Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 12/1 kur. 549-552
  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIASI CHA KIKRISTO
  • DESTURI ZA NDOA
  • MAVAZI YA ARUSI
  • SHEREHE YENYEWE
  • Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Ni Arusi ya Namna Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Arusi Zinazomheshimu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Arusi za Kikristo Ambazo Zinaleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 12/1 kur. 549-552

Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi

PENGINE wewe hujapata kuona arusi ya kutapanya pesa mno. Hata hivyo inaelekea unajua arusi nyingine huwa za kiasi na nyingine zenye mambo mengi mno, nyingine, za kikawaida tu na nyingine zenye gharama nyingi mno, nyingine zenye kumheshimu Mungu na nyingine zisizomcha Mungu.

Basi, je! Mkristo ampendaye Mungu na atakaye kuongozwa na kanuni za Neno lake ataamuaje mipango ya arusi yake mwenyewe? Ataamuaje kiasi kinachofaa? Akifanya mambo yawe magumu zaidi, mwandikaji mmoja alisema: “Hakuna sherehe inayotegemea mapokeo zaidi na mambo ya kidesturi kuliko arusi.” Je! Mkristo ajaribu kufuata mapokeo yote, mengine yayo, au asifuate yo yote? Arusi ya Kikristo yenye kiasi ni nini hasa?

KIASI CHA KIKRISTO

Wakristo wa kweli wanajua kwamba wanapooa au kuolewa, sherehe lazima itimize matakwa ya sheria ya kilimwengu, ndoa iwe ya kidini au ya kiserikali kama vile kortini au katika afisi ya uandikishaji. (Luka 20:25) Katika dunia yote mashahidi wa Yehova wanajua hivyo na kwa hiyo wao hutimiza matakwa ya nchi. Hata hivyo maulizo yanabaki juu ya desturi fulani zinazofuatwa katika sherehe ya arusi. Wakristo wafanye nini hasa?

Sifa kuu inayohitajiwa ili kupata maoni yanayofaa juu ya habari hii ni kiasi. Ni jambo ambalo Wakristo wamepaswa kuonyesha katika utendaji wao wote, lakini linahitajiwa zaidi katika sherehe zinazohusu watu wengi sana na mapokeo. Akiongozwa na Mungu mtume Paulo aliandikia Wakristo wa siku zake mashauri mema, na kumbuka, hata wao walikuwa wakioa na kuolewa na walikuwa na arusi. Alishauri hivi: “Kiasi chenu na kijulikane na watu wote.” (Flp. 4:5, NW) Akikazia hilo, mwanafunzi Yakobo alisema kwamba hekima itokayo kwa Yehova ni “yenye kiasi.”​—⁠Yak. 3:17, NW.

Wakristo waliokomaa kiroho na wanaothamini ubora wa kutumia kanuni za Maandiko huonyesha hivyo kwa kudhihirisha kiasi. Bila ya kuhitaji orodha ndefu yenye sheria za waziwazi, wanajiangalia pande za kiroho za arusi zisifunikwe na mambo ya kisherehe tu.

Walakini, arusi moja Brazil ilikuwa na madoido mengi sana kwa sababu wenye kuoana walikuwa matajiri, tena arusi yenyewe ilikuwa ya utajiri mwingi mno isivyo kawaida ikilinganishwa na Jumba la Ufalme la kikawaida ambamo hotuba ya Biblia ilitolewa. Kwa wengi waliokuwako, gharama nyingi mno za mipango, vazi la kike lenye anasa nyingi mno, wingi mkubwa wa wanawali watumikiaji wa bibi-arusi na wakaribishaji na mambo mengine mengi, yalivuta fikira sana hata yakafunika mashauri mema yaliyotolewa katika Maandiko. Kwa kweli, wakati kiasi kinapopotezwa, mambo hupotezwa na watu wengi, kutia na bibi-arusi na bwana-arusi.

DESTURI ZA NDOA

Kwa sababu yako mapokeo mengi sana, je! Mkristo ajaribu kuepuka desturi zote za arusi za eneo lake? Si lazima. Aweza kuchagua. Desturi nyingine za ndoa huwa na msingi unaofaa, kama vile kuoa au kuolewa siku ambayo watu wengi zaidi hawafanyi kazi ya kimwili, au wakati wa mchana kusipokuwa na joto jingi sana, baada ya mapumziko ya mchana. Au huenda mapokeo fulani yakapendwa zaidi nchini; mtu asingetazamia watu wa Korea wavalie kama wenyeji wa Lebanon, Finland au Fiji.

Bila shaka, desturi nyingine hazilingani na Maandiko na kwa hiyo haziwafai Wakristo. Katika nchi nyingi desturi zisizo za kawaida zinafuatwa ili bibi-arusi na bwana-arusi au wageni wao wawe na “bahati.” Mashahidi wa Yehova hawaabudu mungu wa Bahati Njema. (Isa. 65:11) Wala hawafuati mapokeo yanayoweza kufanya watazamaji wadhani kwamba wanamwabudu. Desturi nyingine huonekana wazi kwamba ni ibada za uongo. Kwa hiyo mtu anayepanga arusi apaswa kuchunguza mazoea yanayofuatwa sana katika eneo lake na kuchunguza watu huyaonaje. Ikijulikana kwamba desturi inahusiana na dini ya uongo au “bahati,” Mkristo ataiepuka.​—2 Kor. 6:14-18.

Mapokeo mengine yanapita kiasi na si ya upendo. Katika nchi nyingi ni jambo la kawaida kutupia bibi-arusi na bwana-arusi wali (mchele). Maana ya desturi hiyo ni nini? “Watu wengine huamini wali huo ni chakula cha kuondolea bibi-arusi na bwana-arusi maongozi maovu. Wengine husema unahakikishia hao wawili kwamba watapata watoto.” (Science News Letter, Juni 8, 1963, uk. 357) Hii yaonyesha kwamba mara nyingi kunakuwa na maoni kadha juu ya asili ya desturi fulani. Lakini hata bila kujali desturi hii ilianzaje, je! kwa kawaida Wakristo huchukua chakula watupie rafiki zao, wakichafua barabara wanapofanya hivyo? Pia, fikiria shauri la kumpenda jirani yako kama nafsi yako mwenyewe. Je! upendo wa Kikristo ungeongoza mtu afanye mizaha kuaibisha bibi-arusi na bwana-arusi? Yesu alisema: “Kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”​—⁠Luka 6:31; 10:27.

Halafu kuna mapokeo ya pete ya arusi. Kuchunguza jambo hili kwaweza kukuacha umevurugika bila kujua asili na maana ya pete ya arusi; madai ni mengi, mambo ya hakika yamevurugika. Hata ikiwa Biblia haitaji pete za arusi moja kwa moja, ni wazi kwamba watumishi wa Yehova wangeweza kuvaa pete. (Ayubu 42:11, 12; Luka 15:22) Lakini namna gani ikiwa watu wa nchi ya mtu wanaamini pete ya arusi yamaanisha imani ya mume na mke, upendo wao na uaminifu wao hauvunjiki? Wakristo hawashikamanishi maana yo yote ya mfano na pete ya arusi, ingawa wanasitawisha sifa hizi katika ndoa, na hata ikiwa wengi katika ulimwengu ni wanafiki wanapodai wanaonyesha sifa hizo. Pete ya arusi haihakikishii lo lote. Huonyesha wengine watu wameoana tu. Si vibaya kwa Mkristo kuonyesha ameoa au ameolewa kwa kuvaa pete ya arusi, iwe mkono wa kuume, kama katika Ujeremani, au iwe katika mkono wa kushoto. Lakini hiyo si lazima kusipokuwa na sheria. Kwa hiyo wanaotazamia kuoana wanaweza kuamua la kufanya kulingana na pesa walizo nazo na mapendezi yao.

Kwa hiyo, kwa habari ya desturi za arusi mtu aweza kuwa mchaguzi, akijiuliza: Maana ya desturi yenyewe ni nini katika nchi siku hizi? Je! itaudhi wengine? Je! ni ya upendo? Je! ni ya kiasi?

MAVAZI YA ARUSI

Uamuzi mmoja ambao itawapasa wanaotazamia kuoana wafanye kabla ya arusi ni mavazi. Arusi ya mtu ni kipindi cha pekee, kwa hiyo kwa kawaida watu huangalia waonekane wenye furaha na wenye kuvutia. Lakini hiyo haimaanishi lazima mtu avae vazi fulani la kike au suti. Yampasa afikirie mitindo ya kwao, gharama na mapendezi yake.

Nyakati za Biblia bibi-arusi na bwana-arusi mara nyingi walivaa mavazi mazuri sana. (Zab. 45:13, 14; Yer. 2:32) Hata mji mtakatifu, Yerusalemu Mpya, unasimuliwa kama “bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe.” (Ufu. 21:2) Yale mavazi ya ndoa yenye mapambo hayapingi Maandiko. Lakini, si ya lazima ili arusi iwe yenye furaha. Mapambo ya kiroho ndiyo ya maana zaidi.​—1 Pet. 3:3, 4.

Watu waliochumbiana wakitaka kununua vazi la kike la pekee na hali ziwaruhusu, ni juu yao kuamua. Lakini, je! kingekuwa kiasi kununua vazi la gharama nyingi hivyo wajiletee wenyewe mzigo na wengine? Mkristo mmoja katika kaskazini ya Ulaya aliacha pendeleo la kutumikia kama mtumishi wa pekee wa wakati wote afanye kazi ya kimwili ndiyo apate vazi la arusi la kike lenye kupendeza sana. Wewe wadhani ni jambo jipi lingalikuwa lenye ubora wa kudumu kwa msichana huyo? Na namna gani wanaotumikia bibi-arusi? Je! watajiona wana lazima ya kununua mavazi ya gharama nyingi ati kwa sababu vazi la bibi-arusi ni la kitajiri?

Jambo hili la mavazi laweza kushughulikwa kwa njia mbalimbali. Ingawa wengi wamenunua au wakakodi mavazi ‘ya arusi,’ mabibi-arusi wengine wamefurahia kutumia vazi la rafiki mpenzi au mtu wa ukoo. Wengine wametosheka sana kwa kujifanyia mavazi yao wenyewe ya kibibi-arusi, labda kwa njia hiyo wakaweza kuwa na vazi la matumizi ya nyakati nyingine siku zijazo.​—⁠Mit. 31:13, 22.

Na inafaa kabisa wanaooana wafanye arusi wakiwa wamevaa mavazi yao ya kawaida yenye kuvuta zaidi, wayafanye malidadi na safi kwa wakati huo. Wengine wamefanya hivyo ili waweze kutumia pesa zinazookolewa ziwasaidie waingie katika utumishi wa upainia au wauendeleze. Wengine walio na uwezo wa kuwa na arusi yenye madoido (mapambo mengi sana) wanaweza wenyewe kutaka wawe na arusi tulivu kwa sababu ya hatari ya nyakati hizi, ‘wakitazamia hata ije siku ile ya Yehova, na kuihimiza.’​—2 Pet. 3:12.

Ingawa marafiki na watu wa ukoo wenye makusudi mema huenda wakawa na mawazo juu ya jinsi wao wangeipanga arusi, na ingawa mawaidha mengine yanayotegemea ujuzi huenda yakasaidia, wenye kuoana wamepaswa kuacha arusi yao iwe na mapendezi yao na mipango yao wenyewe ya wakati ujao. Na ikiwa mawazo yanatofautiana kidogo, bibi-arusi na bwana-arusi wanaweza kutatua hilo kwa upendo. Ndivyo inavyopaswa kuwa baada ya arusi, wote wawili wakiutambua mpango wa Mungu wa ukichwa katika jamaa. Kwa hiyo hii ingekuwa nafasi yao kuonyesha wanaweza kupatana kwa upendo na kulingana na kanuni za kimungu.​—⁠Efe. 5:22-33.

‘Lakini namna gani kuvaa mavazi meupe, na kuwa na shela?’ wengine wameuliza. Kama kwa habari ya mapokeo mengine, mawazo juu ya maana ya vitu hivi yatofautiana sana. Kwa wengine Ujeremani, vazi jeupe la kike humaanisha aliyelivaa ni bikira. Wengine huko huamini kwamba linazuia pepo wabaya wasimtambue bibi-arusi. Katika Japan wengine huona vazi jeupe la kike kama ishara ya maombolezo; bibi-arusi ‘hufa’ kwa wazazi wake na kukaa na mumewe mpaka kufa. Walakini, kwa watu wengi duniani mwote, vazi jeupe ni mapokeo yasiyojulikana yasiyo na maana ya pekee. Bibi-arusi Mkristo asidhani kwamba vazi jeupe ni la lazima, wala halikatazwi ulimwenguni mwote.

Shela yaweza kuonwa kwa njia iyo hiyo. Maandiko hayakatazi mwanamke kuvaa kifuniko cha kichwa anapokuwa mbele ya atakayekuwa mumewe. (Mwa. 24:63-67) Kwa hiyo hakuna katazo la kuvaa shela ya kibibi arusi kama vazi la kuvutia. Walakini, ikiwa watu wa nchi huona shela ya kibibi-arusi kuwa ni ya dini ya uongo au ni ya ushirikina, wenye kuoana wafikirie hilo.

Hakuna haja ya kuzungumza mifano mingine inayohusu mavazi ya arusi. Jambo la kukumbuka juu ya mavazi ya arusi, yawe ya anasa au ya kikawaida tu, ni kwamba mavazi silo jambo la maana zaidi! Yasiachwe yakwaze wengine wala yalete huzuni. (1 Kor. 8:13) Karibuni mtu hatayakumbuka, lakini furaha ya arusi ya Kikristo yenye kiasi itadumu mume na mke wanapotumia mashauri ya Maandiko waliyopokea.

SHEREHE YENYEWE

Mkazo huu unaofaa juu ya pande za kiroho za arusi zenye kuthawabisha wahusu hasa sherehe yenyewe. Si lazima kuwe na namna ya pekee ya sherehe, isipokuwa inayotakiwa na sheria ya nchi. Kwa hiyo mambo mengi yaweza kupangwa na mtu mwenyewe. Hiyo yatia ndani maulizo kama bibi-arusi, bwana-arusi, wasimamizi wao, na wenye kuwatumikia wataingia jumbani kwa mtindo fulani, kama kuna mtu atakayemtoa bibi-arusi awe wa bwana-arusi, kama kutakuwa na mwenye kusimamia bibi-arusi na rafiki ya bwana-arusi (mhenga) au wengine wenye kushiriki sherehe, na mambo mengine kama hayo ambayo kwa kweli ni madogo tu. (Zab. 45:14; Yohana 3:29) Ikiwa kuna jambo kati ya hayo litakaloharibu furaha ya wakati huo likiongezwa, sababu gani litiwe ndani?

Kabla arusi haijafanyika katika Jumba la Ufalme la mashahidi wa Yehova, wanaotazamiwa kuwa mume na mke wapate ruhusa ya mipango itakayofanywa katika jumba kutoka wa wahudumu wanaolisimamia. Wanaume hao waliokomaa hawapaswi kufanya wenye arusi wafuate mapendezi yao juu ya arusi. Lakini wanaangalia sana kusifanywe jambo katika Jumba la Ufalme la kuchafua mikutano inayofanywa humo au linaloweza kukwaza wengine au kuudhi waliomo kundini au mtaani. Wanakumbuka shauri hili: “Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi, ili mpate kuwa bila hitilafu na kutokwaza wengine.”​—⁠Flp. 1:10, NW; Zab. 133:1.

Lakini hilo halipaswi kuleta ugumu wo wote, kwa maana Wakristo wanaooana wanajaribu kutumia shauri ilo hilo la Biblia. Kwa mfano, bibi-arusi na bwana-arusi wanaweza kuonyesha upendo wao wenye kuongozwa na kanuni na huruma kwa wahudhuriaji kwa kuweka wakati wa sherehe kisha kujitahidi kuwapo wakati huo. Kufuata wakati hivyo, kama ilivyopendekezwa katika mfano wa Yesu wa wanawali (bikira) kumi (Mt. 25:10-12), kutaonyesha arusi ya Kikristo ni tofauti na arusi nyingi za ulimwengu, ambamo wengine hudharauliwa na ambamo uke huabudiwa kama mungu mara nyingi maana bibi-arusi huchelewa makusudi.

Ikiwa hii ndiyo mara ya kwanza kwa watu wa ukoo wa kilimwengu wa wenye kuoana kuhudhuria katika Jumba la Ufalme, huenda wakavutwa sana na tofauti hizo. Huenda wakaona kwamba muziki ukitumiwa utakuwa juu ya vichwa vya Maandiko, ukiwa umetolewa katika kitabu cha nyimbo kinachotumiwa na mashahidi wa Yehova, si ngoma za mapokeo (za kimila) zinazotia ndani muziki wa kilimwengu. Na hasa wamepaswa kuvutwa na hotuba ya ndoa yenye kufaidi inayotegemea Neno la Mungu aliloliongoza kwa roho yake.

Naam, mashahidi wa Yehova wana nia ya kuwa tofauti na ulimwengu katika njia nyingi za maisha, kwa hiyo hawajioni wana lazima ya kujifunza vitabu vinavyotoa maelezo juu ya namna arusi “zinapaswa” kufanywa. Hivyo, katika arusi, na katika mambo mengine yo yote, Wakristo waliokomaa wanaonyesha kiasi wanachopata kwa kujifunza Neno la Mungu, wawe wenye kufikiri sawasawa na wenye upendo. Hivyo, wanaacha ‘kiasi chao kijulikane na watu wote.’​—⁠Flp. 4:5, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki