Kuona Ubora wa Hazina ya Utumishi Mtakatifu
“Inakupasa umwabudu Yehova Mungu wako, na inakupasa umtolee yeye peke yake utumishi mtakatifu.”—Mt. 4:10, NW.
1-4. (a) Ni utumishi gani ambao wengi wameihesabu kuwa heshima kujitolea sana kuufanya, na wametazamwa na ulimwengu namna gani? (b) Hata hivyo, wanadamu wanapatwa na hali gani?
KATIKA karne zote za wakati, wanaume na wanawake wameihesabu kuwa heshima kubwa kutumikia kisa fulani kinachofaa, ambacho wameona kuwa bora.
2 Mamilioni wameona kutumikia utawala wa kisiasa ambao ndani yake wanaishi ni jambo lenye maana zaidi kuliko yote. Wale wanaokufa vitani kwa ajili ya taifa lao wanasemekana kuwa ‘wamejitoa sana.’
3 Pahali pa kutumikia mataifa yao tu, watu wengine wamejitoa watumikie wanadamu wote, bila kujali taifa au jamaa. Wametumia akili na mali zao hata kutoa afya na nguvu yao watumikie wanadamu, labda kuvumbua dawa za magonjwa, au labda kuletea maskini na wenye kuonewa faraja. Watu wamesifu wanaume na wanawake hao kama watu “wenye huruma” na “wafadhili.” Wameyakumbuka matendo na kujitoa kwa watu walio mashuhuri zaidi kati yao kwa kujenga makumbusho na kwa kutaja majengo makubwa ya watu wote au njia kuu kwa majina yao.
4 Hata hivyo, ijapokuwa utumishi wote huu, hakuna taifa juu ya uso wa dunia leo lisilopatwa na matatizo makubwa mno. Mataifa mengi yanatatizwa na uvunjaji wa sheria na rushwa, na taratibu za mengi yao ziko katika hali yenye hatari. Wanadamu wote wanaendelea kuwa jamii yenye ugonjwa, yenye kusumbuliwa na yenye kufa.—Mt. 9:36; Rum. 8:22.
5. Ni utumishi gani ambao wanafunzi wa kweli wa Kristo Yesu wanapendezwa nao, na wanaweza kusadikishwa kabisa juu ya nini?
5 Bila shaka Wakristo wa kweli wamepaswa wapendezwe sana na utumishi, kwa maana Ukristo ni utumishi. Lakini kama Mashahidi wa Yehova, utumishi unaotuhusu ni wenye heshima na wenye kufaa zaidi kuliko utumishi mwingine wo wote ambao wanadamu wangeweza kushiriki. Huenda utumishi huo ukatugharimu sana—wakati, jitihada, huenda ukatufanya tujinyime mambo fulani, ndiyo, unaweza hata kutugharimu maisha zetu. Hautatuletea sifa kutokana na ulimwengu; hakuna nyumba za ukumbusho zitakazojengwa wala barabara kutajwa kwa majina yetu ili kutuheshimu. Lakini ijapokuwa sababu zote hizi, sisi twajua hili: Unastahili hasara hizo. Ndiyo, twajua na tunasadiki sana kwamba tunaweza kushiriki utumishi ulio bora, ulio mzuri zaidi kuliko utumishi wote na utakaoleta faida iliyo kubwa zaidi na yenye kudumu zaidi kuliko zote, kwa watu wote. Utumishi huo ni utumishi ule wa Muumba wetu mkuu Yehova Mungu, utumishi mtakatifu kweli kweli. Kama “elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo,” ni hazina ya ajabu.—2 Kor. 4:6-10, 16-18.
SABABU GANI NI BORA?
6. Ni sababu gani moja inayoonyesha kwamba utumishi huo mtakatifu ni bora kuliko mwingine wo wote ambao tungeweza kushiriki?
6 Ni kwa sababu gani tuuone utumishi huu kuwa bora zaidi kuliko utumishi mwingine wo wote tunaoweza kushiriki? Kwanza, utasaidia watu wa jamaa, na mataifa yote waone utimizo wa mambo ambayo wanadamu wametamani katika, historia yote na wamekosa. kuyatimiza—dunia ya amani, na uhuru bila njaa, umaskini, magonjwa, uonevu. Zaidi ya hayo, unawasaidia watumainie jambo fulani ambalo watu wengi wangesita hata kutumainia—uhuru bila mauti yenyewe.—Rum. 8:18-21; Ebr. 2:15.
7-9. (a) Mwana wa Mungu alionyesha namna gani kwamba aliuona ubora wa utumishi huo mtakatifu ukilinganishwa na utumishi wa kilimwengu? (b) Jambo hili laonyesha namna gani sababu yenye nguvu kuliko zote ya kuona ubora wa utumishi huu kuliko utumishi mwingine wote?
7 Hakuna utawala wa wanadamu, hakuna jitihada yenye kuonyesha fadhili wala huruma inayoweza kuleta mambo haya. Bila Mungu na kusudi lake mambo haya hayawezi kuja kamwe. Ndiyo sababu,Mwanawe, Yesu Kristo, alikataa kukubali kuchaguliwa awe mfalme wa nchi yake mwenyewe na makutano ya watu wenye shauku walioona ana uwezo wa kufanya mema mengi katika njia yenye huruma. (Yohana 6:15) Ndiyo sababu alikataa pia toleo la kuwa na utawala wa serikali zote za dunia hii, kwa maana yeye aliyekuwa akitoa toleo hili alitaka Mungu asitumikiwe kabisa. Kwa kweli bei ya kukubali ilikuwa tendo la kumwabudu mtoaji wa toleo hili badala ya kumwabudu Mungu. Jibu la Yesu lilikuwa: “Kwenda zako, Shetani: kwa sababu imeandikwa, Uabudu Bwana Mungu wako, umutumikie yeye peke yake.”—Mt. 4:8-10, Biblia ya Kiswahili ya Zaire.
8 Bado humo mna sababu kubwa zaidi ya sisi kuthamini sana utumishi huu mtakatifu—kwa sababu ya Yeye tunayetolea utumishi huo. Watu wanaoishi chini ya falme hulihesabu kuwa jambo lenye maana sana na fahari wakiwekwa katika cheo ambacho wanaweza kusema kwa kujivuna hivi, “Mimi niko katika utumishi wa Mfalme.” Jinsi lilivyo jambo la maana zaidi kupita na lenye fahari zaidi kuweza kusema, “Mimi niko katika utumishi wa Muumba wa mbingu na dunia,Mungu Mkuu, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote!”
9 Ndiyo, zaidi ya uradhi wote tuwezao kupata kutokana na kujua jinsi utumishi wetu mtakatifu unavyofaidi na utakavyofaidi wanadamu, kuna uradhi wa kujua kwamba unaheshimu jina la Mungu Aliye Juu Zaidi. Kwa sababu ya matendo yote ya upendo ambayo amefanya zamani na yale atakayofanya wakati ujao, zaidi ya watu wote, yeye astahili utumishi wetu wa kujitoa na wa shukrani. Twadaiwa naye uhai na kila kitu tulicho nacho na kufurahia.—Zab. 104:1, 14, 15, 24.
10. Ni thawabu gani yenye maana sana imepaswa ituvute kwenye utumishi huo mtakatifu?
10 Katika kuona ubora wa utumishi wetu, Mungu anatuahidi—si majengo ya ukumbusho ambayo mwishowe huharibika—bali uzima, uzima katika taratibu mpya yenye haki ya amani, afya na furaha. Anaahidi kuokoa mkutano mkubwa usiohesabika wa watu kutoka mataifa yote na jamaa katika dhiki kubwa inayokaribia mbio kisha kuwaingiza katika taratibu mpya ambayo yeye mwenyewe atafanya. Mtume Yohana alipendelewa kuona katika njozi wale watakaookoka kisha akaandika habari zao katika Ufunuo 7:14, 15: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake.”
11, 12. (a) Nani leo wanaojidai kutoa utumishi mtakatifu? (b) Ni hali gani zinazofanya dai hilo kuwa lenye mashaka?
11 Twawezaje kuwa na hakika kwamba tunatoa utumishi mtakatifu wa kweli unaokubaliwa na Mungu? Sasa karibu watu bilioni moja wamejiandikisha katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Wanajiona kuwa wanamtumikia Mungu wa Biblia. Mamilioni ya Wayahudi wa asili waliotahiriwa wanahudhuria masinagogi—yao na kuunga mkono waalimu wao wa Kiyahudi na wanajiona wanafuata njia ya kweli ya kumwabudu Mungu. Mabilioni wengine wanaitumikia miungu ya dini zisizo za Kikristo kuzunguka ulimwengu.
12 Kweli, lakini tunapotazama hali za kidini leo na hali ya adili iliyomo katika kila nchi, yatupasa tuulize kama maoni yao ni yenye makosa. Ushuhuda uko wapi wa kuonyesha kwamba wamejitakasa kwa imani katika “damu ya Mwana-Kondoo” wakautwaa uanafunzi unaokamatana na imani? Je!wamejitenga na ulimwengu na kuwa bila kutiwa madoa na uasherati, kusema uongo, kuiba, na je! wanasaidia wengine wafahamu Neno la Mungu, wakisaidia wanafunzi wapya wamtolee Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote utumishi mtakatifu?—Yohana 15:27–16:3; Matendo 24:13, 14.
13, 14. Sababu gani ni jambo la maana sana kujua ulio utumishi mtakatifu, na ni nini usio utumishi mtakatifu?
13 Sote twahitaji kujua jibu sahihi, kwa kuwa, ikiwa watu hawa wa dini wamekosea, matokeo ya mwendo wao yaweza kuwa yenye kukatisha tumaini sana. Ushuhuda ni kwamba matokeo hayo yataonekana wazi upesi.
14 Katika taabu ile inayokuja Yesu Kristo hatapendelea na kulinda wo wote wasiomtolea Mungu utumishi mtakatifu wa kweli kama alivyofanya. Yeye alisema: “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza. mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mt. 7:22, 23) Utumishi wenye makosa si utumishi mtakatifu kweli na siyo njia ya kuokokea dhiki kubwa inayokaribia itakayotangulia taratibu mpya yenye haki.
KUJUA MAANA YA UTUMISHI MTAKATIFU
15, 16. Neno la Kigiriki linaloonyesha ‘kutoa utumishi mtakatifu (la·treuʹo) linatofautiana namna gani na neno linaloonyesha ‘kuhudumia’ (di·a·ko·neʹo)?
15 Biblia yatupa njia ya kujulia utumishi mtakatifu ulivyo utakaoleta kibali na ulinzi wa Mungu. Neno la Kigiriki ambalo Yesu alitumia katika kupinga kishawishi ni neno linaloonyesha kitendo (verb) la·treuʹo. Neno hili ni tofauti na lile la Kigiriki di·a·ko·neʹo, linalotafsiriwa “kutumikia” katika tafsiri nyingi. Tofauti ni nini?
16 Ijapo maneno yote mawili yanamaanisha utumishi, di·a·ko·neʹo linaweka mkazo juu ya kawaida ya utumishi unaotolewa. Kwa sababu hiyo, linatumiwa kwa kawaida kumaanisha utumishi ambao mtu mmoja anatolea watu wengine. Lakini la·treuʹo, kama linavyotumiwa katika Maandiko, linamaanisha utumishi unaotolewa tu kwa Mungu, au, mara chache, utumishi unaotolewa kwa ile inayodhaniwa kuwa miungu miungu ya uongo.—Matendo 7:42; Rum. 1:25.
17, 18. (a) Ni maana gani inayotolewa na mtume Paulo juu ya utumishi mtakatifu uliofanywa katika nyakati zilizotangulia Ukristo? (b) Je! utumishi mtakatifu wa Wakristo unapaswa utolewe mahali fulani au utolewe na jamii ya pekee tu ya watu katika kundi?
17 Biblia yafunua kwamba utumishi mtakatifu unaotolewa kwa Mungu wa kweli duniani haukutokana na Kristo Yesu na mwanzo wa Ukristo. Mtume Paulo aonyesha hili anapoandika—katika Waebrania 8:5 juu ya makuhani Waisraeli kama wale “watumikiao mfano na kivuli cha mambo ya mbinguni,” walipotumikia katika hema, wakimtolea Mungu dhabihu.—Ebr. 9:1, 6; 10:2; 13:10.
18 Basi, utumishi mtakatifu wa Wakristo unapaswa utolewe mahali fulani pa pekee tu, au utolewe na jamii ya pekee ya watu au kikundi cha ukuhani wa Israeli tu? Sivyo, kwa maana hata miongoni mwa Waisraeli wale waliotakiwa kufanya utumishi hawakuwa wale waliowekwa watumikie katika hema tu. Lilikuwa pendeleo na wajibu wa jamii nzima ya Israeli kushiriki utumishi huo.—Kut. 3:12; Matendo 7:6, 7; Rum. 9:4.
19, 20. Ni kwa sababu gani mtume Paulo aliweza kusema kwamba kabila kumi na mbili za Israeli zilikuwa zikimtumikia “Mungu kwa bidii mchana na usiku” katika siku zake?
19 Alipokuwa akihukumiwa mbele ya Mfalme Agripa, mtume Paulo alisema kwamba katika wakati ule ule, si kabila la Lawi pamoja na ukuhani wa Haruni tu bali ‘kabila kumi na mbili’ za Israeli wa asili zilikuwa bado zikitaraji kuufikia utimizo wa ahadi ya Mungu aliyowapa baba zao. Na walikuwa wakionyesha tumaini hili namna gani? Katika Matendo 26:7, Paulo alisema kwamba walikuwa wakionyesha hili kwa kumtumikia “Mungu kwa bidii mchana na usiku.” Walifanya hivi namna gani?
20 Ana nabii mke alikuwa mmojawapo wa wale, ambao, kulingana na Luka 2:37, NW, “alikuwa hakosi kamwe kwenda [wapi?] kwenye hekalu, kutoa utumishi mtakatifu usiku na mchana [kwa njia gani?] kwa kufunga na kuomba.” Alipatikana sikuzote na kwa kawaida akifanya utumishi wote wa hadhara katika hekalu. Si Wayahudi wote walioishi Yerusalemu, hivyo, hawakuweza kupatikana mara nyingi sana katika hekalu. Lakini Wayahudi katika Israeli wote waliweza, na wengi wao walitumikia “mchana na usiku,” kama Paulo alivyosema, kwa kuonyesha bidii kwa agano la Torati na maamuzi yake, kwa kutoa sehemu ya kumi ya mazao yao kwa utumishi wa hekaluni, kwa dhabihu na kwa sala ya asubuhi na sala ya jioni, pia kwa kuhudhuria kwa kawaida katika masinagogi ambako Neno la Mungu lilizungumzwa.a
21, 22. Sababu gani leo utumishi mtakatifu hautegemei agano la Torati na dhabihu zake?
21 Je! leo utumishi mtakatifu kwa Mungu wategemea agano hilo la Torati na dhabihu zake? Sivyo, kwa maana kama mtume alivyosema yote haya yalikuwa “mfano na kivuli cha” mambo makubwa zaidi yatakayokuja. (Ebr. 8:3) Na katika Waebrania 9:9, 10 alisema kwamba dhabihu hizo katika hema zilikuwa “sheria za jinsi ya mwili tu, . . . zilizoamriwa hata wakati wa matengenezo mapya.”—Linganisha Wafilipi 3:3.
22 “Wakati wa matengenezo mapya” ulikuja pamoja na Kristo Yesu. Alikitimiza “kivuli” cha Torati. (Ebr. 10:1-4) Kama Mwana-Kondoo wa Mungu “alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa,” akitoa uhai wake kama dhabihu, isiyohitaji kufanywa tena. Na, kama mtume anavyoeleza katika Waebrania 9:14, ni damu ya Kristo iliyomwagwa ‘inayoweza kusafisha dhamiri zetu na matendo mafu, tupate kumwabudu Mungu aliye hai,’ kwa sababu ya imani yetu.
MFANO WA UTUMISH! MTAKATIFU WA KIKRISTO
23. Sababu gani utumishi mtakatifu uliotolewa na Wayahudi wengi usiku na mchana haukuwaletea ulinzi wa kimungu wakati Yerusalemu ulipoanguka?
23 Ule utumishi wa usiku na mchana ambao wengi sana kati ya Wayahudi katika siku za Paulo walikuwa wakitoa haukuwapatia ulinzi wa kimungu na wokovu wakati wa dhiki kali iliyoujia Yerusalemu katika karne ya kwanza, dhiki iliyotabiriwa na Mwana wa Mungu. Kwa sababu gani sivyo? Paulo alisema kwa habari zao hivi: “Wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa.” (Rum. 10:2) Walikosa kujua kwamba unabii wa Biblia ulikuwa ukitimizwa katika Kristo Yesu na kufahamu kwamba kupitia kwa yeye Mungu alikuwa akiweka sasa kanuni ya kumtolea Yeye utumishi wote mtakatifu wa wakati ujao. Walikosa kufahamu uhakika wa kwamba moyo ndilo jambo kubwa la kumpendezea Mungu wakaacha mioyo yao isiitikie uongozi wa Mungu. (Kum. 10:12-14, 16; Mt. 15:8) Ikiwa twataka kuepuka matokeo mazito yaliyowapata kwa sababu hii ni lazima tujifunze kadiri tuwezavyo sasa juu ya Mwana wa Mungu ili utumishi wetu kwa Mungu ukubalike.
24, 25. (a) Kristo Yesu aliweka kanuni ya utumishi mtakatifu katika njia gani mbalimbali? (b) Ni katika njia gani alionyesha watu huruma?
24 Kwa habari ya kuja kwake duniani, Yesu Kristo alisema hivi: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.” (Yohana 18:37) Aliishuhudia kweli kwa kusema bila kuogopa, miaka ya mwisho mitatu na nusu ya maisha yake ilikuwa yenye shughuli za kutangaza habari njema za ufalme wa Mungu katika Israeli wote. Lakini haikumtosha kusema tu juu ya kweli. Ilimpasa aifuate. Ilimpasa aonyeshe Neno la Mungu kuwa la kweli kwa kutenda mambo yote ambayo Neno hilo lilitabiri juu yake na kuishi maisha ambayo yangewezesha wanadamu wajue na kumfahamu Baba yake na njia na kanuni za Baba yake. (Yohana 1:14, 18) Aliangalia mwenendo wake wote ili jina la Mungu lisilaumiwe, alilotakasa sikuzote kuliko mambo yote.—Mt. 6:9.
25 Yesu alihurumia sana watu wa siku zake kama Baba yake. Biblia yasema kwamba “alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Aliwafariji kwa habari njema za Ufalme. Yeye hakuwa mtu aliyezungumza au akatoa hotuba tu bali alitendea watu matendo yenye fadhili za kibinadamu. Alipokwisha kusema na makutano makubwa yaliyokuwa yamekuja kumsikia,alisema: “Nawahurumia mkutano kwa sababu yapata siku tatu wamekaa nami, wala hawana kitu cha kula; nami nikiwaaga waende zao nyumbani kwao hali wanafunga, watazimia njiani.” Ndipo akawalisha kwa mwujiza. (Marko 8:2, 3) Wakati mwenye ukoma aliposema kwa imani Yesu amponye kama angetaka, Yesu alisema: “Nataka,” akamponya mara hiyo.—Marko 1:40, 41.
26. Hasa ni nini lililokuwa kusudi la matendo haya ya Yesu yenye huruma?
26 Ni kwa sababu gani Yesu alitenda kazi hizi ili aondolee watu mateso? Je! ni kwa sababu ya kuhurumia au kufadhili watu tu? Sivyo, alitenda mambo haya mema ya kimwili ili uweko msingi kwa watu waamini habari njema kuwa zimetoka kweli kwa Mungu. Hakuelekeza kwenye maneno yake tu bali kwenye kazi kama ushuhuda wa kwamba kweli alikuwa mjumbe wa Mungu. Kama hakuonyesha kwa kazi zake kwamba alikuwa na sifa za Mungu ambaye alikuwa akitaka watu wamjue, watu wangemkubali kama Masihi kwa sababu gani?—Yohana 10:37, 38.
27. Kama tunaona ubora wa pendeleo hili la utumishi mtakatifu, azimio letu limepaswa liwe nini sasa?
27 Ili utumishi wetu kwa Mungu ukubalike, yatupasa tufuate mfano wake. Tukijua faida kubwa sana inayoweza kutokana na kutumia maisha zetu katika njia hii, na tuendelee tukiwa imara tuone kwamba Mungu anatutegemeza katika shida au upinzani wo wote unaoweza kutokea. Mungu na asikie sala yetu, kama sala ya Zekaria, apate “kutupa sisi pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu bila kuogopa kwa ushikamanifu na haki mbele zake siku zetu zote tukisha kuokolewa mikononi mwa adui.”—Luka 1:74, 75, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari ya maneno ya Paulo katika Matendo 26:7, The Pulpit Commentary chasema hivi: “Kutumikia (latreuon), yaani, kutumikia kwa ibada, sala, dhabihu, na kadhalika.”