivyo, kimsingi inaonekana kwamba Mungu huruhusu anayeomba aonyeshe kiwango cha hangaiko lake, anatamani jambo hilo kadiri gani, na unyoofu wa nia yake. (Zb 55:17; 88:1, 13; Ro 1:9-11) Nyakati nyingine lazima watumishi wa Mungu wawe kama Yakobo alipopigana mweleka kwa muda mrefu ili kupata baraka.—Mwa 32:24-26.
Ingawa Yehova Mungu hawezi kushinikizwa na idadi ya watu kuchukua hatua fulani, inaonekana yeye huona hangaiko la watumishi wake wakiwa kikundi, naye anachukua hatua wanapoonyesha kwamba wanahangaishwa sana na jambo fulani na wanapoomba jambo moja wakiwa kikundi chenye umoja. (Linganisha Kut 2:23-25.) Watu wanapokosa kuunga mkono mapenzi ya Mungu, hata iwe ni kwa kadiri ndogo tu, Mungu anaweza kukosa kuchukua hatua. Hekalu la Yerusalemu lilipokuwa likijengwa upya, jambo ambalo kwa muda fulani halikuungwa mkono (Ezr 4:4-7, 23, 24; Hag 1:2-12), ujenzi ulisitishwa na kucheleweshwa, ilhali baadaye Nehemia alipojenga kuta za jiji hilo, kwa sababu ya sala na watu kuunga mkono kazi, ujenzi ulikamilika ndani ya siku 52 tu. (Ne 2:17-20; 4:4-23; 6:15) Akiandikia kutaniko la Korintho, Paulo alisema kwamba Mungu alimkomboa kutoka katika hatari ya kifo, kisha akasema hivi: “Ninyi pia mnaweza kutusaidia kwa kutoa dua kwa ajili yetu, ili wengi watoe shukrani kwa ajili yetu kwa kibali tunachopokea kwa sababu ya majibu ya sala za wengi.” (2Ko 1:8-11; linganisha Flp 1:12-20.) Inakaziwa mara nyingi kwamba sala zinazotolewa kwa niaba ya wengine zina nguvu nyingi, iwe zinatolewa na mtu mmoja au kikundi cha watu. Yakobo alikuwa akizungumza kuhusu “kusali kwa ajili ya mtu na mwenzake” aliposema, “Dua ya mtu mwadilifu ina nguvu nyingi.”—Yak 5:14-20; linganisha Mwa 20:7, 17; 2Th 3:1, 2; Ebr 13:18, 19.
Jambo lingine ni kuhusu ‘kumwomba’ Yehova, Mtawala wa Ulimwengu Wote, mara nyingi kuhusu jambo fulani. Mtu anayesali anaeleza kwa nini anaamini ombi lake linafaa, anaonyesha kwamba nia yake ni nzuri na hana ubinafsi wowote, na anatambua kwamba kuna mambo mengine mazito kuliko mapendezi au mahangaiko yake. Mambo hayo yanaweza kuhusisha kuheshimiwa kwa jina la Mungu mwenyewe au hali nzuri ya watu wake, au hatua ambayo Mungu atachukua itaathirije maoni ya watu wengine. Akiwa Mungu mwenye rehema, tunaweza kumwomba atutekelezee haki na tupokee fadhili zake zisizostahiliwa. (Linganisha Mwa 18:22-33; 19:18-20; Kut 32:11-14; 2Fa 20:1-5; Ezr 8:21-23.) Kristo Yesu pia ‘huwaombea’ wafuasi wake waaminifu.—Ro 8:33, 34.
Kitabu chote cha Zaburi kimejaa sala na nyimbo za kumsifu Mungu, maneno yake yanaonyesha jinsi ambavyo sala zinapaswa kuwa. Baadhi ya sala nyingi zinazojulikana ni sala ya Yakobo (Mwa 32:9-12), Musa (Kum 9:25-29), Ayubu (Ayu 1:21), Hana (1Sa 2:1-10), Daudi (2Sa 7:18-29; 1Nya 29:10-19), Sulemani (1Fa 3:6-9; 8:22-61), Asa (2Nya 14:11), Yehoshafati (2Nya 20:5-12), Eliya (1Fa 18:36, 37), Yona (Yon 2:1-9), Hezekia (2Fa 19:15-19), Yeremia (Yer 20:7-12; kitabu cha Maombolezo), Danieli (Da 9:3-21), Ezra (Ezr 9:6-15) Nehemia (Ne 1:4-11), baadhi ya Walawi (Ne 9:5-38), Habakuki (Hab 3:1-19), Yesu (Yoh 17:1-26; Mk 14:36), na wanafunzi wa Yesu (Mdo 4:24-30).—Ona VIKAO NA ISHARA; UVUMBA (Ufananisho).