Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 4/15 kur. 23-26
  • Arusi Zinazomheshimu Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Arusi Zinazomheshimu Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Habari Zinazolingana
  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Arusi Zenye Shangwe Zinazomletea Yehova Heshima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 4/15 kur. 23-26

Arusi Zinazomheshimu Yehova

Makala ifuatayo juu ya arusi za Kikristo ilitayarishwa awali katika Ethiopia ili kuandaa mwongozo wenye kusaidia katika lugha ya Kiamhara kwa ajili ya watu wengi nchini humo ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova hivi majuzi. Inashughulika na desturi na mazoea ya huko ambayo yaweza kuwa tofauti na yale ya mahali unapoishi. Yamkini utapata tofauti hizo kuwa zenye kupendeza. Wakati uleule, hii makala inatoa shauri la Kibiblia lenye usawaziko utakaloona kuwa lenye kutumika hata ikiwa desturi za arusi za kwenu ni tofauti.

“ARUSI za Kikristo Ambazo Zinaleta [Shangwe]” kilikuwa kichwa cha makala nzuri ya funzo katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1984. Makala iliyofuata katika toleo hilo ilikuwa na kichwa “Jifurahishe kwa Njia Yenye Usawaziko Kwenye Karamu za Arusi.” (Kwa yeyote anayefikiria kufunga ndoa, kuna mashauri zaidi yenye hekima katika vitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha, sura ya 2, na Kupata Faida Zote za Ujana Wako, sura ya 19 na ya 20.)a Wengi wamekuwa Mashahidi wa Yehova tangu makala hizo zitoke, hivyo twataka kupitia hoja kadhaa zinazofaa eneo letu kimahususi, na vilevile mambo mengine yafaayo yatakayotusaidia kufanya sherehe za arusi zinazomheshimu Yehova, Mwanzilishi wa ndoa.

Swali linaloweza kufikiriwa kwanza ni, Arusi yapaswa ifanywe lini? Je, tarehe yapaswa iamuliwe kulingana na tarehe za msimu wa kidesturi wa arusi mahali fulani-fulani? Itikadi ya mahali fulani-fulani ni kwamba ndoa yoyote ifungwayo wakati mwingine wowote wa mwaka haingefanikiwa. Huo ni ushirikina usio na msingi, kwa maana wenzi wengi wa ndoa wanaomtumikia Yehova kwa furaha na muungano hawakuoana katika huo msimu wa kidesturi. Hatuamini katika bahati nzuri au mbaya. (Isaya 65:11; Wakolosai 2:8) Hatungewasaidia watu wa ukoo wasioamini kuona tofauti kati ya kweli na yasiyo kweli ikiwa tungepanga tarehe ya arusi kulingana na shirikina zao. Uhakika ni kwamba, Wakristo waweza kuoana katika mwezi wowote.

Hotuba ya arusi inapopangwa itolewe baada ya sherehe ya lazima ya kiserikali, lingekuwa jambo la hekima kutokuwa na kipindi cha siku nyingi kati ya matukio hayo mawili. Ikiwa hao wenzi wangependa hotuba ya arusi itolewe katika Jumba la Ufalme, wapaswa kuwafikia wazee wa kutaniko kimbele vya kutosha ili kuomba kutumia hilo jumba. Wazee wa mahali hapo watathibitisha kwamba mipango kwa ajili ya hiyo sherehe itawaacha wakiwa na dhamiri safi. Wakati wapaswa kupangwa ili kusiwe na hitilafiano na utendaji wowote wa kutaniko. Ndugu aliyechaguliwa kutoa hotuba ya arusi atatangulia kukutana na wanaotazamia kuwa bwana-arusi na bibi-arusi ili kuwatolea mashauri yenye kusaidia na kuhakikisha kwamba hakuna vizuizi vya kiadili au vya kisheria kwa hiyo ndoa na kwamba yeye anakubaliana na mipango kwa ajili ya kikusanyiko chochote cha kirafiki kitakachofuata. Hotuba ya arusi yapaswa kuwa na urefu wa nusu saa hivi na itolewe katika njia yenye heshima, ikikazia upande wa kiroho. Hotuba ya arusi kwa kweli ni muhimu zaidi ya karamu yoyote iwezayo kufuata.

Arusi ya Kikristo ni fursa nzuri ya kuonyesha kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14; Yakobo 1:27) Utaratibu wetu wapaswa kuwa wenye kutokeza. Hilo lingemaanisha kwamba tungefika kwa wakati badala ya kufanya watu wangojee, labda hilo likiingiliana na utendaji wa kutaniko. Hilo hasa ni jambo la bibi-arusi kufahamu, kwa kuwa huenda watu wa ukoo wa kilimwengu wamsihi sana achelewe—kana kwamba kuongezea umuhimu wake. Akifika kwa wakati dada Mkristo aliye mkomavu aweza kuonyesha kwamba sifa za kiroho, kama unyenyekevu na kufikiria wengine, ni muhimu kwake! Pia, mpiga-picha anapoalikwa kurekodi hiyo pindi, utaratibu ni muhimu. Ingefaa mpiga-picha aombwe aje akiwa amevalia koti, tai, na suruali rasmi na kwamba asiingilie hotuba anapopiga picha. Picha hazipaswi kupigwa wakati wa sala. Utaratibu wetu utamheshimu Yehova na kutoa ushahidi mzuri. Hakuna uhitaji wa kujaribu kujipatanisha na desturi za arusi za kilimwengu ambazo zingefunika maana halisi ya hilo tukio.

Karamu si takwa kwa ndoa yenye mafanikio, lakini hakuna kipingamizi cha Kimaandiko kwa pindi kama hiyo yenye furaha. Hata hivyo, kikusanyiko kama hicho cha Wakristo wa kweli chapaswa kuwa tofauti kutoka karamu za kilimwengu zinazotiwa alama na matumizi ya pesa yapitayo kiasi, kunywa sana, kula kupita kiasi, muziki wenye kichaa na kucheza dansi kwenye kuamsha tamaa mbaya, na hata mapigano. Biblia huainisha “sherehe zenye kelele za ulevi na ulafi” pamoja na kazi za mwili. (Wagalatia 5:21) Ni rahisi zaidi kuwa na udhibiti ufaao kikusanyiko kinapokuwa si kikubwa sana. Hakuna uhitaji wa kupiga hema ili kutosheleza desturi zinazopendwa. Watu fulani wakiamua kutumia hema kwa sababu za nafasi au halihewa, hilo ni jambo la kibinafsi.

Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba njia nzuri ya kuwekea mipaka idadi ya wageni-waalikwa ni kwa kutumia mialiko hususa iliyoandikwa. Ni jambo la hekima zaidi kualika watu mmoja-mmoja kuliko makutaniko mazima-mazima, na tukiwa Wakristo wenye utaratibu, twapaswa kuheshimu mipaka kama hiyo. Mialiko iliyoandikwa pia hutusaidia kuepuka aibu ya kuwa na mtu aliyetengwa na ushirika kwenye karamu, kwa maana ikiwa hilo lingetokea, ndugu na dada wengi wanaweza kuchagua kuondoka. (1 Wakorintho 5:9-11) Ikiwa wenzi waliooana wanaalika watu wa ukoo au watu wanaojuana nao wasioamini, bila shaka idadi yao itakuwa ndogo, wakiwapa umaana mkubwa zaidi wale “ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Watu fulani wamechagua kualika watu wa kilimwengu wanaojuana nao au watu wa ukoo wasioamini kwenye hotuba ya arusi badala ya kwenye karamu. Kwa nini? Kumekuwa na visa ambapo watu wa ukoo walimwengu walitokeza hali yenye kuaibisha sana kwenye karamu ya arusi hivi kwamba ndugu na dada wengi walihisi kwamba hawangebaki huko. Wenzi fulani wamepanga kuwa na mlo mdogo tu pamoja na washiriki wa familia wa karibu na marafiki Wakristo.

Kulingana na Yohana 2:8, 9, ni jambo la busara kuteua “mwelekezi wa karamu.” Bwana-arusi atataka kuchagua Mkristo awezaye kuwa na itibari katika yeye atakayehakikisha kwamba utaratibu na viwango vya juu vinadumishwa. Ikiwa wageni-waalikwa wataleta zawadi, hilo lapaswa kufanywa bila “wonyesho wa mtu wa kujivunia.” (1 Yohana 2:16) Muziki waweza kuwa wenye kufurahisha bila kuchafuliwa na maneno ya kutilika shaka, kelele zenye kupita kiasi, au mdundo wenye kichaa. Wengi wameona ni vizuri zaidi kwa mzee kusikiliza kimbele muziki utakaochezwa. Kucheza dansi kwaweza kuleta mitego, kwa kuwa dansi nyingi za kidesturi zinatokana na dansi za kiuzazi na hukazia kuamsha nyege isivyofaa. “Wakati wa keki na divai” nyakati fulani umekuwa ishara kwa watu walimwengu kutenda kwa njia ya kutojizuia. Kwa hakika, Wakristo wengi wameamua wasiwe na vileo vyovyote kwenye karamu za arusi, hivyo wakiepuka matatizo.

Kwa kuwa twataka kumheshimu Yehova, tutaepuka wonyesho wa kujivuna kwa kuvuta uangalifu kwetu kupita kiasi. Hata vichapo vya kilimwengu vimesema dhidi ya huo mwelekeo unaopendwa wa kuwa na gharama nyingi mno. Lingekuwa jambo la kukosa hekima kama nini kwa wenzi kuingia katika deni kwa sababu ya arusi yenye gharama nyingi mno na kisha wapatwe na uhitaji kwa miaka mingi ili kulipia gharama za siku hiyo moja! Bila shaka, vazi lolote livaliwalo kwenye hiyo pindi lapaswa kuwa lenye kiasi na lenye mpangilio mzuri, ustahilio mtu anayemstahi Mungu. (1 Timotheo 2:9, 10) Ile makala “Arusi za Kikristo Zapaswa Zionyeshe Kiasi” (Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1969 la Kiingereza) ilitoa maelezo haya yenye kupendeza juu ya mavazi:

“Arusi ya mtu ni pindi ya pekee, hivyo uangalifu kikawaida huelekezwa kwenye kuonekana wenye shangwe na wenye kuvutia. Hata hivyo hilo halimaanishi kwamba ni lazima mtu avae aina fulani ya vazi au suti. Mtu anafanya vizuri kufikiria mitindo ya kwao, gharama na mapendezi ya kibinafsi. . . . Hata hivyo, je, lingekuwa jambo lifaalo, kununua vazi ghali sana hivi kwamba wajiletea wao wenyewe au wengine mzigo wa fedha wenye kulemea? . . . Bibi-arusi fulani wamefurahia kutumia vazi la rafiki mpendwa au la mtu wa ukoo. Wengine wamepata uradhi mkubwa kutokana na kushona vazi lao wenyewe la arusi, kwa njia hiyo wakiweza kuwa na vazi liwezalo kutumiwa katika pindi nyingine wakati ujao. Na ni jambo lifaalo kabisa kwa wenzi kuoana wakiwa wamevaa mavazi yao ya kawaida yenye kuvutia zaidi . . . Wengine wanaoweza kuwa na arusi yenye madoido huenda wakatamani kibinafsi kuwa na ‘arusi yenye utulivu’ kwa sababu ya hizi nyakati zenye hatari.”

Vivyo hivyo, wanaoshiriki (marafiki wa bwana-arusi na waandamani wa kike wa bibi-arusi) hawahitaji kuwa wengi. Wao pia hawangetaka kuvuta uangalifu kwao wenyewe kwa mavazi na matendo yao. Ingawa mtu aliyetengwa na ushirika angeweza kuruhusiwa kuhudhuria hotuba kwenye Jumba la Ufalme, Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1984, lilisema hivi: “Haingefaa kuweka katika msafara wa arusi watu ambao wametengwa na ushirika au wale ambao mtindo wao wa maisha wenye kuudhi unapingana sana na kanuni za Biblia.”

Ijapokuwa Yesu alihudhuria arusi, hatuwezi kuwazia kwamba angekubali desturi ipendwayo ya kuwa na msafara wa magari kupitia mjini kwa kelele nyingi; polisi hata wamewatoza faini madereva kwa kupiga honi kwenye msafara wa arusi. (Ona Mathayo 22:21.) Kwa kifupi, badala ya kuiga wonyesho wa kujivuna au matendo ya kawaida ya watu wa mataifa, Wakristo hudhihirisha hekima iliyo mali ya mtu mwenye kiasi.—Mithali 11:2.

Lakini vipi juu ya kuhudhuria arusi za majirani, wafanyakazi wenzetu wa kilimwengu, au watu wa ukoo wa mbali na watu tunaojuana nao? Kila Mkristo lazima aamue kibinafsi juu ya hilo. Ni vizuri kukumbuka kwamba wakati wetu ni wenye thamani, kwa kuwa twahitaji wakati kwa ajili ya huduma yetu, funzo la kibinafsi, na shughuli nyingine za familia na za kutaniko. (Waefeso 5:15, 16) Katika miisho-juma, tuna mikutano na utumishi wa shambani ambao hatutaki kukosa. (Waebrania 10:24, 25) Wakati unaopangiwa arusi nyingi huhitilafiana na makusanyiko au jitihada za kutoa utumishi wa pekee zinazofungamanishwa na Mlo wa Jioni wa Bwana. Hatupaswi kujiruhusu kupata kukengeushwa fikira ili tusifanye jitihada hizohizo za pekee wanazofanya ndugu zetu ulimwenguni pote ili kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana. Kabla ya kupata ujuzi juu ya kweli, tulitumia wakati mwingi pamoja na watu walimwengu, labda katika hali zilizomvunjia Mungu heshima. (1 Petro 4:3, 4) Sasa mambo tunayotanguliza ni tofauti. Siku zote yawezekana kuwatakia wenzi walimwengu furaha kwa kuwatumia kadi au kuwatembelea kwa muda mfupi siku nyingine. Watu fulani wametumia pindi hizo kutoa ushahidi, wakishiriki maandiko fulani yanayowafaa wale waliotoka kufanya arusi.

Arusi ambayo pande za kiroho zakaziwa kuliko njia za kilimwengu itamheshimu Yehova kikweli. Kwa kuhakikisha kwamba wanajitenga na ulimwengu pamoja na ushirikina na mazidio yayo, na kwa kutouruhusu kuingilia utendaji wa kawaida wa kitheokrasi, na kwa kudhihirisha kiasi badala ya wonyesho wa kujivuna, Wakristo watafurahia hiyo pindi. Isitoshe, wataweza kukumbuka hilo tukio kwa dhamiri njema na makumbukumbu mazuri. Kwa kuonyesha hekima na kiasi, arusi zetu zote za Kikristo na zitoe ushahidi kwa watazamaji wenye mioyo ya haki.

[Maelezo ya Chini]

a Vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Wakristo hawafuati kiutumwa kila desturi ya arusi ya kwaoy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki