Kwa Nini Kufuatia Uadilifu?
KATIKA ulimwengu wenyue jeuri kabla ya Gharika, mwanamume mmoja alitokeza akiwa tofauti. Mwanamume huyo alikuwa Noa. Yeye na familia yake alitembea pamoja na Mungu huku wale wengine wa ainabinadamu wakimpuuza Yeye. Tokeo ni kwamba, “Noa alikuwa mwanamume mwadilifu” katika nyakati hizo zenye uovu, na kwa walimwengu wasiotii akawa “mhubiri wa uadilifu.”—Mwanzo 6:9; 2 Petro 2:5, NW.
Wakati fulani karibu na mwaka 56 wa Wakati wa Kawaida wetu, mtume Paulo alikuwa gerezani katika Kaisaria. Alipoagizwa atoke kwenye gereza lake akawepo mbele ya Gavana Feliki, Paulo alibamba fursa hiyo kumhubiri ofisa huyu Mroma wa cheo cha juu. Wazo kuu la maneno yake lilikuwa nini? “Aliongea juu ya uadilifu na kujidhibiti na hukumu ijayo.” (Matendo 24:25, NW) Ndiyo, Paulo pia alikuwa mhubiri wa uadilifu.
Kwa uhakika hangaiko ambalo watumishi hawa waaminifu wa Mungu walionyesha kwa uadilifu lilifaa. Yehova ni “Mungu mwenye haki [mwadilifu, NW], mwokozi.” (Isaya 45:21) Kwa sababu hiyo, mithali iliyovuviwa yatuambia hivi: “Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA [Yehova, NW]; bali humpenda mtu afuatiaye wema [uadilifu, NW].” (Mithali 15:9) Ni lazima watumishi wote wa Mungu wafuatie uadilifu.
Lisilofurahisha ni kwamba, wengi leo wana mtazamo wa kuichukua sifa hii kikawaida tu. Wao husema: ‘Mimi sidhuru jirani yangu, hivyo basi nina uhakika Mungu afurahishwa nami.’ Au huenda wakashikilia hivi: ‘Kuna vijia vingi vya kwenda kwenye uadilifu. Kila kitu kitakuwa sawa maadamu mimi nafuata dini yangu kwa moyo mweupe.’ Je! wewe wafikiri mtazamo huo wa kujistarehesha wakubalika kwa Mungu?
Huenda wengine wakatokeza suala tofauti. Huenda ikawa wana habari juu ya taarifa ya Paulo: ‘Tumekwisha kuhesabiwa haki [uadilifu, NW] itokayo katika imani.’ (Warumi 5:1, NW) Kwa sababu hiyo, huenda wakashangaa hivi: ‘Wakristo, ambao tayari wamejulishwa rasmi kuwa waadilifu, wapaswa kuendeleaje kufuatia uadilifu?’ Wewe ungejibuje swali la jinsi hiyo?
Mungu wa Uadilifu
Kulingana na kamusi, uadilifu ni unyoofu wa kiadili, haki, upatano na sheria ya kimungu au ya kiadili. Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa uadilifu, wowote watakao kumfurahisha ni lazima wahangaikie sifa hii muhimu. “BWANA [Yehova, NW] ndiye mwenye haki [uadilifu, NW],” akasema mtunga zaburi. “Apenda matendo ya haki [uadilifu, NW], wanyofu wa moyo watamwona uso wake.” (Zaburi 11:7; Kumbukumbu 32:4) Mtume Petro alisema hivi: “Macho ya Bwana [Yehova, NW] huwaelekea wenye haki [waadilifu, NW], na masikio yake husikiliza maombi yao.”—1 Petro 3:12.
Kwa sababu hiyo, hatuwezi kuchukua hali kikawaida katika jambo hili, kama wengi wa Wayahudi walivyofanya. Wengi wao bila shaka walikuwa watu wastahifu ambao hawakudhuru jirani zao. Walikuwa na moyo mweupe pia—hata wenye bidii—juu ya dini yao. Lakini katika karne ya kwanza, walio wengi hawakuwa waadilifu machoni pa Mungu. Paulo alisema hivi: “Nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. Kwa maana, wakiwa hawaijui haki [uadilifu, NW] ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki [uadilifu, NW] yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki [uadilifu, NW] ya Mungu.”—Warumi 10:2, 3.
Wayahudi walikosea wapi? Paulo asema hawakufuatia uadilifu kulingana na maarifa sahihi. Kielelezo chao cha kuonya chatuambia kwamba haitoshi kuwa na utu wa kupendeza tu na kuepuka kufanya madhara. Pia chaonyesha kwamba hakuna vijia vingi tofauti vya kwenda kwenye uadilifu. Kwa wazi, kulikuwa na kasoro fulani kuhusu kijia kilichochaguliwa na Wayahudi walio wengi katika siku ya mitume. Sisi twaweza kufuatia uadilifu ikiwa tu twamsikiliza Mungu. Kitabu cha Mithali chasema hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; ndipo utakapofahamu haki [uadilifu, NW] na hukumu, na adili, na kila njia njema.”—Mithali 2:1, 9.
Njia ya Uadilifu
Kuanzia Musa kuteremka hadi Yesu, uadilifu ulihusianishwa na kutii amri za Mungu kama zilivyotaarifiwa katika Sheria ya Kimusa. Kwa kuwa Waisraeli wasiokamilika hawakuweza kuendelea kutozikiuka amri hizi, walilazimika kutoa dhabihu na matoleo ya dhambi yaliyoagizwa na Sheria ili wafunike hatia yao. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Itakuwa haki [uadilifu, NW] kwetu, tukitunza kufanya maagizo haya yote mbele ya BWANA [Yehova, NW], Mungu wetu, kama alivyotuagiza.”—Kumbukumbu 6:25.
Kwa karne nyingi hakuna mtu aliyeitimiza Sheria kikamilifu. Hata hivyo, wengi walijaribu kuitumia ili wafuatie uadilifu, na Biblia huwasema baadhi yao kuwa waadilifu. Kwa kielelezo, wazazi wa Yohana Mbatizaji huele-zwa kuwa “wenye haki [waadilifu, NW] mbele za Mungu, wakiendelea katika amri zote za Bwana [Yehova, NW] na maagizo yake bila lawama.”—Luka 1:6.
Hata hivyo, Yesu alifungua njia mpya ya kufuatia uadilifu. Yeye aliishika Sheria ya Kimusa kikamilifu—mtu aliye wa pekee kufanya hivyo wakati wowote. Yesu alikufa juu ya mti wa mateso, naye Yehova akaikubali thamani ya uhai wake mkamilifu akiwa ukombozi kwa ajili ya ainabinadamu. Kuanzia hapo na kuendelea, dhabihu chini ya agano la Sheria hazikuhitajiwa tena. Dhabihu kamilifu ya Yesu ilifunika dhambi za wanadamu wote wenye moyo wa kufanya yafaayo.—Waebrania 10:4, 12.
Wakristo wa Kweli Wajulishwa Rasmi Kuwa Waadilifu
Basi, tangu kufa na kufufuliwa kwa Yesu uadilifu umehusianishwa na kujizoeza imani katika huyu Mwana mwadilifu wa Mungu. (Yohana 3:16) Ingawa Wayahudi wafuata-desturi wa siku ya Paulo hawakufikia kuwa na uadilifu kwa sababu walikataa maarifa sahihi juu ya Yesu, twasoma hivi juu ya Wakristo waaminifu: “Wanahesabiwa haki [uadilifu, NW] bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu.”—Warumi 3:24.
Katika muktadha, maneno haya yatumika moja kwa moja kwa Wakristo wapakwa mafuta, ambao kwa sababu ya imani yao katika dhabihu ya Yesu, wajulishwa rasmi kuwa waadilifu kwa tazamio la kuwa warithi-wenzi pamoja na Kristo katika Ufalme wa kimbingu. Hata hivyo, leo kama ilivyotangulia kuonwa na mtume Yohana, umati mkubwa wa Wakristo wenye tumaini la kidunia wametokea kwenye tamasha. Hawa pia wajizoeza imani katika ukombozi. Wao ‘wafua mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo’ na hivyo basi wajulishwa rasmi kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu kwa tazamio la kuokoka ile dhiki kubwa.—Ufunuo 7:9, 14; linganisha Yakobo 2:21-26.
Endelea Kufuatia Uadilifu
Ingawa hivyo, angalia kwamba kufuatia uadilifu hakumaliziki na kutia kwetu imani katika Yesu. Timotheo alikuwa amekuwa ni Mkristo mpakwa mafuta aliyejiweka wakfu kwa miaka mingi wakati Paulo alipomwandikia maneno yanayofuata: “Ukafuata haki [uadilifu, NW], utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani.” (1 Timotheo 6:11, 12; 2 Timotheo 2:22) Kwa nini ilikuwa lazima Timotheo ‘afuate uadilifu’ ikiwa tayari Mungu alikuwa amemjulisha rasmi kuwa mwadilifu?
Kwa sababu neno “-adilifu” latumiwa katika Biblia katika maana ya ujumla zaidi pia kurejezea mtu aishiye maisha ya kiadili yaliyo ya ufuataji haki na kufanya yote awezayo kutii amri za Mungu. Hiyo ndiyo maana ambayo katika hiyo wazazi wa Yohana Mbatizaji walikuwa waadilifu. (Luka 1:6) Baba mlezi wa Yesu, Yusufu, na Yusufu wa Arimathaya walikuwa waadilifu pia kwa njia hii. (Mathayo 1:19; Luka 23:50) Uhakika wa kwamba Wakristo wamejulishwa rasmi kuwa waadilifu hauondoi daraka lao la kufuatia uadilifu katika maana hii. Kwa kweli, Mkristo yeyote aachaye kuishi maisha ya kiadili yaliyo ya ufuataji haki au kushindwa kutii amri za Mungu atapoteza msimamo wake wa uadilifu mbele za Yehova.
Kufuatia Uadilifu—Wito wa Ushindani
Kufuatia uadilifu ni wito wa ushindani. Kwa nini? Kwa sababu sisi sote ni wasiokamilika na tuna elekeo imara kuelekea ukosefu wa uadilifu. (Mwanzo 8:21; Warumi 7:21-23) Zaidi ya hilo, tunaishi katika ulimwengu ambao hutia moyo kuwa na mawazo na vitendo vya kukosa uadilifu na ulio chini ya udhibiti wa Shetani Ibilisi, “yule mwovu.” (1 Yohana 5:19; 2 Wakorintho 4:4) Si ajabu kwamba wakati wa kuandikia Timotheo, Paulo alihusianisha kufuatia uadilifu na ‘kupiga vita vile vizuri vya imani’!—1 Timotheo 6:11, 12.
Je! twaweza kufanikiwa katika hivi “vita vizuri”? Ndiyo, lakini ikiwa tu twasitawisha upendo wenye kuhisiwa moyoni kwa viwango vya Yehova na kuchukia lililo baya. Biblia yasema hivi juu ya Yesu: “Umependa haki [uadilifu, NW], umechukia maasi.” (Waebrania 1:9) Sisi twapaswa kuwa na mtazamo uo huo: tamaa nyingi sana ya kusitawisha upendo kwa mambo yampendezayo Mungu na uchukizo mwingi kwa jambo lolote lisilompendeza.
Wakati ule ule, twapaswa kukumbuka kwamba kufuatia uadilifu si mashindano. Tukijiona kuwa bora kuliko watu fulani wengine, au tukiwa na majivuno juu ya uadilifu wetu wenyewe, basi sisi ni kama Mafarisayo Wayahudi. (Mathayo 6:1-4) Wale wafuatiao uadilifu kwa mafanikio hujichukua kwa unyenyekevu kikweli, ‘wakihesabu wenzao kuwa bora kuliko nafsi zao.’—Wafilipi 2:3.
Paulo alikazia umaana wa funzo la Biblia katika kufuatia uadilifu alipoandika hivi: “Kila Andiko limevuviwa na Mungu na lina manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16, NW) Tukijifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ambako Biblia huzungumzwa, tutazoezwa katika uadilifu. Biblia yaweza kutufinyanga hivi kwamba twavaa ‘utu mpya ambao huumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’—Waefeso 4:24, NW.
Uadilifu uwapo sehemu yenye kushikamana kikamili na sisi, tutachukia maasi kikweli. Hatutashawishwa kutafuta washirika wabaya wa ulimwengu huu. (1 Wakorintho 15:33) Hatutavutwa kuyapenda mambo ya ulimwengu huu wala kujipatanisha na viwango vya ulimwengu huu vyenye kuthamini vitu vya kimwili. (Mithali 16:8; 1 Timotheo 6:9, 10; 1 Yohana 2:15-17) Kwa uhakika, hatutavutiwa na vitumbuizo visivyo na adili na vyenye jeuri vilivyopo mahali pengi sana leo.—Waefeso 5:3, 4.
Baraka za Uadilifu
Ndiyo, kufuatia uadilifu kwa njia ya Yehova ni wito wa ushindani, lakini yastahili kufanya jitihada hiyo. Kwa nini? Kwa sababu yatuongoza kuonea shangwe uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova mwenyewe. Lo, pendeleo la kusifika kama nini! Biblia yatuambia hivi: “[Yehova, NW] huibariki maskani ya mwenye haki [uadilifu, NW].” “BWANA [Yehova, NW] yu mbali na wasio haki [wasio waadilifu, NW]; bali huisikia sala ya mwenye haki [mwadilifu, NW].” (Mithali 3:33; 15:29) Kwa kuongezea, sisi twaja kuwa na uelewevu mwingi wa makusudi ya Yehova. “Njia ya wenye haki [waadilifu, NW] ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—Mithali 4:18.
Biblia huahidi ulinzi kwa wenye kutafuta uadilifu wakati ambapo mfumo huu wa mambo usio mwadilifu utakapofikia mwisho. “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki [uadilifu, NW], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].” (Sefania 2:3) Baada ya hapo, kwa wale walio na tumaini la kidunia, Biblia yatoa tarajio zuri kweli kweli: “Waadilifu wenyewe watamiliki dunia, nao watakaa milele juu yayo.”—Zaburi 37:29, NW.
Ni sababu nzuri kama nini za kufuatia uadilifu! Kama vile Mungu mwenyewe asemavyo: “Aandamaye haki [uadilifu, NW] na fadhili, ataona uhai na haki [uadilifu, NW], na heshima.”—Mithali 21:21.
Kwa kuwa Wakristo wajulishwa rasmi kuwa waadilifu, kwa nini ni lazima waendelee ‘kufuatia uadilifu’?