Nyakati za Kujifurahisha Zahitaji Kiasi cha Kikristo
KARAMU za arusi za Kiyahudi nyakati za kale zilikuwa zenye furaha, zenye muziki, kudansi, kula, na kunywa. Katika Yohana, sura ya pili, twajifunza kwamba Yesu Kristo na wanafunzi wake walihudhuria karamu Kana ya Galilaya. Ingawa Biblia haisemi waziwazi kwamba Yesu alishiriki mambo yote yaliyotajwa sasa hivi, aliongeza furaha ya sherehe kwa kutengeneza divai kwa mwujiza, kileo kinachofurahisha mwanadamu.—Zab. 104:15; Yohana 2:1-11.
Je! hiyo yamaanisha Yesu alidhani “lo lote lafaa” nyakati za kujifurahisha? Sivyo. Timotheo wa Kwanza 3:2 wasema kwamba waangalizi wa Kikristo, wanaopaswa kuweka mfano mwema kwa wengine kundini, wanapaswa kuwa ‘wenye kiasi’ katika mazoea. Naye Yesu alilaumu Mafarisayo kwa sababu ya “kutokuwa na kiasi.”—Mt. 23:25.
Wakristo ni watu wenye furaha wanaotumikia “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11, NW) Wanafurahia kuwa na ushirika wenye kujenga mtu na mwenzake. Katika maisha zao zenye shughuli nyingi, wanapokutana nyakati za kujifurahisha, wanapendezwa. Bila shaka, wanajua kwamba mambo yasiyofaa yanaweza kutokea wanapokutana hivyo kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu; wanajitahidi kuyaepuka kwa kuwa na kiasi.
Ni kwa njia gani nyakati za kujifurahisha zapaswa kuonyesha kiasi cha Kikristo? Twaweza kuonyesha hali inayofaa kwa kuangalia nyakati za kujifurahisha zinazohusu ndoa.
CHAI AU KARAMU ZA ARUSI
Uhakika wa kwamba Yesu alihudhuria karamu ya arusi waonyesha kwamba si vibaya bibi-arusi na bwana-arusi Wakristo wakikaribisha marafiki wakubwa na watu wa ukoo wakafurahie pamoja arusi yao kwa kufika kwenye chai. Kristo hata alitunga mifano mitatu juu ya hali ya karamu za arusi.—Mt. 22:1-13; 25:1-13; Luka 14:7-11.
Walakini, tusikate maneno kwamba lazima kuwe na karamu ya arusi. Si lazima. Wenye kuoana wakitaka kuwa na chai, na hali zaruhusu. wanaweza. Lakini Wakristo wengi wameoana kwa furaha bila ya kuwa na karamu ya arusi baada ya sherehe. Na wale wanaopanga kuwe na chai wanapaswa kufikiri sana ili yatakayofanywa yaonyeshe kiasi cha Kikristo.
Mara kwa mara chai za kilimwengu huwa na jambo moja la kutokeza—kupita kiasi! Watu wanakula kupita kiasi, wanakunywa kupita kiasi na kujifurahisha kupita kiasi. Ni jambo la maana Wakristo wasipite kiasi.
Karamu ya arusi iwe na ukubwa gani? Huo ni uamuzi wa wenye kuoana. Wazazi wawili katika Amerika ya Kaskazini walitumia pesa nyingi sana kwa arusi ya binti yao hata wakalazimika kuhamia mahali pengine wakatafute kazi ya ziada wailipie. Je! hicho ni kiasi cha Kikristo, au ni “kujionyesha kwa mtu mali yake” kusikotokana ‘na Baba bali kwatokana na ulimwengu’?—1 Yohana 2:16, NW.
Mwangalizi mmoja katika magharibi ya Afrika alitaja jambo linaloongeza tatizo: “Mara tu ijulikanapo kutakuwa na ndoa, kundi lote na wengine wa makundi ya karibu wanaona lazima wafike kwenye chai, wawe wamekaribishwa au sivyo. Wengine wanadhani wanaooana wana lazima ya kuwa na chai na kutoa chakula kingi na vinywaji kwa wahudhuriaji wote.” Walakini, maoni hayo hayapatani na mafundisho ya Yesu. Katika mifano yake miwili juu ya karamu za arusi, alitaja wageni “walioalikwa.” (Mt. 22:3; Luka 14:8) Hata alisema wengine waliambiwa warudi kulipokuwa hakuna vitu vya kuwawezesha wajiunge karamuni.—Mt. 25:11, 12.
Baada ya arusi katika Toronto, Canada, wenye kuoana walikula chakula na marafiki wakubwa wachache na watu wa ukoo, na baadaye wakakaribisha watu wote kundini kula vitu vidogo vidogo. Baada ya arusi katika Dusseldorf, Ujeremani, ni watu kumi na sita tu waliokuwa karamuni katika mkahawa. Hiyo iliwawezesha kuwa na mazungumzo ya starehe. Pesa walizookoa kwa kuwa na kikusanyiko kidogo zilitumiwa kwa hekima na wenye kuoana katika mgawo wao mpya wakiwa wahudumu mapainia wa pekee. Ni kweli kwamba wengine wangalipenda kuwako, lakini walifahamu kwamba wenye kuoana wasingeweza ‘kualika wote,’ kama alivyosema bwana-arusi. Walakini, walipendezwa kufurahi pamoja na wenye kuoana kwa kuwa katika Jumba la Ufalme wasikie hotuba ya ndoa.
Kwa hiyo karamu ya arusi iwe ya watu wengi, au wachache tu, iwe ya walioalikwa peke yao, au ya watu wote, au kuwe na chai, wenye kuoana ndio watakaoamua. Waliositawisha kiasi cha Kikristo ‘wataishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa.’—Tito 2:12.
KIASI KATIKA UTENDAJI UNAOPANGWA
Je! kuwe na mipango ya wazi juu ya utendaji utakaokuwa kwenye chai? Ndiyo. Katika karamu Kana alikuwako “mkuu wa meza [“wa karamu,” YW].” (Yohana 2:8) Bila shaka, mwishowe bwana-arusi ndiye mwenye daraka la kuona chai inavyoendelea, hata pesa za chai ziwe zimetolewa na nani. Lakini aweza kuwa na mtu wa kumsaidia kuona kwamba “mambo yote yatendeka kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40, NW) Mkristo aliyekomaa kiroho katika Rhodesia alisema hivi: “Kadiri waliopo wanavyozidi kuwa wengi, ndivyo usimamizi zaidi unavyohitajiwa ikiwa mambo yote yatakwenda kwa ulaini. Kupanga orodha ya mambo yatakayofanywa kwasaidia sana.”
Wakristo wawili waliooana Elsinore, Denmark, walikuwa na watu wa ukoo wasiokuwa waabudu wa kweli. Waliona kwamba watu hawa wa ukoo wa kilimwengu wakikaribishwa karamuni ingekuwa vigumu kuhakikisha kutakuwa na kiasi. Kwa hiyo, waliongozwa na usemi wa bwana-arusi: “Wakati huo tulitaka kuwa na ndugu zetu wa kiroho.” Wakati wa chakula, baba ya bwana-arusi, ambaye ni mmoja wa mashahidi wa Yehova, aliomba watu mbalimbali waliokuwa wamepashwa habari mapema watoe maelezo mafupi. Maelezo hayo yaliyokuwa ya kuchangamsha nyakati nyingine na mazito nyakati nyingine yalifurahiwa na watu hao wachache waliokuwapo. Baadaye mume alisema hivi kwa furaha: “Kama ningeanza tena jambo hili, ningefanya ivyo hivyo.”
“Katika Chile, chai ya arusi isipokuwa na dansi haionekani kuwa sherehe halisi,” kasema Mkristo katika Amerika ya Kusini. Ni vibaya kukiwa na dansi katika chai ya arusi ya Kikristo? Dansi si mbaya. Lakini hatari fulani zinazohusu dansi zapaswa kujulikana. Mwangalizi katika Nigeria alisema kwamba badala ya yaliyo safi na yanayofaa kwaweza kutokea ‘muziki wa kilimwengu upendwao na wengi ambao kwa kawaida huamsha nyege katika dansi. Hiyo yaweza kudhuru waliopo.’
Akijua kwamba hilo lingeweza kutokea, hasa kwa kukodi jamii ya wanamuziki walimwengu, mhudumu mmoja katika Nova Scotia alitia katika utepe muziki utakaopigwa kwenye chai yake. Hivyo dansi ilipatana na adili na kiasi cha Kikristo.
Jambo jingine kubwa juu ya chai hiyo ni kwamba hakukuwa na vileo. Si kwamba Wakristo wamekatazwa kuvitumia, maana Yesu hata alitengeneza divai Kana. Lakini katika mfano huu bwana-arusi aliona kwamba huenda wengine wa eneo hilo wakakwazika kukiwa na vileo. Aliyafikiria maneno haya: “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.” (Rum. 14:21) Katika chai kukiwa na vileo, kwapaswa kuwe na vinywaji vya kutosha kama soda kwa ajili ya wale wanaovipendelea. Yaonekana ilikuwa kawaida ya Wayahudi siku za Yesu kulewa katika karamu za arusi. (Yohana 2:10, NW) Basi, yawapasa Wakristo leo wajihadhari sana vipindi hivyo vya furaha visiharibiwe na anasa.—Mit. 23:20, 21.
Je! sherehe iendelee mpaka usiku sana ndiyo ifanikiwe? Hapana. Mwangalizi katika nchi moja ya Amerika ya Kusini alisema kwamba mara kwa mara “chai huendelea mpaka usiku wa manane. Chakula kamili kinapakuliwa karibu saa 5:30 usiku. Inajulikana sana kwamba vikundi vinavyokutana vishiriki huduma ya shambani asubuhi yake haviwi na watu wengi.” Hata ikiwa desturi katika nchi ya mtu ni kusherehekea mpaka saa hizo, je! Wakristo wafuate desturi zitakazofanya wawe wamechoka sana kesho yake hata wasiweze kumtumikia Muumba wao ifaavyo? Je! hiyo ingekuwa kuonyesha kiasi? Sivyo, bali mipango inayofanywa na Wakristo waliokomaa kiroho yapatana na shauri hili: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Kor. 10:31.
Kwa hiyo Wakristo wakichagua kuwa na kikusanyiko cha kujifurahisha kama karamu ya arusi, kisiwe kama karamu za ulimwengu zenye makelele mengi, zisizo na kiasi na zenye anasa nyingi. Bali, kiwe kikusanyiko kilichopangwa vizuri na chenye furaha kikionyesha kiasi cha Kikristo. Mkristo wa Nova Scotia aliyetangulia kutajwa alisema hivi: “Miaka mitatu baadaye tulitembelea kundi hilo, na bado walikumbuka chai yetu ilikuwa mfano mwema.” Matunda ya kiasi cha Kikristo yapendezaje!
ZAWADI ZA ARUSI
Kukipangwa kuwe na wakati wa kutoa zawadi, kanuni za Kikristo zapaswa kuonyeshwa, kutia na kiasi. Yaliyotangulia kusemwa juu ya chakula, vinywaji na kujifurahisha yatatumika.
Hata hivyo, yapaswa maelezo ya pekee yatolewe kuhusu zawadi. Ingesikitisha sana Mkristo ye yote aliyekaribishwa awepo katika mkutano wa pekee wa kutoa zawadi tu akijiona hawezi
kuukubali ukaribishaji wa kutoa maana hawezi kutoa zawadi ya bei kubwa, au zawadi yo yote. Je! Wakristo wa kweli wangetaka kumweka mtu katika hali hiyo? Zawadi ni kitu kinachotolewa kwa hiari ya mtu kuonyesha upendo. Wonyesho huo unaweza kuwa wa namna nyingi, na si lazima mtu atoe zawadi yenye kuonekana katika tukio la pekee.
Mahali pengine wakati kunapokuwa na mkutano wa pekee wa kutoa zawadi, zawadi zinapangwa pamoja bila majina ya wenye kuzitoa. Kwa sababu gani? Wakristo hao wanajua shauri la Yesu kwamba zawadi hazipaswi kutolewa kumtukuza mwenye kutoa. (Mt. 6:1-4) Wanaona kwamba wakionyesha majina na mtu akose kuleta zawadi, mwingine alete kitu kidogo cha kuonyesha upendo, na mwingine alete zawadi ya bei kubwa. huenda watu wakajilinganisha juu ya aliyetoa hiki na kile.—Mt. 7:12.
Je! hii yamaanisha ni vibaya kujijulisha kwamba wewe ndiwe umetoa zawadi fulani? Sivyo, hiyo siyo maana. Mahali pengine arusini na wakati wa mkutano wa pekee wa kutoa zawadi Wakristo hutoa zawadi wao wenyewe au kufunga vikaratasi kwenye zawadi vikionyesha zimetolewa na nani. Lakini zawadi zikifunguliwa au kuonyeshwa wazi, watoaji hawatangazwi. Hivyo watu hawaaibishwi.
Leo watu wasiomwabudu Yehova huwa na matukio ya kujifurahisha yasiyo ya kiasi mara nyingi na yanayowajulisha kuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Tim. 3:4) Lakini watumishi wa Yehova, wanaoongozwa na Neno lake aliloliongoza kwa roho yake, huonyesha wanathamini sana maneno haya: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Hivyo wao wanatoka walikokuwa wakijifurahisha, si wakiwa na dhamiri zenye kusumbuka, bali na uradhi wa kuwa wamejiburudisha na wakajengwa pia kiroho.