Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 12/1 kur. 8-12
  • Wanatangazwa Kuwa Waadilifu “Ili Wapate Uzima”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wanatangazwa Kuwa Waadilifu “Ili Wapate Uzima”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mpango Wenye Rehema wa Kuhesabiwa Ustahili
  • “Watakatifu” 144,000
  • Wanahesabiwa Kuwa Waadilifu —Jinsi Gani na kwa Sababu Gani?
  • Wanachukuliwa Walelewe Kuwa Wana wa Kiroho
  • Warithi wa Ukuhani na Ufalme
  • ‘Kutazamia Kufunuliwa kwa Wana wa Mungu’
  • Alitangazwa Kuwa Mwadilifu Akiwa Rafiki ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Pendezwa na Uadilifu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Waroma Wapata Habari Bora Kabisa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kwa Nini Kufuatia Uadilifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 12/1 kur. 8-12

Wanatangazwa Kuwa Waadilifu “Ili Wapate Uzima”

“Kupitia tendo moja la kuhesabiwa haki matokeo . . . ni kutangazwa kwao kuwa waadilifu ili wapate uzima.”​—WARUMI 5:18, Biblia ya New World Translation.

1. Ni akina nani wanaoona njaa na kiu ya uadilifu, na tamaa yao itatimizwaje?

WENYE furaha ni wale wanaoona njaa na kiu ya uadilifu, kwa kuwa watajazwa.” (Mathayo 5:6, NW) Kiu hiyo ya uadilifu itatoshelezwa kwa ukamili si kwa ajili ya wale tu ambao “ufalme wa mbingu ni wao” bali pia kwa ajili ya wale ‘watakaoirithi dunia.’ (Mathayo 5:10; Zaburi 37:29, NW) Jamii zote mbili zinalishiriki tumaini lililoelezwa na mtume Petro alipoandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13, NW) Ndiyo, Yehova Mungu ameahidi serikali mpya ya kimbingu, “ufalme wa mbingu,” na “dunia mpya” yenye uadilifu, au jamii ya kibinadamu katika dunia-paradiso.

2. Kuna uhusiano gani kati ya Yehova, uadilifu, na tumaini letu la kupata Utaratibu Mpya wenye amani?

2 Lakini mbingu mpya zenye uadilifu na dunia mpya yenye uadilifu ifahamike namna gani hasa? Maana yake ni kwamba lazima serikali mpya ya kimbingu na pia wanadamu wenye kuwa duniani wakitawalwa na serikali hiyo wakubali kiwango kilichowekwa na Mungu juu ya mambo yanayofaa na yasiyofaa. Yehova ndiye “kao linalodumu la uadilifu.” (Yeremia 50:7, NW) Uadilifu ndio msingi wenyewe hasa wa enzi kuu yake, au mahali pa kiti chake cha enzi katika ulimwengu wote. (Ayubu 37:23, 24; Zaburi 89:14, NW) Ili kuwe amani katika ulimwengu wote, viumbe wa Yehova wanapaswa kutambua haki yake ya kuweka viwango vya yaliyo ya uadilifu na yaliyo maovu. Tofauti na hivyo, tumaini letu la kupata Utaratibu Mpya wenye uadilifu linategemea kama Yehova ataendelea kufuata viwango vyake.​—Zaburi 145:17.

3. Kwa sababu ya uadilifu kamili wa Yehova, ni maulizo gani yanayoingia akilini?

3 Hivyo ulizo linatokea juu ya jinsi Mungu yule mtakatifu na mwadilifu, Yehova, angeweza kufanya shughuli zake na watenda dhambi wasio waadilifu. (Linganisha Isaya 59:2; Habakuki 1:13.) Huku yeye akiendelea bado kuwa mwaminifu kwa viwango vyake vilivyotukuka vya uadilifu, angewezaje kuchagua kati ya watenda dhambi watu ambao watashiriki katika zile “mbingu mpya” ambazo ni serikali yenye uadilifu, kisha awakubali wawe rafiki zake watu watakaokuwa sehemu ya “dunia mpya” yenye uadilifu? Ili kujibu ulizo hilo, ni lazima tulifahamu fundisho la Kibiblia la kuhesabiwa haki, au kutangazwa kuwa waadilifu.

Mpango Wenye Rehema wa Kuhesabiwa Ustahili

4. Kwa sababu gani wanadamu walioanguka wana madeni makubwa kwa Mungu, na ni kwa sababu gani sisi wenyewe hatuwezi kujiondolea madeni hayo?

4 Katika Maandiko, dhambi zinafananishwa na madeni. (Ona Mathayo 6:12, 14; 18:21-35; Luka 11:4.) Wanadamu wote ni watenda dhambi, na kwa hiyo wana madeni makubwa mbele za Mungu. “Mshahara wa dhambi ni mauti.” (Warumi 6:23) Kwa kuwa walikuwa ‘wameuzwa chini ya dhambi’ na Adamu babu yao wa kale, wazao wake hawakuwa na la kufanya wajiondolee deni hilo lenye kuwalemea sana. (Warumi 7:14) Ni kifo tu cha mwenye deni ambacho kingeweza kulifuta deni hilo, “kwa maana yeye ambaye amekufa ameachiliwa kuwa hana dhambi.” (Warumi 6:7, NW) Hakuna matendo yo yote mema yenye kufanywa katika muda wa maisha ya mtenda dhambi ambayo yangeweza kukirudisha kilichopotezwa na Adamu, wala hata kumpa msimamo wa uadilifu mbele za Mungu.​—Zaburi 49:7, 9; Warumi 3:20.

5. Yehova aliwatoleaje faraja wanadamu wenye dhambi na bado akaheshimu haki yake iliyo kamilifu?

5 Yehova angeweza kuwatoleaje faraja wanadamu walioanguka, bila kuuacha msimamo wake wa kufuata viwango vyake mwenyewe vya uadilifu? Jibu la ulizo hilo linakazia hekima na fadhili zisizostahilika za Yehova. Mtume Paulo anaeleza jambo hilo vizuri sana katika barua aliyowaandikia Warumi. Anaandika hivi: “Ni kama zawadi ya bure kwamba wao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zisizostahilika zake yeye kupitia kule kufunguliwa kwa njia ya ule ukombozi uliolipwa na Kristo Yesu. Mungu alimtokeza awe toleo la kufanya amani kupitia imani katika damu yake. Hiyo ilikuwa ili kuonyesha uadilifu wake mwenyewe, kwa sababu alikuwa akisamehe dhambi zilizotukia kule nyuma wakati Mungu alipokuwa akitumia subira; ili aonyeshe uadilifu wake mwenyewe katika majira haya ya sasa, ili kwamba awe mwadilifu hata wakati anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu aliye na imani katika Yesu.”​—Warumi 3.24-26, NW.

6. (a) Viwango vya Yehova vya haki vilitoshelezwaje kwa dhabihu ya Kristo, na hivyo Yehova ana nia ya kufanya nini? (b) Mungu anaweza kumpaje mtu mwenye imani ustahili wa kuwa mwenye uadilifu?

6 Kupitia fadhili zisizostahilika zake, Yehova aliikubali dhabihu iliyotolewa na Yesu kwa ajili ya wazao wa Adamu. (1 Petro 2:24) Ilikuwa dhabihu yenye ulinganifu au ufanani kwa sababu, akiwa mwanadamu mkamilifu. Yesu alifanya ununuzi wa kurudisha kile kilichopotezwa na mtu mkamilifu Adamu. (Ona Kutoka 21:23; 1 Timotheo 2:6.) Kwa kuwa malipo ya haki yamekwisha kufanywa, Yehova ana nia ya kupenda ‘kupangusa,’ au ‘kufuta,’ dhambi anazoshtakiwa “mtu aliye na imani katika Yesu.” (Isaya 44:22; Matendo 3:19, NW) Mtu huyo akibaki akiwa mwaminifu, Yehova haachi tu ‘kumhesabia makosa yake’ bali pia anampa ustahili wa kuhesabiwa kuwa mwenye uadilifu. (2 Wakorintho 5:19) Kupitia mpango huo wenye rehema wa kuhesabiwa uadilifu, ‘wengi wamefanywa kuwa waadilifu. (Warumi 5:19, NW) Hiyo ni njia moja ya ‘kuhesabiwa haki,’ nalo ni tendo la Mungu ambalo kupitia hilo mtu anahesabiwa kuwa hana hatia. (Matendo 13:38, 39) Ni akina nani ambao wamehesabiwa kuwa wenye haki, au wakatangazwa kuwa waadilifu wakati wa mfumo huu wa mambo?

“Watakatifu” 144,000

7. Ni kwa njia gani Kristo alitangazwa kuwa mwadilifu, na kwa hiyo ni jambo gani lililowezekana?

7 Ni wazi kwamba Kristo mwenyewe hakuhitaji kupewa ustahili wa kuwa mwenye uadilifu, kwa kuwa yeye alikuwa mwadilifu kweli kweli. (1 Petro 3:18) Baada ya kujithibitisha kuwa mwaminifu mpaka kifo akiwa mwanadamu mkamilifu (“Adamu wa mwisho”) na kutoa uhai wake uwe dhabihu hapa duniani, Yesu alifufuliwa na Baba yake, Yehova. Yesu ‘alitangazwa kuwa mwadilifu katika roho,’ yaani, akatangazwa ‘kuwa mwadilifu kabisa kabisa kwa ustahili wake mwenyewe na kufufuliwa akiwa “roho yenye kuhuisha.” (1 Wakorintho 15:45; 1 Timotheo 3:16) Kwa kifo chake cha dhabihu, yeye aliweka msingi ambao Yehova angeweza kuutumia ili awape wanaume na wanawake wenye imani ustahili wa kuhesabiwa kuwa wenye uadilifu.​—Warumi 10:4.

8, 9. (a) Ni nani wa kwanza kufaidika kutokana na ustahili wanaopewa wa kuwa na uadilifu, na kwa sababu gani? (b) Ni nani wanaokuwa “mbingu mpya,” nao watatawala juu ya nini?

8 Kulingana na kufikiri kuzuri, wale ambao Yehova anachagua wawe ndio “mbingu mpya,” au serikali ya Ufalme chini ya Mfalme Kristo Yesu, ndio wa kwanza kufaidika kwa ukamili kutokana na mpango huo wenye rehema katika mfumo huu wa mambo. Kitabu cha Danieli kinaonyesha sherehe katika mbingu ambayo kwayo Kristo, Mwana wa Adamu, anapokea “mamlaka, na utukufu, na ufalme,” ili “watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote [zilizopo duniani], wamtumikie.” Halafu Danieli anaonyesha kwamba “watakatifu wake Aliye juu,” yaani, Yehova, wanapewa pia ‘ufalme na mamlaka.’​—Danieli 7:13, 14, 18, 27; linganisha Ufunuo 5:8-10.

9 Hesabu ya “watakatifu” hao waliochaguliwa watawale pamoja na Mwana-Kondoo Kristo Yesu wakiwa juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu inafunuliwa kuwa 144,000, ambao “wamenunuliwa katika wanadamu.” (Ufunuo 14:1-5) Wao, pamoja na Kristo, ndio wanao kuwa “mbingu mpya” zenye uadilifu za mfumo mpya wa mambo wa Yehova.

Wanahesabiwa Kuwa Waadilifu —Jinsi Gani na kwa Sababu Gani?

10. (a) Ni kitabu kipi cha Biblia chenye maelezo ya wazi zaidi juu ya kuhesabiwa haki, na ni nani walioandikiwa? (b) Ni nani hasa wanaohusika katika fundisho la Biblia la kuhesabiwa haki?

10 Kitabu cha Biblia ambacho bila shaka ndicho chenye maelezo ya wazi zaidi kuhusu jinsi Mungu anavyotangaza wanadamu kuwa waadilifu ni barua ya Paulo kwa Warumi. Jambo la kuangalia ni kwamba aliandika barua hiyo kwa wale “walioitwa kuwa watakatifu.” (Warumi 1:1, 7) Hiyo inaeleza sababu inayofanya fundisho la ‘kuhesabiwa haki,’ au kutangazwa kuwa waadilifu, kama ilivyoelezwa na Paulo, litumiwe kuhusu wale watakatifu 144,000.

11. Kuna uhusiano gani kati ya imani, matendo, na kuhesabiwa haki?

11 Jambo linalokaziwa na sababu zinazotolewa na Paulo katika Warumi ni kwamba wala Myahudi wala mtu wa Mataifa hawezi kupata msimamo wa uadilifu mbele za Mungu kwa kufanya matendo fulani, yawe yanafanywa ili kujipatanisha na Torati ya Musa au kwa kuheshimu tu sheria ya maadili inayofuatwa kulingana na silika. (Warumi 2:14, 15; 3:9, 10, 19, 20) Myahudi na mtu wa Mataifa ni hali moja, kwa maana wanaweza kutangazwa kuwa waadilifu kama tu wana imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo. (Warumi 3:22-24, 29, 30) Lakini, shauri lililo katika sura za mwisho-mwisho za Warumi (12-15) linaonyesha kwamba ni lazima imani hiyo iungwe mkono na matendo ya kimungu, sawa na vile Yakobo pia anavyoeleza. (Yakobo 2:14-17) Matendo hayo yanathibitisha tu kwamba Mkristo aliyehesabiwa kuwa mwenye haki ana imani ambayo ni lazima kwanza awe nayo ili ahesabiwe na Mungu kuwa mwenye haki.

12, 13. (a) Ni kwa sababu gani wale “watakatifu” 144,000 wanahitaji kutangazwa kuwa waadilifu? (b) Wanafanya nini na haki wanazopewa za kupata uzima?

12 Hata hivyo, ni sababu gani ya lazima inayofanya Wakristo “walioitwa kuwa watakatifu” wahitaji kutangazwa kwamba ni waadilifu? Hapa ndipo ile sehemu ya pili ya ‘kuhesabiwa haki’ inapoingia, yaani, tangazo la Mungu kwamba mtu anastahili uzima akiwa mwana Wake mkamilifu wa kibinadamu. Kwa sababu ya sehemu wanayoitiwa waishiriki katika zile “mbingu mpya” zenye uadilifu, ni lazima wale 144,000 wakatae na kujinyima milele tumaini lo lote la kupata uzima wa milele duniani. (Zaburi 37:29; 115:16) Katika maana hiyo wao wanakufa kifo cha dhabihu. ‘Wanajitoa wafe kifo kama cha Kristo.’​—Wafilipi 3:8-11, NW.

13 Sasa, kupatana na kanuni iliyowekwa katika Torati ya Musa, ni lazima dhabihu yo yote inayotolewa kwa Yehova iwe bila kasoro. (Mambo ya Walawi 22:21; Kumbukumbu la Torati 15:21) Wale “watakatifu” 144,000 wanasemwa kuwa ni “waadilifu ambao wamefanywa wakamilifu.”​—Waebrania 12:23, NW.

Wanachukuliwa Walelewe Kuwa Wana wa Kiroho

14, 15. (a) Wale 144,000 wanapatwa na badiliko gani linalohusiana na dhambi? (b) Ni kwa njia gani wao wanafufuliwa kwenye “upya wa uzima”?

14 Wanapokuwa wangali na maisha ya mwili wenye nyama, “waadilifu” hao wanapatwa na kifo cha mfano. Mtume Paulo anaeleza: “Kwa kuwa sisi tulikufa kwa habari ya kutenda dhambi, tutaendeleaje tena kuishi katika hiyo? Au ninyi hamjui kwamba sisi sote tuliobatizwa ndani ya Kristo Yesu tulibatizwa ndani ya kifo chake? Basi sisi tulizikwa pamoja naye kupitia ubatizo wetu ndani ya kifo chake, ili kwamba, sawa na vile Kristo alivyofufuliwa kutoka kwa wafu kupitia utukufu wa Baba, sisi pia tupaswe vivyo hivyo kutembea katika upya wa uzima . . . kwa sababu tunajua kwamba utu wetu wa zamani ulitundikwa mtini pamoja naye, kwamba mwili wetu wenye dhambi upate kufanywa usiotenda, kwamba sisi tusipaswe tena kuendelea kuwa watumwa kwa dhambi. Kwa maana yeye ambaye amekufa ameachiliwa kuwa hana hatia ya dhambi.”​—Warumi 6:2-7, NW.

15 Wakati wa maisha yao ya kibinadamu, wale “watakatifu” 144,000 ambao ni baki dogo tu kati yao lililopo duniani katika huu wakati wa mwisho, ‘wanakufa kwa habari ya kutenda dhambi.’ Baada ya kifo chao cha mfano, hao “walioitwa kuwa watakatifu” wanafufuliwa kwenye “upya wa uzima.” Baada ya kuwatangaza kuwa waadilifu, Yehova anaweza sasa kuwazaa kwa roho yake wawe “watoto” wake wa kiroho. ‘Wanazaliwa mara ya pili’ na kulelewa wawe “wana wa Mungu.” (Yohana 3:3; Warumi 8:9-16)a Wanaingizwa ndani ya agano jipya na kuwa Waisraeli wa kiroho.​—Yeremia 31:31-34; Luka 22:20; Warumi 9:6.

Warithi wa Ukuhani na Ufalme

16. Wale “watakatifu” 144,000 wanakuwa warithi wa nini?

16 Wakiwa wamelelewa wakawa “wana” wa kiroho wa Mungu, wale “watakatifu” 144,000 wanakuwa “warithi” pia. (Wagalatia 4:5-7) Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake waliozaliwa kwa roho hivi: “Basi, ikiwa sisi tu watoto, sisi tu warithi pia: warithi kweli kweli wa Mungu, lakini warithi washirika pamoja na Kristo, tukiteswa pamoja ili tupate kutukuzwa pamoja pia.” (Warumi 8:17, NW) Urithi wa Kristo ni nini? Yehova amemfanya Mfalme-Kuhani “hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.” (Waebrania 6:19, 20; 7:1) Wakiwa ni “warithi washirika” pamoja na Kristo, Wakristo waliozaliwa kwa roho wanapakwa mafuta pia na Yehova ili wawe makuhani wa kiroho. (2 Wakorintho 1:21; 1 Petro 2:9) Zaidi ya hilo, moja ya shabaha zilizofanya Yehova awatangaze kuwa waadilifu, na ambazo wao wanatazamia kuzifikia mwishowe, ni kwamba baadaye ‘watawale wakiwa wafalme katika uzima kupitia mtu yule mmoja, Yesu Kristo.’​—Warumi 5:17, NW.

17. (a) Ingawa wanatangazwa kuwa waadilifu, Wakristo waliopakwa mafuta wanahitaji kufanya nini kila siku? (b) Wanapokeaje thawabu yao?

17 Ingawa Wakristo hao wapakwa mafuta wanakuwa wametangazwa kuwa waadilifu wanapokuwa wangali duniani, bado wanalazimika kupigana na maelekeo yao yenye dhambi. (Warumi 7:15-20) Wanahitaji damu ya Kristo ili iwasafishe dhambi zao za kila siku za kutokukamilika. (1 Yohana 1:7; 2:1, 2) Wanapobaki wakiwa waaminifu mpaka mwisho wa maisha zao za kidunia, wanakufa kwa uhalisi kisha wanafufuliwa kwenye “urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka” wakiwa sehemu ya “mbingu mpya” zenye uadilifu,—1 Petro 1:3, 4; 2 Petro 3:13, NW.

‘Kutazamia Kufunuliwa kwa Wana wa Mungu’

18, 19. (a) “Viumbe” wa kibinadamu wanangojea nini? (b) “Wana wa Mungu” ‘watafunuliwaje,’ na ni kwa sababu gani “viumbe” wa kibinadamu wanaishi wakilitazamia jambo hilo kwa shauku?

18 Yote hayo yana matokeo gani juu ya watu walio wengi sana kuliko wale “wana wa Mungu” wa kiroho, wanaoona njaa na kiu ya uadilifu lakini walio na tumaini la kuimiliki dunia? Juu ya hao, mtume Paulo anaandika hivi: “Kwa maana viumbe vyote pia vinatazamia kwa shauku nyingi kufunuliwa kwa wana wa Mungu. Kwa maana viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili . . . katika tumaini; kwa kuwa viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”​—Warumi 8:19-21.

19 “Viumbe” hivyo vya kibinadamu ambavyo tumaini lavyo ni kuishi milele katika dunia-paradiso vinaishi ‘vikiutazamia kwa shauku’ muda ambao sasa umekaribia, wakati Mfalme Yesu Kristo na “wana wa Mungu” waliofufuliwa ‘watakapofunuliwa’ wanapouharibu mfumo wa mambo wa sasa ulio mbovu na baada ya hapo watawale wakiwa wafalme na makuhani kwa “miaka elfu.” (Ufunuo 20:4, 6) Wakati wa Utawala wa Mileani ya Kristo, ‘viumbe vyenywe vya kibinadamu vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu.’

20. Ni mambo gani yatakayozungumzwa katika makala inayofuata?

20 Katika makala inayofuata itazungumzwa jinsi hasa wanadamu wenye kuishi katika “dunia mpya” yenye uadilifu watakavyoupata mwishowe ule “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu,” na jinsi fundisho la Biblia juu ya kuhesabiwa haki linavyowahusu hata sasa.

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate mazungumzo ya kindani juu ya ‘kuzaliwa mara ya pili,’ tafadhali ona Mnara wa Mlinzi wa Februari 1, 1982, kurasa 3-14.

Kwa habari ya wanadamu kutangazwa na Mungu kuwa waadilifu​—

◻ Biblia ina maana gani inapotaja mbingu zenye uadilifu na dunia mpya yenye uadilifu?

◻ Ni kwa sababu gani wanadamu wanahitaji kufanywa waonekane wanafaa machoni pa Yehova?

◻ Viwango vya Yehova vya uadilifu vilitoshelezwaje?

◻ Ni kwa sababu gani wale 144,000 ndio wa kwanza kutangazwa kuwa waadilifu, nao wanafanya nini na haki wanazopewa za kupata uzima?

◻ Wale 144,000 wanakuwa warithi wa nini pamoja na Kristo?

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Kuna sehemu mbili za kuhesabiwa haki, au kutangazwa kuwa mwenye uadilifu:

(1) Mtu kuhesabiwa na Mungu kuwa hana hatia

(2) Mungu kumtangaza mtu kuwa ni mkamilifu na anastahili kupata uzima wa milele duniani

Wale Wakristo waliopakwa mafuta 144,000 wanatangazwa kuwa waadilifu katika sehemu zote mbili. Wanazitoa dhabihu haki zao za kuwa na uhai wa kibinadamu kisha wanazaliwa wakiwa “wana” wa kiroho walioitwa kuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo katika “mbingu mpya”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki