Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it kur. 1211-1212
  • Ibada

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ibada
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Inafaa Kumwabudu Yesu?
    Amkeni!—2000
  • Utumishi Mtakatifu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Ni Ibada ya Nani Anayoikubali Mungu?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Ibada ya Kweli Itaongeza Furaha Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it kur. 1211-1212

IBADA

Kitendo cha kutoa heshima kubwa sana au staha ya pekee. Ibada ya kweli kwa Muumba inahusisha nyanja zote za maisha ya mtu. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakorintho: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”​—1Ko 10:31.

Yehova alipomuumba Adamu, hakuorodhesha sherehe fulani au njia fulani ambayo mwanadamu mkamilifu alihitaji kutumia ili amwabudu Mungu. Licha ya hilo, Adamu aliweza kumtumikia na kumwabudu Muumba wake kwa kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni kwa uaminifu. Baadaye, Yehova alitoa mwongozo kwa taifa la Israeli kuhusu njia fulani ya kumkaribia katika ibada, iliyotia ndani dhabihu, ukuhani, na mahali patakatifu. (Ona NJIA YA KUMKARIBIA MUNGU.) Hata hivyo, njia hiyo ilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja, lakini si uhalisi wa mambo hayo.” (Ebr 10:1) Nyakati zote, jambo linalosisitizwa ni kuonyesha imani, yaani, kufanya mapenzi ya Yehova Mungu—​na si sherehe au desturi.​—Mt 7:21; Yak 2:17-26.

Kama vile nabii Mika alivyosema: “Nitakuja mbele za Yehova nikiwa na nini? Nitainama mbele za Mungu aliye juu nikiwa na nini? Je, nitakuja mbele zake nikiwa na dhabihu nzima za kuteketezwa, nikiwa na ndama wenye umri wa mwaka mmoja? Je, Yehova atapendezwa na maelfu ya kondoo dume, na makumi ya maelfu ya mito ya mafuta? Je, nitamtoa mwanangu mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya uasi wangu, uzao wa mwili wangu kwa ajili ya dhambi yangu? Ee mwanadamu, amekuambia yaliyo mema. Na Yehova anataka nini kutoka kwako? Anataka tu utekeleze haki, uthamini sana ushikamanifu, na utembee kwa kiasi na Mungu wako!”​—Mik 6:6-8; linganisha Zb 50:8-15, 23.

Maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki. Maneno mengi ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotumiwa kumaanisha ibada yanaweza pia kutumiwa kuhusiana na matendo mengine tofauti na ibada. Hata hivyo, muktadha ndio unaoamua jinsi neno husika linavyopaswa kueleweka.

Neno moja la Kiebrania linalotokeza wazo la ibada (ʽa·vadhʹ) kihalisi linamaanisha ‘kutumikia.’ (Mwa 14:4; 15:13; 29:15) Kinachohitajiwa ili kumtumikia au kumwabudu Yehova ni kutii amri zake zote, yaani, kufanya mapenzi yake kama mtu aliyejitoa kwake kikamili. (Kut 19:5; Kum 30:15-20; Yos 24:14, 15) Kwa hiyo, kujihusisha na desturi zozote au tendo lolote la kujitoa kwa mungu mwingine yeyote kulionyesha kwamba mtu ameiacha ibada ya kweli.​—Kum 11:13-17; Amu 3:6, 7.

Neno lingine la Kiebrania ambalo linaweza kumaanisha ibada ni hish·ta·chawahʹ, ambalo kimsingi linamaanisha ‘kuinama chini’ (Mwa 18:2), au kusujudu. (Ona SUJUDIA.) Ingawa nyakati nyingine kuinama kunaweza kuwa tu tendo la heshima au la adabu kumwelekea mtu mwingine (Mwa 19:1, 2; 33:1-6; 37:9, 10), linaweza pia kuwa tendo la ibada, likiashiria heshima kubwa na shukrani ambayo mtu anampa Mungu na kujitiisha kwa mapenzi yake. Nyakati nyingine neno hish·ta·chawahʹ linahusianishwa na dhabihu na sala pale linapotumiwa kuhusiana na Mungu wa kweli au miungu ya uwongo. (Mwa 22:5-7; 24:26, 27; Isa 44:17) Hilo linadokeza kwamba ilikuwa kawaida kuinama chini wakati wa sala au wa kutoa dhabihu.​—Ona SALA.

Sa·ghadhʹ (Isa 44:15, 17, 19; 46:6) ni mzizi wa neno la Kiebrania ambao kimsingi unamaanisha ‘kuinama.’ Neno la Kiaramu linalofanana na hilo mara nyingi linahusianishwa na ibada (Da 3:5-7, 10-15, 18, 28), lakini linatumiwa kwenye Danieli 2:46 kurejelea namna Mfalme Nebukadneza alivyompa Danieli heshima kubwa, akiinama kifudifudi mbele ya nabii huyo.

Kitenzi cha Kigiriki la·treuʹo (Lu 1:74; 2:37; 4:8; Mdo 7:7) na nomino yake la·treiʹa (Yoh 16:2; Ro 9:4) havitokezi wazo la kutoa utumishi wa kawaida bali la kutoa utumishi mtakatifu.

Neno la Kigiriki pro·sky·neʹo linaendana kwa ukaribu na neno la Kiebrania hish·ta·chawahʹ katika kuelezea wazo la kusujudu, na wakati mwingine, ibada. Neno pro·sky·neʹo linatumiwa kuhusiana na mtumwa anayemsujudia mfalme (Mt 18:26) na pia kuhusiana na tendo ambalo Shetani alitaka afanyiwe alipoahidi kumpa Yesu falme zote za ulimwengu na utukufu wazo. (Mt 4:8, 9) Ikiwa Yesu angemsujudia Ibilisi, hilo lingeonyesha ujitiisho wake kwa Shetani na angejifanya mwenyewe kuwa mtumwa wa Ibilisi. Lakini Yesu alikataa na kusema: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu [katika Kigr. pro·sky·neʹo au, kwenye simulizi la Kumbukumbu la Torati ambapo Yesu alikuwa akinukuu, Kiebr. hish·ta·chawahʹ], na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu [katika Kigr. la·treuʹo au Kiebr. ʽa·vadhʹ]’” (Mt 4:10; Kum 5:9; 6:13) Vivyo hivyo, ibada, kusujudia, au kumwinamia “mnyama wa mwituni” na “sanamu” yake kunahusianishwa na utumishi, kwa kuwa wale wanaomwabudu wanatambuliwa kuwa wanamuunga mkono “mnyama wa mwituni” na “sanamu” yake kwa kuwa na alama mkononi (kama wale wanaomtumikia) au kwenye paji la uso (ili wote waone). Kwa kuwa Ibilisi anampa mamlaka yake mnyama wa mwituni, kumwabudu mnyama wa mwituni kunamaanisha kumwabudu au kumtumikia Ibilisi moja kwa moja.​—Ufu 13:4, 15-17; 14:9-11.

Maneno mengine ya Kigiriki yanayohusiana na ibada yanatokana na maneno haya: eu·se·beʹo, thre·skeuʹo, na seʹbo·mai. Neno eu·se·beʹo linamaanisha “ujitoaji-kimungu” au “tukuza, stahi.” (Ona UJITOAJI-KIMUNGU.) Neno hilo limetumiwa kwenye Matendo 17:23 kurejelea ujitoaji-kimungu au ibada ambayo wanaume wa Athene walikuwa wakimpa “Mungu Asiyejulikana.” Nomino thre·skeiʹa inatokana na neno thre·skeuʹo linalomaanisha “namna ya ibada,” iwe ni ya kweli au ya uwongo. (Mdo 26:5; Kol 2:18) Ibada ya kweli ya Wakristo ilitambuliwa kwa kuwajali kikweli maskini na kujitenga kabisa na ulimwengu usiomwogopa Mungu. (Yak 1:26, 27) Neno seʹbo·mai (Mt 15:9; Mk 7:7; Mdo 18:7; 19:27) na neno linalohusiana na hilo se·baʹzo·mai (Ro 1:25) yanamaanisha ‘heshimu sana; tukuza; abudu.’ Vitu vinavyotumiwa kuabudu au vinavyopewa ujitoaji-kimungu vinaitwa seʹba·sma. (Mdo 17:23; 2Th 2:4) Kuna maneno mengine mawili yanayotokana na kitenzi kilekile, yenye kiambishi The·osʹ, Mungu. Maneno hayo ni the·o·se·besʹ, linalomaanisha ‘kumwogopa Mungu’ (Yoh 9:31), na the·o·seʹbei·a, linalomaanisha ‘kumtumikia Mungu.’ (1Ti 2:10) Maneno hayo mawili yanafanana kwa kiasi fulani na neno la Kijerumani Gottesdienst (muunganiko wa maneno: “Mungu” na “utumishi”) linalomaanisha “ibada ya hadharani.”

Ibada Ambayo Inakubalika kwa Mungu. Ibada pekee inayokubaliwa na Yehova Mungu ni ya wale ambao wanaishi kupatana na mapenzi yake. (Mt 15:9; Mk 7:7) Yesu alimwambia hivi mwanamke Msamaria: “Saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tunachokijua . . . Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, ambayo waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu. Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.”​—Yoh 4:21-24.

Maneno ya Yesu yanaonyesha wazi kwamba ibada ya kweli haitegemei uwepo au matumizi ya vitu vinavyoonekana wala eneo la kijiografia. Badala ya kutegemea kile anachoona au kugusa, mwabudu wa kweli anaonyesha imani na bila kujali yuko wapi au vitu vilivyopo, anadumisha mtazamo wa ibada. Kwa njia hiyo anaabudu, si kwa msaada wa kitu anachoweza kuona au kugusa, bali kwa imani. Kwa kuwa amejifunza kweli kama ilivyofunuliwa na Mungu, ibada yake inapatana na kweli. Baada ya kumjua Mungu kupitia Biblia na kushuhudia utendaji wa roho ya Mungu maishani mwake, mtu anayeabudu kwa roho na kweli bila shaka ‘anajua kile anachokiabudu.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki