UTUMISHI MTAKATIFU
Huduma, au kazi, ambayo ni takatifu, na inahusiana moja kwa moja na ibada ya mtu kwa Mungu.
Kimsingi, neno la Kiebrania ʽa·vadhʹ linamaanisha “tumikia” (Mwa 14:4; 29:15) au “kufanya kazi” (Kut 34:21) na pia limetafsiriwa “kulima.” (Mwa 4:12) Neno ʽa·vadhʹ linapotumiwa kurejelea utumishi unaotolewa kwa Yehova au kwa miungu ya uwongo, linamaanisha ibada, au utumishi mtakatifu. (Kut 10:26; Kum 11:16) Vivyo hivyo, kitenzi cha Kigiriki la·treuʹo kinamaanisha kutumikia. Kinatumiwa kuhusiana na kumtumikia Mungu (Mt 4:10; Lu 1:74; 2:37; 4:8; Mdo 7:7; Ro 1:9; Flp 3:3; 2Ti 1:3; Ebr 9:14; 12:28; Ufu 7:15; 22:3), kama ilivyokuwa katika hema la mkutano au hekalu (Ebr 8:5; 9:9; 10:2; 13:10) na pia kuhusiana na ibada ya uwongo, yaani kuutolea utumishi mtakatifu uumbaji. (Mdo 7:42; Ro 1:25) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo nomino la·treiʹa hutumiwa tu inapohusu kumtumikia Mungu. (Yoh 16:2; Ro 9:4; 12:1; Ebr 9:1, 6) Neno hilo linatofautiana na neno la Kigiriki di·a·ko·niʹa, ambalo pia linamaanisha “huduma, utumishi,” lakini ambalo hutumiwa kurejelea mambo ya kawaida—mambo ambayo si utumishi mtakatifu.
Ni Yehova Mungu tu anayestahili kupokea ibada, au utumishi mtakatifu. (Mt 4:10; Lu 4:8) Kwa kuwa Wayahudi walikuwa katika agano la pekee pamoja na Yehova Mungu, walipaswa kuwa na pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho na kuwa washiriki wa “ukuhani wa kifalme.” Lakini wengi wao walipoteza pendeleo hilo kwa sababu walikosa kuonyesha imani kwa Yesu Kristo. (Ro 9:3-5, 30-33; 1Pe 2:4-10) Wengi wao, kama vile Sauli aliyekuwa Farisayo kabla ya kuwa Mkristo, walifikiri kwamba walikuwa wakimtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa kuwatesa wafuasi wa Kristo.—Yoh 16:2; Mdo 26:9-11; Gal 1:13, 14.