Kutakuwa na Ufufuo wa Waadilifu
“Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—MATENDO 24:15, NW.
1. Ni hali gani imekabili wanadamu wote tangu Adamu na Hawa watumbukie dhambi?
“LO LOTE mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.” (Mhubiri 9:10) Kwa maneno hayo machache yaliyochaguliwa vema, Mfalme Sulemani mwenye hekima afafanua hali ambayo imekabili kila kizazi cha wanadamu tangu wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, kutumbukia dhambi. Bila kuchagua, kifo kimemeza kila mtu hatimaye—tajiri kwa maskini, mfalme kwa mtu wa kawaida, mwaminifu kwa mtu asiye na imani. Hakika, kifo ‘kimetawala kama mfalme.’—Warumi 5:17, NW.
2. Kwa nini huenda baadhi ya wale walio waaminifu wamevunjika moyo katika wakati huu wa mwisho?
2 Yajapokuwa maendeleo ya karibuni zaidi ya sayansi ya kitiba, kifo bado hutawala kama mfalme hata leo. Ingawa hili halishangazi, huenda wengine walivunjika moyo kwa kadiri fulani walipokabili adui huyu wa tangu zamani. Kwa nini? Huko nyuma katika miaka ya 1920, Watch Tower Society ilitangaza ule ujumbe “Mamilioni wanaoishi sasa hawatakufa kamwe.” Mamilioni hao wangekuwa nani? Wale “kondoo” wanaotajwa katika maneno ya Yesu yaliyohusu kondoo na mbuzi. (Mathayo 25:31-46) Hao wenye mfano wa kondoo walitabiriwa kuwa wangetokea katika kipindi cha wakati wa mwisho, na tumaini lao lingekuwa uhai wa milele katika dunia paradiso. Wakati ulipopita, watu wa Mungu walipata uelewevu bora juu ya fungu la “kondoo” hawa katika makusudi ya Yehova. Iling’amuliwa kwamba watiifu hawa wangetenganishwa na wale “mbuzi” walio wakaidi, na baada ya uharibifu wa mbuzi hao, kondoo wangerithi makao ya kidunia ya ule Ufalme uliokuwa umetayarishwa kwa ajili yao.
Kukusanywa kwa Wenye Mfano wa Kondoo
3. Watu wa Mungu wamekazia akili kazi gani tangu 1935?
3 Tangu 1935, “mtumwa mwaminifu” amekazia akili kutafuta hao wenye mfano wa kondoo na kuwaleta katika tengenezo la Yehova. (Mathayo 24:45; Yohana 10:16) Wakristo hao wenye kuweza kufundishwa wamekuja kung’amua kwamba sasa Yesu anatawala katika Ufalme wa Yehova wa kimbingu na kwamba wakati unakuja mbio wa mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo na kuletwa kwa ulimwengu mpya ambao uadilifu utakaa ndani yao. (2 Petro 3:13; Ufunuo 12:10) Katika ulimwengu huo mpya, maneno yenye kutia moyo ya Isaya yatatimizwa: “Amemeza mauti hata milele.”—Isaya 25:8.
4. Ingawa wanatumaini sana kuona enzi kuu ya Yehova ikitetewa katika Har–Magedoni, ni nini kimewapata wengi wa kondoo wengine?
4 Kwa kuwa mwisho wa ulimwengu wa Shetani uko karibu sana, Wakristo wenye mfano wa kondoo wangependa sana kuendelea kuishi mpaka enzi kuu ya Yehova itetewe wakati wa dhiki inayokuja juu ya Babiloni Mkubwa na sehemu yote ibakiyo ya ulimwengu wa Shetani. (Ufunuo 19:1-3, 19-21) Haijawa hivyo kwa walio wengi. Wengi waliotumaini kuwa miongoni mwa wale “mamilioni” ambao hawangekufa kamwe hakika wamekufa. Baadhi yao walifia imani kwa ajili ya kweli wakiwa gerezani na katika kambi za mateso au mikononi mwa washupavu wa kidini. Wengine wamekufa katika aksidenti au kutokana na zile ziitwazo sababu za asili—ugonjwa na uzee. (Zaburi 90:9, 10; Mhubiri 9:11) Kwa wazi, wengi zaidi watakufa kabla ya mwisho kuja. Hao wataonaje utimizo wa ahadi ya ulimwengu mpya ambao uadilifu utakaa ndani yao?
Tumaini la Ufufuo
5, 6. Ni wakati ujao gani uliopo kwa wale wenye tumaini la kidunia wanaokufa kabla ya Har–Magedoni?
5 Mtume Paulo alitoa jibu alipokuwa akisema mbele ya yule gavana Mroma Feliki. Kama ilivyorekodiwa kwenye Matendo 24:15 (NW), Paulo alijulisha hivi kwa ujasiri: “Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Tumaini la ufufuo hutupa sisi moyo mkuu tunapokabili misiba iliyo mibaya zaidi. Kwa sababu ya tumaini hilo, rafiki zetu wapendwa wanaokuwa wagonjwa na kuhisi kwamba watakufa hawavunjiki moyo. Hata jambo gani litokee, wao wajua kwamba watapata thawabu ya uaminifu. Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, ndugu na dada zetu wenye moyo mkuu wanaokabili kifo mikononi mwa wanyanyasi wanajua kwamba wanyanyasi wao hawawezi kamwe kupata ushindi. (Mathayo 10:28) Mtu fulani afapo kutanikoni, tunahuzunika kumpoteza. Wakati uo huo, ikiwa yeye ni mmoja wa wale kondoo wengine, twashangilia kwamba mwamini mwenzetu amethibitika kuwa mwaminifu hadi mwisho na sasa anapumzika, akiwa amehakikishiwa wakati ujao katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Wathesalonike 4:13.
6 Ndiyo, tumaini la ufufuo ni sehemu muhimu sana ya imani yetu. Lakini, kwa nini itikadi yetu katika ufufuo ni yenye nguvu sana, na ni nani wanaokuwa na tumaini hilo?
7. Ufufuo ni nini, na ni yapi baadhi ya maandiko yaonyeshayo uhakika wao?
7 Neno la Kigiriki la “ufufuo” ni a·naʹsta·sis, limaanishalo kihalisi “kusimama.” Neno hilo larejezea hasa kusimama kutoka kwa wafu. Kwa kupendeza, neno “ufufuo” lenyewe halipatikani katika Maandiko ya Kiebrania, lakini tumaini la ufufuo laonyeshwa wazi humo. Kwa mfano, twaliona katika maneno yaliyosemwa na Ayubu katikati ya mateso yake: “Laiti ungenificha kuzimuni, . . . na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!” (Ayubu 14:13) Vivyo hivyo, kwenye Hosea 13:14, twasoma hivi: “Nitawakomboa na nguvu za kaburi; nitawaokoa na mauti; ewe mauti, ya wapi mapigo yako? ewe kaburi, ku wapi kuharibu kwako?” Katika 1 Wakorintho 15:55, mtume Paulo alinukuu maneno hayo na kuonyesha kwamba ushindi juu ya kifo uliotabiriwa unatimizwa kupitia ufufuo. (Bila shaka, katika andiko hilo Paulo alikuwa akisema juu ya ufufuo wa kimbingu.)
Waamini ‘Watangazwa Kuwa Waadilifu’
8, 9. (a) Wanadamu wasiokamilika wanawezaje kushiriki katika ufufuo wa waadilifu? (b) Ni nini msingi wa tumaini letu katika maisha ambayo hayatakatizwa na kifo?
8 Katika taarifa yake kwa Feliki, iliyonukuliwa katika fungu la 5, Paulo alisema kwamba kungekuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu. Ni nani wale waadilifu watakaoinuliwa? Hakuna binadamu aliye mwadilifu kiasili. Sisi sote ni watenda-dhambi tangu tuzaliwe, nasi hutenda dhambi muda wote wa maisha zetu—jambo linalotufanya tustahili kifo kwa hatia mbili. (Warumi 5:12; 6:23) Hata hivyo, katika Biblia twapata maneno ‘kutangazwa kuwa waadilifu.’ (Warumi 3:28, NW) Hili larejezea wanadamu ambao wamesamehewa dhambi zao na Yehova, ingawa wao si wakamilifu.
9 Usemi huo unatumiwa hasa kwa Wakristo watiwa-mafuta, walio na tumaini la kimbingu. Kwenye Warumi 5:1 (NW), mtume Paulo asema hivi: “Kwa kuwa sasa tumetangazwa kuwa waadilifu likiwa tokeo la imani, na tuonee shangwe amani pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo.” Wakristo wote watiwa-mafuta wanatangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani. Imani katika nini? Kama Paulo aelezavyo kirefu katika kitabu cha Warumi, ni imani katika Yesu Kristo. (Warumi 10:4, 9, 10) Yesu alikufa akiwa mtu mkamilifu kisha akafufuliwa kutoka kwa wafu, akapaa mbinguni ili kutoa thamani ya uhai wake wa kibinadamu kwa ajili yetu. (Waebrania 7:26, 27; 9:11, 12) Yehova alipokubali dhabihu hiyo, ikawa kama Yesu alinunua wanadamu kutoka utumwa wa dhambi na kifo. Wale wanaodhihirisha imani katika mpango huo wanufaika sana nao. (1 Wakorintho 15:45) Kwa msingi huo wanaume na wanawake waaminifu wana tumaini la kurithi uhai ambao hautakatizwa na yule adui mkatili, yaani kifo.—Yohana 3:16.
10, 11. (a) Ni ufufuo upi wangojea Wakristo watiwa-mafuta walio waaminifu? (b) Ni ufufuo wa aina gani uliotumainiwa na waabudu wa kabla ya nyakati za Ukristo?
10 Kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu, watiwa-mafuta waaminifu, kwa kutangazwa kuwa waadilifu, wana tumaini hakika la kufufuliwa wakiwa viumbe-roho wasioweza kufa, kama Yesu. (Ufunuo 2:10) Ufufuo wao unatajwa kwenye Ufunuo 20:6 (NW), lisemalo hivi: “Mwenye furaha na mtakatifu ni yeyote aliye na sehemu katika huo ufufuo wa kwanza; juu ya hao kifo cha pili hakina mamlaka yoyote, bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.” Huo ni ufufuo wa kimbingu. Lakini ona kwamba Biblia huuita “ufufuo wa kwanza,” jambo linalodokeza kwamba kuna mwingine zaidi unaokuja.
11 Katika Waebrania sura ya 11, Paulo alirejezea mstari mrefu wa watumishi wa Mungu wa kabla ya nyakati za Ukristo waliokuwa wameonyesha imani yenye nguvu katika Yehova Mungu. Wao pia walikuwa na imani katika ufufuo. Kwenye mstari wa 35 wa sura hiyo, Paulo asema juu ya ufufuo mbalimbali wa kimuujiza uliotukia wakati wa historia ya Israeli, akisema hivi: “Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora.” Wale mashahidi waaminifu wa kale wangeweza kutazamia ufufuo ulio bora kuliko ule uliohusu Eliya na Elisha kwa mfano. (1 Wafalme 17:17-22; 2 Wafalme 4:32-37; 13:20, 21) Tumaini lao lilikuwa ufufuo wa kuingia katika ulimwengu ambao watumishi wa Mungu wasingeteswa kwa ajili ya imani yao, ulimwengu ambao wanawake wasingepoteza wapendwa wao katika kifo. Ndiyo, walitazamia kuinuka kutoka kwa wafu kuingia katika ulimwengu mpya uleule tunaotumaini. (Isaya 65:17-25) Yehova hakuwa amewafunulia mambo mengi kama ambavyo ametufunulia kuhusu huu ulimwengu mpya. Lakini walijua kwamba ulikuwa ukija, na walitaka kuwa ndani ya huo.
Ufufuo wa Kidunia
12. Je, wale waaminifu wa kabla ya nyakati za Ukristo walitangazwa kuwa waadilifu? Eleza.
12 Je, tuone kuamka kwa wanaume na wanawake hao waaminifu wa kabla ya nyakati za Ukristo katika ulimwengu huo mpya kuwa sehemu ya ufufuo wa waadilifu? Kwa wazi, ndiyo, kwa sababu Biblia yawarejezea kuwa waadilifu. Kwa kielelezo, mwanafunzi Yakobo ataja mwanamume na mwanamke fulani wa nyakati za kale waliotangazwa kuwa waadilifu. Mwanamume huyo alikuwa Abrahamu, mwanzilishi wa jamii ya Waebrania. Twasoma hivi juu yake: “‘Abrahamu aliweka imani katika Yehova, na ilihesabiwa kwake kuwa uadilifu,’ naye akaja kuitwa ‘rafiki ya Yehova.’” Mwanamke yule alikuwa Rahabu, mwanamke asiye Mwisraeli aliyedhihirisha imani katika Yehova. Yeye ‘alitangazwa kuwa mwadilifu’ naye akaja kuwa sehemu ya taifa la Waebrania. (Yakobo 2:23-25, NW) Kwa njia hiyo, wanaume na wanawake wa kale waliodhihirisha imani yenye nguvu katika Yehova na ahadi zake na kubaki wakiwa waaminifu hadi kifo walitangazwa kuwa waadilifu na Yehova kwa msingi wa imani yao, na bila shaka wao watashiriki katika “ufufuo wa waadilifu.”
13, 14. (a) Tunajuaje kwamba Wakristo wenye tumaini la kidunia waweza kutangazwa kuwa waadilifu? (b) Na jambo hilo lamaanisha nini kwao?
13 Hata hivyo, namna gani watu mmoja-mmoja wenye mfano wa kondoo leo, wale wenye tumaini la kidunia wanaojiweka wakfu kwa Yehova na wanaokufa wakiwa waaminifu katika wakati huu wa mwisho? Je! wao watashiriki katika ufufuo wa waadilifu? Kwa hakika ndiyo. Umati mkubwa wa waadilifu hao ulionwa katika njozi na mtume Yohana. Ona jinsi anavyowafafanua: “Nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana [“umati mkubwa,” NW] ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:9, 10.
14 Ona kwamba wanyenyekevu hao wamesadiki kabisa wokovu wao, nao waona umetokana na Yehova na Yesu, yule “Mwana-Kondoo.” Isitoshe, wao wamesimama mbele ya Yehova na Mwana-Kondoo, wote wakiwa wamevaa mavazi meupe. Kwa nini wamevaa mavazi meupe? Kiumbe fulani cha kimbingu chaeleza Yohana hivi: “Wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:14) Katika Biblia, rangi nyeupe ni ufananisho wa usafi, uadilifu. (Zaburi 51:7; Danieli 12:10; Ufunuo 19:8) Jambo la kwamba umati mkubwa waonwa wakiwa wamevaa mavazi meupe lamaanisha kwamba Yehova awaona kuwa waadilifu. Hilo lawezekanaje? Kwa sababu kwa njia ya ufananisho, wao wameyafua mavazi yao katika damu ya Mwana-Kondoo. Wanadhihirisha imani katika damu ya Yesu Kristo iliyomwagwa na kwa hiyo wanatangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu wakitazamia kuokoka dhiki kubwa. Kwa hiyo, Mkristo yeyote mwaminifu aliyejiweka wakfu ambaye sasa ni wa ule “umati mkubwa” afaye kabla ya dhiki kubwa aweza kuwa na uhakika wa kupata ufufuo wa kidunia wa waadilifu.
15. Kwa kuwa wote waadilifu na wasio waadilifu watafufuliwa, ufufuo wa waadilifu una manufaa gani?
15 Ufufuo huo unafafanuliwa kwenye Ufunuo sura ya 20, mstari wa 13, kwa maneno haya: “Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.” Hivyo, katika ile Siku ya Hukumu ya Yehova iliyo kuu ya kipindi cha miaka elfu moja, wote wale walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa—waadilifu na wasio waadilifu pia. (Matendo 17:31) Lakini, utakuwa bora zaidi kama nini kwa waadilifu! Tayari wao wameishi maisha ya imani. Tayari wana uhusiano wa karibu na Yehova na wana uhakika kwamba makusudi yake yatatimizwa. Mashahidi waadilifu wa kabla ya Enzi ya Ukristo wataamka kutoka kwa wafu wakiwa na hamu ya kujifunza jinsi ahadi za Yehova kuhusu ile Mbegu zilivyotimizwa. (1 Petro 1:10-12) Wale wa kondoo wengine ambao Yehova awaona kuwa waadilifu katika siku yetu watatoka makaburini mwao wakiwa na hamu nyingi ya kuona ile dunia Paradiso waliosema juu yayo walipotangaza habari njema katika mfumo huu wa mambo. Huo utakuwa wakati wenye shangwe kama nini!
16. Twaweza kusema nini juu ya ufufuo wa Siku ya Hukumu wa wale wanaokufa katika wakati wetu?
16 Wale waliokufa wakiwa waaminifu katika hii miaka ya mwisho-mwisho ya mfumo wa mambo wa Shetani watafufuliwa lini hasa katika hiyo Siku ya Hukumu ya kipindi cha miaka elfu? Biblia haisemi. Hata hivyo, je, si jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba wale ambao wameonwa kuwa waadilifu wanaokufa katika wakati wetu wangefufuliwa mapema ili waweze kushiriki pamoja na ule umati mkubwa wa waokokaji wa Har–Magedoni katika kazi ya kukaribisha vizazi vya awali kutoka kwa wafu? Bila shaka, ndiyo!
Tumaini Liletalo Faraja
17, 18. (a) Tumaini la ufufuo laleta faraja gani? (b) Sisi husukumwa kutangaza nini juu ya Yehova?
17 Tumaini la ufufuo huwapa nguvu na faraja Wakristo wote leo. Tukibaki tukiwa waaminifu, hakuna tukio lisilotazamiwa wala adui yeyote awezaye kutunyang’anya thawabu yetu! Kwa kielelezo, katika Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1994, ukurasa 177, mna picha za Wakristo wenye moyo mkuu katika Ethiopia waliokufa badala ya kuridhiana imani yao. Maelezo ya picha yasema hivi: “Nyuso tunazotazamia kuona katika ufufuo.” Ni pendeleo kama nini kupata kuwajua hao na wengine wengi ambao wameonyesha uaminifu kama huo wakabilipo kifo!
18 Namna gani wapendwa wetu na rafiki zetu wenyewe ambao kwa sababu ya umri au ugonjwa fulani hawataishi kupitia dhiki kubwa? Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, wao wana wakati ujao mzuri ajabu wakibaki wakiwa waaminifu. Na sisi pia tukidhihirisha imani kwa moyo mkuu katika dhabihu ya fidia ya Yesu, tuna wakati ujao mzuri ajabu. Kwa nini? Kwa sababu, kama Paulo, twatumaini katika “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Twamshukuru Yehova kwa mioyo yetu yote kwa ajili ya tumaini hili. Kwa hakika, hilo hutusukuma turudie kusema maneno haya ya mtunga-zaburi: “Wahubirini mataifa habari za utukufu [wa Mungu], na watu wote habari za maajabu yake. Kwa kuwa BWANA ni mkuu mwenye kusifiwa sana.”—Zaburi 96:3, 4.
Je, Unaweza Kueleza?
◻ Ni maandiko gani husaidia kuthibitisha tumaini letu katika ufufuo wa kidunia?
◻ Ni kwa msingi gani Wakristo sasa watangazwa kuwa waadilifu?
◻ Tumaini la ufufuo hutupatiaje moyo mkuu na azimio la kuendelea?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kama Paulo, Wakristo watiwa-mafuta watumaini ufufuo wa kimbingu