Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 10/15 kur. 459-462
  • Ni Arusi ya Namna Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Arusi ya Namna Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MKAZO JUU YA BIBLIA
  • NADHIRI YA NDOA
  • YENYE FURAHA, YENYE HESHIMA NA YA KIPEKEE
  • NI NANI AWEZAYE KUTUMIA JUMBA?
  • Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 10/15 kur. 459-462

Ni Arusi ya Namna Gani?

HABARI zinazotoka nchi mbalimbali zaeleza arusi za namna nyingi. Kwa mfano, Wajeremani wawili wafanya michezo ya ustadi waliozwa wakiwa katika pembea juu sana ya njia kuu ya mji. Halafu kuna warukaji wawili wa parashuti angani walioshuka duniani, wakiwa wamefuatwa na padre aliyewaoza pale pale waliposhukia.

Ingawa huenda mambo kama hayo yakawa hayafanyiki sana, wavulana na wasichana wengi zaidi na zaidi wanataka kuoana wakiwa peke yao au bila kuwa na watu wengi sana. Watu hao wameona kwamba arusi nyingi zinazokuwa na watu wengi zinakuwa za kidesturi tu wala si za moyoni na zina gharama nyingi na mambo ya mila ili kuvutia marafiki na watu wa ukoo tu. Bila shaka kujionyesha hivyo mara nyingi huondoa fikira za watu katika maana halisi na furaha ya wakati huo.

Kwa kupinga jambo hilo, miaka iliyopita umetokea unaoitwa “Mtindo Mpya wa Arusi.” Katika mtindo huu mvulana na msichana hawafuati mara nyingi desturi na maoni ya wazee wao. Huenda wakaoana kando ya mlima, katika ufuo wa bahari au katika pango, badala ya katika kanisa au chumba cha hakimu. Katika mtindo huo mpya huenda mvulana na msichana wakasoma shairi badala ya kurudia nadhiri zile zile za kidesturi za arusi (wakiiga arusi iliyoonyeshwa katika sinema ya majuzi). Katika arusi moja ya namna hiyo iliyofanywa karibu na Los Angeles, California, mvulana na msichana mmoja walirudia maneno yafuatayo:

“Nafanya langu, wewe wafanya lako. Simo katika ulimwengu huu kutimiza unayotarajia. Nawe humo katika ulimwengu huu kutimiza ninayotarajia. Wewe ni wewe na mimi ni mimi na kwa bahati tukipatana, ni vizuri sana.”

Sasa, kulingana na maoni yako, bila shaka pande zote mbili hazipendezi. Inaelekea utakubali kwamba hakuna haja ya kuwa mtumwa mnyonge wa sheria nyingi nyingi. Lakini pengine waamini pia kwamba arusi haipaswi kuwa tendo la kujionyesha kwa kufanya utakavyo tu bila kufikiria maoni ya wengine na hali na heshima ya wakati huo.

Basi, ni hali gani iliyo ya kiasi? Wakati mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanapopanga arusi, wanafikiria mambo ya lazima hasa waone ni arusi ya namna gani itakayokuwa ya adabu na heshima. Ndiyo sababu watazamaji hushangaa mara nyingi juu ya wanayoona wahudhuriapo arusi katika Majumba ya Ufalme.

MKAZO JUU YA BIBLIA

Ingawa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ni mahali pa maana ambapo kundi hukutana kujifunza Biblia, nyakati nyingine arusi hufanyiwa humo pia.a Hiyo yafaa kwa kuwa Biblia yenyewe yaonyesha kwamba ndoa ni jambo lililoanzishwa na Mungu.​—⁠Mwa. 2:24.

Kama inavyofaa kwa sherehe katika Jumba la Ufalme, hotuba ya Maandiko hutolewa juu ya maana ya ndoa na mapendeleo na madaraka ya mume na mke. Halafu, mwishoni mwa hotuba hiyo yenye kujenga, huenda nadhiri ikawekwa au kukubaliwa, kupatana na matakwa ya sheria ya nchi.

Katika El Salvador na nchi nyingine ndoa haiwezi kufanywa katika jengo la kidini. Lazima iongozwe na hakimu wa mjini, kama vile katika Alcaldia (afisi ya meya). Lakini, katika nchi hizo mashahidi wa Yehova hufuata mara nyingi ndoa hiyo ya mjini halafu hotuba ya Maandiko inatolewa katika Jumba la Ufalme. Ingawa hatua hiyo si ya lazima, ni hatua nzuri. Siku ya arusi ya mtu ni wakati wenye furaha, na pia ni wakati unaofaa kukumbuka shauri lenye hekima la Mwanzishi wa ndoa.​—⁠Zab. 119:1.

NADHIRI YA NDOA

Kama ilivyotajwa, nyakati nyingine sheria ya nchi hutaka bibi-arusi na bwana-arusi watangaze hadharani au waweke nadhiri mbele ya wengine, nao mashahidi wa Yehova hufuata sheria hiyo. Lakini hata katika nchi ambako jambo hilo si lazima lifanywe, kwa kawaida mvulana na msichana hutaja au huitikia nadhiri ya ndoa.

“Mtindo Mpya wa Arusi” uliotajwa mapema waonyesha kwamba hata katika nadhiri ya ndoa kuna maelekeo ya ‘kufanya lako mwenyewe.’ Nyakati nyingine mvulana na msichana hujitungia nadhiri yao wenyewe; nyakati nyingine kiongozi wa dini ndiye hufanya hivyo. Hivyo katika kanisa moja padre ‘alioza’ mwanamke na mwanamke mwenzake ‘maadamu wanapendana.’ Pasta mwingine alioza mvulana na msichana walio uchi ‘maadamu wangethaminiana.’

Tofauti sana na maelekeo hayo, ambayo yanavunja heshima ya hali ya ndoa iliyopewa na Mungu, mashahidi wa Yehova wanatumia nadhiri ifuatayo, kama ilivyopendekezwa katika Mnara wa Mlinzi wa Februari 1970:

Kwa bwana-arusi: “Mimi​—⁠—​—⁠​—⁠​—⁠ nakuchukua wewe​—⁠—​—⁠​—⁠​—⁠ uwe mke wangu wa arusi, nikupende na kukutunza sana kulingana na sheria ya kimungu iliyoonyeshwa katika Maandiko Matakatifu kwa waume wa Kikristo, kwa kadiri sisi wote wawili tutakavyoishi pamoja duniani kulingana na mpango wa Mungu wa ndoa.”

Kwa bibi-arusi: “Mimi​—⁠—​—⁠​—⁠​—⁠ nakuchukua wewe​—⁠—​—⁠​—⁠​—⁠ uwe mume wangu wa arusi, nikupende na kukutunza sana na kukuheshimu sana sana, kulingana na sheria ya kimungu iliyoonyeshwa katika Maandiko Matakatifu kwa wake wa Kikristo, kwa kadiri sisi wote wawili tutakavyoishi pamoja duniani kulingana na mpango wa Mungu wa ndoa.”

Lakini yako mengi zaidi yanayohusika juu ya arusi inayofanywa katika Jumba la Ufalme?

YENYE FURAHA, YENYE HESHIMA NA YA KIPEKEE

Mtoa habari mmoja alisema: “Arusi ya Kiamerika ni wonyesho wa mambo makuu tunayotaka: mapenzi na fedha, pamoja na mahaba mengi na kujitafutia cheo.” Huenda hiyo ikawa ndiyo hali katika nchi nyingine pia. Walakini, Wakristo katika nchi zote wanatia mkazo juu ya pande za Kibiblia, za kiroho za arusi. Hiyo nayo yawasaidia wawe wenye adabu na kiasi, ‘kujulisha kiasi chao kwa watu wote.’​—⁠Flp. 4:5.

Je! maana yake ni kwamba arusi zinazofanywa katika Jumba la Ufalme ni sawa zote, au kwamba hazipendezi na zinafanywa vivi hivi tu? Sivyo. Arusi hizo ni zenye heshima lakini zenye furaha, sawa na arusi za nyakati za Biblia. (Zab. 45:13-15; Isa. 62:5; Ufu. 19:7,8) Mara nyingi kunakuwa na mapambo, maua ya pekee na muziki wa Kibiblia unaotokana na kitabu cha nyimbo kinachotumiwa katika Jumba la Ufalme; hayo yote yafanya arusi iwe yenye shere.

Tena kunakuwa na namna mbalimbali za kufanya mambo kulingana na mapendezi ya mtu. Katika nyakati za Biblia bibi-arusi alijipamba mapambo mbalimbali na mavazi ya kisherehe. (Isa. 49:18; 61:10; Ufu. 21:2) Kwa hiyo katika arusi inayofanywa katika Jumba la Ufalme, njia mbalimbali za kufanyia mambo zaweza kuonekana. Kwa mfano, huenda bibi-arusi akawa amevaa vazi la pekee, au huenda akachagua kuvaa vazi litakalofaa kuvaliwa katika sherehe za wakati ujao.

Huenda pia kukawa na njia tofauti tofauti za kufanyia mambo kuhusu wale wanaoshiriki arusini. Katika Lebanon bibi-arusi na bwana-arusi kwa kawaida huwa na rafiki wakubwa kama wenzi wao. (Mt. 25:1; Yohana 3:29) Kwa kawaida wanaochaguliwa wawe wenzi wa karibu zaidi wakati huu wenye furaha ni ndugu na dada za kiroho, watu ambao wanatumaini pia kumtumikia Yehova milele. Kwingine, huenda ikawa ni desturi mzazi kuketi pamoja na wenye kuoana. Lakini ikiwa hakuna sheria zinazotaka iwe hivyo, wenye kuoana wanaweza kujipangia hilo wapendavyo.

Vivyo hivyo, wenye kuoana wanaweza kupanga namna wanavyopenda kufanya mambo mengine. Ni juu yao kuamua kama watavalishana pete, kama wataingia jumbani kwa njia fulani ya pekee, wawe na viburudisho mahali pengine baada ya arusi, na kadhalika. Wao wanajua desturi za kwao, lakini si lazima wawe watumwa wa mapokeo.b Jambo la maana zaidi ni kuwa na arusi yenye furaha na heshima itakayopendeza na kujenga kiroho wote watakaohudhuria.

NI NANI AWEZAYE KUTUMIA JUMBA?

Bila shaka, mashahidi wa Yehova hawakatazwi kuoana katika nyumba fulani au mahali fulani ambako ndoa huendeshwa na serikali. Lakini ikiwa wanapendezwa na kuwa na arusi katika Jumba la Ufalme, waione halmashauri ya kundi yenye wahudumu watatu wanaosimamia mambo hayo.

Wahudumu hao watahakikisha kwamba wale wawili wote wanaotazamiwa kuoana wako huru kufanya hivyo kulingana na Maandiko na wana msimamo mwema kundini. Pia, watauliza wanaotaka kuoana sherehe wanayofikiria kuwa nayo. Halmashauri yajua kwamba mapendezi ya watu hutofautiana, na haipaswi kutwika mtu ye yote mapendezi yao. Hata hivyo itachunguza ihakikishe hakuna jambo lililopangwa litakalokwaza au kuondoa amani na umoja wa kundi.​—1 Kor. 1:10; 14:33.

Kupatana na shauri la wazi la Biblia, yaani, ‘kuoa katika Bwana tu,’ mashahidi wa Yehova hawatii Mkristo moyo aoe au aolewe na mtu asiyebatizwa bado na asiyemtumikia Yehova. (1 Kor. 7:39) Mtu asipofuata shauri hilo la Biblia, ataelekea kupatwa na matatizo mengi na huzuni nyingi, kama ilivyoonekana kwa wengine. (Neh. 13:25-27) Lakini ndoa ya namna hiyo itaruhusiwa katika Jumba la Ufalme?

Halmashauri ya waangalizi ndiyo itakayoamua. Kisa kimoja huenda kikahusu Mkristo mpya anayetaka kuoa au kuolewa na mtu aliyechumbiana naye kabla ya kujifunza kweli ya Neno la Mungu. Katika kisa kingine huenda hali zikawa tofauti sana. Kwa hiyo, kila hali inaamuliwa peke yake. Kwa kuwa wahudumu hao wanajua mambo ya hakika na maoni yanayoweza kutokea mahali pao, wanawaza kuamua jambo litakalofaidi wote.

Nyakati nyingine wenye kutaka kuoana ambao bado wanajifunza Biblia na Mashahidi wameozwa katika Jumba la Ufalme. Kwa mfano, mume na mke Denmark walitaka kuwa na hotuba ya arusi katika Jumba la Ufalme karibu na nyumbani kwa bibi-arusi, kabla hawajahama kwenda kwa mume, Spania. Wahudumu wenye kuangalia kundi walitoa ruhusa. Waliona kwamba watu hao wawili walikuwa wakifanya maendeleo halisi wakawe Wakristo na waliamini kwamba watu hao na rafiki na watu wa ukoo wao wangefaidika na mashauri ya Biblia ambayo yangetolewa katika hotuba ya ndoa.

Kwa hiyo, ukiwa na wakati wa kuhudhuria arusi katika Jumba la Ufalme, utaona ni ya kufurahisha, yenye heshima na yenye kufaidi kiroho. Huenda ukaona mambo fulani yanayoonyesha desturi za eneo. Mambo mengine yataelekea kuonyesha mapendezi ya bwana-arusi na bibi-arusi. Lakini utasikia pia hotuba yenye kusaidia na kujenga juu ya ndoa kutoka Neno la Mungu aliloliongoza.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa kawaida, arusi na matayarisho yo yote yake yatapangwa yafanyike katika orodha ya kawaida ya utumishi mbalimbali unaofanywa katika Jumba.

b Maoni marefu zaidi juu ya desturi za arusi pamoja na karamu za nyakati hizo yatachapwa katika matoleo yafuatayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki