Jifurahishe kwa Njia Yenye Usawaziko Kwenye Karamu za Arusi
1, 2. (a) Kwa sababu gani tunapaswa kufikiria juu ya karamu za arusi leo? (b) Karamu ni za lazima kadiri gani?
LABDA umeona uthibitisho wa kutosha wa unabii ukitimia kwamba katika “siku za mwisho” watu ‘wanapenda anasa kuliko kumpenda Mungu.’ (2 Timotheo 3:1-4) Ushuhuda wa hilo unaweza kuonekana kwa urahisi kwa namna ambavyo wengi wanaona karamu za arusi na namna wanavyotenda kwenye karamu hizo.a Maoni yetu juu yazo yapasa kuwa nini? Je! Wakristo wanapaswa kuepuka kufanya au kuhudhuria karamu za arusi? Au je, jambo kubwa hapa ni kwamba ili “kumpenda Mungu” tunahitaji kuepuka hatari fulani-fulani?
2 Hata liwe ni jambo la kawaida kama nini katika mahali penu kuwa na mkusanyiko wa kirafiki mara tu baada ya arusi ya wenzi wawili, kwa hakika Wakristo hawako chini ya daraka lo lote la Kimaandiko kufanya hivyo. Badala ya kufanya hivyo, wenzi wengine wanapendelea kukusanyika na jamaa yao ya karibu au rafiki wachache sana wa karibu, pengine kufurahia chakula cha faragha pamoja nao. Lakini kuwa na au kuhudhuria karamu ya arusi kwenyewe tu hakuwezi kulinganishwa na ‘kupenda anasa,’ kwa maana Yesu na wanafunzi wake walihudhuria sherehe kama hiyo katika Kana.
3. Karamu za arusi zilikuwa za kawaida jinsi gani katika nyakati za Biblia?
3 Arusi ni wakati wa kufurahiwa na waliotoka kufanya arusi, na watu wao wa ukoo na marafiki. Karamu za arusi zenye furaha zimekuwa jambo la kawaida kwa muda mrefu. (Mwanzo 29:2, 22; Waamuzi 14:3,10, 17) Kwa sababu Wayahudi walikuwa wanafahamiana na karamu za arusi, Yesu angeweza kuzitumia katika mifano mitatu. (Mathayo 22:2-14; 25:1-13; Luka 14:7-11) Hata kitabu cha mwisho cha Biblia kinasema: “Heri walioalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 19:9.
4. Karamu nyingi za arusi zimekuwaje?
4 Watumishi wa Mungu wakati uliopita—kutia Yesu na wanafunzi wake—walijifurahisha kwa usawaziko kwenye karamu za arusi. Pia maelfu ya Wakristo wakati wetu wamejifurahisha kwa usawaziko. Mtu wa ukoo asiyeamini aliyehudhuria moja katika Afrika ya Kusini alisema: “Sikujua kwamba Mashahidi wana arusi nzuri hivyo. Tumechoka na huku kunywa-kunywa na muziki wenye sauti kubwa unaokuwako kwenye arusi siku hizi.” Karamu nyingi za Kikristo zingestahili sifa kama hiyo.
5. Ni matatizo ya namna gani yametokea?
5 Lakini, mkazo kutoka ulimwengu wa kuwa wenye “kupenda anasa” ni mkubwa. Kwa hiyo wazee fulani Wakristo wanaripoti:
“Hesabu fulani wanatumia [karamu ya arusi] wastarehe. Wanawaza kwamba hakuna nafasi nyingi kama hizo, kwa hiyo wanaitumia kwa njia kubwa wawezavyo ili waondoe mkazo, na kupatia uhuru tamaa zinazozuiwa ndani wakati ule mwingine. Haishangazi kwamba mazingira yanakuwa yenye msukosuko.”—Ulaya.
“Inaonekana kwamba sherehe ya ndoa inatia ndani hotuba, kutafuna kitu halafu kucheza dansi mpaka baada ya usiku wa manane. Wengine wana maoni kwamba kwenye karamu wanaweza kunywa zaidi ya ilivyo kawaida, na mara nyingi wanakunywa sana.”—Amerika ya Latini.
“Karamu ya arusi huenda ikatia ndani ‘kucheza dansi mpaka asubuhi mapema.’ Mengine ya mambo hayo ni ya kilimwengu kweli kweli—yenye mteremo mkubwa, na kunywa sana na kucheza dansi ya kilimwengu. Wengine wanajitahidi kujionyesha kwa mavazi ya bei kubwa-kubwa na visanduku vingi vya pombe.”—Afrika.
Kiasi Kinahitajiwa
6. Tunaweza kujifunza nini juu ya karamu za Kiyahudi kutokana na maneno yaliyosemwa katika Kana?
6 Watu wengi wanajua kwamba kwenye karamu ya arusi katika Kana, Yesu aligeuza maji yakawa divai. Lakini, mkumbuke jambo hili: “Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai..., alimwita bwana arusi, akamwambia, Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu.” (Yohana 2:9,10) Yeye hakusema wakati wa sherehe hiyo wageni ‘walikunywa sana.’b Kwa kweli, ni jambo lisilowazika kwamba Yesu angeunga mkono ulevi halafu azidishe jambo hilo kwa kutengeneza divai zaidi. Ijapokuwa hivyo, mwanamume huyo alijua kwamba kunywa kupita kiasi lilikuwa jambo la kawaida kwenye karamu za arusi za Kiyahudi.
7. Mkristo anapaswa kufikiria nini kuhusiana na kutoa vileo?
7 Kwenye karamu nyingine wenye kuitengeneza hawakutoa kileo cho chote kwa sababu kutumia kupita kiasi kulikuwa jambo la kawaida sana katika eneo hilo, na ili kuepuka kushawishi ye yote aliyekaribishwa ambaye alikuwa amekuwa na tatizo la kunywa. Ndugu fulani Waafrika hata walisema kwamba kutoweka kileo cho chote kumefanya iwe “arusi ya Kikristo kabisa.” Na ni kweli kwamba kutokuwa na vileo kwaweza kuwa jambo la hekima mahali ambapo maoni ya jumuiya ni yenye kupinga sana Wakristo kutumia kileo. (Warumi 14:20, 21) Hata hivyo, uchanganuzi wenye usawaziko unahitajiwa. Jiulize mwenyewe, Je! karamu ambayo Yesu alihudhuria ‘ilikuwa chafu’ kwa sababu divai ilitolewa? Biblia inalaani ulevi, wala si matumizi ya kiasi ya vileo.—Mithali 23:20, 21; 1 Petro 4:3.
8, 9. (a) Vileo vikitolewa, kiasi kinaweza kudumishwaje? (b) Mzee mmoja alisema nini juu ya tatizo hilo?
8 Ikiwa bwana-na-bibi-arusi wanataka kuwepo vileo kwenye karamu yao, ni jambo la hekima na la kujali wengine kwamba waangalie ifaavyo juu ya matumizi ya kiasi. (1 Timotheo 3:2; Mathayo 23:25) Kwa mfano, kwenye karamu katika Kana, waliokaribishwa walitumikiwaje? Kwa wazi walitumikiwa na “watumishi.” (Yohana 2:5, 9) Kwa hiyo wenzi wanaweza kuweka watu wa kutumikia (na pengine kupima kiasi cha) vinywaji. Bila shaka, kwenye karamu yo yote ya Kikristo, kwapasa kuwe vinywaji visivyo vya kulevya kwa ajili ya wale wanaopaswa kunywa hivyo, au ambao huenda wakavipendelea.
9 Mzee mmoja katika Amerika ya Kati alieleza hivi: “Tatizo moja limekuwa kwamba karamu hizo ni kubwa mno, kwa hiyo hakuna namna ya kuwaongoza wote wanaohudhuria. Nyakati nyingine watu wa kilimwengu wamejikaribisha kwenye karamu hizo, na kuingia pamoja na chupa za pombe na kutokeza lawama.” Kwa hiyo ni nani atakayetoa uongozi au mwelekezo? Ni wangapi watakaohudhuria? Ni nini kitakachotukia kwenye karamu hizo?
Mwelekezo Kutoka kwa Nani?
10. Ni kufuata kidokezo gani cha Kibiblia kunaweza kutokeza uongozi mzuri zaidi kwenye karamu?
10 Kwenye karamu iliyokuwa Kana, kulikuwako “mkuu wa meza” (“mkurugenzi wa karamu,” NW). (Yohana 2:9) Vivyo hivyo, kwenye karamu leo ndugu mwenye uwezo, mwenye kuchukua madaraka kwa njia nzuri anaweza kupewa mamlaka ya kuangalia mambo yote. Akiwa anafahamiana na mapendezi ya waliotoka kufanya arusi, anaweza kutoa mwelekezo kwa waimbaji, wenye kutumikia na wengine, au anaweza kushauriana na bwana-na-bibi-arusi halafu kutenda. Hiyo huenda ikatia ndani kusimamia wakaribishaji. Pamoja wangeweza kuwasaidia waliokaribishwa na kushughulika na wo wote wenye ‘kuingia bila kualikwa kwenye karamu.’ Kuhusu jambo hilo la uongozi, angalieni katika mfano wa Yesu yaliyotokea kwa mmoja aliyekaribishwa aliyeonyesha kukosa heshima sana kwenye karamu ya arusi.—Mathayo 22:11-13.
11. Ni mambo gani yanayopasa kufikiriwa katika kuchagua mtu wa kuwasaidia bwana-na-bibi-arusi kutoa mwelekezo wa mambo?
11 Kwenye karamu nyingi za kilimwengu msimamizi wa jumba au kiongozi wa beni (kikundi cha wanamuziki) anakuwa msimamizi wa sherehe. Huenda akajua kawaida ya kufanya mambo na inaelekea ana maneno ya kusema aliyozoea au maneno ya kuchekesha ya kuvuta fikira. Lakini ikiwa unataka karamu inayopatana na kanuni za Kikristo, je, ungekubali mlimwengu—ambaye si ndugu yako wa kiroho wala mshiriki wa jamaa yako—asemeshe wageni wako au kuwa ndiye mwenye kukaziwa fikira? Je! jambo hilo lingepatana na shauri la ‘kutendea watu wote mema; na hasa jamaa yako ya waaminio’?—Wagalatia 6:10.
12. Biblia inatoa kidokezo gani juu ya ni nani hasa aliye na daraka la mambo yatakayofanyika kwenye karamu?
12 Nyakati nyingine wazazi wa bibi-arusi au bwana-arusi wanawasaidia wenzi hao kulipia gharama za karamu ya arusi. Kwa hiyo huenda wazazi wakawa na maoni kwamba wana mamlaka makubwa ya kuamua ni nani watakaoalikwa, ni chakula na kinywaji cha namna gani kitakachotolewa au programu itakuwa nini. Biblia haisemi ni nani alilipia gharama ya karamu katika Kana, lakini inatuambia kwamba wakati jambo la maana lilipotokea “mkuu wa meza alimwita bwana arusi.” (Yohana 2:9) Kwenye karamu ya arusi, Kimaandiko bwana-arusi ndiye kichwa cha jamaa iliyotoka tu kufanywa. (Waefeso 5:22, 23) Basi, ingawa anapaswa kufikiria kwa upendo mapendezi ya bibi-arusi wake katika siku hiyo ya pekee, na mapendezi ya jamaa zao, yeye apaswa kwanza kukubali kubeba daraka la mambo yatakayofanyika na ambayo hayatafanywa.
Ni Nani Watakaokuwako?
13. Karamu za arusi zilikuwa kubwa kadiri gani katika nyakati za Kibiblia?
13 Sisi hatujui karamu za arusi nyakati za Biblia zilikuwa kubwa kadiri gani. Ya Samsoni ilitia ndani wazazi wake, marafiki 30 wa bibi-arusi wake na inaelekea marafiki wengine na watu wa ukoo. (Waamuzi 14:5, 10, 11, 18) Wenye kukaribishwa katika arusi za Kiyahudi walikuwa waabudu wenzi katika mji huo pamoja na wageni. Yesu na wanafunzi wake, waliotoka kwingine huko Galilaya, walienda kwenye karamu katika Kana. Kiasi cha divai iliyotengenezwa chadokeza kulikuwa kikundi kikubwa kidogo.—Yohana 2:1, 2, 6.
14, 15. Wengine wamepangaje kuwako kwa karamu ambazo wote wanaopenda wanakaribishwa, lakini ni matatizo gani yanayoweza kutokea?
14 Leo, desturi na mapendezi yanatofautiana juu ya ni namna gani au ni ukubwa gani wa karamu. Katika maeneo fulani ni desturi kwamba mtu ye yote akipenda kuja anakaribishwa; Wakristo wenzi wote ambao ni marafiki wa waliotoka kufanya arusi wanakaribishwa. Huenda wakapewa viburudisho vidogo-vidogo, kusudi likiwa si kutosheleza hamu ya kutaka kula ya kila mtu bali ili kuwaruhusu wawatakie mema na kufurahia ushirika mchangamfu. Kwingine kwenye mikusanyiko ambayo marafiki wote wanakaribishwa wakitaka, watu wengi wanaleta chakula—mlo uliotayarishwa, kinywaji au kitumbua kidogo cha baada ya chakula kikubwa. Wote wanaojitolea hivyo wana furaha ya kutoa kitu, na kila mtu anaweza kufurahia chakula cha namna mbalimbali bila ya mzigo kuwaangukia wenzi hao wawili au mtu mwingine ye yote.—Matendo 20:35.
15 Kutokana na tunayosoma katika mifano ya Yesu, inaonekana kwamba mara nyingi kwenye arusi za Kiyahudi mlo mkubwa ulitayarishwa. (Mathayo 22:2; Luka 14:8) Bila shaka, kuwa na mlo wa kawaida kwa wote waliokaribishwa leo ni jambo lenye kutaka mpango sana. Mama mmoja katika Amerika ya Kaskazini alisimulia jambo hili lenye kusikitisha:
‘Ilipojulikana kwamba kulikuwako arusi, vijana kutoka eneo kubwa walijitokeza kwa ajili ya chakula cha bure na kucheza dansi. Walioalikwa walipokuwa wangali kwenye Jumba la Ufalme, wengine walienda kwenye jumba la karamu na kujaza meza zote zilizokuwapo. Nilipofika karibu ningelia, kwa maana hakukuwako nafasi. Niliumizwa sana na ukoesfu wa upendo ulioonyeshwa na wale waliojikaribisha kwenye arusi na wakala chakula chote kilichotayarishwa na mwenye karamu kwa ajili ya marafiki wa karibu na watu wa ukoo.’
16. Tunaweza kujifunza nini katika Biblia kuhusu wanaokaribishwa kwenye arusi?
16 Mariamu, Yesu na wanafunzi wake hawakujikaribisha kwenye karamu katika Kana; ‘walialikwa.’ (Yohana 2:1, 2) Yesu alisema, “Ukialikwa na mtu arusini...” (Luka 14:8, 9,16, 17) Katika mfano wa arusi ya mwana wa mfalme, Yesu pia alisema juu ya “walioalikwa.” (Mathayo 22:3, 9, 10) Zaidi ya hilo, mtu mmoja aliyealikwa alipoonyesha kukosa heshima, wakaribishaji walielekezwa wamtoe nje. Katika mfano mwingine, wanawali watano waliotaka kushiriki karamu ya arusi walizuiwa hata wasiingie kuupita mlango. (Mathayo 22:11-13; 25:10-12) Kwa hiyo lisionekane kuwa jambo la ajabu ikiwa karamu ni kwa ajili ya waliokaribishwa peke yao na kwamba wawe wamevaa vizuri. Na ni jambo lenye kufahamika kwamba ukarimu wa mwenye karamu si lazima utie ndani watu ambao mahangaiko yao makubwa ni mlo na anasa.—Wafilipi 3:18, 19; Mhubiri 5:11.
17. Ni tatizo gani ambalo limetokea kuhusiana na ukubwa wa karamu za arusi?
17 Ikiwa bwana-na-bibi-arusi au watu wao wa ukoo wanataka kutayarishia wengi waliokaribishwa chakula kamili, jambo hilo laweza kuwa lenye gharama kubwa. (Linganisha Marko 6:35-37.) Kutoka Pasifiki tunapata ripoti hii:
“Kuna nia ya kufanya karamu kupita kiasi. Wengine wanaingia katika deni ili kufanya karamu kubwa, na hivyo wanaanza maisha ya ndoa wakiwa na deni. Mara nyingi inaonekana kuna tamaa ya kuepuka kutenda isivyo kiungwana, kwa hiyo wanatayarisha karamu ambayo inazidi uwezo wao wa pesa.”
Inasikitisha kama nini wakati wenzi wachanga wanapoanza maisha ya ndoa wakiwa wamelemewa na madeni ambayo yanaweza kuharibu uhusiano wao. Au wangeonaje wakijua kwamba wazazi wao walikabili tatizo kulipia gharama za karamu kubwa? Bila shaka, watu wa ulimwengu huenda wakajiingiza katika deni kubwa sana la arusi kwa sababu ya tamaa ya kiburi ya kuvutia wengine au kujifanya waungwana katika jumuiya yao. (Mithali 15:25; Wagalatia 6:3) Lakini je, iwe hivyo kwa Wakristo, tunapofikiria tunayosoma katika Luka 12:29-31?
18, 19. (a) Kwa sababu gani huenda wengine wakawa waliamua kuwa na karamu kubwa? (b) Tuoneje tusipokaribishwa kwenye karamu ya rafiki? (Luka 14:12)
18 Kichocheo cha karamu nyingine kubwa sana kimekuwa ni tamaa ya kulingana na au kuwapita wengine. Wazee katika Afrika ya Magharibi walieleza hivi:
“Wengine wanajiingiza katika gharama kubwa sana kwa sababu ya viburudisho. Mwenye kutayarisha karamu ya arusi ya pesa nyingi zaidi ndiye mwenye kuwekea wengine kiwango. Jambo hilo limetokezea matatizo wale wasio na ujasiri wa kutosha kuwa tofauti. Kujionyesha kwa mtu mali yake huenda kukakwaza wengine na kujaribu kulingana na wengine si jambo la lazima.”—Ona 1 Yohana 2:15-17.
19 Wengine wamejisikia wanakazwa wafanye karamu kubwa sana kwa sababu ya kuogopa kuudhi wengine. Wanawaza kwamba kama watu fulani wanaofahamu wasipoalikwa, wataona uchungu. Kwa hiyo, wengi wanakaribishwa isivyofaa. Lakini, tukiwa wanyofu, ni nani kati yetu angependa marafiki wetu waogope sana kutudharau hata walemewe na deni na pengine wakose kuingia katika huduma ya wakati wote? Tusipokaribishwa, ni jambo zuri zaidi kuwa na hakika kwamba walichunguza mambo yote kwa njia ya ukomavu, kutia mambo ya pesa. Kwa wao kutotukaribisha huenda hata kukawa ni kuonyesha uhakika wao kwamba sisi tumekomaa wala hatutaudhika upesi. (Mhubiri 7:9; 1 Wakorintho 13:4-7) Bado tunaweza kuishiriki furaha yao kwa kuhudhuria hotuba ya arusi yenye msingi wa Biblia, ambayo ndiyo sehemu yenye maana zaidi. Ikiwa tunaiona hiyo kuwa ya maana ndogo zaidi ya karamu, je, twaweza kuwa tunageuka kuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu”?—2 Timotheo 3:4.
20. Kupima ukubwa wa karamu anayofanya mtu kwaweza kuepusha mazoea ya namna gani?
20 Pia kuwa wenye kiasi kuhusu ukubwa na gharama ya karamu kunasaidia kuepuka mazoea yasiyo mazuri. Kwa mfano, tamaa ya pesa imewasukuma wachache wanunue nguo ya pekee kwa ajili ya mavazi ya arusi, halafu kuuliza msafara wa arusi ununue nguo hiyo kwa bei ya juu zaidi. Waliokaribishwa katika karamu fulani walilazimika “kununua” vipande vya keki au “kutoa malipo” ya kucheza dansi na aliyetoka kuwa bibi-arusi, na kufunga pesa kwenye nguo yake. Pia huenda mkazo huo ukawa ndiyo sababu inayofanya waliokaribishwa wajionyeshe pesa zao kwa “kuzitawanya” (kutupa) pesa zao juu ya wanamuziki au kutoa zawadi kubwa ili wapate viti vya pekee karibu na waliotoka kufanya arusi.—Luka 14:8-11.
Wasaidie Wote Wajifurahishe
21. Muziki unatimiza sehemu gani katika karamu za arusi?
21 Wakati wa vita vya Wamakabayo msafara wa arusi wa Kiyahudi ulifikiwa na kikundi “chenye matari na wanamuziki.” (1 Wamakabayo 9:39, The Oxford Annotated Bible; linganisha Zaburi 45:8.) Leo, pia, mara nyingi muziki unatiwa kwenye karamu za arusi. Unaweza kufanya Mkristo ajifurahishe zaidi kwenye pindi hiyo—au unaweza kuondoa kujifurahisha. Kwa sababu gani huenda ukaondoa kujifurahisha? Katika visa kadha muziki umekuwa wenye sauti kubwa sana na usio na mipaka. Wanamuziki wengine wanapenda muziki wa namna ya disko, au huenda wakawa wenye shangwe ya kupita kiasi katika kujionyesha kiwazimu walivyo na uwezo. Lakini karamu ya Kikristo si mahali pa mambo hayo. Je! waliokaribishwa, vijana au wazee, wanaweza kufurahia ushirika wa Kikristo ikiwa muziki ni wenye sauti kubwa sana hata kwamba mazungumzo ya walio mezani hayawezekani?
22. Matatizo yanayohusu muziki yanaweza kupunguzwaje?
22 Kwa wazi, muziki kwenye karamu za arusi unahitaji kufanyiwa mpango kwa uangalifu na usimamizi, sana-sana muziki unaochezwa na wanamuziki wenyewe wakiwa jukwaani. Ni afadhali kutotumia wanamuziki walimwengu. Kukiwako wanamuziki wenye kulipwa, bwana-arusi au ndugu aliyechaguliwa apaswa kueleza kwa uthabiti wanamuziki hao ni muziki gani unaweza kuchezwa, na ni upi usiopaswa kuchezwa. (Kutoka 32:6, 17, 18) Inapasa kutajwa wazi kwamba hakuna maombi ya pekee ya muziki kutoka kwa waliokaribishwa utachezwa bila ruhusa ya bwana-arusi au “mkurugenzi” (NW) wa karamu. Kwa sababu ya matatizo ya kawaida yanayohusu hali na sauti kubwa ya muziki unaochezwa na wanamuziki wenyewe wakiwa jukwaani, wenzi wengi wamechagua kutumia sahani za santuri au tepu (kanda) zenye muziki ule ambao wao wanataka. Wamehakikisha unachezwa na mtu mzima ambaye hatavutwa kwa urahisi na ule ambao vijana wasiokomaa wanapenda sana.—1 Wakorintho 13:11; Waebrania 5:14.
23-25. Ni hatua gani nyingine zinazofaa ambazo waliotoka kufanya arusi wanaweza kuchukua ili kuhakikisha kuwapo kwa mkusanyiko wa Kikristo wenye kupendeza?
23 Wakristo waliotoka kufanya arusi wanataka watu ambao walikaribisha waweze kutazama nyuma na kuiona karamu hiyo kwa njia ya furaha. Kwa hiyo kukiwa muziki na/au kucheza dansi, unapasa kupatana na kanuni za Kikristo. Ikiwa watu fulani wanaulizwa waseme maneno machache, wale waliochaguliwa na wanayosema yapasa kufaa mkusanyiko wa Kikristo wenye heshima.
24 Katika mfano wa wanawali kumi karamu ilianza “usiku wa manane” kwa sababu msafara wa arusi ulikuwa umechelewa. (Mathayo 25:5, 6) Katika kisa kingine, aliyosema Yesu juu ya mfalme akiwa ameandaa karamu na watumishi kuwakaribisha watu waliokuwa barabarani yanaonyesha kwamba karamu hiyo ilikuwa wakati wa mchana. (Mathayo 22:4, 9) Katika nyakati za kisasa karamu nyingine zimeendelea mpaka usiku, na kuwa zisizoongozeka kwa kuwa Wakristo waliokomaa wanaondoka ili wakapate usingizi wa usiku wa kutosha. Ili kuzuia jambo hilo, bwana-na-bibi-arusi wengi wenye usawaziko wamepanga wakati wa karamu kuanza na wakati wa kumalizika. Kwa njia hiyo wote wanaweza kufanya mipango yao, kutia ndani mipango ya utendaji unaofaa wa Kikristo wa siku inayofuata karamu yenye kufurahisha.
25 Karamu ya arusi yaweza kuwa pindi nzuri sana ya kujifurahisha kwa Kikristo kunakofaa na kwenye usawaziko. Lakini sehemu yake ni nini kuhusiana na kinachofuata—maisha ya ndoa tukiwa Wakristo wa kweli?
[Maelezo ya Chini]
a Katika nchi fulani, baada ya sherehe ya ndoa, wote waliokaribishwa wanaweza kuhudhuria karamu yenye vinywaji visivyolevya au chai na keki. Baadaye waliotoka kufanya arusi, jamaa zao na marafiki fulani wanashiriki mlo wa arusi kwenye nyumba au mkahawa. Kwingine karamu ni mkusanyiko wa baada ya arusi—uwe ni wa viburudisho au karamu.
b Ni kutoka kwa neno la Kigiriki methusko, lenye maana ya “kulewa, kunywa sana.” Waelezaji wengine wanabisha kwamba neno hilo linadokeza kunywa vya kutosha tu kuweza kufisha uwezo wa kuonja au msisimuko mkubwa. Maandishi mengine hayaungi mkono maoni hayo.—Mathayo 24:49; Luka 12:45; Matendo 2:15; Waefeso 5:18; 1 Wathesalonike 5:7.
Kutokana na Yaliyotangulia, Je! Wewe Unakumbuka?
◻ Kwa sababu gani Wakristo wanapaswa kufikiria karamu?
◻ Inafaa iweje kuhusiana na vileo kwenye karamu za arusi?
◻ Ni nani mwenye daraka la yanayofanyika kwenye karamu?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kiongozi wa karamu alishauriana na bwana-arusi juu ya divai