Alitangazwa Kuwa Mwadilifu Akiwa Rafiki ya Mungu
“‘Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa uadilifu,’ naye akaja kuitwa ‘rafiki ya Yehova.’”—YAKOBO 2:23, Biblia ya New World Translation.
1, 2. “Vitu vilivyo katika mbingu” na “vitu vilivyo duniani” vinapatanishwaje kwa Mungu?
“MUNGU aliona vema ujazi wote ukae katika yeye [Kristo], na kupitia kwake apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu ambayo alimwaga juu ya mti wa mateso, si kitu kama ndivyo vitu vilivyo duniani ama vitu vilivyo katika mbingu.” (Wakolosai 1:19, 20, NW) Kusudi hilo la kimungu la upatanisho linasonga mbele likafikie upeo.
2 “Vitu vilivyo katika mbingu” si viumbe wa kiroho, kwa maana malaika hawakombolewi kwa damu ya Kristo. Bali, ni wanadamu walionunuliwa kwa damu ya Mwana-Kondoo wakawe ufalme na makuhani pamoja na Kristo katika zile “mbingu mpya.” (Ufunuo 5:9, 10) Hao wamekwisha kutangazwa kwa ukamili kwamba ni waadilifu kupitia damu ya Kristo. Zaidi ya hilo, kwa miaka karibu 50 sasa, Yehova amekuwa akifanya amani pamoja na “vitu vilivyo juu ya dunia,” yaani, wanadamu wale watakaokuwa sehemu ya “dunia mpya” yenye uadilifu. (Ufunuo 5:9, 10; 2 Petro 3:13, NW) Mkusanyo huo wa “vitu vyote pamoja,” vya kidunia na vya kimbingu pia, “ni kulingana na furaha yake njema ambayo [Yehova] alikusudia ndani yake mwenyewe.”—Waefeso 1:9, 10, NW.
Kusudi la Mungu kwa Adamu Mwanaye
3, 4. Adamu alikuwa na msimamo gani mbele za Mungu, lakini ni kwa njia gani bado alihitaji kutangazwa kuwa mwadilifu?
3 Adamu aliumbwa akiwa mwana wa kibinadamu wa Mungu, aliye mkamilifu na mwadilifu. (Luka 3:38) Yeye hakuhesabiwa kuwa na uadilifu. Aliumbwa akiwa nao. Kwa kuwa kulingana na maoni ya Yehova Adamu hakuwa mwenye hatia, yeye hakuhitaji ‘kutangazwa’ kuwa mwadilifu. Kwa muda ambao yeye aliunyenyekea utawala halali wa Mungu, aliendelea kuwa na msimamo mzuri mbele za Muumba wake.
4 Lakini, bado alikuwa hajajithibitisha kuwa mshika-ukamilifu na kuhukumiwa kuwa anaistahili haki ya kupata uzima wa milele duniani. Ili aipate, ilikuwa lazima aonyeshe kwa kipindi fulani uaminifu kwa Yehova na kufuata sana uadilifu. Kama angalithibitisha ukamilifu wake hivyo akiwa chini ya jaribu, angaliipokea haki ya kupata uzima wa milele duniani. Ingalikuwa ni kama Mungu alitangaza, au akatajwa katika kumbukumbu la maandishi kuwa alisema, kwamba Adamu alistahili kupata uzima usio na mwisho. Ili kuonyesha hivyo, bila shaka Yehova angalimwongoza kwenye “mti wa uzima” na kumruhusu ale sehemu ya matunda yake.—Mwanzo 2:9, 16, 17; 3:22.
5. (a) Adamu alijipotezea nini yeye mwenyewe na wazao wake? (b) Yehova aliwapa “viumbe” wa kibinadamu tumaini gani la kukombolewa katika dhambi na kifo?
5 Lakini Adamu alishindwa alipojaribiwa na hivyo akajipotezea yeye mwenyewe na wazao wake ukamilifu, uadilifu, na uana. (Warumi 5:12) Kwa hiyo, wazao wote wa Adamu walizaliwa wakiwa wametengwa mbali na Mungu, wakiwa wasio waadilifu tangu kuzaliwa. (Waefeso 2:3; Warumi 3:10) Hivyo, viumbe wa kibinadamu ‘walitiishwa chini ya ubatili’ lakini “katika tumaini,” na tumaini hilo la kukombolewa katika dhambi na kifo lilitolewa mara tu baada ya uasi katika Edeni.—Mwanzo 3:15; Warumi 8:20, 21.
Walitangazwa Kuwa Waadilifu Kabla ya Kristo—Jinsi Gani Hivyo?
6, 7. (a) Ni kwa kadiri gani wanadamu fulani walitangazwa kuwa waadilifu kabla ya kifo cha dhabihu ya Kristo? (b) Ni mingine gani kati ya mifano ya watumishi wa Yehova wa nyakati zilizoutangulia Ukristo ambao walipokea msimamo wenye uadilifu?
6 Tumaini la wanadamu kukombolewa katika dhambi na kifo lilitegemea kuja kwa “uzao” ulioahidiwa, Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. (Yohana 3:16) Kabla ya kifo cha dhabihu ya Kristo, hakukuwa na njia ya wanadamu kupata “achilio la dhambi na pia uzima,” au ‘kutangazwa kuwa waadilifu ili wapate uzima.’ (Warumi 5:18, Revised Standard Version; New World Translation) Ingawa hivyo, hata kabla Kristo hajalipa ukombozi ili wanadamu wafunguliwe, wanaume na wanawake fulani waliiamini ahadi ya Mungu na kuunga mkono imani hiyo kwa matendo. Kwa sababu hiyo, Yehova aliwafadhili kwa kusamehe dhambi zao na kuwakubali wawe watumishi wake. Aliwahesabu kwa upendo kuwa wasio na hatia wakilinganishwa na wingi wa wanadamu waliotenganishwa na Mungu. (Zaburi 32:1, 2; Waefeso 2:12) Yeye aliwapa msimamo wenye uadilifu, akawatangaza kuwa waadilifu kwa kadiri iliyoufaa wakati huo.
7 Hivyo, kwa imani Abeli “alishuhudiwa ya kwamba alikuwa mwadilifu.” (Waebrania 11:4, NW) Noa “akawa mrithi wa uadilifu unaolingana na imani.” (Waebrania 11:7, NW) Ijapokuwa Ayubu alipungukiwa katika mambo fulani, yeye alisemwa kuwa “asiye na waa na mnyofu.” (Ayubu 1:1, 22; 7:21, NW) Finehasi alionyesha bidii kwa ajili ya ibada safi, “na jambo hilo likaja kuhesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.” (Zaburi 106:30, 31; Hesabu 25:1-13, NW) “Kwa imani” na kwa matendo yake ya fadhili aliyowafanyia watu wa Mungu, Rahabu kahaba asiye Mwisraeli alipokea msimamo wenye uadilifu, au akatangazwa kuwa mwadilifu.—Waebrania 11:31; Yakobo 2:25, NW.
Jinsi Abrahamu Alivyohesabiwa Kuwa Mwadilifu
8, 9. (a) Ni uadilifu wa nani ambao ndio habari kuu ya mazungumzo katika barua ya Paulo kwa Warumi? (b) Ni kwa njia zipi kutangazwa kwa “watakatifu” kuwa ni waadilifu kunazidi kule kwa Abrahamu?
8 Kisa cha Abrahamu kinastahili kuelekezewa fikira za pekee. Jambo la kwamba alitangazwa kuwa mwadilifu linatajwa na waandikaji wawili wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na wote wawili walikuwa wakiwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza walioitwa wawe sehemu ya washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho.—Warumi 2:28, 29; 9:6; Yakobo 1:1; Ufunuo 7:4.
9 Katika barua aliyowaandikia Warumi, Paulo anasisitiza kwamba wale “walioitwa kuwa watakatifu” (1:7), Wayahudi na watu wa Mataifa pia (1:16, 17), wanatangazwa kuwa waadilifu “kwa imani pasipo matendo ya sheria.” (3:28) Ili kuthibitisha jambo analosisitiza, anaanza maelezo marefu (4:1-22, NW) na kutaja maneno ya Mwanzo 15:6 katika kusema: “Abrahamu alijizoeza imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa uadilifu.” (NW) Halafu, katika mistari inayomalizia sura ya 4, Paulo anasema kwamba Yesu “alitolewa auawe kwa ajili ya makosa yetu kisha akafufuliwa kwa ajili ya kututangaza sisi [yaani, “watakatifu” (Warumi 1:7)] kuwa waadilifu.” Neno “sisi” haliwezi kumtia ndani Abrahamu, kwa kuwa alikufa muda mrefu kabla ya kufa na kufufuliwa kwa Kristo. Kwa hiyo, katika sura zinazofuata wakati Paulo anaposema juu ya wale ‘watakaotawala wakiwa wafalme’ na juu ya kutangazwa kwao kuwa waadilifu “ili wapate uzima” wawe “wana wa Mungu” na “warithi washirika pamoja na Kristo,” kwa wazi alikuwa akisema juu ya jambo lililo tofauti sana, wala hakuwa akisema kwamba Mungu alimhesabia Abrahamu uadilifu.—Warumi 5:17, 18; 8:14, 17, 28-33.
10. Yakobo anasaidiaje kufahamu kadiri ambayo Abrahamu alitangazwa kuwa mwadilifu?
10 Yakobo, pia, anamtaja Abrahamu kuwa mfano wa kuthibitisha kwamba ni lazima imani iungwe mkono na matendo ya kumwogopa Mungu. Baada ya kusema kwamba Abrahamu alitangazwa kuwa mwadilifu, Yakobo anataja maneno ya Mwanzo 15:6 ili kuongezea elezo linalotusaidia tuone ni kwa kadiri gani Abrahamu alihesabiwa haki. Anaandika hivi: “Andiko lilitimizwa ambalo linasema: ‘Abrahamu aliweka imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa uadilifu,’ naye akaja kuitwa ‘rafiki ya Yehova.’” (Yakobo 2:20-23, NW) Ndiyo, kwa sababu ya imani yake, Abrahamu alitangazwa kuwa mwadilifu awe rafiki ya Yehova, si awe mwana mwenye haki ya kupata uzima mkamilifu wa kibinadamu au umaliki pamoja na Kristo. Jambo la kupendeza ni kwamba, katika kitabu chake Synonyms of the Old Testament, Robert Girdlestone aliandika hivi juu ya uadilifu wa Abrahamu: “Uadilifu huo haukuwa wa kabisa kabisa, yaani, ule ambao ungeweza kumfanya Abrahamu apewe na Mungu haki ya kudai urithi wa kuwa mwana wake.”
“Kitabu cha Ukumbusho” cha Yehova
11. Ni majina ya nani yameandikwa katika “kitabu cha ukumbusho” cha Yehova, na kwa sababu gani?
11 Uadilifu wa kiasi uliohesabiwa kwa wanaume na wanawake waaminifu walioishi kabla ya Kristo ulikuwa kionyesho kidogo tu cha uadilifu na ukamilifu ule wa kweli kweli unaohusiana na uzima wa milele ambao wanaweza kuupata katika dunia mpya ya Mungu. Kwa sababu ya mataraja yao ya kupata uzima, majina yao yaliandikwa katika “kitabu cha ukumbusho.” (Malaki 3:16; Kutoka 32:32, 33) Hicho kina majina ya wale wanaoonwa na Yehova kuwa “waadilifu” ambao wameonyesha imani yao kwa matendo ya uadilifu, na ambao pia watakuja kupokea uzima wa milele duniani.—Zaburi 69:28; Habakuki 2:4.
12. “Waadilifu” watakaofufuliwa watapaswa kufanya nini ili majina yao yaendelee kukaa katika kitabu cha ukumbusho cha Yehova?
12 Lakini, bado majina hayo hayajaandikwa katika “kitabu cha uzima” cha Yehova. (Ufunuo 20:15) Wakati wanaume na wanawake hao waaminifu wa zamani watakaporudi duniani katika ‘ufufuo wa walio waadilifu,’ bila shaka wataukubali kwa imani uandalizi wa uzima ambao Yehova amefanya kupitia dhabihu ya ukombozi ya Kristo. (Matendo 24:15, NW) Hivyo watakuwa sehemu ya “kondoo wengine” wa Yesu, pamoja na “mkutano mkubwa” watakaokuwa wameiokoka “dhiki kubwa.” (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9, 14) Kwa kufanya hivyo, majina yao yataandikwa katika “kitabu cha ukumbusho” cha Yehova.
Wanahesabiwa Kuwa Waadilifu Wawe Rafiki Watakaopata Wokovu
13. Sasa Mchungaji Mwema anawaleta nani ndani, nao wanaandikwaje katika kitabu cha ukumbusho cha Yehova?
13 Sasa yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, ‘anawaleta kondoo wengine’ ambao si wa “kundi dogo” la “watakatifu” 144,000 wanaopewa Ufalme wa kimbingu. (Luka 12:32; Danieli 7:18) “Kondoo wengine” hao “wanaisikiliza sauti” ya Mchungaji Mwema. (Yohana 10:16) Wanajizoeza imani katika Yehova na katika Mwanaye. Wanaweka maisha zao wakfu kwa Yehova kwa kuitegemea dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Wanabatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu” na kuutambua uhitaji wa kusitawisha “tunda la roho.” (Mathayo 28:19, 20; Wagalatia 5:22, 23, NW) Majina yao, pia, yanaandikwa katika kitabu cha ukumbusho cha Yehova.
14. Ni nini kinachowapa “kondoo wengine” msimamo safi mbele za Yehova, lakini wanahitaji kumwomba Mungu nini?
14 Hao “kondoo wengine” wanaokusanywa katika huu wakati wa mwisho ndio watakaokuwa “mkutano mkubwa” usiohesabiwa ambao mtume Yohana aliona katika njozi, alipokuwa amekwisha kuwaona washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho. (Ufunuo 7:4-9) Yeye aliueleza huo “mkutano mkubwa” kuwa wamefua mavazi yao, na kufanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Mstari wa14) Kwa sababu ya imani yao katika damu iliyomwagwa ya Mwana-Kondoo, wanahesabiwa kadiri fulani ya uadilifu. Jambo hilo lilionyeshwa na mavazi yao meupe ya mfano. Wao wana msimamo safi mbele za Yehova, na “hiyo ndiyo sababu” yeye anawaruhusu ‘wamtolee utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.’ (Mstari wa 15, NW) Lakini bado ni lazima kila siku wamuungamie Yehova dhambi zao na kuomba msamaha kupita Yesu Kristo.—1 Yohana 1:9–2:2.
15. (a) Mfano wa kondoo na mbuzi unaonyeshaje kwamba “kondoo wengine” wana msimamo wenye uadilifu mbele za Mungu? (b) Ni kwa kadiri gani wao wanatangazwa kuwa waadilifu wakati wa sasa?
15 Jambo la kwamba “kondoo wengine” ni rafiki za Mungu na kwamba hata sasa wana msimamo wenye uadilifu wa kiasi mbele zake Yeye linaonyeshwa wazi pia katika unabii wa Yesu juu ya ‘ishara ya kuwapo kwake,’ ambayo inautia ndani mfano wa kondoo na mbuzi. Kwa sababu “kondoo” wanatendea mema mabaki ya “ndugu” za Kristo 144,000 ambao wangali duniani, ‘wanabarikiwa’ na Baba ya Yesu na kuitwa “waadilifu.” Wakiwa kama Abrahamu, wanahesabiwa au wanatangazwa kuwa waadilifu walio rafiki za Mungu. Msimamo wao wenye uadilifu utafanya pia waokolewe wakati “mbuzi” watakapoondoka wakaingie katika “kukatiliwa mbali kwa milele.” (Mathayo 24:3–25:46, NW) Wao ‘watatoka katika ile dhiki kubwa’ ambayo ndiyo itakayayokuwa mwisho wa mfumo mbovu wa mambo ya sasa.—Ufunuo 7:14, NW.
Wanainuliwa Wafikie Ukamilifu
16. Tunajuaje kwamba mkutano mkubwa hawatangazwi kuwa waadilifu ili wapate uzima kabla ya “dhiki kubwa”?
16 “Mkutano mkubwa,” ambao wataiokoka “dhiki kubwa.” bado hawajatangazwa kuwa ni waadilifu ili wapate uzima. Tunaweza kuona jambo hilo kutokana na uhakika wa kwamba sura inayowataja inaendelea kusema: “Huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” (Ufunuo 7:17) Kwa hiyo, ingawa hapo kwanza Mungu aliwahesabu kuwa waadilifu wakilinganishwa na wanadamu kwa ujumla na pia wakiwa ni rafiki zake, walihitaji msaada wa ziada, au hatua zichukuliwe ndiyo waweze kutangazwa kuwa waadilifu ili wapate uzima.
17. (a) Ni nini maana ya “kuwaponya mataifa”? (b) Ni nani watakaohitaji kuandikwa majina yao katika “kitabu cha uzima”?
17 Wakati wa Mileani, Mwana-Kondoo aliyetawazwa, Kristo Yesu, pamoja na wafalme na makuhani wenzake 144,000, atatumia programu ya “kuwaponya mataifa” kiroho na kimwili. (Ufunuo 22:1, 2) “Mataifa” hayo yatakuwa ni wale waokokaji wa dhiki kubwa, pia watoto wo wote watakaowazaa baada ya Har–Magedoni, na wale watakaorudi katika “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15, NW) Wote wanaoonyesha imani katika damu ya Kristo na kufanya “matendo” yanayofaa, wataandikisha mwishowe majina yao katika “kitabu cha uzima “—Ufunuo 20:11-15.
18. Wakaaji wa dunia watakuwa wameinuliwa wakafikia hali gani mwishoni mwa Mileani?
18 Kufikia mwishoni mwa Utawala wa Mileani ya Kristo, wale kati ya wakaaji wa dunia watakaokuwa wameonyesha kwamba wanaukubali ukombozi wa Kristo na kwamba wataishi kwa kufuata viwango vya Yehova watakuwa wameinuliwa kwenye ukamilifu. Watakuwa kama vile Adamu alivyokuwa kabla hajatenda dhambi. Kama yeye, watajaribiwa utii wao.
“Uhuru wa Utukufu” Wakiwa “Watoto wa Mungu”
19. (a) Ni jambo gani litakalotokea mara tu baada ya Mileani? (b) Ni jambo gani litakalowapata wale ambao majina yao hayataonekana yameandikwa katika “kitabu cha uzima”?
19 Mara tu baada ya Mileani, Kristo atamrudishia Baba yake jamii ya wanadamu walio wakamilifu. (1 Wakorintho 15:28) “Shetani atafunguliwa” ili wanadamu wapate jaribu la kukata maneno. (Ufunuo 20:7, 8) Majina ya wo wote watakaoshindwa na jaribu hayataonekana ‘yameandikwa katika kitabu cha uzima.’ ‘Watatupwa katika ziwa la moto’ kwa njia ya mfano, nalo linamaanisha “mauti ya pili.”—Ufunuo 20:15; 21:8.
20. (a) Ni nani watakaotangazwa na Yehova kuwa waadilifu ili wapate uzima, na kwa sababu gani? (b) Mpango wa rehema uliofanywa na Yehova kuhesabia watu haki utakuwaje umetimiza kusudi lao?
20 Wale watakaojithibitisha kuwa washikamanifu kwa Yehova wataandikwa majina yao katika “kitabu cha uzima” yasiweze kufutwa humo, kuonyesha kwamba ni watimilifu katika ukamilifu na wanaistahili haki ya kupata uzima wa milele duniani. Ndipo Yehova mwenyewe atakapowatangaza kuwa waadilifu katika maana kamili. (Warumi 8:33) Watakuwa wamehesabiwa haki ya kuustahili uzima wa milele. (Ufunuo 20:5) Mungu atawachukua wawe ni wanaye kwa malezi hapa duniani, nao wataingia ndani ya ule “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Warumi 8:20, 21) Amani na upatano vitakuwa vimerudishwa katika ulimwengu wote. “Vitu vilivyo duniani” na “vitu vilivyo katika mbingu” vitakuwa vimefanyiwa upatanisho kamili pamoja na Mungu. (Wakolosai 1:20, NW) Mpango wa rehema uliofanywa na Yehova wa kuhesabiwa haki utakuwa umetimiza kusudi lao. Kwa lile ulizo, “Je! Wewe Una Msimamo Unaofaa na Mungu?” kila kiumbe aliye mbinguni na duniani ataweza kujibu kwa kusema ndivyo na kuongezea hivi: “Kwake yeye aketiye katika kiti cha enzi, na kwa Mwana-kondoo, iwe sifa na heshima na utukufu na enzi milele na milele.”—Ufunuo 5:13, HNWW.
Kwa habari ya msimamo wa kondoo wengine mbele za Mungu—
◻ Kwa sababu gani Adamu hakutangazwa kuwa mwadilifu?
◻ Ni kwa kadiri gani Abrahamu na wanaume na wanawake wengine walioishi kabla ya Kristo walitangazwa kuwa waadilifu?
◻ Ni majina ya nani yaliyoandikwa katika kitabu cha ukumbusho cha Yehova?
◻ Ni kwa kadiri gani “kondoo wengine” wana msimamo wenye uadilifu wakati wa sasa, na ni wakati gani watakaooinuliwa wafikie ukamilifu?
[Blabu katika ukurasa wa 18]
Kwa kuonyesha imani katika “damu ya Mwana-Kondoo,” “kondoo wengine” wanapewa msimamo unaokubaliwa mbele za Yehova na hivyo wanatangazwa kuwa waadilifu ili wapate urafiki wake na ili waje waokolewe wakati wa ile “dhiki kubwa.” Wataufikia ukamilifu mwishoni mwa Mileani. Baada ya jaribu la mwisho watatangazwa kuwa waadilifu ili wapate uzima.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Majina ya waadilifu yameandikwa katika kitabu cha ukumbusho cha Yehova
Abeli
Ayubu
Rahabu
“Mkutano mkubwa” wa kisasa