Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 9/15 kur. 7-12
  • Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tatizo la Kupita Kiasi
  • Kufunga Ndoa Kisheria—Nyakati za Biblia na Leo
  • Arusi Kwenye Jumba la Ufalme
  • Ni Arusi ya Namna Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Arusi Zinazomheshimu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 9/15 kur. 7-12

Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha

1, 2. Itikio la watu wengi kwa neno “arusi” ni nini, na kwa sababu gani? (Mathayo 19:4-6)

MTUME Yohana, shahidi aliyejionea, anaripoti hivi: “Palikuwa na arusi huko Kana, mji wa Galilaya; naye mama yake Yesu alikuwapo. Yesu naye alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake.” (Italiki ni zetu.)—Yohana 2:1, 2.

2 Itikio lako kuelekea maneno hayo katika Yohana 2:1, 2 ni nini? Haingeshangaza kama unaitikia kwa uchangamfu, kwa maana neno “arusi” lina kidokezo cha furaha. Watu wanafurahia arusi. Kama tunavyosoma katika Mwanzo 2:18-24, arusi ya kwanza ilitokea katika Paradiso, wakati wanadamu walikuwa bila dhambi. Arusi ya mwanamume mkamilifu na mwanamke mkamilifu ilipangwa na kukubaliwa na Muumba wetu. Ilikuwa ya hali ya juu na ikaweka utangulizi wenye furaha kwa ajili ya arusi za wakati ujao.

3. Maandiko yanahusianisha arusi na roho gani, lakini ni gumu gani limetokea? (Yeremia 7:34)

3 Kufurahia kwako arusi kunakubaliana na yale tunayosoma katika Neno la Mungu. Andiko la Zaburi 45:15 likisimulia wenye kushiriki arusi ya kifalme, linasema: “Watapelekwa kwa furaha na shangwe, na kuingia katika nyumba ya mfalme.” Pia furaha inaonyeshwa katika mitajo ya mfano ya ndoa katika Biblia. (Mathayo 22:2-4; 25:1-10; Ufunuo 19:6-9) Ndiyo, ingawa ni hatua nzito inayochukuliwa, yaani, wenzi wawili kuingia ndani ya mpango mtakatifu wa ndoa, arusi zapasa kukumbukwa kuwa matukio yenye furaha, yenye heshima. Lakini, ripoti kutoka ulimwenguni pote zinaonyesha kwamba arusi nyingi zinakosa shabaha hiyo, na kutokeza matatizo na sikitiko kwa wenzi hao na huzuni kwa wale wanaohudhuria. Ndivyo imekuwa hata kwa arusi fulani zinazohusu watumishi wa Yehova. Kwa sababu gani?

4. (a) Kwa sababu gani arusi nyingi zinahusu watu wote? (b) Yesu alisema nini juu ya kuoa katika wakati wetu?

4 Katika nchi nyingi wenzi wanaweza kufunga ndoa katika sherehe ya faragha inayotimiza matakwa ya kisheria. Wenzi wawili wakichagua sherehe ya namna hiyo, wengine hawapaswi kuwalaumu au kufikiria kwamba lazima wawe wanaona haya kwa sababu ya jambo fulani. Inaweza kuwa ni kwa sababu tu wanapendelea hivyo na huenda hata kufanya hivyo kukawa na faida kubwa kweli kweli, kwa mfano, kiuchumi ili kujitayarisha kwa ajili ya ushiriki kamili zaidi katika utumishi wa Yehova. (Luka 12:29-31) Lakini, arusi nyingi zinakuwa za mahali peupe zaidi, na kunakuwako rafiki na watu wa ukoo wengi. Kwa njia hiyo badiliko la cheo la wenzi hao wawili linajulika zaidi katika jumuiya. Kukiwako sherehe ya kidini au hotuba ya Biblia, hali ya kiroho inaingizwa. Na wengine wanaweza kushiriki furaha ya wenzi hao wawili. Hayo ni mambo yanayofaa. Hata hivyo, arusi kubwa-kubwa zinatokeza hatari, hasa leo wakati ulimwengu unajihusisha sana katika ‘kuoa na kuolewa’ hata ‘hawatambui’ kwamba mfumo mbovu wa mambo uko karibu kufikia mwisho.​—Mathayo 24:37-39.

5. Ni nani wanaopaswa kupendezwa na mashauri ya Mungu juu ya arusi?

5 Ikiwa unatangulia kupiga picha ya kuona arusi yako ya Kikristo yenye furaha wakati ujao, kuna mambo yanayostahili kufikiriwa nawe. Lakini sisi sote ambao huenda tukawa waliokaribishwa au washiriki kwenye arusi za Kikristo twaweza pia kufaidika kwa kufikiria mashauri ya Biblia juu ya habari hii.

Tatizo la Kupita Kiasi

6. Arusi kubwa-kubwa zinaweza kutokeza matatizo ya namna gani?

6 Kwa watu wengi walimwengu, arusi kubwa yaweza kuwa ishara ya cheo, uthibitisho wenye kuonekana kuwa ni wenye pesa zaidi au wao ni maarufu (waheshimiwa) zaidi. Ni sikitisho kwamba hata Wakristo wanaweza kunaswa na kujaribu kushtua wengine kwa mavazi ya bei-bei au mipango mikubwa-mikubwa. (Wagalatia 5:26) Hivi karibuni wazee fulani Wakristo katika Afrika ya Magharibi walilalamika juu ya “mwelekeo mkubwa wa ‘kuiga’ ulimwengu katika desturi, kujionyesha na tafrija zenye kupita kiasi” kwenye arusi. Jambo hilo linaondoa heshima na furaha ambayo ni mambo yanayofaa katika maisha za wale ‘wasioenenda tena katika tamaa za mwili, wala mapenzi ya mwili.’ (Waefeso 2:3) Badala ya furaha na kumbukumbu nzuri, arusi hizo mara nyingi zinatokeza ‘mwenendo wenye kukosa adili, uadui, wivu, ugomvi, fitina, ulevi’​—kazi za mwili.​—Wagalatia 5:19-21.

7. Ni nini kinachoweza kuwasukuma wengine watake arusi za gharama kubwa-kubwa?

7 Maandishi ya historia yanatuambia kwamba wakati Ptolemi wa Tano Filometa alipomwoza bintiye kwa Aleksanda Balasi wa Siria, ‘walisherehekea arusi yake katika Ptolemaisi kwa kujionyesha kwingi, kama wafanyavyo wafalme.’ (1 Wamakabayo 10:58, The Oxford Annotated Bible) Leo, wengi ambao hawana pesa nyingi wana maoni kwamba wao (au watoto wao) ni lazima pia waoe “kwa kujionyesha kwingi, kama wafanyavyo wafalme.” Huenda wakawa wameingizwa katika kuwaza huko kwa kupita kiasi na matangazo ya kibiashara. Wafanyi biashara wanaotaka faida kwa arusi kubwa-kubwa zenye mapambo wanakazia sura ya bibi-arusi ambaye ndiye “malkia wa siku moja,” kama kwamba karatasi za ukaribishi za namna fulani, picha, maua au pete zinakuhakikishia kuwa na arusi kamilifu. Wanataka uwe na maoni, ‘Mara hii moja nastahili vilivyo bora zaidi’​—viwe vi katika uwezo wako wa kuvinunua au la. Huko “kujionyesha kwa mtu mali yake” ni kwa ulimwengu unaopita. (1 Yohana 2:15-17) Wazee fulani Wakristo walitoa maelezo haya: “Roho ya kushindana imeonekana. [Kwa mfano,] wakiwa wanaongozwa na desturi za kilimwengu, bibi-arusi na msafara wake huenda wakabadili na kuvaa mavazi ya bei mara nne au tano.”’

8. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mistari ya Biblia juu ya mavazi ya arusi? (b) Kwa sababu gani Wakristo wengine wakachagua vazi la arusi walilovaa?

8 Biblia haidokezi kwamba arusi zapasa kuwa shughuli zisizo na raha, za kujinyima starehe. Kwa mfano, tunasoma juu ya ‘bwana arusi ajipambaye kwa kilemba cha maua, na bibi arusi ajipambaye kwa vyombo vya dhahabu.’ (Isaya 61:10; Zaburi 45:13, 14; Isaya 49:18; Yeremia 2:32; Ezekieli 16:9-13; Ufunuo 21:2) Bibi-arusi wa mfano wa Kristo anasimuliwa kuwa ‘amevikwa kitani nzuri, ing’arayo, safi.’ Kwa hiyo, inafaa bibi-arusi na bwana-arusi (na walioko katika msafara wao) wavae mavazi safi, yenye kuvutia, lakini hawahitaji vazi linalotokeza magumu ya kifedha. Wenzi fulani wamechagua makusudi mavazi ya pesa chache zaidi ya wangaliyoweza kununua. Kwa sababu gani? Ili kuepuka mavazi ambayo huenda yakashtua, lakini yafanye wageni wasistarehe au ambayo yangeondoa heshima, furaha na hali ya kiroho ya arusi.​—Ufunuo 19:8; Mithali 11:2; 1 Timotheo 2:9.

9. Twapaswa kuwa na maoni gani juu ya desturi au mapokeo ya arusi?

9 Kisababishi kingine cha kupita kiasi kwenye arusi ni kukazia isivyofaa desturi za kiungwana​—sherehe nyingi ambazo “wataalamu” wa mambo ya kiungwana wanasema lazima zifuatwe. Hiyo maana yake si kwamba watumishi wa Mungu wanakataa kwa makusudi kila jambo ambalo ni desturi ya mahali kuhusiana na arusi.a Biblia inasimulia kwamba kwa kukamatana na kufunga ndoa, ‘Samsoni alifanya karamu; kwa kuwa vijana ndivyo walivyokuwa wakifanya.’ (Waamuzi 14:10) Lakini, kuiga kabisa sherehe za mikusanyiko ya watu kunaweza kujaa katika arusi, na kufunika maana halisi ya mwadhimisho huo na kumnyang’anya kila mtu furaha anayopasa kuona.

Kufunga Ndoa Kisheria—Nyakati za Biblia na Leo

10. Arusi zilikuwa namna gani katika nyakati za Biblia?

10 Tunaweza kufaidika na yale ambayo Biblia inasema juu ya arusi, hata ikiwa mazoea yanatofautiana wakati wetu na katika mahali petu. Katika kipindi cha Kibiblia hakuna sherehe ya pekee ya kisheria au kidini iliyohitajiwa. Bwana-arusi angeenda kwenye nyumba ya aliyemposa na kumsindikiza mbele ya watu wote mpaka kwenye nyumba yake. Jambo hilo lilifanywa kwa furaha na wenzi hao, watu wao wa ukoo wa karibu na watazamaji wengine ambao walionyesha msisimuko wa kupendezwa na tukio hilo la furaha. Mara nyingi bibi-arusi na bwana-arusi walikuwa wamevaa mavazi mazuri, na nyumbani mwake wangekuwa na karamu ya arusi pamoja na walioalikwa.​—Mwanzo 24:65-67; Mathayo 1:24; 25:1-10; linganisha 1 Wamakabayo 9:37, 39.

11. Maandishi ya ndoa yaliyohitajiwa nyakati za kale yalikuwa namna gani?

11 Mataifa yaliyowazunguka Waebrania yalikuwa na sheria zilizotaka mikataba ya ndoa iandikwe. Ingawa Biblia haitaji maandishi hayo, inasema juu ya ndoa kuwa “agano.” (Malaki 2:14) Maandishi ya Biblia ya nasaba za kijamaa yanadokeza kwamba ndoa ziliandikwa kwa njia fulani, na, jambo la kupendeza ni kwamba Yusufu na Mariamu walifuata namna fulani ya kujiandikisha kisheria. (Luka 2:1-5; 3:23-38) Vitabu vya mafunjo vya karne ya tano K.W.K. kutoka koloni ya Kiyahudi katika Elefantini (Misri) vina mikataba ya ndoa, na mmoja unasema:

‘ . . . Nimekuja nyumbani mwako ili unipe bintiyo Mifthaya katika ndoa. Yeye ni mke wangu na mimi ni mume wake tangu leo mpaka milele. Nimekupa wewe kuwa mahari ya bintiyo Mifthaya (jumla ya) shekeli 5 . . . . ’

12. (a) Mashahidi wa Yehova wana maoni gani juu ya ndoa za kiserikali? (b) Inafaa iweje ikiwa kuna sherehe ya kiserikali na ya kidini?

12 Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba lazima arusi ipatane na sheria za mahali, kwa njia hiyo ‘kumpa Kaisari yaliyo ya Kaisari.’ (Marko 12:17; Warumi 13:1, 7) Huenda sheria ikataka wenzi hao wachunguzwe damu, wajipatie kibali na kusema nadhiri mbele ya wakili wa ndoa mwenye mamlaka. Katika nchi fulani, ni maofisa wa serikali peke yao, kama vile meya au hakimu, wanaoweza kufanyisha ndoa. Lakini, washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo mara nyingi wanakuwa na maoni kwamba hawajafunga ndoa kabisa mpaka wafanye arusi kanisani. Wakristo wa kweli wanatambua kwamba ndoa ya serikali inatimiza kusudi, lakini wengine bado wanapendelea (au maoni ya watu wa mahali hapo huenda yakapendekeza iwe hivyo) shughuli hiyo ya kiserikali ifuatwe na hotuba ya Kimaandiko. Inapokuwa hilo lifanywe, ni vizuri zaidi kwamba jambo hilo lifuatishwe upesi baada ya ndoa ya serikali.b

13. Ikiwa mzee Mkristo ndiye atakayesimamia, inaelekea kutakuwa nini kabla ya arusi?

13 Nchi nyingine zinawapa mamlaka wahudumu wa Mashahidi wa Yehova kuwapa watu nadhiri za ndoa. Mara nyingi zinafanyishwa na wazee wa kundi, wanaume wenye ujuzi, ufahamu, ukomavu na maarifa ya Neno la Mungu. Mzee anayeulizwa asimamie yaelekea atatangulia kukutana na wanaotazamia kuwa bibi-arusi na bwana-arusi. Kama ilivyo, watataka kumhakikishia kwamba hakuna vizuizi vya kiadili wala kisheria vya kuwafanya wasifunge ndoa. Huenda akatoa mashauri mazuri ya Kimaandiko na ya kibaba. Pia yaelekea atazungumza pamoja nao juu ya mipango ya sherehe na mkusanyiko wo wote wa kirafiki utakaofuata, kwa kuwa atataka kuwa na dhamiri safi kuhusiana na tukio hilo ambalo anaombwa atimize sehemu kubwa.​—Mithali 1:1-4; 2:1; 3:1; 5:15-21; Waebrania 13:17, 18.

14. Ni hotuba za arusi za namna gani zinazofaa?

14 Iwe inatanguliwa na sherehe ya kiserikali au la, hotuba ya arusi inayotolewa na mhudumu wa Mashahidi wa Yehova yaweza kusaidia kukazia tangu mwanzo wake kwamba ndoa yapasa kuwa na hali ya kiroho. Hotuba hizo si ndefu sana, kama kwamba zinasema yote ambayo Biblia inasema juu ya ndoa, wala hazipasi kujawa sana na ucheshi wala kuwasifu wenzi hao wawili kupita kiasi. Mambo yenye usawaziko, ya furaha na ya Kimaandiko ya hotuba hizo yaweza kuwafaidi wale wanaofunga ndoa, na pia wale waliohudhuria.c—2 Timotheo 3:16.

15. Nadhiri zinazotumiwa na Mashahidi wa Yehova zinatofautianaje na zile zinazotumiwa leo?

15 Nadhiri zinakuwa sehemu ya arusi nyingi. Nadhiri zinazotumiwa katika arusi fulani za kilimwengu za “kisasa” zimetungwa kutokana na mashairi ya kiajabu-ajabu, au zinataja juu ya vitabia-tabia vya mtu maishani. Insha ya gazeti Time juu ya “hatari za Nadhiri Zilizobuniwa Nyumbani” ilieleza juu ya kiongozi mmoja wa dini aliyeuliza: “Gina, unakubli kumpenda Peter zaidi ya unavyopenda chokoleti?” Halafu kwa Peter: “Unakubali kumpenda Gina zaidi ya unavyopenda gazeti la asubuhi?” Lakini makala hiyo ilikazia kwamba “arusi ni shughuli inayohusu watu wote” na yapasa kutoa heshima kwa hatua hiyo ya kijamii inayochukuliwa. Kwenye arusi za Mashahidi wa Yehova nadhiri zitapatana na matakwa ya sheria ya mahali. Mahali zinapokubalika, nadhiri hizi zinazomheshimu Mungu, aliye Chanzo cha ndoa, zinatumiwa:

“Mimi​——nakuchukua wewe​——uwe mke wangu wa ndoa, nikupende na kukutunza sana kulingana na sheria ya kimungu iliyoonyeshwa katika Maandiko Matakatifu kwa ajili ya waume Wakristo, kwa muda wote ambao sisi wawili tutaishi pamoja duniani kulingana na mpango wa ndoa wa Mungu.”

“Mimi​——nakuchukua wewe​——uwe mume wangu wa ndoa, nikupende na kukutunza na kukuheshimu sana sana, kulingana na sheria ya kimungu iliyoonyeshwa katika Maandiko Matakatifu kwa ajili ya wake Wakristo, kwa muda wote ambao sisi wawili tutaishi pamoja duniani kulingana na mpango wa ndoa wa Mungu.”

Nadhiri hizo hazipasi kubadilishwa wala nyingine kuwekwa mahali pazo ili kufaa mapendezi fulani ya wenzi hao wawili.d

Arusi Kwenye Jumba la Ufalme

16, 17. (a) Baraza la wazee linahusikaje na arusi kwenye Jumba la Ufalme? (Yakobo 3:17) (b) Kwa sababu gani inafaa wahusike hivyo?

16 Wakristo wanaambiwa waoe “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Wakati Wakristo wawili wenye msimamo mzuri katika kundi wanataka kufanya arusi yao (au, hotuba ya arusi) kwenye Jumba la Ufalme, wanapaswa kuomba ruhusa kwa baraza la wazee.e Wanaume hao hawataweka mapendezi yao ya kibinafsi kuhusiana na mipango ya arusi, bali watauliza wajue mipango ya wenzi hao wawili ili jambo lo lote lisifanywe kwenye Jumba ambalo litaelekea kulisumbua kundi.​—Linganisha 1 Wakorintho 14:26-33.

17 Kwa mfano, mambo yenye kusumbua yameripotiwa juu ya arusi ambazo hazikuwa kwenye Jumba la Ufalme. Kabla ya arusi moja, muziki wenye sauti kubwa ulichezwa, na bibi-arusi, bwana-arusi na msafara wao waliingia ndani ya jumba lililokodishwa wakicheza dansi. Waliokaribishwa wakajiunga katika kucheza dansi hiyo mpaka mwenyekiti mmoja alipokatisha jambo hilo ili, baada ya sala, hotuba ya arusi ianze. Kwa wazi, hiyo haikuwa hali inayofaa arusi ya Kikristo. Lakini, jambo hilo linaonyesha ni kwa sababu gani wazee wanajihadhari kuhusiana na arusi kwenye Jumba la Ufalme. Kwenye Jumba hilo, ni muziki wenye kujenga peke yake, kama ule unaopatikana katika kitabu cha nyimbo cha Mashahidi wa Yehova, ndio unaotumiwa. Maua yo yote au mapambo kama hayo yapasa kuwa ya kiasi, ndivyo pia na jinsi ambayo msafara wa arusi unaingia kwenye Jumba na jinsi picha zinavyopigwa.​—Wafilipi 4:5.

18. Ni nani wanaoweza kuwa pamoja na bibi-arusi na bwana-arusi kwenye arusi? (1 Wakorintho 5:13; Yakobo 2:1-4)

18 Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida kulikuwako “rafiki yake bwana arusi” na wenzi wa kike wa bibi-arusi. (Yohana 3:29; Zaburi 45:14) Pia hivyo ndivyo ilivyo mara nyingi kwenye arusi za Jumba la Ufalme. Hata hivyo, kiasi kinahitajiwa juu ya ni wangapi watakuwa kati ya washiriki hao, na pia jinsi wanavyovaa na kutenda. Haingefaa kuweka katika msafara wa arusi watu ambao wametengwa na ushirika au wale ambao mtindo wao wa maisha wenye kuudhi unapingana sana na kanuni za Biblia. (2 Wakorintho 6:14-16) Badala ya kuchagua watu ambao ni mashuhuri au ambao huenda wakatoa zawadi ya pesa nyingi, wenzi wengi Wakristo (na wasemaji) wanapendelea katika msafara kuwemo watu ambao wako karibu nao katika kumtumikia Yehova.

19. Ni kukaza fikira kwenye mambo gani mengine kutasaidia arusi kwenye Jumba la Ufalme iwe yenye furaha?

19 Ikiwa Jumba la Ufalme litatumiwa, tangazo fupi laweza kutolewa kuhusu wakati wa arusi. Kwa njia hiyo kundi litajua kwamba Jumba litatumiwa na wanaweza kuhudhuria wakichagua kufanya hivyo. Kwa kuwa Jumba la Ufalme liko kwanza kwa ajili ya mikutano ya Kikristo, arusi itakuwa wakati ambao hautaingiliana nayo. Wakati wo wote itakaopangiwa, inaonyesha upendo na kujali kwa wote kufika bila kuchelewa. Katika mfano ambao Yesu alitoa unaohusu arusi ‘bwana arusi alikawia,’ na jambo hilo likasababisha matatizo makubwa kwa wengine.​—Mathayo 25:1-12.

20. Ni sehemu gani nyingine ya arusi inayostahili kukaziwa fikira zetu?

20 Nabii Isaya aliandika juu ya ‘bwana arusi kumfurahia bibi arusi.’ (Isaya 62:5) Bibi-arusi pia anafurahi wakati wa arusi yake. Wengi wenye kuwatakia mema pia, ‘wanafurahia sana’ arusi za Kikristo. (Yohana 3:29) Mara nyingi furaha hiyo inaonyeshwa na kuongezwa na mkusanyiko wa kirafiki baada ya arusi, karamu ya arusi. Ni mashauri gani ambayo Yehova anatoa katika Neno lake yatakayotokeza furaha badala ya matatizo kwenye mikusanyiko hiyo? Ebu tuone.

[Maelezo ya Chini]

a Kuhusu mazungumzo ya desturi za arusi, ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Januari 15, 1969, kurasa 58 na 59.

b Ikiwa kipindi kirefu kinaruhusiwa kipite, watu katika jumuiya wanaweza kukwazwa na mwendo wa wenzi hao wawili, juu ya kama wameishi wakiwa mume na mke au wamejiepusha kufanya hivyo.​—2 Wakorintho 6:3.

c Mazungumzo ya Kimaandiko ambayo yaweza kuwa msingi wa hotuba hizo yaweza kupatikana katika Mnara wa Mlinzi wa Februari 1,1970, kurasa 39-44 (w3/15/69, kur. 174-9); Oktoba 15,1976, kurasa 459-63 (w5/1/74, kur. 274-7); Agosti 15, 1977, kurasa 370-81 (w3/15/77, kur. 172-85).

d Ikiwa nadhiri za ndoa zilikuwa zimetangulia kufanyishwa na afisa wa serikali na ndoa hiyo inafuatwa na hotuba ya arusi ya Kikristo, mhudumu huenda akataja kwamba hatua ya kisheria imekwisha kuchukuliwa. Wenzi wengine wangali wanachagua kurudia nadhiri hizo mbele za Mungu na kundi.

e Pindi fulani fulani watu wawili wanaomtumikia Mungu wakingojea kusanyiko wabatizwe wamefanyia arusi kwenye Jumba la Ufalme.

Wewe Unakumbuka Jambo Hili?

◻ Wakristo wanapaswa kuwa macho kuona hatari gani zinazohusu arusi za gharama kubwa-kubwa?

◻ Mashahidi wa Yehova wanachukua msimamo gani kuhusu sherehe za arusi za kiserikali au kidini?

◻ Maamuzi ya wenzi wawili wa ndoa kuhusu sherehe yao ya arusi yanawezaje kuongeza furaha ya Kikristo ya tukio hilo?

◻ Ni arusi za namna gani zinazoweza kufanyiwa kwenye Jumba la Ufalme?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa furaha na heshima bwana-arusi Mwebrania angemleta nyumbani bibi-arusi wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki