Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 2/15 kur. 87-91
  • Kutoa Utumishi Mtakatifu Usiku na Mchana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoa Utumishi Mtakatifu Usiku na Mchana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MWENDO WETU WOTE WA MAISHA NI UTUMISHI MTAKATIFU
  • Kuona Ubora wa Hazina ya Utumishi Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Utumishi Mtakatifu Katika Huu “Wakati wa Mwisho”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Wakristo Hupata Furaha Kutumikia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kutoa Utumishi Mtakatifu Kama Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 2/15 kur. 87-91

Kutoa Utumishi Mtakatifu Usiku na Mchana

“Mungu ninayetolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na habari njema juu ya Mwanawe.”​—Rum. 1:9, NW.

1, 2. Biblia inaonyesha namna gani kwamba ziko dhabihu (sadaka) zinazotiwa ndani ya utumishi wetu mtakatifu tunaomtolea Mungu?

LEO watumishi wa Mungu hawatakiwi kutoa dhabihu kulingana na agano la Torati ambalo Kristo Yesu alitimiza na ambalo Mungu aliondoa. Lakini ziko dhabihu ambazo ni sehemu ya maana ya utumishi wetu mtakatifu. Ni dhabihu gani?

2 Paulo mtume wa Kristo Yesu anatuonyesha katika Waebrania 13:15, 16. Akiisha kuzungumza juu ya utumishi mtakatifu uliofanywa na makuhani wa Israeli katika hema na namna Yesu alivyoutimiza huu, Paulo asema hivi: “Kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.”

3. Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na Mungu katika Waebrania 13:15 yanatutaka tufanye nini?

3 Jambo hilo lina maana gani kwetu? Lina maana kwamba imetupasa tutake kuizungumza kweli juu ya Yehova Mungu na juu ya habari njema za Ufalme wake. Imetupasa tuwe tukifanya hivi si mara tu, mwishoni mwa juma wala siku za mikutano tu, bali “daima” (sikuzote)​—kila siku, usiku na mchana, kuwa waangalifu kupata nafasi za kufanya hivi, kama asemavyo mtume.

4. Je! utumishi wetu mtakatifu unafanywa kwa midomo yetu tu? (1 Yohana 3:18)

4 Je! hiyo ina maana kwamba utumishi wetu mtakatifu ni kuzungumza tu? Sivyo, kwa maana akiisha kusema juu ya “dhabihu ya sifa,” mtume anaendelea kusema juu ya dhabihu nyingine ambazo Mungu ataka tutoe. Katika mstari wa 16 anasema hivi: “Lakini msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizi ndizo zimpendezazo Mungu.” Ndiyo, utumishi wetu mtakatifu wahitaji usawazike, unaosawazisha maneno na matendo, unaosawazisha sifa na “kutenda mema na kushirikiana” na wengine.

5. (a) Maisha yetu yote yanaweza kushuhudia habari njema namna gani? (b) Huku kutatokeza nini kwa wengine katika mtaa wetu?

5 Basi, twataka maisha yetu yote yawe ushuhuda wa kweli kama Yesu. Kweli, sisi hatuwezi kufanya miujiza kama Yesu ili kusaidia watu, lakini mwenendo wetu mwema, uaminifu, unyofu wa moyo na kusaidia watu wakati tunapoweza na kwa kile tulicho nacho hukubalika. Tunaweza kufanya kama Wagalatia 6:10 linavyosihi: “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” Kwa mwendo huu tunawekea watu msingi wa kufungua masikio yao waisikie kweli. Basi, haitupasi kuacha kutangazia wote habari njema, ‘yaijazayo mioyo yetu’ bila kusita na bila kuogopa. Bila hivyo, watu wanaotazama matendo yetu mema na maisha yetu mema watasaidiwaje? Yatupasa tujulishe watu kwamba ni habari njema za Mungu ndizo zimetuongoza tutende matendo mema. (Mt. 5:16; 12:34, 35) Ndipo watakapojua kwamba kuna uwezekano wa kuwa kama sisi, ikiwa nao wanazijua habari njema. Tusipokuwa na matendo mema, yenye msaada na fadhili pamoja na mwenendo mwema na pia “dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake,” hatumtolei Mungu kabisa utumishi mtakatifu.​—Ebr. 13:15.

6. Basi, ni jambo gani linalotakiwa ili utumishi wetu mtakatifu ukamilike?

6 Basi, kwa mfano wa Yesu na ule wa mitume ni wazi kwamba utumishi wetu mtakatifu si kugeuza nyutu zetu tu na kutenda mambo yenye fadhili. Hii ni sehemu, msingi, wa utumishi wetu, tunaoongezea dhabihu ya sifa. (Zab. 106:12) Bila kuishi na kutangaza habari njema hatuwezi kukamilika.

7. Ni nani anayeamua kadiri ya wakati ambao tutatumia katika dhabihu mbalimbali zinazokuwa utumishi wetu mtakatifu?

7 Sisi sote leo twaweza kujionyesha kuwa kati ya wale wanaomtolea Mungu utumishi mtakatifu mchana na usiku. Yehova Mungu hakutuwekea sheria yo yote ya kuamuru kadiri ya wakati tunaopaswa kutumia katika kutoa dhabihu ya sifa (isipokuwa kusema “daima”) wala kadiri ya wakati wa kutumia katika dhabihu nyingine ambazo Mungu anapendezwa nazo sana. Inatupasa sisi wenyewe tusawazishe hili. Lakini dhabihu hizi zote​—tunda la midomo yetu linalotangaza jina lake na kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine​—haya yote yapaswa yaweko na kuonekana katika maisha zetu, katika nyakati za mchana na katika nyakati za jioni.​—Linganisha Matendo 26:7.

8. Ni mfano gani wa utumishi wa “usiku na mchana” ambao Yesu alituwekea? (Marko 1:35; Luka 6:12)

8 Yesu alizifikiria habari njema na aliona namna angeweza kutolea watu ujumbe huo. Yeye alikuwa tayari sikuzote, “usiku na mchana,” asimulie habari njema, hata alipokuwa amechoka sana. Sikuzote alikuwa mwenye bidii ya kuitangaza kweli. (Yohana 2:17) Kumbuka alivyozungumza na mwanamke, Msamaria, ambaye Wayahudi walidhani hawezi kuthamini mambo matakatifu. (Yohana 4:7-26) Lakini Yesu hakumlaumu mwanamke yule, ijapokuwa alijua pia kwamba alikuwa mwasherati. Ushuhuda wake aliompa mwanamke huyo ulitokeza tangazo la ajabu na lenye kuenea pote la jina na makusudi ya Mungu.​—Yohana 4:39-42.

MWENDO WETU WOTE WA MAISHA NI UTUMISHI MTAKATIFU

9. Kwanza utumishi wetu mtakatifu unatia ndani nini, na maandishi ya Paulo yaliyoongozwa na Mungu yanaonyesha hili namna gani? (Kol. 3:17)

9 Basi, utumishi mtakatifu si jambo linalochukua kisehemu kidogo tu cha maisha zetu. Hautii ndani utendaji mmoja tu, wala matendo fulani, bali kila sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Kwa kifupi. unamaanisha ‘kufanya mambo yote kama kumfanyia Yehova,’ katika kula ama katika kunywa ama kutenda jambo jingine lo lote. (1 Kor. l0:31) Akionyesha namna utumishi huu umepaswa kutia ndani mambo yote, mtume anasema katika Warumi 12:1, 2, NW hivi: “Nawasihi kwa huruma za Mungu, ndugu, mtoe miili yenu dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu yenu ya akili. Na mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo.”a

10. (a) Ni nini linaloamua kama utendaji wo wote ni sehemu ya utumishi wetu mtakatifu au sivyo? (b) Ni utumishi gani wa “usiku na mchana” ambao Neno la Mungu linawataka wazazi wafanye, nao waone hili namna gani?

10 Mambo mengi yanatiwa ndani, lakini shabaha yako, mradi wako na kusudi lako la moyo ndizo sababu kubwa za kuamulia kama unalofanya kweli ni “utumishi mtakatifu” ama sivyo. Kwa mfano, katikati yetu wako wazazi wengi. Kwa kweli, sehemu kubwa ya utumishi wenu mtakatifu kwa Mungu inatia watoto wenu. Zaburi 127:3 yasema kwamba watoto “ndio urithi wa [Yehova].” Je! wewe wauangalia urithi huo kana kwamba ni wake na kwa utukufu wake? Hii pia ni sehemu ya utumishi wako wa “usiku na mchana,” kwa maana Neno la Mungu laeleza kwamba imewapasa wazazi wawe wakitia kanuni njema za Mungu katika watoto wao tangu wanapoamka mpaka wanapolala. (Kum. 6:4-9) Ili kufanya hivi, jambo la kwanza ni kujifunza Biblia pamoja nao. Lakini mzazi asijisemeshe hivi, ‘Mimi najifunza Biblia kila juma na watoto wangu, kama ninavyojifunza na watu wengine. Kwa hiyo inatosha kwao kujua yaliyo mema na kufuata kanuni za Biblia.’ Hii si kweli. Kumbuka, Biblia yasema kwamba watoto wako Wanaonwa na Mungu kama “watakatifu.” (1 Kor. 7:14) Ungekitendeaje kitu ulichoachiwa utunze ulichojua kilikuwa kitakatifu kwa Mungu? Je! hungekilinda kwa uangalifu sana kila siku, mchana na usiku?

11. Ni kwa sababu gani sehemu hii ya utumishi mtakatifu isiachwe kutimizwa na wazazi?

11 Unalofanya sasa ili ufundishe na kuadibisha watoto wako laweza kuwaokoa. Kwa upande mwingine, ukifanya ulegevu (uvivu) sasa, utawapoteza. Yaani, utakuja wakati ghafula​—kabla ya wewe kujua​—​maneno yako yatakapokosa kusikiwa. Ulimwengu utawavuta zaidi kuliko wewe. Halafu, Mungu ataonaje namna umetendea mali iliyo takatifu kwake?

12, 13. (a) Wazazi wanaweza namna gani kutimiza kwa hekima na kwa kufaa maneno yenye kutia moyo katika Kumbukumbu la Torati 6:4-9? (b) Ni kwa sababu gani haitatosha wazazi wa Kikristo wawe na “mtoto mzuri” tu kama yalivyo maoni ya kilimwengu? (Mit. 3:1-4)?

12 Kutia Neno la Mungu katika watoto siku kutwa hakuna maana ya kuwashauri-shauri kila mara. Kunataka uonyeshe mfano wa namna kweli ya Mungu ilivyo kwa maisha na maongezi yalo ya kila siku. Kila pindi, ama kwa uhusiano wako wa upendo na wa karibu sana pamoja nao na kwa ushirika wako wa kirafiki na wa karibu sana na kupashana habari bila kusita, unaweza kuwasaidia wamfahamu Yehova Mungu, hekima yake, upendo wake na usahihi wa njia zake. Wasikilize, zungumza nao kwa kuwaeleza sababu. Unapotoa maagizo au kuwapa kazi ya kufanya, au unapotoa adabu, onyesha sababu, na kueleza matokeo mema ya kukutii wewe kama mzazi na, hivyo, matokeo mema ya kumtii Mungu kama Kichwa juu ya wote.

13 Huwezi kujaribu kuwa na “mtoto mzuri” katika maana ambayo ulimwengu unatumia neno hilo. Bila shaka wataka mtoto wako awe mwenye adabu, mwenye staha, mnyofu na mwenye kufikiria wengine. Lakini wamtaka awe hivyo kwa sababu, zaidi ya yote mtoto wako amemjua na kumpenda Yehova Mungu. Ili kulea mtoto wako kuwe tofauti na kulea vijana wa ulimwengu, na kuwa utumishi mtakatifu kweli kweli, ni lazima akili na moyo wa mtoto vielekezwe kwa Yehova, ili awe msifaji wa Yehova.​—Zab. 148:12, 13.

14. Waume na wake wanaweza namna gani kutoa utumishi mtakatifu kupitia kwa mpango wa ndoa?

14 Waume na wake wanaweza kutoa utumishi mtakatifu kwa kufanya ndoa yao iwe na matokeo mazuri na kuwa heshima kwa Mungu aliyeanzisha ndoa. Huenda mwanamume au mwanamke ni mwenye huruma na mtu mzuri kwa wengine, anavumilia makosa yao hata anavumilia matusi na mambo mabaya kutoka kwao bila kulipa kisasi. Lakini akiwa mwenzi wa ndoa, mume au mke anakuwa mwepesi wa hasira, anatafuta makosa kwa kila analosema mwenzi wake kwa moyo wa kutaka ugomvi, akitafuta sababu ya kulaumu. Au huenda mume na mke wakaacha kusemezana. Bila kujali mambo mengine ambayo mtu aliyeoa au kuolewa anafanya, ikiwa anapuza mapatano matakatifu ya ndoa, hamtolei kabisa Mungu utumishi mtakatifu unaokubalika.​—Efe. 5:22-25, 29.

15. Mke wa nyumbani anaweza kutoa msaada gani wenye nguvu ili kueneza habari njema katika mtaa wake?

15 Wake wana nafasi nzuri ya kumtolea Mungu utumishi mtakatifu unaokubalika. Kazi zao nzuri ambazo wengine wanaweza kuona zingetia ndani bila shaka kupamba vizuri na kusafisha nyumba, kupika chakula na kununua na kufua nguo za jamaa. Kwa maana kinachotazamwa zaidi na wengine ni nini kuliko nyumba ya mtu? Ukaribishaji-wageni wa mke, utayari wake wa kusaidia jirani zake, hasa nia yake ya kujitolea kusaidia akina dada wengine katika kundi katika mahitaji yao yo yote​—hizi ndizo dhabihu (sadaka) ambazo Mungu anapendezwa nazo sana. Watu wanapojua mambo haya juu yake, ndipo kutangaza kwake habari njema hadharani katika eneo la kundi kutakuwa na matokeo yenye nguvu.​—Matendo 9:36-41; Tito 2:4, 5.

16. Watoto na vijana wanaweza namna gani kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kila siku kwa matokeo mazuri?

16 Ikiwa watoto katika jamaa wanapendezwa sana kumtolea Yehova utumishi mtakatifu wanaweza kuonyesha heshima kwa baba yao na kumsaidia mama amletee Mungu heshima kwa kuwasaidia waitunze nyumba katika utaratibu mzuri na safi. Na ikiwa wazazi hawako katika kweli watoto wanaweza kusaidia sana katika njia hii wawajulishe wazazi wao Mungu. Mwenendo wao mbele ya wanashule wenzao, kuheshimu waalimu, kuwaambia wengine habari njema wakati nafasi inapopatikana nakushirikiana na kundi katika mambo yanayofanywa katika Jumba la Ufalme na kushiriki utumishi wa shambani, ndiyo mambo ambayo Mungu anahesabu kuwa utumishi mtakatifu kwake bila shaka. (Mit. 20:11; Tito 2:6-8) Unaweza kujiuliza ulizo hili ili uone kama utumishi wako ni utumishi mtakatifu wa kweli: ‘Je! mimi naenda katika utumishi wa shambani, labda kupelekea wengine vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia’? Hilo ni jambo lenye kusifika. Lakini, basi, jiulize tena: ‘Shuleni na mahali kwingine, mwenendo wangu uko namna gani? Je! mimi nafanya wanayofanya vijana wa ulimwengu? Au nakumbuka kwamba yanipasa nimtolee Yehova utumishi mtakatifu usiku na mchana?’ Unaweza kuwavuta sana watu wapendezwe na habari njema kwa mwenendo na moyo wako mzuri wa kila siku kama wengine.

17. Ni utumishi gani ambao wazee wanatakiwa wafanye?

17 Wazee wa Kikristo vilevile wanatakiwa kutumikia usiku na mchana. Sehemu ya utumishi wenu mtakatifu ni kutumikia ndugu zenu, kuwatimizia mahitaji yao ya kiroho. Mtume Paulo aliweza kuwaambia wazee wa kundi la Efeso hivi: “Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi.” (Matendo 20:31) Ndugu zenu leo wanahitaji msaada wenu kama wale ndugu katika Efeso karne ya kwanza walivyohitaji msaada wa Paulo.

18-21. (a) Utumishi mtakatifu wa Paulo wa mchana na usiku ulikuwa na nini ndani yake? (b) Ni kwa sababu gani kazi yake ya kimwili ilifaa kama sehemu ya utumishi wake mtakatifu kwa Mungu, na hapa tunawekewa mfano gani?

18 Je! mnaweza kufanya alilofanya Paulo, kutumikia mchana na usiku? Maneno ya Paulo hayana maana kwamba alitumia kila dakika akizungumza au kuhubiri. Sivyo, kwa maana katika Matendo 20:34 anaendelea kutaja namna alivyofanya kazi kwa mikono yake mwenyewe akifanya kazi ya kimwili apate mahitaji yake mwenyewe ya kimwili na ya wale waliokuwa wakifanya kazi pamoja naye. Hasa, alipokuwa akiwaandikia Wathesalonike, alisema hivi: “Mnakumbuka taabu yetu na masumbufu yetu: kwa kuwa mchana na usiku tulifanya kazi tusije tukamlemea mtu wa kwenu awaye yote, tukawahubiri hivi Injili ya Mungu.”​—1 The. 2:9.

19 Ndiyo, Paulo alikuwa akifanya kazi ya kimwili, kama ile ya kutengeneza hema, mchana na jioni pia. Lakini ni jambo la maana tuulize: Ni kwa sababu gani alifanya hivi? Je! ilikuwa kwa sababu za kupenda mno vitu vya kimwili au kutamani vitu vya anasa? Sivyo, lakini kama mwenyewe alivyosema, ‘asije akawalemea’ ndugu zake. Aliweka mfano wa hili kusiwe mtu wa kumshtaki kuwa anaishi maisha yasiyo na jasho kwa kusaidiwa fedha na wale ambao alikuwa akipelekea habari njema. Kwa sababu kusudi na shabaha yake ilikuwa kuendeleza kweli na kuondoa vizuizi vyo vyote katika akili za wale aliotumikia, aliweza kusemekana kuwa alikuwa akifanya utumishi wa Mungu hata wakati wa saa hizo za kazi ya kimwili. Namna gani kama kusudi lake lingekuwa la kichoyo, kama hangekuwa akifanya mambo yote kama kwa Yehova na kwa kuendelezwa kwa faida za Ufalme? Hapo kazi yake isingalikuwa tofauti na kazi nyingine yo yote ya kimwili. Usingalikuwa utumishi mtakatifu.

20 Walakini, kwa vile Paulo alikuwa na dhamiri safi na kusudi jema katika kazi yake ya kimwili, aliweza kuifanya sehemu hii ya utumishi wake mtakatifu kwa Mungu ipatane na agizo alilopewa na Mungu kwa kuzitangaza habari njema kwa ujasiri mkubwa na bidii. Na utumishi huo mtakatifu ulibarikiwa sana na Mungu. Kama Paulo alivyosema, katika andiko letu la kichwa: “Mungu, ninayetolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana [na nini?] na habari njema juu ya Mwanawe.” (Rum. 1:9, NW) Bila shaka yatupasa sote tustaajabie matokeo makubwa ya jitihada za uaminifu za Paulo za kumtolea Mungu utumishi mtakatifu.

21 Kwa hiyo, ni lazima kila mmoja wa sisi ajiulize mwenyewe, Maoni yangu juu ya kazi yangu ni nini na shabaha yangu ni nini? Jibu la busara peke yake lapatikana katika shauri ambalo mtume alimpa kijana Timotheo: “Ujizoeze kupata utauwa [kama shabaha yako]. Kwa maana . . . utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.”​—1 Tim. 4:7, 8.

22. Tunatimiza kusudi gani la namna mbili kupitia kwa utawa wetu?

22 Ndiyo, shabaha kubwa ya utawa wetu ni kumtolea Yehova utumishi mtakatifu na kuheshimu jina lake, kusaidia wengine katika njia hiyo wafahamu namna Mungu alivyo waje katika uhusiano wa karibu sana naye. Lakini kwa kufanya hivi sisi pia twaishi kwa furaha zaidi hata sasa, katika wakati huu, Na kunamaanisha ‘uzima ule utakaokuwapo baadaye,’ si kwetu peke yetu, bali pia kwa jamaa zetu na kwa ‘wote wanaovutwa na mwenendo wetu na tangazo letu la habari njema.

23, 24. Ni nini linalotutia moyo tuendelee kujijaribu wenyewe tuone kama utumishi wetu mtakatifu ni wa kweli?

23 Kwa habari ya ‘uzima ule utakaokuwapo baadaye,’ na hata zaidi, nafasi ya kuwa na maisha yenye kuendelea tangu sasa mpaka milele, njozi ya mtume Yohana juu ya mkutano mkubwa utakaookoka ni yenye kutia moyo ‘tujijaribu wenyewe kwamba tumo katika imani,’ tuhakikishe tuone kama kweli tunatoa kabisa utumishi mtakatifu. (2 Kor. 13:5) Ndiyo, Mungu anatutolea tumaini lenye kuthawabisha la kuwa sehemu ya mkutano huo mkubwa usiohesabika atakaohifadhi katika dhiki kubwa inayokuja na kuingiza katika taratibu yake mpya.

24 Lo! tumaini gani la ajabu lililowekwa mbele yetu kwa kufanya tu jambo linalofaa, jambo lenye busara na lenye kupendeza sana! Ndiyo, karibuni kila mtu duniani atakuwa akimtolea Mungu utumishi mtakatifu, tena lo! jinsi dunia itakavyokuwa paradiso ya kweli wakati huo!

25. Imetupasa tuwe tukifanya nini hata sasa ili tuje tuokoke dhiki kubwa inayokaribia?

25 Ikiwa tutakuwa kati ya wale watakaookoka uharibifu wakati wa dhiki kubwa, sasa hivi yatupasa tuwe tukifanya lile ambalo Yohana aliona mkutano mkubwa ukifanya baada ya kupita dhiki hiyo. Walikuwa “wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” (Ufu. 7:10) Si kwa kusita, si kwa mashaka, bali kana kwamba “kwa sauti kuu,” tukiongozwa na uhakika na kwa upendo wa moyo wote na kujitoa kwa nafsi yote​—ndivyo tunavyotaka tutangaze waziwazi jina la Yehova Mungu na mambo yote bora linalo yafananisha na ahadi zote zenye utukufu zinazotegemezwa na jina hilo. Twataka tuwe tukimsifu Yehova na Mwanawe “sikuzote,” sisi kwa sisi katika nyumba zetu, penye mikutano yetu, na kwa wote watakaosikiliza katika mtaa wetu au po pote tulipo. Na tukifanya hivi, majeshi yote ya kimbinguni, ambayo “sikuzote huutazama uso wa Baba [ya Kristo],” yatatutegemeza sana, yakisema “Amina” kwa tangazo la habari njema tunalotoa kama sehemu ya utumishi wetu mtakatifu wa kweli tunaomtolea Mungu.​—Mt 18:10; Ufu. 7:12.

26. Ni nini kinachovuta maelfu ya watu duniani pote wamtafute Yehova leo, na huku kunatuletea sababu gani ya kufurahi?

26 Utumishi mtakatifu unaotolewa na watu wa Yehova ndio unaovuta maelfu waje kwake leo. Wanaona hali yenye upendo na msaada, usafi, ukamilifu wa kweli, utulivu, mahubiri yenye bidii ya Mashahidi wa Yehova. Kisha wanasikia na kuongozwa kuzisikiliza habari njema ambazo watumishi wa Mungu wanatangaza kwa bidii. Kwa njia hiyo Yehova Mungu anatukuzwa sasa na bado atatukuzwa kwa uzuri mkubwa zaidi katika dunia yote, akisifiwa sana na waokokaji wenye kushukuru wa dhiki​—yote haya, yakiwa matokeo mema na yenye furaha ya kumtolea Mungu kweli kweli utumishi mtakatifu mchana na usiku.

​—Kutoka The Watchtower, Oct. 1, 1976.

[Maelezo ya Chini]

a Kikieleza juu ya matumizi ya kiarifa la·treuʹein (kutoa utumishi mtakatifu), Theological Dictionary of the New Testament kinasema: “Matumizi yenye maana nyingi ya latreuin kuonyesha mwenendo wote wa wenye haki kuelekea Mungu yanapatikana katika Lk. 1:74,” “.  .  . katika Flp. 3:3 twaona tena latreuʹein likiwa na maana kubwa katika namna ya kuwaza inayotia maisha yote ya Kikristo.”​—Vol. IV, kur. 63, 64.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki