Je! Wewe Unaacha Wengine Wakukwaze?
YEYE alikuwa Mzungu—kwa wazi mwaminifu, mwenye adabu, na mwenye kuipenda kweli. Wakati mashahidi wa Kikristo wa Yehova walipofika nyumbani kwake katika mji wa New York yeye na mkewe waliwasikiliza. Karibuni wakaanza kufurahia funzo la Biblia la kawaida la kila juma katika nyumba yao.
Lakini jambo fulani likatokea. Mtu ambaye alielekea kuwa Shahidi na ambaye mtu huyu aliyeanza kupendezwa karibuni aliheshimu sana alitenda kosa zito akafukuzwa katika kundi la Kikristo. Mwenendo wa mtenda kosa ulimfisha moyo mtu huyo hata akakwazika na kuanguka, akaacha kujifunza Biblia na Mashahidi. Lakini mke wake hakuacha. Aliendelea kujifunza, akabatizwa, akalea wana wawili, na wote wawili leo ni wahubiri wa wakati wote wa habari njema za ufalme wa Mungu, baada ya miaka mingi. Mara nyingi anajiunga nao miezi mingine katika kuhubiri huko kwenye furaha na kwenye kuthawabisha sana na katika utendaji wa kufundisha Biblia. Kwa habari ya mume, angali hajaamua, anapendezwa kukutana na Mashahidi na kuhudhuria mikutano mara kwa mara, lakini bado ameudhika, amekwazika.
Hadithi hii ya kweli inaonyesha msiba wa kuacha wengine watukwaze. Fikiria hilo. Waza. Fikiri. Kwa sababu tu mtu amefanya kosa, liwe kubwa au dogo, hiyo si sababu ya kukufanya ufuate mwendo usio wa hekima. Kwa sababu gani ujidhuru ati kwa sababu mtu mwingine amefanya jambo lililokuudhi?
Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alituachia kielelezo katika jambo hili, sawa na alivyofanya katika mambo mengine mengi. (1 Pet. 2:21) Je! aliudhika, alikwazika kwa sababu mmoja wa mitume wake mwenyewe, Yuda, aligeuka akawa msaliti, kwa sababu mwingine, Petro, alimkana mara tatu kwamba hata hamjui, au kwa sababu wote walimwacha akiwa katika wakati wa hatari? Je! aliudhika akakwazika? Hilo lingalikuwa jambo la upumbavu namna gani! Si kwamba angalijidhuru sana sana mwenyewe tu bali pia angaliharibu kusudi la Baba yake wa kimbinguni na wanadamu wote!
Lililo zito zaidi kuliko kujidhuru wenyewe na wengine tunapoacha watu watukwaze ni kushindwa kufanya yaliyo haki machoni pa Mungu. “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Hata mtu mwingine ye yote afanye nini au asifanye nini, huo si udhuru wa kutomlipa Mungu anayotuomba.—Mik. 6:8.
Kwa mfano: Wakaaji wa nchi wana wajibu wa kuzitii sheria zake, kutia na kulipa kodi mbalimbali na kutii sheria za barabarani. Tuseme raia anapunjwa, ananyang’anywa au kutendwa kwa udhalimu na raia wenzake kwa njia nyingine. Je! anaweza kutumia huo kama udhuru wa kuvunja sheria zo zote za nchi anazotaka kuvunja, akikataa kulipa kodi na kupuza sheria za barabarani? Ingawa wachache leo wangeshikilia maoni hayo, wote wakifanya hivyo ungekuwa ni uasi juu ya serikali. Mambo hayo mawili hayahusiani kabisa kwa kadiri wajibu unavyohusika.
Raia anaweza kupata kisasi mahakmani tu kisha aachie serikali kuadhibu watenda makosa huku yeye mwenyewe akizitii sheria za nchi. Ndivyo ulivyo uhusiano wetu na Mungu, Muumba wetu. Tuna wajibu wa kuzitii amri zake na kumwachia yeye aamue mambo. Ni kama vile mtume Paulo alivyoshauri: “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena [Yehova].” Yesu Kristo naye anatuhakikishia kwamba, katika wakati wake Mungu, Atasawazisha makosa yote, anaposema hivi: “Ole wake mtu yule aliletaye jambo la [kukwaza]!”—Rum. 12:19; Mt. 18:7.
Jambo jingine: Kuacha wengine watukwaze ni jambo lisilo la upendo. Kunaonyesha hatumpendi Mungu kwa mambo ambayo ametufanyia. Imetupasa tuthaminije mambo yote ambayo ametufanyia kwa kutupa uhai na mambo yote yaliyo ya lazima kuendeleza uhai! Na ebu wazia zawadi ya kutoa Mwanawe mzaliwa wa pekee, ambaye kupitia kwake tunaweza kutumaini kupata uzima wa milele! (Yohana 3:16) Kwa hakika imetupasa tufanye yote tuwezayo kuonyesha tunathamini fadhili zote za upendo ambazo Mungu ametutendea!
Tena, ikiwa tunampenda Mungu na sheria yake kweli, hakuna kitakachotukwaza. Biblia inasema hivi: “Wana amani nyingi waipendao sheria yako, wala hawana la kuwakwaza.”—Zab. 119:165.
Mara kwa mara, maneno au matendo yanayoweza kuudhi mtu si ya namna yenye kufanya asiyefikiria afukuzwe kundini. Ingawaje, kama alivyosema Mfalme Sulemani katika sala yake ya kuweka hekalu wakf, “Hakuna mtu asiyetenda dhambi.” Kama Mungu angekumbuka kutokamilika kwetu na makosa yetu yote, ye yote kati yetu angekuwa wapi? Naam, “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee [Yehova], nani angesimama?”—1 Fal. 8:46; Zab. 130:3.
Inatupasa tutendee wengine vile tunavyotaka Mungu atutendee. Tukiacha wengine watukwaze, hatuwi wenye kusamehe, nasi tusiposamehe wengine makosa yao, wala sisi hatuwezi kutazamia Baba yetu wa kimbinguni atusamehe yetu. (Mt. 5:7; 6:14, 15; 18:21-35) Kwa upande mwingine, tukiwa na upendo kwa washiriki wa jamaa zetu na/au kwa waabudu wenzetu, hatutaendelea kufikiria makosa yao tu bali ‘tutakuwa na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.’—1 Pet. 4:8.
Hasa wale wanaojidai kuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo hawawezi kutumia mambo ambayo wengine wamefanya kama udhuru wa kuacha kujifunza Neno la Mungu, kuacha kushirikiana na Wakristo wenzao, kuacha kushiriki katika kujulisha habari njema za ufalme wa Mungu. Kwa kweli, wakiacha mambo ambayo wengine wanafanya yawazuie wasitimize matakwa haya ya Kikristo, wanaleta mashaka juu ya ukweli wa dai lao kwamba ni wanafunzi wa kweli wa Kristo. Wakikwazika hiyo ingeleta shuku ya kufikiri wanatafuta udhuru, kwa kujua au bila kujua, waache kumtumikia Mungu.
Si kwamba imetupasa tujihadhari tusiache wengine watukwaze sisi tu, bali pia imetupasa tujihadhari kwa upendo na hekima tusikwaze wengine. Haki inataka tufanyie wengine vile ambavyo tungetaka watufanyie. (Luka 6:31) Hatungetaka ye yote awe mzembe au asiyefikiri hata atukwaze, sivyo? Basi imetupasa tujiangalie tusikwaze wengine. Kwa mfano, barua iliyopokewa majuzi na Watch Tower Society ilikuwa na malalamiko ya kwamba watu fulani wasiokomaa walikuwa wakikwazika kwa sababu wengine waliotazamwa kama mifano myema walijionyesha mno kuwa wapenda vileo. Kufuata mwendo huo katika matumizi ya vileo hakukuwa kutii shauri la mtume Paulo: “Mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe.” Zaidi ya hilo, Yesu hivi: “Atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.” Kwa hakika hakuna ye yote kati yetu angetaka kupatwa na jambo hilo, sivyo?—Ebr. 12:13; Mt. 18:6.
Kwa hiyo wote na wajiangalie wafanye mambo ya hekima, ya upendo na haki, kwa njia hiyo wakijiepusha wasikwazwe na wengine na pia wao wenyewe wasikwaze wengine.