Washauri Wenye Kuonyesha “Upole wa Hekima”
KUNDI la Kikristo lililo na wanaume wenye hekima na ufahamu ndani yake linabarikiwa kweli kweli. Kwa maana namna ilivyo kwa jamaa ya nyumbani ndivyo ilivyo vile vile na kwa ‘nyumba yake Mungu’—kwamba “nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika, na kwa maarifa vyumba vyake hujazwa vitu vyote vya thamani na vya kupendeza.”—Efe. 2:19; Mit. 24:3, 4.
Wale wanaotumikia kama wazee wa Kikristo wanalo pendeleo la kushauri ndugu zao kutokana na Neno la Mungu. Awezaje mzee kujionyesha mwenyewe kuwa ‘mwenye hekima na ufahamu’ katika kufanya hivyo? Mwanafunzi Yakobo anajibu: “Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima [“katika unyenyekevu wa hekima,” An American Translation; “kwa adabu inayotokana na hekima,” New English Bible].” Upole huo unatokana na ustahifu na shukrani kwa hekima ya Mungu, “hekima itokayo juu,” na kukubali makosa ya mtu mwenyewe kwa unyenyekevu. Nia hii ya unyenyekevu itamlinda mshauri asifanye makosa yenye kudhuru. Itayaongezea matokeo ya shauri lake.—Yak. 3:13, 17.
UPOLE WA ROHO WAONGOZA SHAURI LA MWENYE HEKIMA
Mara kwa mara huenda mtu mmoja akamfikia mzee, au hata kufikia mzee mmoja nyuma ya mwingine, akijaribu kumpata mtu fulani atakayempa jibu analolitaka—hata kama si sawa kwa kulingana na kanuni za Maandiko. Hii ni sawa na maarifa ya watoto fulani wanaomlinganisha mzazi mmoja na mwingine. Nyakati nyingine huenda ikawa kwamba mzee atataka amwulize kwanza yule anayetafuta shauri kama amekwisha kusema na wengine au sivyo na shauri walilolitoa. Unyenyekevu ungemfanya asiwe mwepesi wa kulipinga shauri hilo, zaidi ikiwa hajapata nafasi ya kuzungumza kwanza na yule mshauri mwingine.
Upole hauruhusu kuwa mkatili ama kuwa mnyofu isivyotakiwa. Hata hivyo lazima mzee ajihadhari kwamba haruhusu kupendezwa na urafiki wa kipekee ama kupata ukubali wa mwingine kumsukume atoe shauri lililokusudiwa kupendeza, mahali pa kutoa shauri la Neno la Mungu kwa uaminifu. (Mit. 24:25, 26) Hatuwezi kupunguza nguvu za Neno la Mungu tuwapendeze watu, tukizitumia kanuni zake ovyo ovyo ili tuitulize dhamiri yao. Hii ingeleta wema gani, kwa kuwa inayaweka mapendezi yao ya maisha hatarini? Ingekuwa kama shauri alilopewa Amnoni na binamu yake. Shauri hilo lilimletea Amnoni matokeo mazuri ya muda katika kuitosheleza tamaa yake, lakini nyumaye lilimletea hasara ya uhai wake.—2 Sam. 13:1-19, 28, 29.
Mahali pa ‘kuyatekenya masikio ya ndugu zetu,’ lazima tuliseme “Neno,” Neno la Mungu kwa uaminifu. (2 Tim. 4:1-4, NW) Mwige mtume Paulo, asiyesita kuwaambia ndugu zake “shauri lote la Mungu.” Kwa njia hiyo utajiepusha na hatia ya damu mbele za Mungu. (Matendo 20:26, 27, NW) Mshauri mwenye “unyenyekevu wa hekima,” basi, ataonyesha wazi woga wa kimungu naye atashauri au kukaripia kwa haki inapokuwa lazima na, mwishowe, atashukuriwa zaidi na ndugu zake kuliko kama angekuwa amejitia katika kusifu-sifu kwa uongo.—Mit. 28:23.
Ingawa hawasiti kutoa shauri linalohitajiwa, wazee watafahamu vile vile kwa unyenyekevu kwamba wao hawawezi kuwafanyia wengine maamuzi yao. Ambapo Biblia inasema waziwazi, nao vile vile waweza kusema waziwazi. Lakini mambo mengi sana ni yanayopaswa kuamuliwa na dhamiri ya mtu mwenyewe na maamuzi juu ya atakachofanya au ambacho hatafanya. Kumfanyia uamuzi wake kungemweka mzee lawamani kwa ajili ya matokeo. Yeye angeshiriki lawama kwa mabaya yo yote ambayo huenda yatokee.—Gal. 6:5; Rum. 14:5, 12.
Huenda Mkristo mwenzetu akasaidiwa mara kwa mara kufikia uamuzi wa kipekee kwa maulizo tu yanayomsaidia kufikiri juu ya faida na ubaya wa jambo lenyewe nayo yatamsaidia ayafikirie mambo yanayoweza kutokea ya njia za hiari yake zilizo wazi kwake.
“WAKATI WA KUNYAMAZA, NA WAKATI WA KUNENA”
Huenda mzee asijue kabisa jibu la maulizo fulani anayoulizwa. Au huenda asiwe na hakika juu ya namna kanuni za Maandiko zinavyotumika katika jambo fulani. Yampasa afanye nini?
Mtu angeweza kuruhusu woga wa kupungukiwa na heshima machoni pa mwulizaji umsukume atoe jibu la namna fulani. Lakini huu sio ‘upole wala unyenyekevu wa hekima.’ Kiburi kinaelekeza kwenye aibu; unyenyekevu waonyesha hekima. (Mit. 11:2) Mithali 21:23 inashauri: “Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake, atajilinda nafsi yake na taabu.” Ni bora zaidi kukubali kwamba hujui kuliko kutoa jibu lisilo sawa ambalo lingeweza kutokeza magumu yenye kutaabisha. Ndiyo, kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena,” nao wakati wa kunena ni unapokuwa umepata nafasi ya kupata jibu lililo sawa.—Mhu. 3:7.
Kwa kweli, inakuwa bora kuacha maulizo fulani bila kuyajibu. Huenda yakawa ya kuchunguza-chunguza tu, bila ya kuwa yanayokamatana na hali fulani iliyoko ama ugumu. Maulizo kama hayo mara nyingi ‘hayawi na ukomo,’ yanaleta tu “maswali wala si madaraka ya Mungu yaliyo katika imani,” ndiyo, ni “maneno ya ubatili” tu. (1 Tim. 1:4-7; 2 Tim. 2:14) Hata ingawa huenda mwulizaji akasisitiza sana, mshauri mwenye busara anaweza kuamua kutojitia ndani.—Mit. 12:8; 17:27.
“KWA WINGI WA WASHAURI KUNA UKOMO”
Unapokutana na maulizo magumu au yenye mashaka, sala na funzo la kipekee ni vya muhimu sikuzote. Lakini, mtu mwenye hekima vile vile atakumbuka kwamba “kwa wingi wa washauri kuna ukomo.” (Mit. 15:22, NW) Kufikiri pamoja na wengine kunatokeza wingi wa hekima na ujuzi. (Mit. 13:10) Vile vile huenda maoni yaliyosawazika yakatokea. Halafu, tena, mzee mwingine akikaribishwa ashiriki katika mazungumzo ambapo mtu fulani anatafuta shauri juu ya jambo zito, ni ulinzi wa mzee kutosingiziwa nyumaye kwamba alitaja mambo ambayo kwa kweli hakuyataja. (Kum. 19:15; linganisha Waamuzi 12:1-3.) Hata hivyo, kwamba unamkaribisha tu mzee mwingine aungane nawe katika kuangalia ulizo la mtu, siyo sababu ya kumfanya mwulizaji ajione sasa yumo katika kesi fulani ya hukumu. Bali, kama wewe ndiwe mzee anayefikiwa kwanza, waweza kuarifu kwa unyenyekevu kwamba unajisikia ungeweza kufaidika kutokana na usaidizi wa mwingine.
Wazee fulani katika kundi wanakabidhiwa wajibu wa kutumikia kama halmashauri ya hukumu, lakini hii haizuii kutafuta kwao msaada wanapokutana na uamuzi mgumu. Wanaweza kujifaidi kwa msaada wa wazee wengine, wajapokuwa watajifanyia uamuzi wa mwisho wenyewe. Linalopendeza, Mishnah ya Kiyahudi yasema kwamba baraza za vijijini katika Israeli zilitofautiana katika hesabu kwa kulingana na uzito wa kesi iliyokuwako mbele yao.—Tazama Aid to Bible Understanding, uk. 385.
Kuna ubora kweli kweli katika “wingi wa washauri.” Lakini wingi peke yake hauhakikishi usawa. Wingi waweza kukosea. Mambo ya kukatia maneno yanayohakikisha maamuzi yafaayo sikuzote ni Biblia na roho takatifu ya Mungu. Upole wa hekima ya kweli unahitaji kujitiisha kwa hivi kwa unyenyekevu na kwa makini.