Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it kur. 809-811
  • Uadilifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uadilifu
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Kufuatia Uadilifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Pendezwa na Uadilifu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Penda Uadilifu kwa Moyo Wako Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Wanatangazwa Kuwa Waadilifu “Ili Wapate Uzima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it kur. 809-811

UADILIFU

Neno la Kiebrania tseʹdheq na tsedha·qahʹ na pia la Kigiriki di·kai·o·syʹne yana wazo la “uaminifu,” “unyoofu,” na yanaonyesha kiwango au kigezo cha kuamua mambo manyoofu. “Uadilifu” hutumiwa mara nyingi kuhusu hakimu, au hukumu, na hivyo neno hilo linahusiana na mambo ya kisheria (kwa sababu hiyo nyakati nyingine maneno ya lugha ya awali hutafsiriwa kuwa “haki”). (Zb 35:24; 72:2; 96:13; Isa 11:4; Ufu 19:11) Katika Sheria ya Musa, kwenye Walawi 19:36, neno tseʹdheq linatumiwa mara nne kuhusiana na mambo ya kibiashara: “Mnapaswa kutumia mizani sahihi [“ya haki,” AT, KJ, Le], vipimo sahihi, kipimo sahihi cha vitu vikavu, na kipimo sahihi cha vitu vya majimaji.”

Mungu Huweka Kiwango cha Uadilifu. Msomi Mgiriki Kenneth S. Wuest anasema hivi: “Mungu ndiye anayeweka kiwango kinachofaa kuhusu maana ya dikaios [uadilifu], na wakati uleule anadumisha maana hiyo bila kuibadilisha, kwa sababu Yeye habadiliki.” Kisha anamnukuu Cremer aliyesema hivi: “Katika Biblia uadilifu ni hali ya kuwa sawa kulingana na kiwango cha Mungu, na inapimwa kulingana na matendo yanayompendeza Mungu, na zaidi ya yote inategemea uhusiano pamoja na Mungu, na jinsi unavyojiendesha mbele Zake. Sifa hiyo ni, na inajulikana kuwa dikaiosune theou (uadilifu wa Mungu) (Rom. 3:21; 1:17), uadilifu unaotoka kwa Mungu, na ni yenye thamani mbele zake, uadilifu wa Kimungu, ona Efe. 4:24; baada ya kufafanua uadilifu kwa njia hiyo, injili hiyo (Rom. 1:17) ilifika kwenye ulimwengu wa mataifa ambao hupima uadilifu kwa kiwango tofauti.”​—Studies in the Vocabulary of the Greek New Testament, 1946, uku. 37.

Luka anaonyesha maana ya mtu kuwa mwadilifu anaposema hivi kuhusu kuhani Zekaria na mke wake Elisabeti (wazazi wa Yohana Mbatizaji): “Wote wawili walikuwa waadilifu mbele za Mungu na walitembea bila lawama kulingana na amri na sheria zote za Yehova.” (Lu 1:6) Mtu mwadilifu ni yule anayefanya mapenzi ya Mungu na kushika amri zake. Huenda Mungu akawapa watu mbalimbali amri tofauti ikitegemea wakati​—amri ya kujenga safina aliyompa Noa haijawahi kurudiwa tena na amri kuhusu tohara haiwahusu Wakristo. Hata hivyo, viwango vya Mungu mwenyewe, utu wake, na jinsi alivyo, kama anavyodhihirisha kupitia maneno yake na njia zake, ni mambo yasiyobadilika, kwa hiyo yanakuwa kiwango kikamilifu, kilicho imara na thabiti kama “mwamba,” kinachotumiwa kupima mwenendo wa viumbe wake wote.​—Kum 32:4; Ayu 34:10; Zb 92:15; Eze 18:25-31; 33:17-20.

Wema na Uadilifu. Inaonekana kwamba mtume Paulo anatofautisha wema na uadilifu anapozungumza kuhusu kifo cha kidhabihu cha Kristo, anasema hivi: “Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; hata hivyo, labda mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema. Lakini Mungu hupendekeza upendo wake kwetu kwa kuwa tulipokuwa bado watenda dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Ro 5:7, 8) Mtu anaweza kuitwa “mwadilifu” ikiwa anatimiza majukumu anayopaswa kutimiza, ikiwa ni mwenye haki, hana ubaguzi, ni mnyoofu, hana hatia ya kutenda kosa au upotovu wa maadili, na hivyo anajulikana kuwa mtu anayejiendesha kwa utimilifu na unyoofu. Hata hivyo, maneno ya Paulo yanadokeza kwamba mtu “mwema” ni bora zaidi. Mtu “mwema,” bila shaka, ni mwadilifu na anafuata haki; lakini ana sifa nyingine zinazomtofautisha na mtu anayejulikana hasa kwa sababu ya uadilifu wake. Matumizi ya neno hilo la Kigiriki yanaonyesha kwamba mtu aliye tofauti au anayejulikana kuwa mwema ni mtu mwenye fadhili (anayependa kutenda mema au anayewanufaisha wengine) na mkarimu (anayeonyesha wema huo kwa matendo). Hahangaikii tu kufanya yaliyo haki lakini anafanya mengi zaidi, anachochewa kuwajali wengine na anatamani kuwanufaisha na kuwasaidia.​—Linganisha na Mt 12:35; 20:10-15; Lu 6:9, 33, 35, 36; Yoh 7:12; Mdo 14:17; Ro 12:20, 21; 1Th 5:15.

Kwa hiyo, Paulo anaonyesha wazi kwamba, ingawa mtu anayejulikana kuwa “mwadilifu” huenda akaheshimiwa, na hata kusifiwa na watu, hawezi kugusa mioyo yao sana hivi kwamba mtu yeyote awe tayari kufa kwa ajili yake. Hata hivyo, mtu anayejulikana kuwa mwema, ambaye ni mchangamfu, anayewasaidia wengine, anayewajali wengine, mwenye rehema, anayejitahidi kabisa kuwanufaisha, anapendwa na watu; na wema wake unaweza kugusa moyo wa mtu hivi kwamba mtu huyo anaweza kuwa tayari kufa kwa ajili yake.

Zingatia kwamba katika Maandiko, “mema” yanatofautishwa na “maovu” (Mt 5:45; Yoh 5:29; Ro 9:11; 12:9; 16:19; 2Ko 5:10), na, bila shaka na “mabaya” pia (1Pe 3:11; 3Yo 11). Kwa upande mwingine, mtu “mwadilifu,” anatofautishwa na “mtenda-dhambi” (mtu asiye mwadilifu). (Mk 2:17; Lu 15:7) Kama vile tu ambavyo mtu anaweza kuwa mtenda dhambi (kwa sababu ya kukosa kutimiza viwango vya uadilifu) lakini asiwe “mwovu,” vivyo hivyo, mtu anaweza kuwa “mwadilifu” lakini asiwe “mwema,” kulingana na maelezo yaliyotolewa juu.

Yosefu wa Arimathea alijulikana kuwa mtu “mwema na mwadilifu,” maneno hayo, bila shaka, hutumiwa kwa kawaida katika maana isiyo kamili kuwahusu wanadamu ambao hawajakamilika. (Lu 23:50; linganisha na Mt 19:16, 17; Mk 10:17, 18; tazama WEMA [Wema wa Yehova].) Amri za sheria ya Mungu kwa Waisraeli zilikuwa ‘takatifu [zilitoka kwa Mungu] na zenye uadilifu [zilifuata haki kamilifu] na njema [ziliwanufaisha katika kila sehemu ya maisha wale waliozifuata].”​—Ro 7:12; linganisha na Efe 5:9.

Yehova, Yule Aliye Mwadilifu. Maneno ya Kiebrania tseʹdheq na tsedha·qahʹ na neno la Kigiriki di·kai·o·syʹne yanatumiwa mara nyingi kurejelea uadilifu wa njia za Mungu: akiwa Mwenye Enzi Kuu (Ayu 37:23; Zb 71:19; 89:14), anapotoa na kutekeleza hukumu na haki (Zb 9:8; 85:11; Isa 26:9; 2Ko 3:9), anapowaadhibu watu wake (Isa 10:22), anapojitetea mwenyewe katika hukumu (Zb 51:4; Ro 3:4, 5), na anapowatetea watu wake (Mik 7:9).

Yehova mwenyewe anaitwa “makao ya uadilifu.” (Yer 50:7) Kwa hiyo, yeye ndiye Yule Aliye Mwadilifu, na uadilifu wote walio nao viumbe wake unatokana na uhusiano walio nao pamoja naye. Yehova anafuata kabisa kiwango chake mwenyewe cha uadilifu bila kukengeuka. Kwa hiyo, viumbe wake wanaweza kumtumaini kabisa. Imeandikwa hivi kumhusu: “Uadilifu na haki ndio msingi wa kiti chako cha ufalme.”​—Zb 89:14.

Ni mwadilifu anapoonyesha rehema. Uadilifu, haki, utakatifu, na usafi wa Yehova ni mwingi sana hivi kwamba hawezi kuvumilia dhambi. (Zb 5:4; Isa 6:3, 5; Hab 1:13; 1Pe 1:15) Kwa hiyo, hangesamehe dhambi za wanadamu bila kufuata haki​—yaani, bila msingi wa kisheria. Lakini kupitia fadhili zake zisizostahiliwa alifanya mpango wa haki kwa kumtoa Mwana wake awe dhabihu, upatanisho, au kifuniko cha dhambi. Kwa njia hiyo anaweza kwa haki kuwaonyesha rehema watenda dhambi wanaokubali mpango huo. Paulo anasema hivi kuhusu mpango huo: “Lakini sasa uadilifu wa Mungu umefunuliwa bila sheria, . . . ndiyo, uadilifu wa Mungu kupitia imani katika Yesu Kristo . . . Kwa maana wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu, nayo ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa. . . . ili [Mungu] awe mwadilifu hata anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu [mtu mwenye dhambi] aliye na imani katika Yesu.​—Ro 3:21-26; ona KUTANGAZWA KUWA MWADILIFU.

Tafuta Uadilifu wa Mungu. Yesu aliwahimiza hivi wasikilizaji wake: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake [wa Mungu], nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mt 6:33) Mtu anahitaji kuendelea kuutafuta Ufalme; lazima atamani na kuwa mshikamanifu kwa serikali hiyo. Lakini hapaswi kusahau kwamba ni Ufalme wa Mungu; lazima aishi kulingana na mapenzi ya Mungu, afuate viwango vya Mungu vinavyohusu mwenendo unaofaa na usiofaa, na lazima aendelee ‘kugeuzwa kwa kufanya upya akili yake’ ili kila sehemu ya maisha yake ipatane na uadilifu wa Mungu. (Ro 12:2) Lazima ‘avae utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’​—Efe 4:23, 24.

Wayahudi walifikiri kwamba wako salama na kwamba wangeingia katika Ufalme wa Mungu kwa kujiwekea uadilifu wao wenyewe, badala ya kujitiisha kwa uadilifu wa Mungu. (Ro 10:1-3) Kwa sababu hiyo Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kwa maana ninawaambia ikiwa uadilifu wenu hauzidi ule wa waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika Ufalme wa mbinguni.” Watu hao walikuwa wanaonyesha aina fulani ya uadilifu kwa kutii matakwa fulani ya Sheria na mapokeo yao ambayo walijiongezea. Lakini kwa kweli walikuwa wamelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yao, nao walimkataa Kristo, njia ya Mungu ya kufikia uadilifu wa kweli.​—Mt 5:17-20; 15:3-9; Ro 10:4.

Uadilifu hautegemei matendo ya mtu. Kwa hiyo, ni wazi kwamba wanadamu ambao si wakamilifu hawawezi kamwe kufikia uadilifu wa kweli​—hawawezi kufikia uadilifu wa Mungu—​kwa kutegemea kazi za Sheria ya Musa au kwa matendo yao wenyewe ya uadilifu. (Ro 3:10; 9:30-32; Gal 2:21; 3:21; Tit 3:5) Wanadamu ambao Mungu aliwaita ‘waadilifu’ walionyesha imani katika Mungu na hawakutegemea matendo yao wenyewe, badala yake, walionyesha imani kupitia kazi zilizopatana na kiwango cha Mungu cha uadilifu.​—Mwa 15:6; Ro 4:3-9; Yak 2:18-24.

Sheria ilikuwa ya uadilifu. Hilo halimaanishi kwamba Sheria iliyotolewa kupitia Musa haikuwa na kiwango cha Mungu cha uadilifu. Ilikuwa nacho. Mtume Paulo anasema hivi: “Basi Sheria yenyewe ni takatifu, na amri ni takatifu na yenye uadilifu na ni njema.” (Ro 7:12; Kum 4:8) Ilitimiza kusudi la Mungu kwa kufanya makosa yawe wazi na kuwaongoza kwa Kristo Wayahudi waliokuwa na mioyo minyoofu, na vilevile ilikuwa na kivuli cha mambo mema ambayo yangekuja. (Gal 3:19, 24; Ebr 10:1) Lakini haingewawezesha wale walioifuata kuwa na uadilifu wa kweli ulio kamili. Wote walikuwa watenda dhambi; hawangeweza kutii Sheria hiyo kikamili; na kuhani mkuu wao hangeweza kuondoa dhambi zao kupitia dhabihu na utumishi wake. Kwa hiyo, wangeweza kuwa waadilifu kwa kukubali tu uandalizi wa Mungu wa kumtoa Mwana wake. (Ro 8:3, 4; Ebr 7:18-28) Wale waliomkubali Kristo walitangazwa kuwa waadilifu, si kama malipo kwao, bali kama zawadi, kisha Kristo akawa kwao “hekima kutoka kwa Mungu, pia uadilifu na utakaso na kuachiliwa huru kupitia fidia.” Hivyo, uadilifu wa kweli unaweza kupatikana tu kupitia Kristo. Jambo hilo linamkweza Yehova, nalo linamsifu yeye, wala si mwanadamu au kazi zake, kuwa Chanzo cha uadilifu wote, “ili iwe kama ilivyoandikwa: ‘Yule anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.’”​—1Ko 1:30, 31; Ro 5:17.

Faida za Uadilifu. Mungu anawapenda na kuwajali walio waadilifu. Daudi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana lakini sasa nimezeeka, lakini sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate.” (Zb 37:25) Sulemani alisema: “Yehova hatamwacha mwadilifu akae njaa, lakini atawanyima waovu wanachotamani.” (Met 10:3) Mungu ataihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia Yesu Kristo, naye ataumba “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo uadilifu utakaa. (Mdo 17:31; 2Pe 3:13) Waadilifu wameahidiwa kwamba watairithi dunia; waovu wataondolewa kabisa duniani wakiwa “fidia” ya mwadilifu, kwa sababu mwadilifu hawezi kuwa na amani mtu mwovu akiwepo. Na waadilifu watapewa mali ya waovu, kama methali hii inavyosema: “Mali ya mtenda dhambi itawekwa akiba kwa ajili ya mwadilifu.”​—Met 13:22; 21:18.

Mtu anayeendelea kutenda uadilifu anahakikishiwa baraka za Mungu na kibali cha watu wenye mioyo minyoofu sasa na kwa umilele wote, kwa sababu “kumbukumbu ya mwadilifu itabarikiwa [“milele”], lakini jina la mwovu litaoza.”​—Met 10:7; Zb 112:6.

Waheshimu na Kuwatii Waadilifu. Ni jambo la hekima kuwaheshimu wale ambao Yehova anawahesabu kuwa waadilifu na kufuata ushauri na karipio lao, ambalo litawaletea mema wale wanaolikubali. Daudi alikaripiwa na Yehova kupitia watu waadilifu, watumishi wa Mungu na manabii, naye alisema hivi: “Mwadilifu akinipiga, hilo litakuwa tendo la upendo mshikamanifu; akinikaripia, hilo litakuwa kama mafuta kwenye kichwa changu, ambayo kichwa changu hakiwezi kukataa.”​—Zb 141:5.

“Bamba la Kifuani la Uadilifu.” Kwa kuwa Biblia inatuambia hivi: “Ulinde moyo wako kuliko vitu vyote unavyolinda, kwa maana humo ndimo zinamotoka chemchemi za uzima,” Wakristo wanahitaji kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu.” (Met 4:23; Efe 6:14) Ili kuulinda moyo usibadilike na kuwa mbaya, ni lazima mtu afuate uadilifu wa Mungu kwa sababu moyo wa mwanadamu aliyepungukiwa na mwenye dhambi ni wenye hila na ni hatari. (Yer 17:9) Moyo unahitaji kutiwa nidhamu kabisa na kuzoezwa sana. Mkristo atafanya hivyo tu ikiwa atashikamana kabisa na Maandiko, ambayo, mtume Paulo anasema kwamba ‘ni yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ Anapaswa kukubali nidhamu inayotolewa na wanaume waadilifu kupitia Neno la Mungu.​—2Ti 3:16, 17.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki