Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 8/15 kur. 19-22
  • Wewe Umekwazwa na Mambo Yaliyofanywa na Wengine?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Umekwazwa na Mambo Yaliyofanywa na Wengine?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MIFANO YA MAANDIKO
  • HAKUNA SABABU ZA KUKWAZWA
  • KWA SABABU GANI UMEKWAZWA?
  • HESABU BARAKA ZAKO
  • ONYO LA KUTOWAKWAZA WENGINE
  • Hakuna Kitu Chochote Kinachoweza Kuwakwaza Waadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Je! Wewe Unaacha Wengine Wakukwaze?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je, Utakwazika kwa Sababu ya Yesu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • “Simameni Imara”—Msijikwae
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 8/15 kur. 19-22

Wewe Umekwazwa na Mambo Yaliyofanywa na Wengine?

ALIKUWA mhudumu Mkristo kwa miaka mingi. Vilevile alikuwa amelea watoto wake katika “adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” Lakini siku moja, aliacha kushirikiana na Wakristo wenzake akaandikia Watch Tower Society akieleza sababu zake. Ni jambo gani lililokuwa limemkwaza? Alikuwa ameona kwamba alikuwa ametendewa vibaya na wengine katika kundi lake.​—⁠ Efe. 6:4, NW.

Tena, kulikuwa na mtumishi wa huduma katika kundi kubwa ambaye aliacha kupendezwa kabisa na kazi ya Yehova akaacha kushirikiana na watu wa Yehova. Alikwazwa na mwenendo wa babaye, ambaye alikuwa amekuwa mwangalizi wake, ambaye alikuwa ametengwa na ushirika kwa sababu ya uzinzi.

Kati ya wale waliokwazwa wakaacha kupendezwa kabisa na kazi ya Yehova walikuwa watu wawili wazee waliooana. Kwa sababu gani? Kwa sababu mipango fulani ya kibiashara waliyokuwa wamefanya na Mkristo mwenzao ilionekana kwao kama ilikuwa ya udanganyifu.

Na tena, kulikuwa na mwanamke kijana Mkristo ambaye alikuwa ameweka maisha yake wakf kwa Yehova Mungu lakini sasa alikuwa anasita-sita katika kujitoa abatizwe. Ni jambo gani lililokuwa karibu kumkwaza? Ni mwenendo usio wa hekima wa mtumishi fulani katika kundi lake.

Ni jambo gani linalofanana katika mambo haya yote yaliyoonwa. Yote yanaonyesha watu wanaofanya kosa la kuacha mwenendo usio wa hekima au mbaya wa mtu mwingine uwakwaze hata kupoteza tumaini la uzima wa milele.

Ni kweli kwamba sisi sote tunayo maono yetu ya ndani. Mtu anapotukosea au kutukatisha tamaa sana, kawaida ya wanadamu ni kuudhika, kama vile tunavyoona maumivu tunapojichoma kidole chetu cha mguu au tunapojigonga kidole chetu cha mkono kwa nyundo. Lakini je! ni jambo la hekima kukasirika na kupiga teke au kuvunja kitu kwa sababu tu tumeudhiwa? Kwa hiyo tunaweza kujiuliza, Je! ni jambo la hekima tujiachilie tukwazwe tutoke katika njia ya uzima kwa sababu tu ya mwenendo usio wa hekima au mbaya wa wengine, hata ukiwa ulitukatisha tamaa sana au kutuletea taabu?

Badala ya kukwazwa tutoke katika kweli ya Mungu kwa sababu ya kuudhika sana, ingekuwa vizuri kujikumbusha kwamba hakuna ye yote kati ya watumishi wa Mungu wa kidunia leo aliye mkamilifu. Kwa sababu ya kutokamilika watafanya makosa mara kwa mara. (Mwa. 8:21) Ulimwengu pamoja na mtawala wake, Shetani Ibilisi ndio wanaowakaza watende hivyo. Kwa sababu ya uhakika huu, je! hatupaswi kuwaona ndugu zetu Wakristo katika njia inayofaa na kwa huruma?​—⁠Yohana 12:31; 1 Yohana 2:15-17.

MIFANO YA MAANDIKO

Maandiko yanaonyesha wazi kwamba makosa na dhambi za watumishi wenzetu wa Mungu si sababu halali za kutufanya tukwazwe tutoke katika utumishi wa Mungu. Wakati wa safari yao jangwani Waisraeli walinung’unika, wakaasi na mara kwa mara hata wakafanya ibada ya uongo. Lakini je! kupotoka kwao kungekuwa sababu halali ya kumfanya Mwisraeli ye yote akwazike na kuacha kushirikiana na watu wa Yehova? Sivyo kama angetaka baadaye afike katika “nchi ijaayo maziwa na asali.”​—⁠Kut. 3:8.

Hata Mfalme Daudi, ambaye alitajwa na Yehova kama “mtu aupendezaye moyo wake,” alifanya makosa mazito. Lile lililokuwa zito zaidi lilikuwa juu ya mke wa Uria, ambalo kwalo Mungu alimwadhibu vikali sana. Lakini makosa haya yote ya Mfalme Daudi au mojawapo lingempa Mwisraeli ye yote sababu halali ya kukwazwa na kujitenga na taifa la Yehova? Je! Mungu angesikiliza sala zake kama angefanya hivyo? Je! angeweza kutoa sadaka kwa ajili ya dhambi zake akiwa amejitenga na ukuhani wa Walawi?

Tena kuna mifano ya mitume wa Yesu na wanafunzi wengine. Wale mitume kumi waliudhika sana walipojua kwamba Yakobo na Yohana, pamoja na mama yao, walikuwa wamemwomba Yesu vyeo vilivyo vikubwa zaidi katika ufalme wake. Lakini je! walikwazwa? Je! walikuwa na kinyongo juu ya Yakobo na Yohana na kuacha kushirikiana na Yesu? Au je! Yesu mwenyewe alikwazwa na kuacha kutumikia Baba yake wa mbinguni kwa sababu mmoja wa mitume wake aligeuka akawa msaliti, mwingine akamkana mara tatu na wote wakakimbia wakati aliposhikwa? Mwenendo wao haukuharibu uhusiano (urafiki) wake na Mungu.​—⁠Mt. 20:20-28; 26:20-75.

Vilevile habari ya Maandiko iliyoongozwa na Mungu inatuambia kwamba Paulo na Barnaba walikuwa na kutopatana kati yao juu ya kumchukua Yohana Marko pamoja nao, na kwa sababu hiyo wakaachana kila mmoja akaenda njia yake. Lakini je! ye yote kati yao aliacha kumtumikia Mungu kwa sababu hiyo? Hata kidogo! Badala yake tunasoma kwamba miaka mingi baadaye mtume Paulo aliuliza kwamba Yohana Marko aje kwake kwa sababu ya utumishi wake unaomfaa.​—⁠Matendo 15:36-41; 2 Tim. 4:11.

Ee ndiyo, kulikuwako na wengine wa wanafunzi wa Yesu waliokwazwa. Alipowaambia kwamba wangehitaji kula nyama ya mwili wake na kunywa damu yake, walipaza sauti wakasema: “Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia?” na kama matokeo hawakutembea tena na Yesu. Lakini ni mwenendo wa upumbavu namna gani! Kama alivyosema Petro wakati huo, hakukuwa na mtu mwingine wa kumwendea: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.”​—⁠Yohana 6:53-69.

Ndivyo ilivyo na leo. Yehova Mungu na Yesu Kristo wanaachilia kutokamilika kwa watumishi na wajumbe wao wa kibinadamu. Mungu anatumia ‘ndugu za Kristo,’ wanaoitwa kwa jumla “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wafanye kazi Yake duniani. Wale washiriki wa kikundi hicho ni watu wasiokamilika, wanafanya makosa, hata hivyo Mungu anawatumia na kuwabarikia. Naye Yesu alisema kwamba mambo ambayo wamefanyiwa angehesabu kama yamefanywa kwako, wajapokuwa si wakamilifu.​—⁠Mt. 24:45-47; 25:31- 46.

HAKUNA SABABU ZA KUKWAZWA

Tunapofikiria habari hii tunaona kwamba mtu kujiachilia akwazwe na yanayofanywa na wengine atoke katika utumishi wa Mungu ni kukosa kuonyesha hekima, haki ya hukumu, na zaidi ya yote, upendo. Neno la Mungu linatuambia kwamba furaha ni fungu la watumishi wa Mungu. (Isa. 65:14) Kwa sababu gani ujiachilie unyang’anywe furaha yako na yanayofanywa na mtu mwingine? Neno la Mungu linashauri kwa kufaa: “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.” Ikiwa ni jambo lisilo la hekima kujiachilia unyang’anywe na mwingine furaha ya kumtumikia Yehova, na ndivyo ilivyo, basi ni ujinga mkubwa kujiachilia unyang’anywe na mwingine taraja lako la uzima wa milele katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu. Je! mtu kujiachilia akwazwe namna hiyo si sawasawa na kujiua?​—⁠Mhu. 7:9.

Kuchukua mwenendo wa namna hiyo vilevile ni kukosa kuonyesha haki ya hukumu. Namna gani hivyo? Kwa sababu mtu anayefanya hivyo anachukua mwenendo uliyo kinyume cha maagizo ya Yesu. Yeye alituagiza kwanza tumwendee yule aliyetukosea sisi wenyewe peke yetu, tujaribu kutengeneza mambo. Hatua hiyo ikishindwa, yeye alituamuru kwamba tuchukue mtu mwingine mmoja au mawili pamoja nasi. Na hiyo ikishindwa, aliamuru kwamba liwe jambo la kundi. Hilo likishindwa? Mwenye kukosa, wala si yule aliyekosewa, angeondolewa kundini.​—⁠Mt. 18:15-17.

Unapokwazwa na mwenendo wa mwingine unajitangaza kwamba humsamehi mtu huyo. Lakini unataka kuwa asiyesamehe? Yesu alisema kwamba Mungu angetuhukumu kwa ukali ule tunaowahukumu wengine nao, kwamba hangetusamehe ikiwa sisi hatuwasamehi wale wanaotukose. Na kwamba tunapaswa kusamehe, si mara moja au mara mbili tu bali kama Yesu alivyomwambia Petro, “Hata mara sabini na saba.”​—⁠Mt. 6:14, 15; 18:21-35, NW.

Si hayo tu, bali kujiachilia ukwazwe na kukataa kumsamehe ingekuwa kujitanguliza. Namna gani hivyo? Kwa sababu unajitanguliza kuchukua cheo cha Mungu katika kumhukumu ndugu yako. Ni kama vile Yusufu, mwana wa mzee wa ukoo Yakobo alivyosema wakati ndugu zake walipoona mashaka juu ya vile mwenendo wake ungekuwa baada ya kifo cha baba yao: “Msiogope, je! mimi ni badala ya Mungu?” Ndiyo, hata ingawa walikuwa wamemwuza kama mtumwa na alikuwa ametaabika kwa miaka mingi akiwa mtumwa, yeye hakuweka kinyongo juu yao. Yeye hakuweka roho ya kulipiza kisasi bali aliwasamehe.​—⁠Mwa. 50:19-21.

Wala si hayo tu. Ukiacha kushirikiana na watu wa Yehova kwa sababu ya mambo yaliyofanywa na mtu mmoja au na watu wengi, je! wewe hukosi kuwaonyesha upendo wengine wote? Ni kama kwamba unawaambia kwamba ushirika wao wenye upendo haulingani na maono yako. Lakini je! kweli hivyo ndivyo ilivyo? Zaidi ya hayo, ukijiachilia ukwazwe na mambo yanayofanywa na mwingine utoke katika utumishi wa Yehova, upendo wako kwa jirani uko wapi? Upendo wako kwa wale wanaoona njaa na kiu ya mambo ya haki, wale wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote wanayoyaona yakitendeka, na zaidi ndani ya Jumuiya ya Wakristo? Njia peke yake ya kuwaonyesha upendo ni kuvumilia katika utumishi wa Kikristo bila kujali mwingine amefanya jambo gani?

Zaidi ya hayo, unapokwazwa na mambo yanayofanywa na wengine unakosa kuonyesha upendo kwa Yehova Mungu vilevile. Namna gani hivyo? Kwa sababu ameruhusu iwe hivyo? Yehova Mungu ni mstahimilivu. Yeye anaruhusu mambo mengi ambayo hayakubali yatokee kama jaribu kwa watumishi wake. Ebu tazama alivyowaruhusu Ayubu na Mwanawe Yesu Kristo, wateseke. Walakini, Yeye ameahidi kwamba hatutaulizwa kuvumilia zaidi ya yale tuwezayo kuvumilia. (1 Kor. 10:13) Ukijiachilia ukwazwe na jambo lo lote ambalo ameruhusu utoke katika utumishi wake ungekuwa ukimlaumu Yehova Mungu na kuonyesha kwamba humpendi. Hiyo inakuwa na maana ya kwamba unamtumikia Mungu katika njia unayotaka. Je! hilo ni jambo la akili? Je! unaweza kumwamuru? Je! wewe unaweza kumwekea Mungu masharti? Je! yeye anakuhitaji, au wewe ndiwe unayemhitaji? Mtunga zaburi anasema nini? “Wana amani nyingi waipendao sheria yako. Wala hawana la kuwakwaza.”​—⁠-Zab. 119:165.

KWA SABABU GANI UMEKWAZWA?

Kama umekwazwa ingekuwa vizuri ujiulize hivi, Kwa sababu gani nimekwazwa? Kwa juujuu tu unaweza kuona kwamba umetendewa isivyo haki, au umekosewa au mtu mwingine amekukatiza tamaa. Walakini Neno la Mungu linatoa mpango wa kuadhibu wenye kufanya makosa mazito na kusawazisha makosa waliofanyiwa watu mmoja mmoja. Je! inaweza kuwa unaelekea kuongozwa na hasira badala ya akili? Mara nyingi inamfanya mtu afuate faida zake mwenyewe. Au je! inaweza, kuwa kwamba unaelekea kujifikiria sana hivi kwamba unachukua kwa uzito sana yanayosemwa na kufanywa na wengine?

Kumbuka, moyo wa mwanadamu ni mdanganyifu na una ugonjwa wa kufisha. (Yer. 17:9) Je! inaweza kuwa kwamba bila kujua ulikuwa ukitafuta sababu ya kuacha kumtumikia Mungu? Kwa hiyo wakati mtu amekwazwa na jambo ambalo mwingine amesema au kufanya inaweza kuwa vizuri ajiulize mwenyewe hivi: Sababu yenyewe iliyonifanya nikwazwe ilikuwa nini? Je! kosa lilikuwa kubwa sana, au kuna kusudi au sababu iliyofichwa iliyonifanya nikwazwe? Mungu anajua jibu.

HESABU BARAKA ZAKO

Jibu la mtume Petro kwamba hakuna pahali pengine pa kwenda, kwamba Yesu peke yake ndiye aliyekuwa na maneno ya uzima wa milele, ndilo unalopaswa kukumbuka unapoelekea kukwazwa na jambo ambalo mwingine amesema au kufanya. Kuna pengine wapi pa kwenda? Je! pendeleo la kumtumikia Yehova Mungu si ndilo jambo kubwa zaidi kupita yote? Je! si ndio utendaji wenye kuheshimika sana kupita mwingine wote ambao katika huo ye yote anaweza kushiriki, kuwa balozi au mjumbe wa serikali ya kimbinguni, kwa kumwakilisha Kristo na kuwaomba watu wapatanishwe na Mungu?​—⁠2 Kor. 5:20, NW.

Ni kazi gani nyingine yenye kuthawabisha (kutoa zawadi) hivyo ambayo mtu anaweza kufanya? Inamletea Yehova Mungu sifa na kulitetea jina lake. Kwa kufanya kazi hii unawatolea wengine tumaini la uzima wa milele katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu itakayofuata Har–​Magedoni. Na kwa sababu kazi yake si ya kichoyo, unapata furaha kubwa kutokana nayo, kwa sababu “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”​—⁠Matendo 20:35, NW.

Na kwa kuwa Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Mungu, anakumbuka utumishi wetu wa uaminifu na kwamba kazi yetu tunayomfanyia si ya bure, unaweza kuwa na hakika ya kupata thawabu (zawadi) wakati ujao. Thawabu gani? Ama ile ya kutawala pamoja na Kristo kwa miaka elfu au kuingia katika “nchi mpya” itakayofuata Har–​Magedoni ambayo katika hiyo Mungu atafuta kila chozi katika macho ya wanadamu wala mauti haitakuwapo, wala huzuni wala kilio wala maumivu. Kwa sababu gani ujiachilie unyang’anywe haya yote na jambo ambalo mwingine alifanya?​—⁠1 Kor. 15:58; Ebr. 6:10; 2 Pet. 3:13; Ufu. 21:4.

Ebu na tuyaangalie mambo ya hakika. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova walio wakf wamejipatia sifa nzuri ya kuwa mifano mizuri kwa sababu ya unyofu wao, amani, umoja na furaha. Wao ni watu wanaompenda Yehova kwa moyo wao wote, akili, nafsi na nguvu na wanaowapenda jirani zao kama wanavyojipenda wenyewe. (Marko 12:29-31) Ukijitenga nao unaweza kutazamia kupata kikundi kingine cha watu wanaojaribu kuishi kulingana na kanuni za Biblia kuliko wanavyofanya? Kama ilivyokwisha kuonyeshwa, wao hawaachilii wale wanaozoea kutenda maovu bali wanawaondoa watoke kati yao.​—⁠1 Kor. 5:13; 6:9-11.

ONYO LA KUTOWAKWAZA WENGINE

Hata hivyo, uhakika wa kwamba Maandiko hayampi ye yote sababu ya kujiachilia akwazwe na jambo linalofanywa na mwingine haupaswi uonwe ukiwa na maana ya kwamba Mkristo anaweza kukosa kujali au aone kumfanya mwingine akwazwe kama jambo dogo. Hata kidogo! Kumkwaza mwingine ni kosa zito sana. Yesu Kristo hakuacha shaka lo lote katika jambo hilo, kwa sababu pindi moja alisema hivi: “[Atakayemkwaza] mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.”​—⁠Mt. 18:6.

Vilevile mtume Paulo alijua uzito wa kumkwaza mwenzi Mkristo na kwa hiyo mara kwa mara alionya juu ya jambo hilo. Yeye alionyesha kwamba hata kama jambo linafaa kabisa, ikiwa linaweza kumkwaza mwingine hatupaswi kulifanya: “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.” Wala si kwamba tu Paulo alilihubiri jambo hili, bali pia alifanya hivyo: “Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.”​—⁠Rum. 14:21; 1 Kor. 8:13.

Ikiwa hatupaswi kufanya hata mambo yanayofaa ikiwa yanaweza kukwaza wengine, basi tunapaswa kuwa waangalifu namna gani ili tusifanye kosa ambalo linaweza kuwakwaza wengine! Akikumbuka jambo hili Paulo alisali kwa ajili ya ndugu zake katika Filipi hivi: “Kwamba upendo wenu uzidi kuongezeka pamoja na maarifa yaliyo sahihi na ufahamu kamili; mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi, ili mpate kuwa bila hitilafu na kutokuwa mkikwaza wengine mpaka siku ya Kristo.” Kwa kuwaonya katika njia hii yeye alikuwa akiwaomba tu wamwige yeye, kwa sababu kama alivyowaandikia ndugu zake katika Korintho: “Sisi hatutoi kwazo lo lote kwa njia yo yote, ili huduma yetu isilaumiwe.”​—⁠Flp. 1:9, 10, NW; 2 Kor. 6:3, NW.

Kazi ambayo Yehova Mungu anatoa ifanywe wakati huu ni jambo la kufanywa kwa kushirikiana. Kama vile viungo vya mwili wa kibinadamu, kila mmoja anasaidia hali njema ya mwingine na kila mmoja anawahitaji wengine. Je! mkono au kidole cha mguu kinaweza kuendelea kuishi bila mwili? Je! kinaweza kufanya kazi yo yote ya maana kikikatwa? Kama vile kila kiungo cha mwili kinavyohangaikia hali njema ya viungo vingine, ndivyo Wakristo wanavyopaswa kuwa. (1 Kor. 12:12-26) Kwa hiyo kila Mkristo anapaswa kujiangalia asimkwaze Mkristo mwenzake. Unaposhirikiana na Wakristo wa kabila au taifa jingine, fikiria mambo ambayo yanaweza kuwaudhi uepuke kuwaudhi. Je! wewe ni mhudumu aliyekomaa? Jiangalie usiwakwaze wale wachanga na wapya ambao wanaelekea kutazamia mengi mno kutoka kwenu.

Wakati ule ule kila mmoja ni lazima atambue kwamba hakuna aliye mkamilifu, na kwamba wakati wengine wamekosa, wawe wamekosa kufuata kanuni za Biblia au ni wewe wamekosea, hiyo si sababu halali ya kukukwaza. Mtu kujiachilia akwazwe na wengine ni kukosa hekima, haki ya hukumu, na upendo, kama vile tumekwisha kuona. Je! kosa ni zito sana? Ni juu ya kundi lichukue hatua. Je! ni wewe mwenyewe umekosewa? Basi fuata maagizo ya Yesu yanayopatikana katika Mathayo 18:15-17. Ni jambo la aina nyingine? Liondoe akilini mwako, uonyeshe upendo unaofunika wingi wa dhambi.​—⁠1 Pet. 4:8.

Unapojiachilia ukwazwe na wengine utoke katika utumishi wa Mungu unamchukiza Yehova Mungu. Unawaondolea wengine furaha pamoja na wewe mwenyewe. Yule peke yake unayenipendeza ni Shetani Ibilisi, kwa sababu anafurahia kuona kutopatana na kukosa furaha miongoni mwa watu wa Mungu. Bila shaka wewe hutaki hivyo!

Ndiyo, usimruhusu ye yote akunyang’anye furaha yako. Lishikilie sana tumaini lako la uzima wa milele. Hesabu baraka nyingi unazopata ukiwa mshiriki mwenye bidii katika kuzihubiri habari hizi njema za ufalme wa Mungu kwa wote watakaosikia. Uone ubora walio nao watumishi wenzako ushiriki pamoja nao furaha inayotokana na kutoa!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki